Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sababu Uepuke Uwasiliani-roho

Sababu Uepuke Uwasiliani-roho

Sababu Uepuke Uwasiliani-roho

IKIWA umefunzwa kwamba namna fulani za uwasiliani-roho ni njia za kuwasiliana na roho wema, huenda ukashangaa kujua jinsi Biblia inavyosema kuhusu uwasiliani-roho. Mathalani, inasema: “Msiwaendee waaguzi wa mizimu wala wachawi ili kuwaomba wawaagulie na hivyo mkajitia najisi.”Mambo ya Walawi 19:31; 20:6, 27, Biblia Habari Njema, italiki ni zetu.

Kwa kweli, Biblia husema kwamba mtu anayezoea uwasiliani-roho ni “chukizo kwa BWANA.” (Kumbukumbu la Torati 18:11, 12) Kwa nini? Swali hilo litajibiwa tuchunguzapo kwa makini inavyosema Biblia kuhusu zoea moja lihusianalo na uwasiliani-roho—dai la kuwasiliana na wafu.

Je, Wafu Wako Hai?

Tofauti na maoni ya watu wengi, Neno la Mungu, Biblia, hufundisha kwamba wanadamu hawawezi kuwasiliana na wapendwa wao waliokufa. Kwa nini? Ni wazi kwamba endapo mtu yeyote atawasiliana na wafu, lazima wafu hao wawe hai. Lazima wawe na sehemu isiyokufa. Baadhi ya watu hudai kwamba nafsi huendelea kuishi baada ya mwili kufa. Je, ni kweli?

Simulizi la Biblia kuhusu kuumbwa kwa mwanadamu husema: “Bwana Mungu akamfanya mtu kwa mavumbi ya ardhi, akampulizia puani pumzi ya uhai; mtu akawa nafsi hai.” (Mwanzo 2:7, italiki ni zetu.) Je, hilo halifunui kwamba mtu mwenyewe ni nafsi na kwamba hana nafsi isiyoweza kufa ambayo huendelea kuishi baada ya mwili kufa? Kwa kweli, Maandiko husema: “Nafsi inayofanya zambi, itakufa.” (Ezekieli 18:4, Zaire Swahili Bible) “Walio hai wanajua ya kwamba watakufa; lakini wafu hawajui neno lo lote . . . Hakuna kazi, wala shauri, wala maarifa, wala hekima, huko kuzimu,” kaburi la kawaida la wanadamu.—Mhubiri 9:5, 10.

Kwa hiyo kulingana na Biblia, nafsi si kitu kinachoendelea kuishi mwili ufapo na ambacho wanadamu walio hai wanaweza kuwasiliana nacho baadaye. Hapa pana mifano ya wasomi wawili wa Biblia wenye kuheshimiwa ambao wamefikia mkataa wa kwamba nafsi hufa. Mwanatheolojia Mkanada Clark H. Pinnock alisema: “Dhana [ya kwamba nafsi ya mwanadamu haifi] imeathiri theolojia kwa muda mrefu sana, lakini haitegemei Biblia. Biblia haifundishi kutokufa kiasili kwa nafsi.” Vivyo hivyo, msomi Mwingereza John R. W. Stott alisema: “Hali ya kutokufa—yaani kutoharibika—kwa nafsi ni dhana ya Kigiriki si ya kibiblia.”

Hata hivyo, watu hupokea ujumbe na kusikia sauti ambazo huonekana ni kana kwamba zimetoka kwa wafu. Ni nani, basi, wanaosema?

Wanawasiliana na Nani?

Biblia husimulia kwamba mtu fulani wa kiroho asiyeonekana alitumia nyoka, kama mtaalamu wa kutoa sauti atumiavyo sanamu, ili awasiliane na mwanamke wa kwanza, Hawa, na kumfanya amwasi Mungu. (Mwanzo 3:1-5) Biblia humwita mtu huyo wa kiroho, au malaika, “nyoka wa awali, yeye aitwaye Ibilisi na Shetani, anayeiongoza vibaya dunia nzima inayokaliwa.” (Ufunuo 12:9) Huyo Shetani, alifaulu kuwashawishi malaika wengine waasi. (Yuda 6) Malaika hao waovu huitwa roho waovu na ni adui za Mungu.

Biblia huonyesha kwamba roho waovu wana uwezo wa kuwaathiri wanadamu. (Luka 8:26-34) Basi, si ajabu kwamba Sheria ya Mungu husema: “Pasiwe mtu yeyote miongoni mwenu . . . mwenye kutaka kauli kwa mizimu na pepo au kutoka kwa wafu. Maana yeyote atendaye mambo haya ni chukizo kwa Mwenyezi-Mungu.” (Kumbukumbu la Torati 18:10-12, BHN) Hatari za kupuuza sheria hiyo ni gani?

Jambo lililompata Mfalme Sauli wa Israeli la kale hujibu swali hilo. Mfalme Sauli alimwendea mwasiliani-roho kwa sababu ya kuwaogopa adui zake. Alimwomba awasiliane na nabii Samweli aliyekufa. Sauli aliposikia maelezo ya huyo mwasiliani-roho kuhusu mzee fulani, alifikiri mzuka huo ni Samweli. Naye Sauli alipokea ujumbe gani? Israeli litatiwa mikononi mwa adui, na Sauli na wanawe watakuwa pamoja na “Samweli,” kuonyesha kwamba wangekufa. (1 Samweli 28:4-19) Mungu alitendaje kwa sababu ya uamuzi wa Sauli wa kumwendea mwasiliani-roho? Maandiko hutueleza: “Sauli alikufa kwa sababu ya kutokuwa mwaminifu . . . alikwenda kwa mwaguzi kumtaka shauri.” (1 Mambo ya Nyakati 10:13, BHN) Ni matokeo mabaya kama nini!

Hali kadhalika leo, wale wanaojihusisha na uwasiliani-roho wanajihatarisha sana. Biblia huonya kwamba “wale wanaozoea kuwasiliana na roho” watapata “kifo cha pili [au, cha milele].” (Ufunuo 21:8; 22:15) Kwa wazi basi, mwendo wenye hekima na wenye kuokoa uhai ni kuepuka uwasiliani-roho wa namna yoyote.

Jinsi ya Kukinza Roho Waovu

Namna gani ikiwa tayari umejihusisha na uwasiliani-roho? Basi utafanya vyema kuchukua hatua madhubuti za kujilinda na kulinda familia yako dhidi ya madhara ya roho waovu. Hatua gani? Kutoa kielezi: Mtu hulindaje nyumba yake na familia yake dhidi ya wadudu waharibifu? Baada ya kuwaangamiza kutoka nyumbani mwake, yeye huondoa vifaa vinavyovutia wadudu hao. Anaziba mianya na kuimarisha kuta ili kuepuka uvamizi wa wadudu waharibifu, na iwapo wadudu hao wazidi kuongezeka, aweza kuomba msaada wa wataalamu walio karibu.

Utaratibu kama huo waweza kukusaidia ukinze roho waovu na kuepukana nao kabisa. Fikiria mfano wa Wakristo wa karne ya kwanza huko Efeso ambao walizoea uwasiliani-roho kabla ya kuwa Wakristo. Baada ya kuazimia kuacha kabisa uwasiliani-roho, walichukua hatua tatu za kujilinda wenyewe dhidi ya mashambulizi ya roho waovu yanayoshabihi ya wadudu waharibifu. Walifanya nini?

Hatua ya Kwanza

Biblia hueleza: “Idadi kubwa ya wale waliozoea kufanya ufundi wa kimzungu wakaleta pamoja vitabu vyao wakavichoma kabisa mbele ya kila mtu.” (Matendo 19:19) Kwa kuharibu vitabu vyao vya uaguzi, Wakristo hao wapya waliwawekea kielelezo wale wote wanaotaka kukinza roho waovu leo. Haribu kabisa vitu vyote vinavyohusiana na uwasiliani-roho. Hivyo vyatia ndani vitabu vyote, magazeti, vitabu vya katuni, vidio, picha za ukutani, vitu vyovyote vya kielektroni, na kanda za muziki zenye mambo ya uwasiliani-roho, na vilevile hirizi au vifaa vinginevyo vinavyovaliwa kwa ajili ya “ulinzi.”—Kumbukumbu la Torati 7:25, 26; 1 Wakorintho 10:21.

Mtu mmoja huko Amerika Kusini ambaye alikuwa ametumbukia kwenye uwasiliani-roho kwa miongo mingi alizingatia moyoni shauri hilo la Kimaandiko. “Siku moja,” yeye akumbuka, “nilikusanya vitu vyangu vyote vya uwasiliani-roho mbele ya nyumba yangu, nikavipasua vipande-vipande kwa shoka.” Kisha akavichoma vyote vikawa jivu. Baadaye alifanya maendeleo mazuri ya kiroho na punde si punde akawa mhudumu mwenye bidii katika mojawapo ya makutaniko ya Mashahidi wa Yehova.

Lakini, hatua hiyo ya kwanza haitoshi. Kwa nini? Kwa kweli, miaka kadhaa baada ya wale Wakristo katika Efeso kuchoma vitabu vyao vya kimizungu, mtume Paulo aliandika: “Tuna kushindana mwereka . . . dhidi ya majeshi ya roho waovu.” (Waefeso 6:12) Roho waovu hawakuwa wamechoka. Waliendelea kutafuta fursa za kuwanasa. Wakristo hao walihitaji kuchukua hatua gani nyingine?

Hatua ya Pili

Paulo aliwasihi sana Waefeso hao wa karne ya kwanza: “Vaeni suti kamili ya silaha kutoka kwa Mungu ili mpate kuweza kusimama imara dhidi ya mbinu za Ibilisi.” (Waefeso 6:11) Shauri hilo lingali latumika leo. Sawa na yule mtu anayejaribu kuzuia wadudu waharibifu wasiingie nyumbani mwake, lazima Mkristo aimarishe ulinzi wake ulio kama ukuta ili asiangushwe na roho waovu. Hatua hii ya pili huhusisha nini?

“Juu ya mambo yote,” akazia Paulo, “chukueni ngao kubwa ya imani, ambayo kwayo mtaweza kuzima vishale vyote vinavyowaka moto vya yule mwovu.” (Waefeso 6:16) Ngao hiyo ni muhimu sana. Kadiri imani yako iwavyo thabiti, ndivyo uwavyo na nguvu za kukinza majeshi ya roho waovu.—Mathayo 17:20.

Hivyo basi, utaimarishaje ulinzi wako? Kwa kuendelea kujifunza Biblia. Kujifunza Biblia huhusianaje na imani? Kama vile uthabiti wa ukuta utegemeavyo nguvu za msingi wake, vivyo hivyo uthabiti wa imani ya mtu hutegemea sana nguvu za msingi wake. Msingi huo ni nini?

Ujuzi sahihi wa Neno la Mungu. Mtume Paulo aeleza: “Imani hufuata jambo lisikiwalo. Nalo jambo lisikiwalo ni kupitia neno juu ya Kristo.” (Waroma 10:17) Twakualika uombe funzo la Biblia bila malipo kutoka kwa mmojawapo wa Mashahidi wa Yehova, kwa wakati na mahali panapokufaa. Funzo hilo litaimarisha imani yako. (Waroma 1:11, 12; Wakolosai 2:6, 7) Matokeo yatakuwa nini? Muda si muda imani yako itakuwa ngome itakayokulinda dhidi ya uvutano wa roho waovu.—Zaburi 91:4; 1 Yohana 5:5.

Wakristo katika Efeso walihitaji kuchukua hatua gani ya tatu?

Hatua ya Tatu

Wale waamini wapya katika Efeso la kale walichukua hatua za kukinza roho waovu, lakini bado Wakristo hao walikuwa wakiishi kwenye jiji lililojaa ibada ya roho waovu. Walihitaji ulinzi zaidi. Kwa hiyo mtume Paulo alipowaandikia waamini wenzake, aliwaambia jambo la kufanya: “Kwa kila namna ya sala na dua mkiendeleza sala kila wakati katika roho. Na kwa lengo hilo fulizeni kuwa macho kwa udumifu wote na kwa dua kwa niaba ya watakatifu wote.”—Waefeso 6:18.

Kwa hakika, kusali kwa bidii na daima ili kupata ulinzi wa Yehova kulikuwa, na kungali, hatua muhimu sana ya kupokea ulinzi dhidi ya roho waovu. Na inafariji kujua kwamba Yehova atajibu sala zako za moyoni kwa kukulinda, hata utategemezwa na malaika zake. (Zaburi 34:7; 91:2, 3, 11, 14; 145:19) Kwa hiyo, ni muhimu sana kusali hivi daima kwa Mungu, “Utukomboe kutokana na yule mwovu.”—Mathayo 6:13; 1 Yohana 5:18, 19.

Antônio, aliyekuwa mwasiliani-roho huko Brazili, alipata kuthamini umuhimu wa sala. Baada ya kukubali funzo la Biblia na kujifunza jina la Mungu, Yehova, alianza kusali kwa bidii kwa Yehova Mungu na kuomba msaada wa kuachana kabisa na uwasiliani-roho. Atazamapo nyuma, yeye asema: “Kusali kwa Yehova kumethibitika kuwa kimbilio kwangu na kwa wengine wengi ambao awali walikuwa watumwa wa roho waovu.”—Mithali 18:10.

Unaweza Kufaulu

Ni muhimu kwamba baada ya kumjua Yehova, umtumaini kikamili, ujitiishe kwa mamlaka yake, na utii amri zake. Ukifanya hivyo, ukimwomba msaada kwa jina lake binafsi, atakulinda. Antônio alipata ulinzi huo. Leo yeye ni mzee Mkristo katika mojawapo ya makutaniko ya Mashahidi wa Yehova huko São Paulo naye ni mwenye shukrani kwa kupokea kweli iliyomweka huru.—Yohana 8:32.

Waweza pia kufaulu kuachana kabisa na uwasiliani-roho kama Antônio na maelfu mengine ya watu waliokuwa wawasiliani-roho, ambao sasa wanamtumikia Yehova Mungu. Kwa hiyo, haribu kabisa vyombo vinavyohusiana na uwasiliani-roho, imarisha imani yako kwa kujifunza Biblia, na sali upate ulinzi wa Yehova. Chukua hatua hizo—uhai wako unategemea hilo!

[Blabu katika ukurasa wa 5]

Kulingana na Biblia, walio hai hawawezi kuwasiliana na wafu

[Picha katika ukurasa wa 6]

1. Haribu kabisa vyombo vyote vinavyohusiana na uwasiliani-roho

[Picha katika ukurasa wa 7]

2. Endelea kujifunza Biblia

[Picha katika ukurasa wa 8]

3. Sali kwa bidii na mara nyingi