Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuwasaidia Walio na MCS

Kuwasaidia Walio na MCS

Kuwasaidia Walio na MCS

KUATHIRIWA na vitu vya kawaida, kama ni marashi au sabuni za maji, si tatizo la afya tu bali pia ni tatizo la kijamii. Kwa kawaida watu hupenda kushirikiana na wengine, hata hivyo, hali ya kuathiriwa na kemikali mbalimbali (MCS) huwalazimisha wengi wenye MCS kuishi maisha ya upweke ingawa wao ni watu wenye shauku na hupenda kujifurahisha pamoja na wengine. Shelly aliye na MCS asema hivi “nimekuwa na matatizo mengine ya afya, lakini tatizo hili ni baya zaidi. Jambo gumu zaidi ni upweke.”

Kwa kusikitisha, walio na MCS mara nyingi huonwa kuwa watu tofauti sana. Bila shaka sababu moja ni kwamba MCS ni hali tata sana ambayo watu hawajajua bado jinsi ya kuishughulikia. Hata hivyo, kutoelewa MCS vizuri si sababu ya kuwashuku walio na tatizo hilo. Jarida liitwalo American Family Physician lasema hivi: “Wagonjwa hao wanateswa kwelikweli na matatizo yao.”

Badala ya kushuku watu wenye MCS kwa kuwa hali yao inatatanisha na haieleweki vizuri, mtu mwenye hekima apaswa kuongozwa na kanuni iliyo katika Mithali 18:13: “Yeye ajibuye kabla hajasikia, ni upumbavu na aibu kwake.” Ni bora kama nini kuwaonyesha wote wanaougua upendo wa Kikristo bila kubagua! Hatutajuta kamwe kwamba tumeonyesha upendo wa aina hiyo, hata wanasayansi wa kitiba wagundue nini kuhusu hali hiyo wakati ujao.

Kuonyesha Upendo wa Kikristo

Upendo wa Kikristo ni kama almasi yenye pande nzuri zinazofaa kila hali. Wakati rafiki ana MCS, upendo wetu wa Kikristo wapaswa kutusaidia kujiweka katika hali yake. Pia upendo “hautafuti masilahi yao wenyewe”—au twaweza kusema, hautafuti haki yake yenyewe. Unatanguliza hali njema ya wengine. Hutusaidia ‘kustahimili, kuhimili mambo yote, kuamini mambo yote, na kuvumilia mambo yote.’ Upendo wa aina hiyo “haushindwi kamwe.”—1 Wakorintho 13:4-8.

Mary hana tatizo la MCS, walakini baadhi ya rafiki zake wana tatizo hilo. “Mimi napenda marashi, hata hivyo situmii marashi ninapowatembelea walio na MCS.” Kwa njia hiyo Mary anajitahidi kumwiga Yesu; ni kana kwamba anasema, “nataka kusaidia.” (Marko 1:41) Trevor alipatwa na MCS alipokuwa mtoto mchanga. Mamake asema hivi: “Wafanyakazi wenzangu wamejitahidi sana kuonyesha mwana wangu fadhili.” Joy ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova aishiye Australia, anasumbuliwa sana na MCS, naye asema kwamba anatiwa moyo wakati rafiki na watu wa ukoo wanapomtembelea na kuonyesha kuwa wanaelewa matatizo yake.

Kwa upande mwingine, wale wenye MCS wapaswa kuwa na uvumilivu wakati wengine wanapotumia marashi mahali walipo. Ernest aliyetajwa katika makala yaliyotangulia alimwambia mwandishi wa Amkeni!: “Ugonjwa wetu ni mzigo wetu. Wengine wana matatizo yao pia, kwa hiyo twashukuru wanapotusaidia.” Naam, kuomba msaada wala si kuudai, sikuzote ndiyo njia bora. Lorraine asema hivi: “Wakati mtu ambaye ametumia marashi anaponiuliza kwa nini naonekana mgonjwa, namwambia kwamba ‘mimi huathiriwa na marashi na leo yaonekana nazidiwa.’ Watu wenye ufahamu wanaelewa bila maelezo zaidi.” Bila shaka, ikiwa una tatizo la MCS waweza kwa fadhili kuomba rafiki zako msaada.

Pam aliyetajwa awali aonyesha jambo la kutia moyo aandikapo hivi: “Mateso yote ya leo ni ya muda tu.” Kwa nini Pam alisema ni “ya muda tu”? Kwa sababu tumaini lake linalotegemea Biblia ni kwamba hivi karibuni Ufalme wa Mungu utaondoa mateso yote duniani. Utaondoa hata kifo—hali ambayo hata mtu mwenye afya njema kabisa atakabili hatimaye.—Danieli 2:44; Ufunuo 21:3, 4.

Kwa sasa, wale walio na ugonjwa ambao hauna dawa wakati huu waweza kuwa na tumaini la kuishi chini ya utawala wa Ufalme wa Mungu, wakati ambapo, ‘hapana mtu atakayesema, Mimi mgonjwa.’ (Isaya 33:24) Tunapovumilia majaribu yoyote yatupatayo katika mfumo huu wa mambo, na tujitahidi kuwa kama Yesu tukaziapo macho zawadi iliyoko mbele yetu.—Waebrania 12:2; Yakobo 1:2-4.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 9]

Kupendana

Kanuni za Biblia zifuatazo huenda zikasaidia ikiwa rafiki au mtu wa ukoo au wewe mwenyewe waathiriwa na kemikali mbalimbali:

“Kwa hiyo, mambo yote mtakayo watu wawafanyie nyinyi, lazima mwafanyie wao pia hivyohivyo.”Mathayo 7:12.

“Lazima umpende jirani yako kama wewe mwenyewe.”Mathayo 22:39.

“Acheni tufikiriane ili kuchocheana kwenye upendo na kazi zilizo bora, si kuachilia mbali kukusanyika pamoja sisi wenyewe, kama vile wengine walivyo na desturi, bali kutiana moyo, na zaidi sana hivyo kwa kadiri mwonavyo siku ikikaribia.” (Waebrania 10:24, 25) Sisi sote twahitaji kitia-moyo cha kiroho, hasa tukiwa wagonjwa. Wakristo wengi wenye MCS wastahili sifa kwa kuwa wao hujitahidi kuhudhuria mikutano; baadhi ya wale wanaoumwa sana wakati mwingine husikiliza mikutano kupitia simu. Katika baadhi ya Majumba ya Ufalme sehemu imetengwa kwa ajili ya wale wenye MCS wanaoathiriwa na marashi. Hata hivyo jambo hilo huenda lisiwezekane katika Majumba yote ya Ufalme.

“Msisahau kule kutenda mema . . . , kwa maana kwa dhabihu za namna hiyo Mungu hupendezwa vema.” (Waebrania 13:16) Ona jinsi kutenda mema mara nyingi kwataka kujitolea. Je, wewe u tayari kujitoa ili kusaidia mtu mwenye MCS? Kwa upande mwingine, wale wenye MCS hawapaswi kutarajia mengi mno kutoka kwa wengine. Kwa mfano, wazee Wakristo hawawezi kutunga sheria kuhusu utumizi wa marashi, wala kufanya matangazo juu ya habari hiyo. Watu wanaopendezwa na wageni wanaotumia marashi huhudhuria mikutano ya kutaniko—nasi twawakaribisha. Hatutaki kamwe kuwaaibisha wala kuwafanya wasistarehe kwa sababu wanatumia marashi.

‘Tafuteni sana amani na kuifuatia.’ (1 Petro 3:11) Ni dhahiri kwamba masuala ya afya hayapasi kamwe kuharibu amani ya Wakristo. ‘Hekima ya kutoka juu ni . . . yenye kufanya amani, yenye kukubali sababu, . . . yenye kujaa rehema,’ lasema andiko la Yakobo 3:17. Watu wanaotaka amani, wakiwa na tatizo la MCS au la, si wenye kudai mno au wenye kukosa kiasi kuhusiana na suala la kutumia au kutotumia vitu vyenye kemikali. Hali kadhalika, watu wenye kukubali sababu ambao ni ‘wenye kujaa rehema’ hawatasisitiza kutumia marashi wakijua kwamba afya ya mwingine itaathiriwa. Kwa njia hiyo waonyesha kwamba wao pia wanatafuta “hali zenye amani” nao ‘wanafanya amani.’—Yakobo 3:18.

Kwa upande mwingine, mtazamo usionyumbuka, na usio kubali sababu wa mtu mwenye MCS au mtu mwingine, ni kama kabari inayotenganisha watu. Mtazamo kama huo haufaidi yeyote nao waweza kudhuru uhusiano kati ya mtu mwenye mtazamo huo na Mungu.—1 Yohana 4:20.

Bila shaka, Wakristo wana msaada mkubwa sana—roho ya Yehova. Wanaomba Yehova kwa ukawaida awape roho yake, huku wakisitawisha matunda yake mazuri, hasa upendo—“kifungo kikamilifu cha muungano.” (Wakolosai 3:14) Wakati uo huo, wanaruhusu kwa subira roho hiyo isitawishe sifa za Kikristo katika wengine.—Wagalatia 5:22, 23.

[Picha katika ukurasa wa 10]

Watu wenye “MCS” wahitaji rafiki sawa na wengine