Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mapambo ya Mwili—Uhitaji wa Kuwa na Kiasi

Mapambo ya Mwili—Uhitaji wa Kuwa na Kiasi

Maoni ya Biblia

Mapambo ya Mwili—Uhitaji wa Kuwa na Kiasi

“UBATILI huzuia kusababu,” ndivyo alivyoandika mwandishi wa riwaya Mfaransa. Hakika, kusababu hakuhusiki katika mambo mengi ambayo wanadamu wamejifanyia wenyewe kwa ubatili katika karne nyingi. Kwa kielelezo, katika kujitahidi kuwa na kiuno kidogo zaidi, wanawake wa karne ya 19 walivaa koseti (nguo ya ndani ya kubana kiunoni hadi mapajani) wakijiumiza mpaka wasiweze kupumua vizuri. Wengine walidai kuwa na viuno vyenye wembamba wa inchi 13. Wanawake wengine walibanwa sana na koseti zao hivi kwamba kwa kweli mbavu zao zilisukumwa kwenye maini yao, ikisababisha kifo.

Ijapokuwa ni vema kwamba mtindo huo umekwisha, ubatili ulioutokeza ungali waonekana waziwazi leo kama siku hizo. Wanaume na wanawake wangali wanafanya mambo magumu, hata yenye hatari, ili kurekebisha sura yao ya asili. Kwa mfano, vituo vya kuchanja alama mwilini na kutoboa mwili, ambavyo hapo zamani vilitembelewa sana na watu wasio na adili katika jamii, sasa vinaongezeka kwa kasi katika sehemu zenye maduka na viungani. Kwa kweli, katika mwaka wa hivi majuzi, kuchanja alama mwilini kulikuwa biashara ya sita yenye kuenea haraka zaidi katika Marekani.

Mapambo ya mwili ya kupita kiasi yanaongezeka pia, hasa miongoni mwa vijana. Kutoboa sehemu za mwili kupita kiasi—kutia ndani chuchu za matiti, pua, ndimi, na hata viungo vya uzazi—kumeendelea kupendwa na watu wengi. Tayari kuna watu wachache, ambao hawasisimuliwi vya kutosha na utoboaji huo wenye kupita kiasi. Wanajaribu njia zenye kupita kiasi kabisa kama vile kujichoma chapa, kujikata, * na kujitia nakshi, ambapo vifaa huingizwa chini ya ngozi ili kutokeza mashimo makubwa sana na mistari iliyoinuka.

Zoea la Tangu Kale

Kupamba au kubadili mwili si jambo jipya. Katika sehemu fulani za Afrika, kutia alama kidesturi na kujichanja alama mwilini kumetumiwa kwa karne nyingi ili kutambulisha vikundi hususa vya familia au makabila. Jambo la kushangaza ni kwamba katika nchi nyingi, mazoea hayo sasa hayapendwi na yanadidimia.

Kujichanja alama mwilini, kutoboa, na kukatakata mwili kulikuwako nyakati za Biblia. Mara nyingi mazoea hayo yalifanywa na mataifa ya kipagani kuhusiana na dini yao. Inaeleweka kwamba, Yehova alikataza watu wake, Wayahudi, kuiga wapagani hao. (Mambo ya Walawi 19:28) Wakiwa ‘watu [wa Mungu] mwenyewe,’ Wayahudi walilindwa kutokana na mazoea ya kidini yenye kudhalilisha.—Kumbukumbu la Torati 14:2, Zaire Swahili Bible.

Uhuru wa Kikristo

Wakristo hawako chini ya Sheria ya Kimusa, ijapokuwa inatoa kanuni fulani ambazo hutumika katika kutaniko la Kikristo. (Wakolosai 2:14) Basi wanaweza kujiendesha wenyewe kwa adabu inapohusu aina ya mapambo wanayochagua kuvaa. (Wagalatia 5:1; 1 Timotheo 2:9, 10) Hata hivyo, uhuru huo una mipaka.—1 Petro 2:16.

Kwenye 1 Wakorintho 6:12, Paulo aliandika hivi: “Mambo yote yaruhusika kisheria kwangu; lakini si mambo yote yenye faida.” Paulo alielewa kwamba uhuru wake akiwa Mkristo haukumruhusu kufanya lolote alilotaka bila kuwafikiria wengine. Upendo kwa wengine uliathiri mwenendo wake. (Wagalatia 5:13) Fulizeni “kuangalia, si masilahi ya kibinafsi ya mambo yenu wenyewe tu,” akasihi, “bali pia masilahi ya kibinafsi yale ya wengine.” (Wafilipi 2:4) Maoni yake yasiyo ya kibinafsi ni kielelezo bora kwa Mkristo yeyote anayefikiria aina fulani ya mapambo ya mwili.

Kanuni za Biblia za Kufikiriwa

Mojawapo ya amri kwa Wakristo ni kuhubiri na kufundisha habari njema. (Mathayo 28:19, 20; Wafilipi 2:15) Mkristo hangependa kuruhusu chochote, kutia ndani sura yake, ikengeushe watu wasisikilize ujumbe huo.—2 Wakorintho 4:2.

Ingawa huenda mapambo kama vile kutoboa au kuchanja alama mwilini yakapendwa na watu fulani, Mkristo anahitaji kujiuliza, ‘Jirani zangu watayaonaje mapambo kama hayo? Je, nitahusianishwa na vikundi fulani vya kiajabu katika jamii? Hata kama dhamiri yangu ingeniruhusu, kujitoboa au kujichanja alama mwilini kungeathirije wengine katika kutaniko? Je, wangeona jambo hilo kuwa linadhihirisha “roho ya ulimwengu”? Je, kwaweza kutokeza shaka kuhusu “utimamu [wangu] wa akili”?’—1 Wakorintho 2:12; 10:29-32; Tito 2:12.

Aina fulani za kurekebisha mwili hutokeza hatari kubwa za kitiba. Kuchanja kwa sindano zisizo safi yasemekana kumeeneza mchochota wa ini na virusi vya UKIMWI. Matatizo ya ngozi nyakati nyingine hutokana na rangi mbalimbali zilizotumiwa. Sehemu zilizotobolewa zaweza kuchukua miezi kadhaa kabla hazijapona nazo zaweza kuuma kwa muda mrefu. Pia zaweza kusababisha sumu katika damu, kuvuja damu, na kuganda kwa damu, kuharibiwa kwa neva, na maambukizo mabaya. Kwa kuongezea, matokeo ya mapambo fulani yaweza kudumu daima. Kwa mfano, ikitegemea saizi na rangi, alama iliyochanjwa mwilini yaweza kuondolewa kwa tiba ya leza ambayo ni ghali na yenye maumivu. Kutoboa kwaweza kuacha alama za vidonda za kudumu.

Kukubali au kutokubali hatari hizo ni uamuzi wa mtu binafsi. Lakini mtu anayejitahidi kumpendeza Mungu anatambua kwamba kuwa Mkristo hutia ndani kujitoa binafsi kwa Mungu. Miili yetu ni dhabihu zilizo hai zitolewazo kwa Mungu ili azitumie. (Waroma 12:1) Kwa sababu hiyo, Wakristo wakomavu hawaoni miili yao kuwa mali yao tu ya kuharibu au kuumbua kama watakavyo. Hasa wale wanaostahili kuongoza kutanikoni wanajulikana kwa mazoea yao ya kiasi, utimamu wa akili, na kukubali kwao sababu.—1 Timotheo 3:2, 3.

Kusitawisha na kudhihirisha nguvu za kufikiri zilizozoezwa na Biblia kutasaidia Wakristo waepuke mazoea yenye kupita kiasi, ya kupenda kuteseka ya ulimwengu huu, ‘uliotengwa mbali [kabisa] na uzima wa Mungu.’ (Waefeso 4:18, ZSB) Hivyo basi, wanaweza kuacha hali yao ya kiasi ijulikane kwa watu wote.—Wafilipi 4:5.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Kuna tofauti kati ya kukata kwa ajili ya kitiba au hata kwa makusudi ya sanaa na kujikatakata kwa kulazimishwa au kujikatakata ambako vijana wengi hufanya, hasa wasichana matineja. Kujichanja kunakotajwa hapa huwa ni ishara ya mkazo mbaya sana wa kihisia-moyo au kutendwa vibaya, ambako huenda kukahitaji kushughulikiwa na wataalamu.