Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wewe Huona Zaidi ya Vinavyoonekana?

Je, Wewe Huona Zaidi ya Vinavyoonekana?

Je, Wewe Huona Zaidi ya Vinavyoonekana?

KWA kawaida madereva wa magari hawawezi kuona mbele penye kona bubu. Lakini kwa kutumia kioo kilichowekwa penye kona hiyo, madereva waweza kuona magari yanayokuja na hivyo kuepuka aksidenti. Vivyo hivyo, wanadamu hawawezi kumwona Muumba asiyeonekana. Je, kuna njia ya kujua kwamba Muumba yupo?

Mwandikaji mmoja wa karne ya kwanza alionyesha namna tunavyoweza kuona kisichoonekana. Aliandika: “Kwa maana sifa [za Mungu] zisizoonekana zaonwa waziwazi tangu uumbaji wa ulimwengu na kuendelea, kwa sababu zafahamiwa kwa vitu vilivyofanywa, hata nguvu zake za milele na Uungu, hivi kwamba hawana sababu ya kujitetea.”—Waroma 1:20.

Hebu wazia hilo. Je, wewe huona akili ikidhihirishwa na vitu vinavyotuzunguka ambavyo haviwezi hata kidogo kutengenezwa na wanadamu? Je, vitu hivyo hukusaidia kuona kwa “macho yako ya ufahamu” kwamba kuna mtu mkuu kupita mwanadamu? Acheni tufikirie mifano kadhaa.—Waefeso 1:18, King James Version.

Kujifunza Kutokana na Uumbaji

Umewahi kustaajabia fahari ya anga jangavu la usiku, lisilokuwa na mwezi na lenye kutapakaa nyota, na kuona uthibitisho wa kuwapo kwa Mfanyi Mtukufu? “Mbingu zauhubiri utukufu wa Mungu, na anga laitangaza kazi ya mikono yake,” akasema kwa mshangao mtazamaji mmoja wa kale. “Nikiziangalia mbingu zako, kazi ya vidole vyako, mwezi na nyota ulizoziratibisha,” mtu huyo akawaza, “mtu ni kitu gani hata umkumbuke, na binadamu hata umwangalie?”—Zaburi 8:3, 4; 19:1.

Ni jambo la kawaida kwetu kustaajabia uumbaji ulio bora kiasi cha kutoweza kuigwa na wanadamu. Mstari mmoja wa shairi linalopendwa husema: “Ni Mungu tu awezaye kuumba mti.” Lakini uumbaji wa mtoto mchanga, unaotukia pasipo mwelekezo wa wazazi hustaajabisha hata zaidi. Shahawa ya baba iunganapo na yai la mama, mara moja mipango huratibiwa katika DNA ya chembe hiyo mpya ili kutokeza mtoto mchanga. Yasemekana kwamba maagizo yaliyo katika DNA “endapo yangeandikwa, yangejaza vitabu elfu moja vyenye kurasa 600 kila kimoja.”

Na hicho ni kionjo tu. Chembe ya kwanza hujigawanya na kuwa mbili, kisha nne, kisha nane, na kuendelea. Baada ya siku 270 hivi, mtoto mchanga mwenye maelfu ya mamilioni ya chembe zaidi ya aina 200 huzaliwa. Fikiria pia kwamba chembe ya kwanza ilibeba habari zinazohitajiwa ili kufanyiza aina hizo zote za chembe kwa wakati barabara! Je, wewe huchochewi kumsifu Muumba wetu? Angalia sifa aliyotoa mtunga-zaburi aliyeandika: “Wewe ndiwe uliyeniumba mtima wangu, uliniunga tumboni mwa mama yangu. Nitakushukuru kwa kuwa nimeumbwa kwa jinsi ya ajabu ya kutisha.”—Zaburi 139:13-16.

Wale ambao wamejifunza “miujiza” hiyo hutiwa kicho. Dakt. James H. Hutton, aliyepata kuwa msimamizi wa vyama vya Tiba vya Majimbo ya Chicago na Illinois, alisema kwamba alishangazwa na “uwezo wa ajabu [wa chembe] wa kupitisha habari muhimu za urithi kwa chembe mpya kwa wakati barabara. Kwa kweli ni jambo la kupendeza kwamba wanasayansi wetu wa utafiti wameweza kujifunza mambo hayo. Lakini lazima mambo hayo yawe yalipangwa na Mtu fulani wa Kimungu Mwenye Akili.”

Dakt. Hutton akaendelea: “Taaluma yangu ya utafiti wa tezi-ndani, elimu ya utendaji na magonjwa ya tezi-ndani huthibitisha hata zaidi kwamba Mtu wa Kimungu Mwenye Nguvu ndiye mbuni wa utata na utendaji wa ajabu wa viungo hivyo muhimu.” Alikata kauli hivi: “Kufikiria kwa uzito maajabu hayo hunichochea sana niamini kwamba ulimwengu wote mzima ulibuniwa na mtu fulani mwenye uweza wote na mwenye kujua yote, ambaye ni mwanzilishi na mwelekezaji wake.”

Baada ya kusema maneno hayo, Dakt. Hutton aliuliza: “Je, Ndiye Mungu yuleyule anayekumbuka kila shore anayeanguka?” Akajibu: “Nina shaka. Wala siamini kwamba Yeye hupendezwa na shughuli zangu za kawaida za kila siku.”

Mbona wengi hukubali kwamba “miujiza” ya uumbaji ilibuniwa kwa akili lakini wanatilia shaka kuwapo kwa Mungu ambaye hupendezwa na wanadamu?

Je, Kweli Mungu Anatujali?

Wengi husababu kwamba kama Mungu angekuwako, hangeruhusu wanadamu wateseke. Swali ambalo huulizwa kwa kawaida na baadhi ya watu ni, “Mungu alikuwa wapi tulipomhitaji?” Mtu mmoja aliyeokoka mauaji ya mamilioni yaliyofanywa na Wanazi katika Vita ya Ulimwengu ya Pili alihuzunishwa sana na kuteseka alikoona hata akasema: “Kama ungeramba moyo wangu, ungekutia sumu.”

Kwa hiyo watu wengi hutatanika. Kama mtazamaji wa angani wa kale aliyetajwa awali alivyosema, uthibitisho wa kuwapo kwa Muumba ni wazi tuchunguzapo utaratibu na ubuni ajabu wa vitu. Lakini, ikiwa Yeye ni Mungu anayetujali, Awezaje kuruhusu mateso hayo mabaya? Hatuna budi kupata jibu la swali hilo muhimu, endapo twataka kuelewa na kumwabudu Mungu ifaavyo. Twaweza kupata jibu wapi?

Twakualika upokee nakala ya broshua Je! Kweli Mungu Anatujali? Ukurasa wa 32 wa gazeti hili la Amkeni!, utakusaidia kufanya ombi. Twahisi kwamba utapata majibu yenye kuridhisha kwa kusoma kwa uangalifu sehemu yenye kichwa “Sababu Kwa Nini Mungu Ameruhusu Kuteseka” na “Matokeo ya Uasi Yamekuwa Nini?”

[Picha katika ukurasa wa 11]

Je, vitu hivi hukuthibitishia kuwapo kwa Muumba?