Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jitihada Yangu ya Kufanya Uchaguzi Wenye Hekima

Jitihada Yangu ya Kufanya Uchaguzi Wenye Hekima

Jitihada Yangu ya Kufanya Uchaguzi Wenye Hekima

KAMA ILIVYOSIMULIWA NA GUSTAVO SISSON

Ijapokuwa nilijishughulisha sana na uogeleaji nilipokuwa na umri wa miaka 12, niliamua kuwa daktari. Lakini wakati huohuo, nilianza kujifunza Biblia na kama tokeo, nikataka kuwa mhudumu. Ni nini kilichotukia kwa mapendezi na miradi yangu tofauti-tofauti? Je, ilipatana?

MNAMO 1961, Olive Springate, ambaye ni mishonari wa Mashahidi wa Yehova katika Brazili, alianza kujifunza Biblia pamoja nami na Mama. Kwa sababu ya upinzani kutoka kwa Baba, aliyekuwa daktari mashuhuri katika Pôrto Alegre, tuliacha kujifunza. Hata hivyo, Olive aliendelea kuwasiliana nasi, na hatimaye nilianza kuona ukweli fulani katika yale niliyojifunza. Lakini kufikia wakati huo kuogelea kulikuwa kumenikengeusha kutoka kwa mambo yangu ya kiroho.

Nilipokuwa na umri wa miaka 19, nilikutana na msichana mmoja mchanga mwenye sura ya kuvutia anayeitwa Vera Lúcia kwenye klabu nilikokuwa nikiogelea, na tukaanza kujuana. Mama alizungumza naye kuhusu itikadi zetu, na akapendezwa. Kwa hiyo niliwasiliana na Olive, naye akaanza kujifunza Biblia pamoja nasi, licha ya upinzani kutoka kwa babake Vera Lúcia.

Vera Lúcia aliendelea kujifunza, na akaongeza ujuzi wake wa Biblia. Hata alianza kujifunza Biblia pamoja na wafanyakazi kwenye klabu changu cha kuogelea. Wakati huohuo, nilikuwa nikifanya mazoezi kwa bidii kwa ajili ya mashindano ya kitaifa ya kuogelea yaliyokuwa yanakaribia.

Baada ya kujifunza na kuhudhuria mikutano ya Kikristo kwa zaidi ya mwaka mmoja, babake Vera Lúcia alianza kushuku kwamba kuna jambo fulani linaloendelea. Siku moja tuliporudi kutoka kwenye mkutano, alikuwa akingoja na akataka kujua mahali tulipokuwa tumeenda. Nilimwambia kwamba tulihudhuria mkutano wa Kikristo na kwamba ijapokuwa yeye hakuona umuhimu wa dini, kwa upande wetu dini ilikuwa suala la kufa na kupona. Alivuta pumzi na kusema: “Ikiwa ni suala la kufa na kupona, basi nitalazimika kukubali mambo hayo.” Kuanzia siku hiyo na kuendelea, alibadili mtazamo wake, na ijapokuwa hakuwahi kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova, alikuwa rafiki wa karibu na mwandamani wakati wa uhitaji.

Kufanya Uchaguzi

Nilikuwa nimeamua kuacha mashindano ya kuogelea baada ya mashindano ya kitaifa, lakini baada ya kushinda mara mbili na kuvunja rekodi ya kuogelea ya meta 400 na meta 1,500 katika Brazili, nilialikwa kwenye Mashindano ya Pan Amerika huko Cali, Kolombia, mwaka wa 1970. Ijapokuwa Vera Lúcia hakutaka niende, nilianza kufanya mazoezi kwa ajili ya mashindano hayo.

Nilipoogelea vizuri huko Cali, makocha waliniuliza ikiwa ningependa kufanya mazoezi kwa ajili ya michezo ya Olimpiki. Nilifikiri juu ya masomo yangu ya udaktari ambayo sikuwa nimeyamaliza na kweli nzuri nilizokuwa nimejifunza kuhusu makusudi ya Yehova kisha nikatupilia mbali wazo la kufuatia mradi wa kuogelea. Kuanzia wakati huo na kuendelea, nilifanya maendeleo ya kiroho haraka. Katika 1972, mwaka ambao michezo ya Olimpiki ilifanywa huko Munich, Ujerumani, mimi na Vera Lúcia tulionyesha wakfu wetu kwa Yehova kwa kubatizwa katika maji. Hilo lilimtia moyo Mama aanze kujifunza Biblia tena, na baada ya muda yeye pia akabatizwa.

Baada ya Mama kubatizwa, Baba alizidisha upinzani. Hatimaye familia yetu ilivunjika, na kwa kuwa bado nilikuwa kwenye chuo kikuu, tulihitaji kujikimu kwa malipo madogo ya uzeeni ya Mama na pesa tulizopata baada ya kuuza nyumba yetu. Mimi na Vera tulilazimika kuahirisha arusi yetu. Kwa kweli masomo mazuri niliyopokea kutoka kwa Baba yalinisaidia kufanya maamuzi niliyofikia. Mara nyingi angesema: “Usiogope kuwa tofauti” na, “Maoni ya umati hayawi sawa wakati wote.” Moja ya misemo aliyopenda zaidi ulikuwa, “Wema wa mtu hutegemea mambo anayowafanyia wengine.”

Nikiwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova, nimeweza kutumia mashauri mazuri sana ya Baba. Nilikuwa kando ya kitanda chake alipokufa mwaka wa 1986. Tulikuwa tumekuwa marafiki tena na tuliheshimiana. Nasadiki kwamba alinionea fahari, kwa kuwa nilikuwa daktari wa kitiba kama yeye.

Wakati huo, nilihitimu kutoka shule ya kitiba mwaka wa 1974. Niliamua kuwa daktari wa kawaida, lakini baada ya kufikiria zaidi jambo hilo, niliamua kwamba ningeweza kusaidia ndugu zangu Wakristo zaidi kwa kuwa daktari-mpasuaji. (Matendo 15:28, 29) Kwa hiyo nilikubali kazi hiyo ngumu na kutumia miaka mitatu iliyofuata nikizoezwa kuwa daktari-mpasuaji.

Pigano Gumu la Kisheria

Nilihusika katika kisa chenye kusikitisha sana cha msichana mmoja Shahidi mwenye umri wa miaka 15 aliyekuwa akivuja damu katika sehemu za ndani za mwili. Alikuwa na msukumo mdogo wa damu tena dhaifu lakini timamu na thabiti kabisa katika uamuzi wake wa kukataa damu. Baada ya kuongeza kiwango chake cha damu, nilimfanyia uchunguzi katika sehemu za ndani za mwili na kuosha sehemu iliyoathiriwa kwa maji baridi yenye chumvi ili kuzuia kuvuja damu. Hapo mwanzoni alipata nafuu, lakini baada ya saa 36, alipokuwa katika chumba cha kutunzia wagonjwa mahututi, alianza kuvuja damu kwa ghafula. Licha ya jitihada zenye bidii, daktari aliyekuwa katika zamu, alishindwa kuzuia kuvuja damu na kudumisha kiwango chake cha damu, hivyo msichana huyo akafa.

Baada ya kifo hicho, halmashauri ya elimu-maadili iliniachisha ukufunzi wa udaktari, kisha kesi yangu ikapelekwa kwa baraza la kitiba la mkoa. Nilishtakiwa kwa kukiuka vifungu vitatu vya sheria za tiba, na hivyo kuhatarisha leseni yangu ya kitiba na kazi yangu pia.

Halmashauri ilinipa muda wa siku 30 ambapo ningehitaji kujitetea kupitia barua. Mawakili wangu walitayarisha hoja za kisheria na za kikatiba, nami nikatayarisha kujitetea kwa kutegemea mambo ya kitiba na ya kisayansi kupitia msaada wa Halmashauri ya Uhusiano na Hospitali (HLC) ya kwetu, kikundi cha Mashahidi wa Yehova ambacho hujaribu kudumisha ushirikiano kati ya hospitali na mgonjwa. Wakati wa kusikizwa kwa kesi hiyo halmashauri ya kufundisha iliuliza maswali hasa kuhusu wadhifa wangu nikiwa daktari na mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Hata hivyo, nilijitetea hasa kwa kutegemea hoja za kitiba na za kisayansi na ripoti za madaktari-wapasuaji mashuhuri.

Uthibitisho uliotolewa ulithibitisha kwamba mgonjwa huyo alikuwa amekataa kukubali kutiwa damu mishipani na kwamba sikufanya chochote kumchochea afikie uamuzi huo. Kesi hiyo ilipokuwa ikisikilizwa ilithibitishwa pia kwamba kati ya madaktari wanne walioombwa mashauri, ni mimi pekee niliyekuwa nimeanzisha tiba ya aina fulani inayopatana na mapenzi ya mgonjwa na hali yake ya kitiba.

Kisha kesi yangu ikapelekwa kwa halmashauri ambayo ingepiga kura kwenye mkutano ambao ungehudhuriwa na wote. Nilizungumza na kujitetea kwa dakika kumi ambapo, kama ilivyokuwa wakati wa kujitetea kwa barua, nilikazia fikira hasa mambo ya kitiba. Baada ya kunisikiliza, washiriki wawili wa halmashauri walisema kwamba ijapokuwa sikuwa nimemtia damu mishipani, tiba niliyompa ilikuwa na msingi thabiti wa kisayansi. Daktari mwingine alikazia kwamba tiba bila damu ina matokeo na kwamba watu wachache zaidi hufa. Wakili wa mwisho alisema kwamba suala halikuwa kama kutiwa damu mishipani ni dawa nzuri au la. Suala lilikuwa kama daktari angeweza kumlazimisha mgonjwa tiba fulani ambayo mgonjwa hakuitaka, na wakili huyo alifikiri kwamba daktari hana haki ya kufanya hivyo. Hivyo, kwa kufuata kura ya wengi, mawakili 12 dhidi ya 2 walipiga kura iliyotupilia mbali mashtaka yote, na hivyo kuniondolea hatia.

Kutetea Haki za Mgonjwa

Wasimamizi fulani wa kitiba wamepata amri kutoka mahakamani za kuwalazimisha wagonjwa Mashahidi wakubali kutiwa damu mishipani, na pindi kwa pindi nimetoa uthibitisho wakati wa kusikizwa kwa kesi hizo mahakamani na hilo limesaidia kubatilisha amri hizo. Kesi moja ilihusisha Shahidi mmoja ambaye mishipa yake ya damu ilikuwa imevimba ndani ya umio, tatizo ambalo husababisha kuvuja damu ndani ya tumbo. Wakati alipolazwa hospitalini, tayari alikuwa ameishiwa kabisa na damu—himoglobini yake ilikuwa gramu 4.7 kwa kila desilita. * Mwanzoni, hakusongwa akubali damu, alipatiwa tu matibabu ya kumtegemeza.

Kisha, baada ya kumaliza juma moja hospitalini, mgonjwa alishangaa kutembelewa na ofisa wa mahakama aliyekuwa na amri ya kumtia damu mishipani. Kufikia wakati huo himoglobini yake ilikuwa imeongezeka hadi kufikia gramu 6.4 kwa kila desilita, na alikuwa thabiti kitiba. Yaonekana kwamba hakimu alifanya uamuzi kwa kutegemea kiwango cha kwanza cha himoglobini wala si cha pili, ambacho kilikuwa juu zaidi.

HLC ilikubali kusaidia. Mgonjwa aliniomba nimpime. Nilimpima na baada ya hapo nikafaulu kumpeleka kwenye hospitali ambayo angeweza kutibiwa bila damu. Wakati huohuo, mawakili wake walipinga amri ya mahakama ya kumtia mgonjwa damu mishipani.

Niliamriwa nitoe ushuhuda wa kesi hiyo mbele ya hakimu, aliyeniuliza hali ya mgonjwa. Wakati wa kusikilizwa kwa kesi hiyo, aliniamuru niendelee kumtibu mgonjwa huku ikijadiliwa ikiwa amri ya mahakama ilifaa. Wakati wa kusikilizwa upya kwa kesi hiyo, mgonjwa alikuwa amepata nafuu na alikuwa ametolewa hospitalini. Nilipoombwa nitoe ushuhuda tena, wakili wa hospitali aliniuliza nithibitishe kwamba matibabu niliyopendekeza yalikuwa na msingi wa kisayansi. Aliaibika nilipotoa makala fulani kutoka kwenye jarida moja la kitiba lililochapishwa na hospitali ileile aliyowakilisha, ambayo ilipendekeza matibabu hayo!

Uamuzi ulipotangazwa, tulifurahi kusikia kwamba msimamo wetu wa kutegemea matibabu mengine badala ya kutia damu mishipani ulikuwa umetetewa. Hospitali iliamriwa ilipe gharama zote, kutia ndani gharama za kesi. Ingawa hospitali ilikata rufani, ilishindwa tena.

Kutunza Familia Yetu

Tangu nilipokuwa Shahidi, Vera Lúcia amekuwa akinitegemeza akiwa mwandamani mwaminifu na mwenye kujitoa na mke mwema na mama aliye kielelezo bora kwa watoto wetu. Ameweza kukabilianaje na ugumu huo wote, kutunza nyumba yetu na kusaidia kutunza watoto, ambao sasa ni vijana wachangamfu? Ameweza kufanya hivyo kwa sababu anampenda sana Yehova na huduma ya Kikristo.

Tukiwa wazazi, tumefundisha watoto wetu mafundisho na kanuni za Biblia tangu walipokuwa wadogo. Licha ya kuwa na shughuli nyingi maishani, tunajitahidi kutumikia katika huduma ya wakati wote miezi michache kila mwaka. Tunajitahidi vilivyo kushikamana na ratiba yetu, inayotia ndani kusoma Biblia kwa ukawaida, kuzungumzia andiko la Biblia kila siku, na kushiriki itikadi zetu na wengine katika huduma ya Kikristo. Hivi karibuni familia yetu imeongoza mafunzo ya Biblia 12 mara nyingi na watu ambao si Mashahidi.

Mimi na Vera Lúcia pia hujaribu kuhusisha wana wetu katika utendaji wetu huku, wakati uleule, tukistahi mapendezi yao ya kibinafsi. Tunaamini kwamba kuna mambo matatu yanayohitajika ili wazazi watunze familia zao ifaavyo. Kwanza, mafundisho yanayofaa, yanayotegemea Neno la Mungu, Biblia. Pili, kielelezo kinachofaa, kinachowapa watoto uthibitisho dhahiri kwamba wazazi wao wana hofu inayofaa ya Mungu. Na tatu, mashirika yanayofaa pamoja na Wakristo wenye umri mbalimbali na hali mbalimbali, wanaoweza kuwafunza washiriki wa familia vipawa na uwezo mbalimbali. Tukiwa wenzi, tumeweka mradi wa kuandalia familia yetu vitu hivyo.

Tunapokumbuka miaka 30 hivi ya kumtumikia Yehova, mimi na mke wangu twaweza kusema kwamba bila shaka, ametupa mambo yaliyo bora maishani na kutuandalia raha na baraka tele. Ijapokuwa sikufaulu kwenda kwenye michezo ya Olimpiki, ningali nafurahia kuogelea kilometa kadhaa kila juma. Ni kweli kwamba kuwa daktari na mmoja wa Mashahidi wa Yehova kumenifanya niwe na shughuli nyingi zaidi maishani, lakini nimethawabishwa kusaidia ndugu na dada zangu Wakristo kuvumilia katika utumishi wao kwa Mungu wanapokabili majaribu.

Mara nyingi ninaulizwa ikiwa nina wasiwasi kwamba nitapoteza kazi yangu wakati Mungu atakapoleta mfumo wake mpya na ambapo hakutakuwa na magonjwa tena. Mimi hujibu kwamba nitakuwa wa kwanza kuruka kwa furaha wakati ‘kilema atakaporuka-ruka kama kulungu, na ulimi wake aliye bubu utakapoimba,’ na “hapana mwenyeji atakayesema, Mimi mgonjwa.”—Isaya 33:24; 35:6.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 21 Mwanamume mwenye afya ana himoglobini ya takriban gramu 15 kwa kila desilita.

[Picha katika ukurasa wa 15]

Nikimfanyia mgonjwa upasuaji

[Picha katika ukurasa wa 15]

Nikiwa na Vera Lúcia, na funzo letu la familia