Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Naweza Kupambanaje na Kusumbuliwa Kingono?

Naweza Kupambanaje na Kusumbuliwa Kingono?

Vijana Huuliza . . . .

Naweza Kupambanaje na Kusumbuliwa Kingono?

“Wavulana hukupigia miluzi ya ashiki na kukuzomea.”—Carla, Ireland.

“Wasichana hukupigia-pigia simu. Wao hujaribu kukushawishi uwapende.”—Jason, Marekani.

“Alizidi kunigusagusa na kujaribu kunishika mkono.”—Yukiko, Japani.

“Wasichana hunishawishi kwa maneno matamu.” —Alexander, Ireland.

“Mvulana mmoja alinirushia maneno akiwa katika basi la shule. Kwa kweli hakutaka kufanya miadi ya kijinsia nami. Alikuwa akinisumbua-sumbua tu.”—Rosilyn, Marekani.

KUMTUPIA mtu jicho kwa mapenzi, “pongezi” yenye kuamsha ashiki, mzaha mchafu, kumgusa mtu ili kuamsha hamu ya ngono—kwa kawaida mambo hayo yanapofanywa bila idhini ya mtu na kwa kurudiwarudiwa, ni kumsumbua mtu kingono. Ingawa ni nadra mno kupata takwimu za ulimwenguni pote, uchunguzi huonyesha kwamba vijana wengi wanaoenda shuleni huko Marekani wamepatwa na jambo hilo.

Kusumbuliwa kingono ni nini? Kitabu Coping With Sexual Harassment and Gender Bias, kilichoandikwa na Dakt. Victoria Shaw, husema ni “kumchokoza mtu kwa njia ya kingono . . . Yaweza kuwa kwa vitendo (kama vile kumgusa mtu kwa njia ya kingono), kwa usemi (kama vile kutoa maelezo yasiyotakiwa juu ya umbo la mtu), au kwa ishara.” Nyakati nyingine kusumbua huko kwahusisha kumwomba mtu afanye mambo machafu.

Labda unasumbuliwa sana shuleni na marika wako. Lakini, nyakati nyingine tabia hiyo yenye kuudhi hufanywa na watu wazima, kama walimu. Makala moja katika gazeti Redbook yakisia kwamba walimu wanaopatikana na hatia ya makosa ya kingono “huenda ni wachache mno walinganishwapo na idadi kubwa ya walimu walio na hatia.”

Wanawake—na nyakati nyingine wanaume—walitendwa vibaya hata katika nyakati za Biblia. (Mwanzo 39:7; Ruthu 2:8, 9, 15) Biblia ilitoa utabiri huu wenye kutia hofu: ‘Siku za mwisho kutakuwako nyakati za hatari. Watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda fedha, wenye kujisifu, wenye kiburi, wenye kutukana . . . ; wasiotaka kufanya suluhu, wasingiziaji, wasiojizuia, wakali.’ (2 Timotheo 3:1-3, Union Version) Kwa hiyo inawezekana, hata yaelekea kwamba utasumbuliwa kingono.

Maoni ya Mungu

Kwa wazi, si vijana wote wanaosononeshwa na uchokozi wa kingono. Huenda wengine wakaufurahia—au wakaliona kuwa zoea la kurairai. Uchunguzi mmoja wa Marekani wenye kushtua mno ulionyesha kwamba asilimia 75 ya watu wanaosumbuliwa kingono, walikiri kuwa wao pia waliwasumbua wengine. Watu wazima fulani waweza kuzidisha tatizo hilo kwa kupunguza uzito wa uchokozi wa kingono unaochukiza, wakiutupilia mbali kana kwamba si kitu. Lakini Mungu anaionaje tabia hiyo?

Neno la Mungu, Biblia, hushutumu waziwazi kusumbua kingono kwa aina yoyote. Twaambiwa ‘tusiingilie haki’ za wengine kwa kuvuka mipaka ya kingono. (1 Wathesalonike 4:3-8) Hata, wanaume vijana wanaamriwa kihususa wawatendee “wanawake vijana zaidi kama dada kwa usafi wote wa kiadili.” (1 Timotheo 5:1, 2) Zaidi ya hayo, Biblia hushutumu “mzaha wenye aibu.” (Waefeso 5:3, 4) Kwa hiyo, una haki ya kukasirika, kuudhika, kutatanika, na hata kuhisi umedhalilishwa unaposumbuliwa!

Niseme Nini?

Hivyo basi, wapaswa kutendaje mtu anapokusumbua kingono? Nyakati nyingine jibu lisilo thabiti au wazi humchochea tu anayekusumbua. Biblia hutuambia kwamba Yosefu aliposhawishiwa afanye ngono na mke wa mwajiri wake, hakumpuuza tu. Badala yake, alikataa katakata ushawishi wake usio wa adili. (Mwanzo 39:8, 9, 12) Leo, kuwa na msimamo thabiti na kusema waziwazi ingali njia bora zaidi ya kuzuia kusumbuliwa kingono.

Huenda isiwe kwamba yule anayekusumbua ananuia kukuudhi. Ule unaoonekana kuwa usumbufu waweza kuwa tu jaribio la kuvutia uangalifu wako pasipo ustadi. Kwa hiyo usihisi kwamba ni lazima utende vibaya ili kuzuia ushawishi usiopenda. Kusema tu, ‘Sipendi mazungumzo hayo’ au, ‘Usiniguse tafadhali’ kwaweza kudhihirisha msimamo wako. Hakikisha unatenda kupatana na usemayo. Acha la yako iwe la! Kijana Andrea asema hivi: “Wasipoelewa maombi yako ya upole, lazima uwaonye waziwazi. Mara nyingi utahitaji kusema waziwazi.” Kusema kwa mkataa ‘Nikome!’ kwaweza kufaa.

Hali ikizidi kuwa mbaya, usijaribu kupambana peke yako. Jaribu kuzungumza jambo hilo na wazazi wako au watu wengine wakomavu. Wao waweza kukupa madokezo yenye kutumika ya kutatua tatizo hilo. Mwisho kabisa, waweza hata kuona ni muhimu kuwaeleza wasimamizi wa shule. Huenda hatua hiyo ikakutahayarisha, lakini inaweza kukulinda na uonevu zaidi.

Kujilinda Dhidi ya Kusumbuliwa Kingono

Bila shaka, inafaa kwanza ujilinde dhidi ya kusumbuliwa. Ni nini kinachoweza kukusaidia? Andrea ashauri: “Usionyeshe kamwe kwamba unapendezwa na mtu kwa njia fulani. Wengine watasikia jambo hilo, na msongo utaendelea.” Mavazi yako yaweza kuchangia sana. Kijana aitwaye Mara asema: “Sipendi kuvaa kama bibi kizee, lakini mimi huepuka mavazi yanayofanya watu wavutiwe na mwili wangu.” Kukataa kusumbuliwa kingono na wakati huohuo kuvalia mavazi yanayoamsha ashiki hutatanisha. Biblia hupendekeza kuvaa kwa “kiasi na utimamu wa akili.”—1 Timotheo 2:9.

Marafiki wako pia huathiri namna unavyotendewa. (Mithali 13:20) Rosilyn asema: “Wasichana kadhaa katika kikundi fulani wanapopenda kutongozwa na wavulana, wavulana hao hudhani kwamba wasichana wote katika kikundi hicho wako hivyo.” Carla alisema vivyo hivyo: “Ukishirikiana na watu wanaofurahia mazungumzo hayo au wanaofurahia kutongozwa na wavulana, basi utasumbuliwa pia.”

Biblia husimulia kuhusu msichana mmoja anayeitwa Dina ambaye alishirikiana na mabinti wa Kanaani—ambako wanawake walikuwa na sifa ya kuishi maisha mapotovu. Tokeo ni kwamba alibakwa. (Mwanzo 34:1, 2) Biblia husema hivi kwa sababu nzuri: “Fulizeni kuangalia sana kwamba jinsi mnavyotembea si kama wasio na hekima bali kama watu wenye hekima.” (Waefeso 5:15) Naam, “kufuliza” kuangalia namna unavyovalia, unavyonena, na mashirika yako kwaweza kukulinda sana dhidi ya kusumbuliwa.

Hata hivyo, mojawapo ya njia zenye matokeo zaidi kwa vijana Wakristo kujilinda dhidi ya kusumbuliwa ni kuwaeleza wengine msimamo wako wa kidini. Kijana Timon, mmoja wa Mashahidi wa Yehova, akumbuka: “Vijana wenzangu walijua kwamba mimi ni Shahidi, kwa hiyo walikoma kunisumbua.” Andrea asema: “Kuwaeleza wewe ni Shahidi husaidia sana. Watang’amua kwamba wewe ni tofauti nao na kwamba una viwango vya juu vya adili.”—Mathayo 5:15, 16.

Ukisumbuliwa

Licha ya jitihada zako, huwezi kuepuka kabisa watu fidhuli na watukanaji. Lakini endapo unasumbuliwa, hakuna haja ya kuteswa na hisia za hatia—maadamu unadumisha mwenendo wa Kikristo. (1 Petro 3:16, 17) Ikiwa hali hiyo inakusononesha kihisia-moyo, tafuta msaada kwa kuzungumza na wazazi wako au na watu wengine wakomavu katika kutaniko la Kikristo. Rosilyn akiri kwamba ni vigumu kuwa na furaha unaposumbuliwa. “Kuwa tu na rafiki,” yeye asema, “mtu fulani uwezaye kuzungumza naye, husaidia sana.” Pia kumbuka kwamba “BWANA yu karibu na wote wamwitao.”—Zaburi 145:18, 19.

Kupambana na kutendwa vibaya si rahisi, lakini kunafaa. Kwa mfano, fikiria simulizi la Biblia la mwanamke mmoja kijana kutoka Shunemu. Ingawa hakusumbuliwa kingono kama inavyoeleweka leo, alishawishiwa na Solomoni, yule mfalme tajiri na mwenye nguvu wa Yuda. Alikinza ushawishi huo kwani alikuwa mpenzi wa mwanamume mwingine. Kwa hiyo aliweza kusema hivi kwa fahari kujihusu, “Mimi nalikuwa ukuta.”—Wimbo Ulio Bora 8:4, 10.

Uwe na azimio na uwezo huohuo wa kiadili. Uwe “ukuta” unapokabili vishawishi visivyofaa. Waeleze washiriki wako msimamo wako wa Kikristo waziwazi. Ukifanya hivyo, utabaki ‘bila lawama na hatia’ nawe utakuwa na hakika kwamba umempendeza Mungu.—Wafilipi 2:15. *

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 27 Mashauri zaidi kuhusu kusumbuliwa kingono yameandaliwa katika Amkeni! la Mei 22, 1996; Agosti 22, 1995; na Mei 22, 1991 la Kiingereza.

[Picha katika ukurasa wa 26]

Kueleza waziwazi itikadi zako za Kikristo kwaweza kukulinda

[Picha katika ukurasa wa 26]

Waweza kuepuka kusumbuliwa kingono kwa kutoshirikiana na marafiki wabaya