Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutafakari Ambako Hunufaisha

Kutafakari Ambako Hunufaisha

Maoni ya Biblia

Kutafakari Ambako Hunufaisha

“MANENO YA KINYWA CHANGU, NA MAWAZO YA MOYO WANGU, YAPATE KIBALI MBELE ZAKO, EE BWANA, MWAMBA WANGU, NA MWOKOZI WANGU.”—ZABURI 19:14.

“KUTAFAKARI” humaanisha nini kwako? Ukifuata mafundisho ya dini fulani za Mashariki, huenda ukaamini kwamba ni jambo fulani ambalo huelewesha mawazo zaidi au ni nuru ya pekee. Kutafakari kunakofanywa na Wabudha hutia watu moyo waondoe mawazo yote akilini. Aina nyingine za kutafakari zasemekana kuwa hutia mtu moyo ajaze akili zake “kweli zenye hekima zinazojulikana ulimwenguni pote.”

Maoni ya Biblia juu ya kutafakari hutofautiana na hilo. Katika njia gani? Ufikirie mfano unaotajwa katika Biblia wa mwanamume anayeitwa Isaka, ambaye alipokuwa na umri wa miaka 40 alikuwa na mengi ya kutafakari. Mwanzo 24:63 husema: “Isaka akatoka ili kutafakari kondeni wakati wa jioni.” Hakuna sababu ya kudhani kwamba Isaka aliondoa mawazo yote akilini mwake au kwamba alikuwa akifikiri kwa makini tu ‘kweli yenye hekima inayojulikana ulimwenguni pote’ isiyo dhahiri. Yaelekea Isaka alikuwa na mambo hususa ya kufikiria, kama vile wakati wake ujao, kumpoteza mama yake, au ni nani angekuwa mke wake. Alitumia muda fulani wa faragha jioni ili kutafakari, labda kuhusu mambo hayo muhimu. Katika Biblia, kutafakari kwahusisha mengi zaidi kuliko kuota ndoto za mchana.

Kutafakari Kwahusisha Mengi Zaidi

Fikiria mfano wa mtunga-zaburi Daudi. Alikabili matatizo mengi sana ambayo yalionekana kuwa yasiyoshindika, naye alifahamu kwamba akiwa mwanadamu asiyekamilika, alihitaji msaada wa Mungu ili ajiendeshe ifaavyo. Ni nini kilichomwimarisha Daudi alipokabili hali ngumu? Daudi alisema hivi, kama ilivyorekodiwa kwenye Zaburi 19:14: “Maneno ya kinywa changu, na mawazo ya moyo wangu, yapate kibali mbele zako, Ee BWANA, Mwamba wangu, na mwokozi wangu.” Neno la Kiebrania ambalo limetafsiriwa hapa “kutafakari” lamaanisha kihalisi “kujizungumzia mwenyewe.” Naam, Daudi ‘alijizungumzia mwenyewe’ kuhusu Yehova, utendaji wake, kazi zake, sheria zake, na uadilifu wake.—Zaburi 143:5.

Hali kadhalika, Wakristo wa mapema waliona kutenga wakati wa kutafakari mambo ya kiroho kuwa sehemu ya ibada ya kweli. Mtume Paulo alionya hivi kwa upole: “Mambo yoyote yaliyo ya kweli, mambo yoyote yaliyo ya hangaikio zito, mambo yoyote yaliyo ya uadilifu, mambo yoyote yaliyo safi kiadili, mambo yoyote yaliyo ya kupendeka, mambo yoyote yaliyo ya kusemwa vema, wema wa adili wowote ulioko na jambo lolote la kustahili sifa likiwako, endeleeni kufikiria mambo haya.” (Wafilipi 4:8) Bila shaka, ili kufikiri juu ya mawazo yajengayo, “mambo” hayo ambayo Paulo alizungumza juu yake yapasa kuingizwa akilini mwetu. Jinsi gani?

Mtunga-zaburi atoa jibu. Twasoma hivi katika Zaburi 1:1, 2: “Heri mtu yule asiyekwenda katika shauri la wasio haki . . . Bali sheria ya BWANA ndiyo impendezayo, na sheria yake huitafakari mchana na usiku.” Naam, mtunga-zaburi alisoma sheria ya Mungu kwa ukawaida. Kisha angeweza kutafakari juu ya mambo aliyojifunza kuhusu Muumba.

Kutafakari Leo

Kuna manufaa yasiyo na kifani katika kusoma Biblia, lakini baada ya kusoma, lazima tutafakari, tufikiri kwa uzito au “tujizungumzie wenyewe” kuhusu yale tuliyosoma. Kama vile umeng’enyaji unavyohitajiwa ili tunufaike kikamili na chakula tunachokula, tunahitaji kutafakari ili kuingiza mioyoni mwetu yale tusomayo katika Biblia. Kutafakari kunakofaa hufanya mengi zaidi ya kuondoa tu mawazo yasiyofaa. Pia huturuhusu kufikiria utatuzi wa matatizo yetu unaotegemea Biblia. Kutafakari kwa namna hiyo kwaweza kutusaidia tushughulike kwa mafanikio na mahangaiko ya maisha ya kila siku.—Mathayo 6:25-32.

Mtunga-zaburi Daudi alitambua kwamba kutafakari ni muhimu ikiwa twataka kumpendeza Mungu. Alisema: “Kinywa chake mwenye haki hunena hekima.” (Zaburi 37:30) Naam, kutafakari ni alama inayotambulisha mwabudu mwaminifu. Kuonwa na Mungu kuwa mwadilifu ni baraka kwelikweli, nako hunufaisha kiroho. Kwa mfano, Biblia husema kwamba “njia ya wenye haki ni kama nuru ing’aayo, ikizidi kung’aa hata mchana mkamilifu.” (Mithali 4:18) Hivyo, Mkristo mtiifu ‘anayenena hekima’ anaweza kutarajia kukua katika uelewevu wa Biblia.

Pia Biblia huonya Wakristo kwa upole watafakari kuhusu madaraka yao ya Kimaandiko. Mtume Paulo alimwambia hivi Timotheo: “Fikiri kwa uzito juu ya mambo haya; vama katika hayo, ili kusonga mbele kwako kupate kuwa dhahiri kwa watu wote. Daima kaza uangalifu kwako mwenyewe na kwa kufundisha kwako. Kaa katika mambo haya, kwa maana kwa kufanya hivi utajiokoa wewe mwenyewe na wale wakusikilizao pia.” (1 Timotheo 4:15, 16) Naam, yale tusemayo na kufanya yaweza kuathiri sana wengine.

Ni wazi kwamba tuna sababu nyingi za kufikiri kwa uzito na kwa makini juu ya mambo ya maana. Ni muhimu kufikiria mambo yaliyotupata wakati uliopita, kufikiria kwa uzito mambo ya sasa, na kufikiria kwa makini wakati wetu ujao. Lakini zaidi ya yote, kutafakari kutatuletea nuru kubwa zaidi ikiwa fikira zetu zitakazwa kwenye hekima ya Muumba wetu, Yehova Mungu.

[Picha katika ukurasa wa 20]

“Mtu Anayefikiri,” sanamu ya kuchongwa ya Rodin