Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutimiza Hayo Malengo

Kutimiza Hayo Malengo

Kutimiza Hayo Malengo

NIA njema, udugu, amani ya kimataifa—ni nani ambaye hawezi kusifu malengo bora kama hayo? Baron Pierre de Coubertin, aliyeanzisha upya Michezo ya Olimpiki, aliamini kwamba michezo hiyo ingeshinda chuki za kitaifa kwa kudumisha staha ya washiriki bila kujali jamii, dini, au jinsia. Alihisi kwamba “ulimwengu bora ungeweza kuletwa tu na watu walio bora.” Lakini je, michezo yaweza kuleta amani ulimwenguni? Hatuna budi kujibu la, tuchunguzapo historia yake.

Ingawa michezo ina sehemu yake, elimu ya Biblia ndiyo ufunguo wa kudumisha amani ya kweli. Kwa kweli, kanuni za Biblia zaweza kutokeza “watu walio bora,” kama walivyoitwa na Coubertin. Chunguza maandiko kadhaa yanayoweza kudumisha amani miongoni mwa watu wanaoyatumia, bila kujali taifa lao.

“Kwa hilo wote watajua kwamba nyinyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo miongoni mwenu wenyewe.”—Yohana 13:35.

“Ikiwezekana, kwa kadiri itegemeavyo nyinyi, iweni wenye kufanya amani na watu wote.”—Waroma 12:18.

“Maadamu tuna wakati wenye kufaa kwa ajili ya hilo, acheni sisi tufanye lililo jema kuelekea wote.”—Wagalatia 6:10.

“Bila kufanya jambo lolote kwa ugomvi au kwa majisifu ya bure, bali kwa hali ya akili ya kujishusha chini mkifikiria kwamba wengine ni wakubwa kuliko nyinyi.”—Wafilipi 2:3.

“Mazoezi ya kimwili ni yenye manufaa kidogo; lakini ujitoaji-kimungu ni wenye manufaa kwa mambo yote, kwa kuwa una ahadi ya uhai wa sasa na ule utakaokuja.”—1 Timotheo 4:8.

Je, kweli kanuni hizo za kimaandiko hufanya kazi? Fikiria jambo lililotukia huko Munich, Ujerumani. Mnamo mwaka wa 1974, miaka miwili tu baada ya michezo ya Olimpiki iliyofanyika katika jiji hilo kuvurugwa na ugaidi na mauaji, Mashahidi wa Yehova walikuwa na mkusanyiko wa kimataifa katika Uwanja wa Olimpiki. Baadhi ya wajumbe waliohudhuria walitoka Ugiriki na Uturuki—nchi zilizokuwa zikipigana. Wakati huohuo wa kiangazi, wanajeshi wa Ugiriki na Uturuki walikuwa wakigombania kisiwa cha Cyprus. Je, hilo lingeathiri Wakristo waliokuwa wakihudhuria mkusanyiko huo? La! Iligusa moyo kama nini kuona Wagiriki na Waturuki wakikumbatiana na kuitana ndugu na dada!

Mashahidi wa Yehova wanajulikana ulimwenguni pote kwa sababu ya kuwa na mahusiano ya amani yanayokiuka mipaka ya kitaifa, kimbari, na kikabila. Bila shaka, wao hawadai kwamba wametimiza kikamili lengo la muungano na ushirikiano wa ulimwenguni pote. Kama mtu yeyote yule, ni sharti wajitahidi kufuata shauri la mtume Mkristo Paulo: “Uvueni utu wa zamani pamoja na mazoea ya huo, na mjivike wenyewe utu mpya.” (Wakolosai 3:9, 10) Hata hivyo, wao huamini kwa dhati kwamba kufuata kanuni za Biblia kwaweza kuwasaidia watu ‘watafute sana amani na kuifuatia.’—1 Petro 3:11.

Jambo la kusikitisha ni kwamba watu wengi wamedhihirisha sifa mbaya sana licha ya malengo bora ya Michezo ya Olimpiki. Kinyume cha hilo, Neno la Mungu lenye nguvu husaidia watu wawe na sifa bora zaidi, na kudumisha nia njema na amani ya kimataifa.

[Picha katika ukurasa wa 8]

Michezo ya Olimpiki huchochea mashindano

[Hisani]

Aus dem Fundus der MÜNCHNER OLYMPIAPARK GMBH, München

[Picha katika ukurasa wa 9]

Biblia huchochea amani