Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tetemeko la Dunia!

Tetemeko la Dunia!

Tetemeko la Dunia!

NA MLETA-HABARI WA AMKENI! KATIKA TAIWAN

“Nilikuwa nimelala chini, nikisoma katika chumba changu kwenye ghorofa ya tisa huko Taipei wakati taa zilipoanza kufifia. Kisha chumba kikaanza kutetemeka kwa nguvu. Ilikuwa ni kana kwamba dubwana fulani lilikuwa limebamba jengo hilo na kulitikisa kutoka upande mmoja hadi mwingine. Niliruka na kuingia mvunguni mwa meza huku nikishtuliwa na kelele za vitu vilivyokuwa vikianguka kutoka juu na kufanya nifikiri dari lingeanguka. Ilionekana ni kana kwamba hali hiyo ingeendelea daima.”—Mwandishi wa habari anayeishi Taiwan.

TETEMEKO la dunia. Kutajwa tu kwa neno hilo husababisha hofu, na hivi karibuni huenda umelisikia kwa ukawaida sana mpaka ukafadhaika. Kulingana na Uchunguzi wa Jiolojia wa Marekani, idadi isiyo ya kawaida ya matetemeko makubwa ya dunia yalitukia mwaka 1999, na watu waliokufa walikuwa maradufu ya wastani wa kila mwaka.

Tetemeko kubwa zaidi la dunia la mwaka 1999 lilitukia Taiwan, ambapo mabamba mawili makubwa ya kontinenti hukutania. Kwa ujumla, kuna mabamba 51 katika Taiwan nzima. Hivyo, haishangazi kwamba kuna matetemeko ya dunia yapatayo 15,000 ambayo hurekodiwa hapa kila mwaka. Hata hivyo, mengi ni madogo sana hivi kwamba hayasikiki.

Mambo yalikuwa tofauti Septemba 21, 1999. Saa 7:47 za usiku, Taiwan ilikumbwa na tetemeko la dunia kubwa sana hivi kwamba Rais Lee Teng-hui aliliita “tukio baya zaidi katika kisiwa hicho karne hii.” Lilichukua muda wa sekunde 30 tu lakini lilifikia kipimo cha 7.6 kwenye skeli ya Richter. * Kina cha tetemeko hilo la dunia kilikuwa tu cha kilometa moja hivi, na kwa kuwa hicho si kina kirefu lilikuwa na matokeo makubwa. “Niliamshwa na mtikiso mkubwa,” asema Liu Xiu-Xia, anayeishi karibu na kitovu cha tetemeko hilo la dunia. “Fanicha na vyombo, na hata taa iliyo kwenye dari iliporomoka chini. Nilishindwa kutoka kwa sababu mlango ulikuwa umezuiliwa na vitu vilivyoanguka na vioo vilivyovunjika.” Huang Shu-Hong, aliyetupwa kutoka kitandani na tetemeko hilo, alikabili ugumu tofauti. “Stima ilipotea mara moja, kwa hiyo kulikuwa na giza tititi,” asema. “Nilitoka nje huku nikijikwaa kwenye vitu na kukaa nje usiku kucha pamoja na majirani wengine kando ya barabara. Ardhi iliendelea kutikisika.”

Jitihada za Uokoaji

Madhara yaliyosababishwa na tetemeko la dunia yalionekana kulipopambazuka. Majengo yapatayo 12,000 yaliporomoka, kuanzia nyumba za ghorofa moja hadi majengo yenye ghorofa nyingi. Habari za msiba huo zilipoenea, wataalamu wa kutoa misaada kutoka nchi 23 walikuja Taiwan kusaidia wafanyakazi wa kujitolea wa hapa. Watu wengi walikuwa bado wamenaswa kwenye vifusi.

Saa 72 baada tu ya kutokea msiba huwa muhimu katika kupata waokokaji, lakini katika kisa hiki wafanyakazi walikabili mambo yenye kushangaza. Kwa mfano, mvulana mmoja mwenye umri wa miaka sita aliokolewa baada ya kunaswa kwa muda wa saa 87. Na katika Taipei, waokoaji walipokuwa wakitumia vifaa vizito kuondoa mabaki ya jengo la ghorofa 12 lililokuwa limebomoka, kijana mmoja aliibuka kwa ghafula. Yeye na ndugu yake walikuwa wamenaswa ndani kwa zaidi ya siku tano, na wote waliokoka masaibu hayo!

Hata hivyo, kwa kusikitisha, si wote ambao waliweza kufikiwa, na waokoaji walihuzunika sana pindi fulani-fulani. Mathalani, kiongozi mmoja wa kikundi cha uokoaji aliomboleza hivi: “Tulisikia mtoto akilia hadi muda wa saa nane zilizopita. Lakini akanyamaza.” Mwishowe, idadi ya waliokufa katika Taiwan ilizidi 2,300, na zaidi ya watu 8,500 walijeruhiwa.

Kukabiliana na Matokeo ya Baadaye

Jitihada kubwa ilianzishwa ya kuandaa makao kwa ajili ya mamia ya maelfu ya watu walioachwa bila makao na tetemeko hilo la dunia. Hapo kwanza, wahasiriwa fulani walisitasita kuingia ndani ya nyumba. Hilo laeleweka kwa sababu katika siku kumi baada ya tetemeko la dunia la kwanza, matetemeko madogo-madogo karibu 10,000 yalirekodiwa! Mojawapo kati ya hayo lilifikia kiwango cha 6.8 kwenye skeli ya Richter, na kusababisha majengo kadhaa ambayo tayari yalikuwa yameharibika yaporomoke.

Hata hivyo, kazi ya kutoa misaada iliendelea. Mashirika kadhaa yasiyo ya kiserikali—kutia ndani vikundi vya kigeni vya waokoaji, kikundi cha Wabudha cha Tzu Chi, na wazima-moto—walitumia stadi na wakati wao kufanya kazi hiyo. Pia Mashahidi wa Yehova walihusika katika kazi ya kutoa misaada. Kwa kufuata shauri la Biblia lipatikanalo kwenye Wagalatia 6:10, walikuwa na miradi miwili. Walitaka (1) kusaidia wale ambao katika imani ni jamaa zao na (2) kufanya lililo jema kuelekea wote, kutia ndani wale wasioshiriki itikadi zao.

Mwishoni mwa siku ya kwanza, Mashahidi wa Yehova walikuwa wakileta chakula, maji, mahema na vifaa vya kupikia nje kwa kutumia lori. Kwa kuwa mawasiliano yote yalikuwa yamekatishwa, wazee kutoka makutaniko sita katika eneo lililoathiriwa walifanya jitihada ya pamoja kutafuta Mashahidi wenzao na watu wao wa jamaa pamoja na wanafunzi wa Biblia na watu wenye kupendezwa. Mashahidi ambao hawakuwa na makao walitiwa moyo wapige kambi pamoja ili wote waweze kutunzwa ifaavyo na kupashwa habari kwa urahisi. Waangalizi wasafirio na washiriki wa Halmashauri ya Tawi la Taiwan walizuru kila kikundi na kutaniko ili kulitia moyo.

Hatua ya pili ilikuwa kurekebisha nyumba na Majumba ya Ufalme yaliyokuwa yameharibiwa. Kila kutaniko lilitayarisha orodha ya wale waliohitaji msaada. Kisha, chini ya mwongozo wa Halmashauri ya Ujenzi ya Mkoa, vikundi vya wafanyakazi wa kujitolea walitumwa kufanya marekebisho yaliyohitajiwa. Kazi ilikamilika mwezi mmoja baada ya tetemeko hilo.

Mashahidi wa Yehova waliwasaidia pia majirani wao ambao si Mashahidi. Kwa mfano, Mashahidi walizuru hospitali na watu walioishi kwenye mahema ili kuwafariji. Pia waligawanya fotokopi za makala “Misiba ya Asili—Kumsaidia Mtoto Wako Akabili Hali,” iliyochapishwa katika toleo la Amkeni! la Juni 22, 1996. Watu wengi walishukuru kupokea habari hiyo na wakaanza kuisoma mara moja. Barabara zilipofunguliwa, Mashahidi wa Yehova walituma misaada kwa kutumia lori katika maeneo ya milimani yaliyojitenga ambayo yaliathiriwa sana na tetemeko hilo la dunia.

Wale wanaojifunza Biblia wanatambua kwamba ilitabiri muda mrefu uliopita kwamba siku za mwisho za mfumo huu wa mambo zingeashiriwa na “matetemeko ya dunia mahali pamoja baada ya pengine.” (Mathayo 24:7) Lakini Biblia hutoa uhakikisho pia kwamba hivi karibuni, chini ya utawala wa Ufalme wa Mungu wenye amani, wanadamu hawataishi kwa kuogopa tena misiba ya asili. Wakati huo dunia itakuwa paradiso kwelikweli.—Isaya 65:17, 21, 23; Luka 23:43.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Kwa kutofautisha, tetemeko la dunia lenye kuhuzunisha lililotukia Uturuki, Agosti 1999 lilifikia kipimo cha 7.4, hata hivyo liliua watu mara saba zaidi ya waliokufa huko Taiwan.

[Picha katika ukurasa wa 25]

San Hong R-C Picture Company

[Picha katika ukurasa wa 26]

Mashahidi wa Yehova walifanya mikutano yao, huku wakiishi katika kambi

[Picha katika ukurasa wa 27]

Tetemeko hilo la dunia liliharibu barabara nyingi

[Hisani]

San Hong R-C Picture Company

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 27]

Grafu ya tetemeko kwenye ukurasa wa 2, 25-27: Figure courtesy of the Berkeley Seismological Laboratory