Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Mliandika Kuhusu Mambo Yanayonipata!”

“Mliandika Kuhusu Mambo Yanayonipata!”

“Mliandika Kuhusu Mambo Yanayonipata!”

Kwa miaka mingi Amkeni! limechapisha makala kuhusu magonjwa mbalimbali. Bila shaka, Amkeni! si jarida la kitiba, kwa hiyo halikuzi tiba moja kuliko nyingine. Hata hivyo, linapozungumzia maradhi fulani, gazeti hili hujaribu kueleza tatizo lenyewe, kutambulisha visababishi, na kuandaa shauri linalotumika na la Kimaandiko ili kunufaisha wenye maradhi hayo na watunzaji wao.

Kwa mfano, makala “Kuelewa na Kuvumilia Uyabisi wa Misuli” iliyochapishwa katika toleo la Juni 8, 1998, ilivutia watu wengi sana ulimwenguni. Kwa kweli, barua za uthamini zilipokewa hata miezi mingi baada ya makala hiyo kuchapishwa. “Ninahisi kana kwamba nimeondolewa mlima fulani,” akaandika mwanamke mmoja. “Ni kana kwamba mliandika kuhusu mambo yanayonipata!” akaandika mwingine, huku akiongezea, “sasa najua namna ya kushughulika na ugonjwa huu.”

Wataalamu pia walifurahia makala hiyo. Makamu mkuu wa msimamizi wa mambo ya kitiba ya Shirika la Uyabisi wa Misuli nchini Marekani aliandika hivi: “Naona makala hiyo kuhusu uyabisi wa misuli ni yenye usawaziko, ina habari kamili, na ni nzuri sana. Pia ninasifu jinsi Biblia inavyonukuliwa na umuhimu wa imani katika hali hii na hali nyingine zote za kitiba.”

Barua nyingine nyingi zilipokewa. Yafuatayo ni baadhi ya madondoo.

“Daktari wangu alinitia moyo nisome kila kitu ambacho ningepata kuhusu habari hiyo. Makala yenu ndiyo makala bora zaidi niliyopata kusoma.”—L. R.

‘Wengi wameniuliza kuhusu ugonjwa wangu. Kwa kawaida nilikuwa nikiwapatia kijitabu. Sasa naweza kuwaonyesha toleo hilo la Amkeni! Bila shaka hakuna habari inayofariji zaidi kuliko habari iliyokuwa katika makala hiyo!’—K. K.

‘Makala hiyo ilinikumbusha kwamba ninafaa na kwamba bado Yehova huniona kuwa mwenye thamani.’—D. C.

“Kwa mara ya kwanza nilihisi kana kwamba wengine wanaelewa kinachonipata.”—C. H.

‘Inafariji kujua kwamba si sisi peke yetu tunaoteseka.’—C. A.

‘Ninahisi vibaya sana kwamba siwezi kufanya mambo niliyokuwa nikifanya hapo awali. Nitaweka makala hii karibu na kitanda changu ili niisome mara kwa mara ninapohitaji kitia-moyo.’—K. B.

‘Hadi kufikia sasa, nimejaribu kupuuza maumivu hayo kadiri niwezavyo, nimefanya kazi kadiri nilivyoweza, kisha nikashindwa kabisa kwa muda. Madokezo yenu yanaonyesha njia bora ya kushughulikia hali yangu.’—M. C.

“Nina umri wa miaka 14, na nilipimwa na kujulishwa kwamba nina uyabisi wa misuli nilipokuwa na umri wa miaka 12. Nilidondokwa na machozi kujua kwamba Yehova anatujali. Tafadhali endeleeni kuandika makala zenye kutia moyo kama hii!”—K.A.M.