Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Hangaiko Langu Kuu Kudumu Mwaminifu

Hangaiko Langu Kuu Kudumu Mwaminifu

Hangaiko Langu Kuu Kudumu Mwaminifu

KAMA ILIVYOSIMULIWA NA ALEXEI DAVIDJUK

Ulikuwa mwaka wa 1947; mahali palikuwa kilometa chache kutoka kijiji chetu cha Laskiv, Ukrainia, karibu na mpaka wa Poland. Stepan, rafiki yangu mwenye umri mkubwa kuliko mimi, alitumikia kama mjumbe aliyepeleka kwa siri vichapo vya Biblia Ukrainia kutoka Poland. Usiku mmoja mlinzi wa mpakani alimwona, akamfuata, akampiga risasi. Miaka 12 baadaye kifo cha Stepan kiliathiri sana maisha yangu, kama nitakavyoeleza baadaye.

NILIPOZALIWA Laskiv mwaka wa 1932, familia kumi katika kijiji chetu zilikuwa Wanafunzi wa Biblia, kama Mashahidi wa Yehova walivyojulikana wakati huo. Wazazi wangu, ambao walidumisha uaminifu-mshikamanifu wao kwa Yehova hadi kifo chao katikati ya miaka ya 1970, walikuwapo pia. Hangaiko langu kuu maishani limekuwa pia kudumu mwaminifu kwa Mungu.—Zaburi 18:25.

Katika mwaka wa 1939, Vita ya Ulimwengu ya Pili ilipoanza, eneo tulimoishi katika sehemu ya mashariki ya Poland likawa sehemu ya Muungano wa Sovieti. Tulikuwa chini ya utawala wa Muungano wa Sovieti hadi mwezi wa Juni mwaka wa 1941, wakati Wajerumani walipovamia na kumiliki eneo letu.

Wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Pili, nilikabili hali ngumu shuleni. Watoto walifundishwa kuimba nyimbo za kizalendo na kufanya mazoezi ya kijeshi. Mazoezi yetu yalitia ndani kujifunza jinsi ya kutupa makombora. Hata hivyo, nilikataa kuimba nyimbo za kizalendo wala sikukubali mazoezi ya kijeshi. Kujifunza mapema maishani kusimama imara kuhusiana na itikadi zangu za Biblia kulinisaidia kudumu mwaminifu kwa Mungu katika miaka iliyofuata.

Watu wengi sana walipendezwa na kweli za Biblia katika eneo la kutaniko letu hivi kwamba mapainia wawili, kama wanavyoitwa watumishi wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova, walitumwa kwenye eneo letu kusaidia kuwafundisha. Painia mmoja aitwaye Ilja Fedorovitsch, alijifunza Biblia pamoja nami pia na kunizoeza katika huduma. Wakati Ujerumani ilipoteka sehemu hiyo, Ilja alihamishwa na kufungwa katika mojawapo ya kambi za mateso za Wanazi, ambamo alifia.

Pambano la Baba la Kutokuwamo

Katika mwaka wa 1941 mamlaka za Sovieti zilijaribu kumshawishi Baba atie sahihi hati ya kuahidi kulipa fedha kusaidia kugharamia vita. Aliwaambia kwamba hangeweza kuunga mkono upande wowote katika vita na kwamba akiwa mtumishi wa Mungu wa kweli, ameazimia kutokuwamo. Baba aliitwa adui, akahukumiwa kufungwa gerezani kwa miaka minne. Lakini alifungwa siku nne tu. Kwa nini? Kwa sababu Jumapili iliyofuata kufungwa kwake, jeshi la Ujerumani liliteka eneo tulimoishi.

Walinzi wa gereza waliposikia kwamba Wajerumani wamekaribia, walifungua milango ya gereza na kukimbia. Nje, karibu wafungwa wote walipigwa risasi na wanajeshi wa Sovieti. Baba hakuondoka mara moja lakini baadaye alitoroka na kufika nyumba ya marafiki. Alipokuwa huko alimtumia mama ujumbe alete hati zake zilizothibitisha kwamba alikuwa amefungwa kwa sababu ya kukataa kuunga mkono Wasovieti vitani. Baba alipowaonyesha Wajerumani hati hizo hawakumwua.

Wajerumani walitaka kujua majina ya wote waliokuwa wameunga mkono Wasovieti. Walimshurutisha Baba awataje, lakini alikataa. Alieleza msimamo wake wa kutokuwamo. Angemtaja mtu yeyote, basi mtu huyo angepigwa risasi. Kwa hiyo, msimamo wa kutokuwamo wa Baba uliokoa uhai wa wengine pia, nao walimshukuru sana.

Kufanya Kazi Kisiri

Wasovieti walirudi Ukrainia mwezi wa Agosti 1944, na Vita ya Ulimwengu ya Pili ilikoma huko Ulaya mwezi wa Mei 1945. Baadaye, sisi tulioishi Muungano wa Sovieti tulitengwa na sehemu nyingine za ulimwengu na kile kilichoitwa Pazia la Chuma. Hata ilikuwa vigumu kuwasiliana na Mashahidi wa Yehova waliokuwa upande mwingine wa mpaka huko Poland. Mashahidi wajasiri walivuka mpaka na kurudi na nakala chache zenye thamani za gazeti la Mnara wa Mlinzi. Kwa kuwa mpaka ulikuwa umbali wa kilometa nane tu kutoka nyumbani kwetu Laskiv, nilisikia kuhusu hatari ambazo wajumbe hao walipitia.

Kwa mfano, Shahidi mmoja aitwaye Silvester alivuka mpaka mara mbili na kurudi bila matatizo. Lakini safari ya tatu walinzi wa mpakani na mbwa wao walimwona. Wanajeshi hao walimpaazia sauti asimame, lakini Silvester alikimbia kuokoa uhai wake. Hakuwa na njia nyingine kuepuka mbwa hao isipokuwa kuingia katika ziwa lililokuwa karibu. Alikaa usiku kucha katika maji yaliyomfika shingoni, akijificha katikati ya nyasi ndefu. Hatimaye, walinzi walipoacha kumtafuta, Silvester alirudi nyumbani, akiwa amechoka kabisa.

Kama ilivyotajwa mwanzoni, mpwa wa Silvester, Stepan, aliuawa alipojaribu kuvuka mpaka huo. Hata hivyo, kuwasiliana na watu wa Yehova kulikuwa jambo muhimu. Kupitia jitihada za wajumbe wajasiri, tuliweza kupokea chakula cha kiroho na maagizo yaliyotusaidia.

Mwaka uliofuata, 1948, nilibatizwa usiku katika ziwa dogo karibu na nyumbani kwetu. Waliotaka kubatizwa walikutana nyumbani kwetu, lakini sikujua ni nani, kwa kuwa kulikuwa na giza na mambo yote yalifanywa kimya-kimya na kwa siri. Sisi tuliotaka kubatizwa hatukuzungumza. Sijui ni nani aliyetoa hotuba ya ubatizo, wala aliyeniuliza maswali ya ubatizo huku tukisimama karibu na ziwa hilo, wala aliyenizamisha. Miaka mingi baadaye, nilipozungumza na rafiki mmoja, tuligundua kwamba sote tulibatizwa usiku ule!

Katika mwaka wa 1949 Mashahidi nchini Ukrainia walipata habari kutoka Brooklyn iliyowatia moyo waiombe Serikali ya Muungano wa Sovieti ihalalishe kazi ya kuhubiri katika eneo la Muungano huo. Kwa kupatana na maagizo hayo, maombi yalitumwa kupitia waziri wa wizara ya mambo ya ndani kwa Kamati ya Kudumu ya Muungano wa Jamhuri za Kisoshalisti za Sovieti. Baadaye Mykola Pyatokha na Ilya Babijchuk waliombwa kwenda Moscow kupokea jibu la serikali kwa ombi letu. Walikubali, wakasafiri hadi Moscow majira ya kiangazi mwaka huo.

Ofisa aliyepokea wajumbe hao alisikiliza walipoeleza msingi wa Biblia wa kazi yetu. Walieleza kwamba tunafanya kazi yetu ili kutimiza unabii wa Yesu kwamba “habari njema hii ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa kwa ajili ya kuwa ushahidi kwa mataifa yote.” (Mathayo 24:14) Hata hivyo, ofisa huyo alisema kwamba Serikali haingehalalisha kazi yetu kamwe.

Mashahidi hao walirudi nyumbani, wakaenda kwenye mji mkuu wa Ukrainia, Kiev, na kufanya ombi la kuhalalisha kazi yetu huku Ukrainia. Tena wenye mamlaka walikataa ombi letu. Walisema kwamba Mashahidi wa Yehova wangeruhusiwa kukaa kwa amani iwapo tu wangeunga mkono Serikali. Walisema kwamba, lazima Mashahidi wafanye kazi jeshini na kupiga kura. Kwa mara nyingine msimamo wetu wa kutokuwamo ulielezwa, kwamba kama vile Bwana wetu, Yesu Kristo, hatupaswi kuwa sehemu ya ulimwengu.—Yohana 17:14-16.

Muda mfupi tu baadaye, Ndugu Pyatokha na Babijchuk walikamatwa, wakashtakiwa, na kuhukumiwa kifungo cha miaka 25 gerezani. Wakati huo, mwaka wa 1950, Mashahidi wengi, kutia ndani baba yangu, walihamishwa na mamlaka. Baba alihukumiwa kifungo cha miaka 25 gerezani na kupelekwa Khabarovsk kwenye mpaka wa mashariki wa Muungano wa Sovieti umbali wa kilometa 7,000 hivi!

Kuhamishwa Hadi Siberia

Baadaye mwezi wa Aprili 1951, Serikali ya Sovieti ilipanga kuwashambulia Mashahidi katika jamhuri zake za magharibi za Latvia, Estonia, Lithuania, Moldova, Belarus, na Ukrainia. Mwezi huo Mashahidi 7,000, kutia ndani mimi na Mama, walihamishwa hadi Siberia. Wanajeshi walikuja nyumbani kwetu usiku na kutupeleka kwenye kituo cha garimoshi. Tulifungiwa ndani ya mabehewa ya kusafirishia ng’ombe—watu 50 hivi katika kila behewa—na baada ya majuma mawili tukaachwa mahali paitwapo Zalari, karibu na Ziwa Baikal katika wilaya ya Irkutsk.

Tukiwa tumezingirwa na wanajeshi wenye silaha, huku nikiwa nimesimama katika theluji na kupigwa na upepo baridi niliwaza na kuwazua hali yetu ya baadaye. Ningeweza kudumuje mwaminifu kwa Yehova nikiwa huku? Tulianza kuimba nyimbo za Ufalme ili kusahau hali ya baridi. Mameneja wa makampuni ya kibiashara ya huko yanayomilikiwa na serikali waliwasili. Baadhi yao walihitaji wanaume wa kufanya kazi ngumu ya sulubu, na wengine walitaka wanawake wa kufanya kazi kama vile kutunza wanyama. Mimi na Mama tulipelekwa mahali palipokuwa pakijengwa Kituo cha Umeme wa nguvu za maji cha Tagninskaya.

Tulipowasili, tuliona safu za mabanda ya mbao, makao ya waliohamishwa. Nilipewa kazi ya kuendesha tingatinga na ya fundi umeme, naye Mama alifanya kazi ya shamba. Kirasmi tulikuwa wahamishwa, wala si wafungwa. Kwa hiyo, tulikuwa huru kutembea katika ujirani wa kituo cha umeme, ijapokuwa hatukuruhusiwa kutembelea kambi iliyofuata iliyokuwa umbali wa kilometa 50. Wenye mamlaka walijaribu kutushawishi kutia sahihi mkataba wa kubaki humo milele. Milele ni muda mrefu sana kwa kijana mwenye umri wa miaka 19 kama mimi, kwa hiyo nilikataa kutia sahihi. Hata hivyo, tulibaki huko kwa muda wa miaka 15.

Huko Siberia, mpaka wa Poland haukuwa umbali wa kilometa 8 tu kutoka tulipokuwa bali umbali wa zaidi ya kilometa 6,000! Sisi Mashahidi tulijitahidi sana kufanya mipango ya kuwa na makutaniko tena, na kuweka rasmi ndugu wa kutoa mwongozo. Mwanzoni hatukuwa na vichapo vyovyote vya Biblia isipokuwa vichapo vichache ambavyo Mashahidi wengine walifaulu kuleta kutoka Ukrainia. Tulivinakili kwa mkono, na kupitisha miongoni mwetu.

Muda si muda tukaanza kufanya mikutano. Kwa kuwa wengi wetu tuliishi katika mabanda, tulikutana karibu kila jioni. Kutaniko letu lilikuwa na watu 50 hivi, nami niliongoza Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Kutaniko letu halikuwa na wanaume wengi, kwa hiyo wanawake pia walitoa hotuba za wanafunzi, jambo lililoanzishwa katika makutaniko ya Mashahidi wa Yehova penginepo mwaka wa 1958. Wote walijitahidi kutimiza sehemu zao, wakiona shule kuwa njia ya kumsifu Yehova na ya kutia moyo wengine kutanikoni.

Huduma Yetu Yabarikiwa

Kwa kuwa tuliishi katika mabanda pamoja na watu wasio Mashahidi, siku haikupita bila sisi kuongea na wengine juu ya imani yetu, hata ingawa jambo hilo lilikatazwa kabisa. Baada ya kifo cha Joseph Stalin, waziri mkuu wa Sovieti, mwaka wa 1953, hali ikawa afadhali. Tuliruhusiwa kuongea na wengine kwa uhuru zaidi juu ya itikadi zetu za Biblia. Kupitia barua kutoka kwa marafiki huko Ukrainia, tulikuja kujua mahali walipokuwa Mashahidi wengine katika eneo letu, tukawasiliana nao. Jambo hilo lilituwezesha kupanga makutaniko mbalimbali iwe mizunguko.

Nilimwoa Olga mwaka wa 1954. Yeye pia alikuwa amehamishwa kutoka Ukrainia. Kwa miaka mingi alinisaidia sana katika utumishi wangu kwa Yehova. Stepan aliyeuawa mpakani mwa Ukrainia na Poland mwaka wa 1947 alikuwa ndugu ya Olga. Baadaye tulimpata binti, Valentina.

Mimi na Olga tulipata baraka nyingi katika huduma yetu ya Kikristo kule Siberia. Kwa mfano, tulikutana na George, aliyekuwa kiongozi wa kikundi cha Wabaptisti. Tulimtembelea kwa ukawaida na kujifunza naye magazeti ya Mnara wa Mlinzi tuliyokuwa nayo. Muda si muda George alikuja kuamini kwamba mambo ambayo watumishi wa Yehova wanahubiri kutoka kwa Biblia ni kweli. Tulianza kujifunza pia na baadhi ya marafiki wake Wabaptisti. Tulifurahi kama nini wakati George na marafiki wake kadhaa walipobatizwa na kuwa ndugu zetu wa kiroho!

Mwaka wa 1956, niliwekwa kuwa mwangalizi asafiriye, ikanibidi kutembelea kutaniko moja katika eneo letu kila juma. Nilifanya kazi siku nzima na baadaye kusafiri kwa pikipiki yangu ili kukutana na kutaniko jioni. Mapema asubuhi iliyofuata nikarudi na kwenda kazini. Mykhailo Serdinsky, aliyewekwa kunisaidia katika kazi ya kusafiri, alikufa katika aksidenti ya barabarani mwaka wa 1958. Alikufa siku ya Jumatano, lakini tuliahirisha mazishi yake hadi Jumapili ili Mashahidi wengi iwezekanavyo wapate fursa ya kuhudhuria.

Polisi wa Baraza la Usalama wa Nchi walitufuata tulipoanza kutembea kuelekea makaburi tukiwa umati mkubwa. Kutoa hotuba kuhusu tumaini letu la ufufuo linalotegemea Biblia kungeweza kufanya tukamatwe. Lakini nilisukumwa kusema kuhusu Mykhailo na tumaini lake la ajabu la wakati ujao. Ijapokuwa nilitumia Biblia, polisi wa Baraza la Usalama wa Nchi hawakunikamata. Yaonekana hawakuona faida yoyote katika kufanya hivyo, na kwa vyovyote walinijua vizuri, kwa kuwa mara nyingi nilikuwa nimekuwa “mgeni” kwa kusudi la kuhojiwa katika makao yao makuu.

Kusalitiwa na Mtoa Habari

Mwaka wa 1959 Polisi wa Baraza la Usalama wa Nchi waliwakamata Mashahidi 12 waliokuwa wakiongoza kazi ya kuhubiri. Wengine waliitwa ili kuhojiwa, kutia ndani mimi. Walipoanza kunihoji, nilipigwa butwaa niliposikia maofisa wakieleza mambo ya siri juu ya kazi yetu. Walijuaje mambo hayo? Kwa wazi kulikuwapo mtoa habari aliyejua mengi juu yetu na aliyekuwa amefanyia Serikali kazi kwa muda fulani.

Wale 12 waliokuwa wamekamatwa walikaa katika vyumba vilivyopakana, nao wakakubaliana kutowaambia wenye mamlaka neno lolote jingine. Jambo hilo lingemlazimu yule mtoa habari mwenyewe kuja mahakamani kutoa ushahidi. Ijapokuwa sikushtakiwa, nilienda mahakamani nikaone matokeo. Hakimu aliuliza maswali, na wale 12 hawakujibu. Halafu Shahidi aitwaye Konstantyn Polishchuk ambaye nilikuwa nimemfahamu kwa miaka mingi alitoa ushahidi dhidi ya wale 12. Kesi hiyo iliisha na baadhi ya Mashahidi walifungwa gerezani. Barabarani, nje ya mahakama nilikutana ghafula na Polishchuk.

“Kwa nini unatusaliti?” nikamwuliza.

“Kwa sababu siamini tena,” alijibu.

“Ni nini usichoamini tena?” nilimwuliza.

“Siwezi kuiamini Biblia tena,” alijibu.

Polishchuk angaliweza kunisaliti pia, lakini hakutaja jina langu alipotoa ushahidi wake. Kwa hiyo, nilimwuliza sababu ya kutotaja jina langu.

“Sitaki ufungwe gerezani,” alieleza. “Bado ninahisi kuwa nina hatia kwa sababu ya kifo cha Stepan ndugu ya mke wako. Mimi ndimi nilimtuma mpakani usiku ule alipouawa. Ninasikitika sana kwa sababu ya jambo hilo.”

Maneno yake yalinitatanisha. Jinsi dhamiri yake ilivyokuwa imepotoshwa! Alisikitikia kifo cha Stepan, na bado sasa alikuwa akiwasaliti watumishi wa Yehova. Sikumwona Polishchuk tena. Alikufa miezi michache baadaye. Kumwona mtu ambaye nilimwamini kwa miaka mingi akisaliti ndugu zetu kulinichoma sana moyoni. Lakini jambo hilo lilinifundisha jambo muhimu: Polishchuk alikosa kuwa mwaminifu kwa sababu aliacha kusoma na kuamini Biblia.

Kwa hakika twapaswa kukumbuka fundisho hili: Ikiwa tutadumisha uaminifu-mshikamanifu wetu kwa Yehova, twahitaji kujifunza Maandiko Matakatifu kwa ukawaida. Biblia yasema hivi: “Linda moyo wako kuliko yote uyalindayo: maana ndiko zitokako chemchemi za uzima.” Zaidi ya hayo, mtume Paulo aliwaambia Wakristo wajihadhari. Kwa nini? “Kwa kuhofu kusije kamwe kukasitawi katika yeyote kati yenu moyo mwovu unaokosa imani kwa kujiondoa kwa Mungu aliye hai.”—Mithali 4:23; Waebrania 3:12.

Kurudi Ukrainia

Wakati uhamisho wetu kule Siberia ulipokoma mwaka wa 1966, mimi na Olga tulirudi Ukrainia tena, tukahamia mji uitwao Sokal, umbali wa kilometa 80 hivi kutoka jiji la L’viv. Tulikuwa na mengi ya kufanya kwa kuwa kulikuwa na Mashahidi 34 tu Sokal na miji ya karibu ya Cervonograd na Sosnivka. Leo kuna makutaniko 11 katika eneo hilo!

Olga alidumu mwaminifu hadi kifo chake mwaka wa 1993. Miaka mitatu baadaye nilimwoa Lidiya, na tangu wakati huo amenitia nguvu sana. Mbali na hayo, binti yangu, Valentina, na jamaa yake ni watumishi wa Yehova wenye bidii na wananitia moyo pia. Hata hivyo, jambo linaloniletea shangwe zaidi ni kwamba nimedumu mwaminifu kwa Yehova, Mungu anayetenda kwa uaminifu.—2 Samweli 22:26.

Alexei Davidjuk alikuwa mwaminifu kwa Yehova hadi kifo chake Februari 18, 2000, makala hii ilipokuwa ikitayarishwa kuchapishwa.

[Picha katika ukurasa wa 20]

Kutaniko letu lililokuwa likikutanikia katika mabanda mwaka wa 1952 mashariki mwa Siberia

[Picha katika ukurasa wa 23]

Shule yetu ya Huduma ya Kitheokrasi mwaka wa 1953

[Picha katika ukurasa wa 23]

Mazishi ya Mykhailo Serdinsky mwaka wa 1958

[Picha katika ukurasa wa 24]

Nikiwa na mke wangu Lidiya