Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Nimwambie Mtu Fulani Kwamba Nimeshuka Moyo?

Je, Nimwambie Mtu Fulani Kwamba Nimeshuka Moyo?

Vijana Huuliza . . .

Je, Nimwambie Mtu Fulani Kwamba Nimeshuka Moyo?

“Ninapohisi nimeshuka moyo, kwanza sipendi kuzungumza juu ya jambo hilo kwa sababu huenda watu wakafikiri kwamba mimi ni mtoto mwenye matata. Kisha natambua ya kuwa nahitaji kumwambia mtu fulani ili nipate msaada.” —Alejandro, mwenye umri wa miaka 13.

“Ninapohisi nimeshuka moyo, siwaendei rafiki zangu, kwa sababu sidhani wanaweza kunisaidia. Watanidhihaki tu.”—Arturo, mwenye umri wa miaka 13.

KARIBU kila mtu huhuzunika nyakati nyingine. * Hata hivyo, kwa sababu wewe ni mchanga na huna uzoefu sana, waweza kuhisi kwa urahisi kwamba umelemewa na mikazo ya maisha. Madai kutoka kwa wazazi wako, rafiki zako, na walimu wako; mabadiliko ya kimwili na ya kihisia-moyo ya ubalehe; au kuhisi kwamba hufai kwa sababu ya makosa madogo-madogo—yote hayo yanaweza kukufanya uhisi ukiwa mpweke na mwenye huzuni.

Hilo litukiapo, ni vizuri kuwa na mtu wa karibu zaidi wa kuwasiliana naye. “Kama singeongea na mtu fulani juu ya matatizo yangu, nafikiri ningelipuka,” asema Beatriz mwenye umri wa miaka wa 17. Inasikitisha kusema kwamba, vijana wengi huwa hawasemi juu ya matatizo yao—na mara nyingi wao hujikuta wakididimia zaidi na zaidi kwa kukata tamaa. María de Jesús Mardomingo, profesa katika Kitivo cha Tiba cha Madrid, asema kwamba vijana ambao hufikia hatua ya kujaribu kujiua mara nyingi huwa wapweke sana. Vijana wengi waliookoka majaribio ya kujiua walisema kwamba hawakuweza kupata hata mtu mzima mmoja ambaye wangeweza kuwa wakizungumza naye na kumfunulia mambo yao ya ndani.

Vipi wewe? Je, una mtu wa kuzungumza naye unaposhuka moyo? Ikiwa huna, waweza kumwendea nani?

Zungumza na Wazazi Wako

Alejandro, aliyenukuliwa mwanzoni, anaeleza kile ambacho yeye hufanya anaposhuka moyo: “Mimi humwendea mama yangu kwa sababu tangu nizaliwe amekuwa akinitegemeza, naye hunifanya niwe na tumaini. Pia mimi humwendea baba yangu kwa sababu alipatwa na mambo kama yangu. Nikihisi vibaya na nisimwambie mtu yeyote, basi mimi huhisi vibaya zaidi.” Rodolfo, mwenye umri wa miaka 11, akumbuka hivi: “Nyakati nyingine mwalimu angenidharau na kunikemea, kwa hiyo nilihuzunika sana. Nilikuwa nikienda msalani na kulia. Kisha baadaye, niliongea na mama yangu naye akanisaidia kutatua tatizo langu. Kama singeliongea naye, ningelihuzunika hata zaidi.”

Je, umefikiria kuwa na mazungumzo ya kutoka moyoni pamoja na wazazi wako? Labda unahisi kwamba hawawezi kuelewa matatizo yako. Lakini je, ni kweli? Huenda wasielewe kikamili mikazo yote ambayo vijana hukabili katika ulimwengu wa leo; hata hivyo, je, si kweli kwamba labda wanakujua zaidi kuliko mtu mwingine yeyote ulimwenguni? Alejandro asema hivi: “Nyakati nyingine si rahisi wazazi wangu kunihurumia na kuelewa ninavyohisi hasa.” Hata hivyo, yeye akubali hivi: “Najua kwamba naweza kuwaendea.” Mara nyingi vijana hushangaa kujua jinsi wazazi wao waelewavyo kabisa matatizo yao! Kwa sababu wana umri mkubwa na uzoefu mwingi, mara nyingi wanaweza kutoa ushauri wenye kusaidia—hilo ni kweli hasa kama wao wana uzoefu wa kutumia kanuni za Biblia.

“Ninapoongea na wazazi wangu, mimi hupata kitia-moyo na suluhisho lenye kutumika la matatizo yangu,” asema Beatriz, aliyetajwa awali. Kwa sababu iliyo muhimu, Biblia hutolea vijana shauri hili: “Mwanangu, shika maagizo ya baba yako, wala usiiache sheria ya mama yako. Msikilize baba yako aliyekuzaa, wala usimdharau mama yako akiwa mzee.”—Mithali 6:20; 23:22.

Bila shaka, ni vigumu kuwaendea wazazi wako kama huna uhusiano mzuri pamoja nao. Kulingana na Dakt. Catalina González Forteza, uchunguzi uliofanywa miongoni mwa wanafunzi wa shule ya sekondari ulionyesha kwamba wale waliosema kwamba walikuwa wamejaribu kujiua walikuwa na hisia za kutojistahi na hawakuwa na uhusiano mzuri pamoja na wazazi wao. Kwa upande mwingine, vijana ambao huepuka maoni ya kujiangamiza kwa kawaida “ni wale wanaofurahia uhusiano mzuri pamoja na mama na baba yao.”

Kwa hiyo, fanya bidii kwa hekima kusitawisha uhusiano mzuri pamoja na wazazi wako. Zoea kuongea nao kwa ukawaida. Waambie kinachotukia maishani mwako. Waulize maswali. Mazungumzo hayo yenye uchangamfu huenda yakafanya iwe rahisi kwako kuwafikia unapokuwa na tatizo kubwa.

Kuzungumza na Rafiki

Lakini je, haingekuwa rahisi kumwendea rika lako ukiwa na matatizo? Ni vizuri kuwa na rafiki ambao unaweza kuwatumaini. Mithali 18:24 husema kwamba “yuko rafiki aambatanaye na mtu kuliko ndugu.” Lakini ijapokuwa marika wanaweza kukuhurumia na kukutegemeza, huenda sikuzote wasitoe ushauri bora. Kwa kuwa mara nyingi hawana uzoefu mwingi maishani kuliko wewe. Wamkumbuka Rehoboamu? Alikuwa mfalme nyakati za Biblia. Badala ya kukubali shauri la wanaume wenye uzoefu, wakomavu, alisikiliza marika wake. Matokeo yakawaje? Msiba! Rehoboamu alipoteza tegemezo la taifa lake na kibali cha Mungu.—1 Wafalme 12:8-19.

Tatizo jingine la kuwaendea marika laweza kuwa kuweka siri. Arturo, aliyenukuliwa mwanzoni, asema hivi: “Wavulana wengi ninaowajua huongea na rafiki zao wanapokuwa na huzuni. Lakini baadaye, rafiki zao huwaambia wengine kila kitu na kuwadhihaki.” Gabriela mwenye umri wa miaka 13 amepatwa na jambo hilohilo. Yeye asema: “Siku moja niligundua kuwa rafiki yangu alikuwa akiwaambia rafiki zake mambo yangu ya kibinafsi, kwa hiyo sikumwendea tena. Naam, naongea na watu wa umri wangu, lakini najaribu kutowaambia mambo ambayo yangeniathiri vibaya kama wangewaambia wengine.” Kwa hiyo ukitafuta msaada, ni muhimu kutafuta mtu ambaye ‘hafunui siri ya mtu mwingine.’ (Mithali 25:9) Mtu kama huyo lazima awe amekupita kwa umri.

Kwa hiyo ikiwa kwa sababu fulani unashindwa kupata tegemezo nyumbani, ni sawa kutafuta rafiki wa kumwendea, lakini hakikisha kwamba ana uzoefu maishani na ujuzi wa kanuni za Biblia. Katika kutaniko la kwenu la Mashahidi wa Yehova, bila shaka kuna watu ambao wanafaana na ufafanuzi huo. Liliana mwenye umri wa miaka 16 asema: “Nimewaendea baadhi ya dada zangu Wakristo, na nimekuwa na matokeo mazuri. Kwa kuwa wamenipita kwa umri, ushauri wao ni mzuri. Wamekuwa rafiki zangu.”

Vipi ikiwa umeanza kudhoofika kiroho pia? Labda umehuzunika sana hivi kwamba umeanza kupuuza sala au usomaji wa Biblia. Kwenye Yakobo 5:14, 15, Biblia hutoa ushauri huu: “Je, kuna yeyote mgonjwa miongoni mwenu? Acheni awaite kwake wanaume wazee wa kutaniko, na acheni wasali juu yake, wakimpaka mafuta katika jina la Yehova. Na sala ya imani itamfanya huyo asiyejisikia vizuri apone, na Yehova atamwinua.” Kutaniko la kwenu la Mashahidi wa Yehova lina wazee ambao wana uzoefu katika kusaidia watu ambao wamevunjika moyo au wagonjwa kiroho. Ongea nao kwa uhuru. Biblia husema kwamba wanaume hao wanaweza kuwa “mahali pa kujificha na upepo, na mahali pa kujisitiri na dhoruba.”—Isaya 32:2.

“Acheni Maombi Yenu ya Bidii Yajulishwe kwa Mungu”

Hata hivyo, chanzo kifaacho cha msaada ni “Mungu wa faraja yote.” (2 Wakorintho 1:3) Unapohuzunika na kushuka moyo, fuata ushauri wa Wafilipi 4:6, 7: “Msihangaikie kitu chochote, bali katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na utoaji-shukrani acheni maombi yenu ya bidii yajulishwe kwa Mungu; na amani ya Mungu izidiyo fikira yote kwa ubora italinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili kwa njia ya Kristo Yesu.” Sikuzote Yehova yuko tayari kukusikiliza. (Zaburi 46:1; 77:1) Na nyakati nyingine ni sala tu unayohitaji ili kupumzisha akili yako.

Ukiwa na huzuni au mshuko wa moyo mara kwa mara, usisahau kamwe kwamba vijana wengine wengi wamekuwa na hisia kama hizo. Kwa kawaida, baada ya muda, hisia hizo zitakwisha. Lakini kwa wakati huu, usiteseke kimya-kimya. Mjulishe mtu fulani kwamba unaumia. Mithali 12:25 husema: “Uzito katika moyo wa mtu huuinamisha; bali neno jema huufurahisha.” Utapataje hilo “neno jema” la kitia-moyo? Kwa kumwambia mtu fulani—mtu fulani aliye na uzoefu, ujuzi, na hekima ya kimungu ya kukupatia faraja na msaada unaohitaji.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Ukiendelea kuhisi huzuni, huenda hiyo ikawa dalili ya kasoro kubwa ya kihisia-moyo au ya kimwili. Inapendekezwa utafute msaada wa kitiba bila kukawia. Ona makala “Kulishinda Pigano Dhidi ya Mshuko wa Moyo,” katika toleo la Mnara wa Mlinzi la Machi 1, 1990, lile jarida letu jingine.

[Blabu katika ukurasa wa 14]

“Ninapoongea na wazazi wangu, mimi hupata kitia-moyo na suluhisho lenye kutumika”

[Picha katika ukurasa wa 15]

Wazazi wenye kumhofu Mungu, badala ya marika wako, ndio wawezao kukupa ushauri