Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kukabili Majaribu kwa Nguvu za Mungu

Kukabili Majaribu kwa Nguvu za Mungu

Kukabili Majaribu kwa Nguvu za Mungu

KAMA ILIVYOSIMULIWA NA STEPAN KOZHEMBA

Usiku mmoja mapema mwezi wa Aprili mwaka wa 1951, malori yaliyojaa wanajeshi wa Sovieti yaliingia katika kijiji chetu cha Stenyatyn huko Ukrainia. Wanajeshi wenye silaha walizingira nyumba fulani hususa na kuwachukua washiriki wa familia nzimanzima za Mashahidi wa Yehova na kuwahamisha hadi Siberia. Nikiwa mvulana wa miaka 12 mwenye kuathirika upesi kihisia, nilibaki nikijiuliza kwa nini walitendewa hivyo na jinsi walivyoweza kuvumilia mnyanyaso huo.

NILIZALIWA katika mwezi wa Oktoba mwaka wa 1938 katika kijiji cha Stenyatyn. Mama yangu alikufa majuma mawili baada ya mimi kuzaliwa, na Baba aliuawa vitani katika mwaka wa 1944 akiwa askari wa Sovieti ilipokuwa ikipigana na Ujerumani. Dada wawili wa baba yangu, Olena na Anna walinichukua na kunilea.

Nikiwa mvulana mdogo, niliwafahamu Mashahidi wa Yehova kadhaa katika mji wetu. Walisema nami pamoja na wengine kuhusu Ufalme wa Kimesiya kwenye pindi yoyote iliyofaa. Baada ya muda, nikaja kuwa rafiki wa baadhi ya Mashahidi wenye umri mchanga. Nilishangazwa sana waliposhikwa na askari wa Sovieti na kuhamishwa hadi Siberia.

Lakini si Mashahidi wote waliopelekwa uhamishoni. Stepan, Shahidi aliyeishi karibu na nyumba yetu, aliruhusiwa kubaki, kwa sababu washiriki wengine wa familia yao hawakuwa Mashahidi. Alinizidi umri kwa miaka sita, na nilipoacha shule, tulifanya kazi ya useremala pamoja. Alinifundisha Biblia, akitumia nakala zozote zilizopatikana za Mnara wa Mlinzi. Stepan, ambaye sasa anamtumikia Mungu wa kweli, Yehova, katika Estonia, alifurahi sana nilipobatizwa mnamo Julai mwaka wa 1956.

Upinzani ulikuwa jambo la kawaida kwa mtumishi yeyote wa Yehova katika Ukrainia. Kwa kuwa askari walifanya msako wakitafuta vichapo vya Biblia, nilikuwa na mahali mbalimbali pa kuvificha. Shangazi yangu, Olena na Anna, ambao walikuwa washiriki wa kanisa Katoliki la Ugiriki, hawakufurahia ushirika wangu pamoja na Mashahidi. Hata walijaribu kunishawishi niache kushirikiana nao. Kama mtume Paulo, nyakati nyingine nilihisi nikiwa ‘chini ya mkazo mkali mno upitao nguvu yangu.’ Hata hivyo, uhusiano wangu na Yehova Mungu ulinitia nguvu kuvumilia kila jaribu.—2 Wakorintho 1:8; Wafilipi 4:13.

Jitihada Yangu ya Kudumisha Kutokuwamo

Utumishi katika jeshi la Sovieti ulikuwa wa lazima kwa vijana wenye umri wa miaka 18. Kwa sababu ya ujuzi niliokuwa nao wa Biblia, niliazimia kudumisha kutokuwamo katika mambo ya ulimwengu, na hivyo nikakataa kujiunga na jeshi hilo la Sovieti. (Isaya 2:4; Yohana 17:14-16) Olena na Anna walinitia moyo niwe askari, licha ya kuwa ndugu yao, yaani baba yangu alikuwa ameuawa vitani.

Nilipopata barua ya kunitaka nijiandikishe katika jeshi, nilienda kwenye makao makuu ya jeshi yaliyo karibu na kueleza msimamo wangu. Nilikamatwa mara hiyo na kuwekwa korokoroni huku nikisubiri mashtaka yatayarishwe. Umma haukuruhusiwa kuwepo wakati wa kesi yangu; hata shangazi wangu hawakujulishwa tarehe ya kufanywa kesi. Nilitoa ushahidi mzuri kwa hakimu, mwendesha-mashtaka, na baraza la mahakama la watu wawili. Kesi hiyo ilichukua muda wa dakika 20. Hukumu—miaka mitano gerezani na mingine mitano ambayo ningepoteza haki fulani za kiraia.

Kutumikia Kifungo

Baada ya hukumu hiyo nilifungwa gerezani huko Lviv. Kwa miezi mitatu tangu kukamatwa na hatimaye kuhamishwa kwenye kambi ya kazi ngumu, sikupata kushirikiana na Mashahidi wengine, sikuwa na Biblia, wala vichapo vya Biblia. Hata hivyo, nilidumisha hali yangu ya kiroho kwa kuwahubiria wafungwa wenzangu ambao walikuwa wakiona vigumu kuelewa sababu zangu za kukataa kutumika jeshini. Katika miezi hiyo, nilitegemea yale niliyokuwa nimejifunza kwenye funzo langu la kibinafsi kabla ya kukamatwa. Jambo hilo lilinifunza somo muhimu: Funzo la Biblia la kibinafsi hujenga ndani yetu akiba ya kiroho ambayo hututegemeza wakati wa majaribu.—Yohana 14:26.

Mnamo Aprili 1958, nilipelekwa kwa kambi nambari 21 ya kazi ngumu, karibu na mji wa Dnepropetrovsk, zaidi ya kilometa 700 kutoka nyumbani ili kumalizia huko muda uliobaki wa kifungo changu. Huko tuliamka saa 12:00 asubuhi, na baada ya kufungua kinywa tulipakiwa kwenye malori, na kupelekwa mahali pa kazi, kilometa 50 kutoka kwa kambi yetu. Tulifanya kazi kwenye ujenzi kwa muda wa saa nane, kisha kurudishwa kambini jioni.

Makao yetu yalikuwa vibanda na kila kimoja kilikuwa na wafungwa 100 hivi. Chakula kilikuwa kibovu na maisha yalikuwa magumu; lakini angalau nilifurahia ushirika wa Mashahidi wawili ambao tuliishi pamoja katika kambi moja. Kila mmoja wetu alijitahidi kutoa kitia-moyo kwa wenzake wawili. Hii ni njia nyingine ambayo Yehova hutumia kuwatia moyo watumishi wake nyakati za taabu—kupitia ushirika wa waamini wenzetu.—2 Wakorintho 7:6.

Kulikuwa na jumla ya Mashahidi 12 kambini. Baadhi yao walikuwa na watu wa ukoo nje ya kambi na hawa walituletea kisiri kurasa za Mnara wa Mlinzi zikiwa zimefichwa ndani ya vifurushi vya chakula. Vingi vya vifurushi hivyo vilikaguliwa na walinzi kabla ya kutufikia. Hivyo, ili kuepuka kurasa hizo za Mnara wa Mlinzi kugunduliwa, zilifungwa kwa karatasi ya plastiki na kuwekwa ndani ya mikebe yenye jemu ambayo hao walinzi hawakujali kuifungua. Mara tu tulipozipokea, tulizinakili kwa mkono na kuzigawanya miongoni mwetu.

Tulijitahidi tuwezavyo kuhubiri juu ya Ufalme wa Mungu, na Yehova alibariki jitihada zetu. Kwa mfano, nilikuja kumjua mfungwa mmoja aliyeitwa Sergei, aliyekuwa mhasibu katika kampuni moja ya serikali katika mashariki ya Ukrainia. Udanganyifu ulipogunduliwa mahali pake pa kazi, alishtakiwa kwa kosa hilo na kufungwa gerezani miaka kumi. Mashahidi kadhaa walijifunza naye hapo gerezani, wakitumia gazeti lolote walilokuwa nalo. Sergei alivutiwa na yale aliyokuwa akijifunza na mwishowe akaniambia hivi: “Nitakapofunguliwa kutoka katika kambi hii, ningependa kubatizwa na kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova!” Kama alivyokuwa amesema, Sergei alibatizwa punde tu baada ya kutoka gerezani, naye alimtumikia Yehova kwa uaminifu-mshikamanifu hadi kifo chake.

Utatanishi Juu ya Waroma Sura ya 13

Niliachiliwa huru mnamo Januari mwaka wa 1963 na nikarudi kwenye kijiji changu cha Stenyatyn. Nilitambua mara moja kwamba kulikuwa na tatizo katika kutaniko letu la Sokal. Ndugu walikuwa katika hali ya wasiwasi. Tatizo lilikuwa nini? Hali hii yenye shaka ilikuwa imesababishwa na nini?

Kwa miaka fulani utawala wa Sovieti ulikuwa ukijaribu kupanda mbegu za mafarakano kati ya watu wa Yehova, kwa kuwakamata na kudokeza kwao wakati wa mahoji kwamba Mashahidi walikuwa wakitumiwa kuendeleza masilahi ya Marekani. Maofisa wenye kuwahoji walipendekeza kwamba Mashahidi wanaoishi katika Muungano wa Sovieti waanzishe tengenezo lao wenyewe, na kuongezea kwamba kwa kufanya hivyo wangefurahia uhusiano mzuri na Serikali ya Sovieti na kwamba wangeweza kuruhusiwa kuendesha ibada yao bila mnyanyaso. Maofisa hao walifanya jambo hili lionekane kuwa lenye kufaa.

Kisha Mnara wa Mlinzi la Novemba 15, 1962, ambalo lilichapishwa baadaye katika Kiukrainia kama toleo la Julai 1, 1964, likatoa uelewevu mpya wa Waroma sura 13. Kufikia wakati huo tulielewa “mamlaka zilizo kubwa” zinazotajwa katika mstari wa 1 wa sura hiyo kuwa ni Yehova Mungu na Yesu Kristo, lakini toleo hilo la Mnara wa Mlinzi lilisema kwamba “mamlaka zilizo kubwa” hasa ziliwakilisha serikali za kilimwengu na kwamba zilikuwa “zimewekwa na Mungu katika mahali pa vyeo vyazo vyenye kuhusu.”—Waroma 13:1.

Baadhi ya Mashahidi wengine waliona ugumu kulikubali sahihisho hilo, kwa kuwa viongozi wa serikali ya kilimwengu katika Muungano wa Sovieti walikuwa wamewanyanyasa vibaya sana katika jitihada yao ya kutaka kuangamiza kabisa ibada ya kweli ya Mungu. Kwa sababu hiyo, Mashahidi hao walifikiri kuwa toleo hilo la Mnara wa Mlinzi, lenye uelewevu huo mpya, halikutokana na tengenezo rasmi la Mashahidi wa Yehova. Badala yake, waliamini kwamba lazima habari hiyo iwe ilibuniwa na Mashahidi wenye kuridhiana na utawala ili kuwafanya Mashahidi waweze kuwa watiifu zaidi kwa Serikali ya Sovieti.

Kwa hivyo, kila mtumishi wa Yehova katika Ukrainia akawa anakabili swali hili, Kundi la kweli ni jipi na lisilo la kweli ni jipi? Nilipoona Mashahidi wakiunga mkono upande huu na huu, nikawa najiuliza, ‘Kusudi lao ni nini?’ Punde si punde niliweza kutambua wazi tofauti kati ya makundi hayo mawili.

Walio wengi wa Mashahidi wa Yehova, ambao baadhi yao hawakufahamu kikamili uelewevu mpya wa Waroma sura ya 13, walitaka kudumisha uaminifu-mshikamanifu kwa Yehova na tengenezo lake. Wengine, hata hivyo, walikuwa wakitilia shaka kama vichapo vya hivi karibuni vyenye kuchapishwa na Watch Tower Bible and Tract Society vilikuwa vikitolewa na tengenezo rasmi la Mashahidi wa Yehova. Watu wenye mwelekeo kama huo walikuwa pia na maoni yenye kupita kiasi kuhusu mambo kadha wa kadha. Kwa mfano, waliliona kuwa kosa kwa bibi-arusi kuvaa vazi jeupe na wanaofunga ndoa kuvaa pete. Watu fulani mmoja-mmoja wakaliacha tengenezo. Hata hivyo, baada ya muda fulani, baadhi yao walitambua kosa lao na wakarejea kumtumikia Yehova.

Utendaji wa Kichinichini

Ingawa utendaji wetu wa Kikristo ulikuwa umepigwa marufuku, ilipowezekana tulifanya mikutano ya kila juma tukiwa vikundi vyenye watu wapatao 10 hadi 15. Tuliimarishwa kiroho kwenye mikutano hiyo, kutokana na usomaji wetu wa Biblia na ushirika wa baada ya mkutano. Tulilinganisha matukio ya maishani ya kila mmoja wetu, na tukaja kutambua kwamba sote tulikabili mambo yaleyale. Tulihimizwa na maneno haya ya mtume Petro: “Mambo yaleyale kwa njia ya mateso yanatimizwa katika ushirika mzima wa ndugu zenu katika ulimwengu.”—1 Petro 5:9.

Makala katika Mnara wa Mlinzi yalikuwa msingi wa mazungumzo yetu. Tuliyapataje magazeti hayo? Mashahidi fulani walitumiwa kuleta Ukrainia filamu za nakala ndogo sana za magazeti zilizopunguzwa ukubwa kupitia mpakani. Nakala hizo zilipitishwa kutoka kwa Shahidi mmoja hadi mwingine kwa kufuata utaratibu fulani uliopangwa mapema. Kisha kila mmoja wao alitokeza nakala za kuwatosha washiriki wa kutaniko lake. Nyakati nyingine nilifanyiza nakala hizo. Nilifanya kazi mchana kutwa halafu nikamtumikia Yehova kwa bidii usiku, kwa kutokeza magazeti na kufanya kazi nyinginezo. Ilikuwa vigumu sana kutimiza mambo hayo yote, lakini sisi tuliokuwa wenye daraka katika tengenezo tulitambua kwamba Yehova “huwapa nguvu wazimiao.”—Isaya 40:29.

Tulibuni mbinu za kuanzisha mazungumzo ya Biblia pamoja na watu tuliokutana nao. Wengi wetu tulifanya hivyo tulipokuwa tukisafiri kwenye magari ya umma. Kawaida moja ya kuanzisha mazungumzo ilikuwa kusoma tu gazeti na kutaja habari ya karibuni kwa abiria aliyeketi karibu nasi. Mara tu mazungumzo yalipoanza, tuliyaunganisha na habari iliyo katika Biblia. Tulihubiri habari njema katika eneo letu kupitia njia hiyo.

Mke Mwema

Mnamo mwaka wa 1965, nilifunga ndoa na Tamara, aliyelelewa katika utumishi wa Mungu wa kweli na alifahamu jinsi ya kudumisha imani chini ya majaribu. Ndugu yake aliyeitwa Sergei alikuwa amekamatwa na kuhukumiwa mara tatu kwa sababu ya utendaji wake akiwa Shahidi. Mara ya mwisho alipokamatwa, alipatikana na magazeti ya Mnara wa Mlinzi, na akafungwa gerezani miaka kumi. Naye Tamara alipelekwa na watawala kwenye makao yao makuu ili kuhojiwa na wakawa wanamtisha kumfunga gerezani.

Ilikuwa vigumu kupata makao baada ya kufunga ndoa, lakini familia fulani iliyoishi huko Sokal iliyowapenda Mashahidi ilitupatia chumba kidogo katika nyumba yao kwa malipo kidogo. Familia hiyo ilituhakikishia kwamba Tamara angeweza kuendelea kuishi katika chumba hicho iwapo ningekamatwa na kufungwa tena gerezani. Mimi na mke wangu tulimshukuru Yehova kwa wema wake na pia familia hiyo kwa sababu ya fadhili yao. Baadaye mshiriki mmoja wa familia hiyo alipokufa, Tamara alitumia fursa hiyo kumweleza binti yao, Galina, tumaini la ufufuo. Mbegu hizo za kweli ya Biblia zilikuwa na matokeo kwa sababu Galina alikuja kumpenda Muumba wetu. Alibatizwa na sasa anamtumikia Yehova pamoja na mume wake.

Kwenye miisho-juma katika miaka ya 1970, nilizuru sehemu mbalimbali za Ukrainia vilevile Moldavia (Moldova) na Milima ya Carpathia, nikikutana na kuwajenga waliokuwa na madaraka katika tengenezo la Yehova. Kwa kawaida nilianza safari yangu Ijumaa jioni na kurudi nyumbani Jumapili jioni. Mara nyingi Tamara hakujua nilikokuwa nikienda na nyakati nyingine hata hakujua iwapo ningerudi. Hali iliendelea hivyo kwa miaka mingi. Ninaweza tu kuthibitisha ukweli wa maneno haya ya Biblia kuhusu mke mwema: “Kima chake chapita kima cha marijani.”—Mithali 31:10.

Wakati huo utendaji wowote wa Mashahidi wa Yehova ulikabili hatari fulani. Tuliweza tu kufaulu kwa uwezo wa Yehova. Mara nyingi nilijikuta katika hali ngumu bila kujua la kufanya. Kwa hiyo, ningetoa sala kimya-kimya na kumtegemea Yehova anitie nguvu. Hali hiyo ikawa njia yetu ya maisha.—Matendo 4:29.

Nyakati za Karibuni

Kadiri wakati ulivyopita, ndivyo hali ya watumishi wa Yehova katika Ukrainia ilivyobadilika na kuwa bora. Mnyanyaso ulipungua, na badala ya kufungwa gerezani walihukumiwa kulipa faini. Katika miaka ya 1980, serikali ilikuja kufahamu kwamba kwa kweli Mashahidi wa Yehova ni tengenezo la ulimwenguni pote. Hivyo, kwa kuwafunga Mashahidi katika Ukrainia na kwingineko katika Muungano wa Sovieti, Serikali hiyo ilikuwa ikijiharibia jina ulimwenguni pote. Nakumbuka ofisa mmoja alisema hivi alipokuwa akinihoji: “Sasa tunafahamu kuwa dini si lazima iwe na madhara. Hangaiko letu kuu ni kuzuia kikundi cha kidini kisidhuru Serikali.”

Pazia la Chuma lilianza kufunguliwa huko Ulaya Mashariki mwishoni mwa miaka ya 1980, na tangu wakati huo kumekuwa na uhuru zaidi katika Ukrainia. Mnamo mwaka wa 1991 kazi yetu ya kuhubiri iliandikishwa kisheria. Kisha, mnamo Septemba 1998, Watch Tower Society ikafungua ofisi ya tawi katika mji wa Lviv. Ujenzi wa majengo mapya ya ofisi ya tawi ambayo itakuwa na zaidi ya wafanyakazi 170, ulianza mwanzoni mwa mwaka wa 1999. Kwa sasa, kuna zaidi ya watu 112,000 wenye kushiriki kazi ya kuhubiri katika Ukrainia, na zaidi ya watu 250,000 walihudhuria Ukumbusho mwaka huu wa 2000. Kinachopendeza zaidi ni idadi ya vijana Mashahidi. Kwenye mkusanyiko huko Kiev katika mwaka wa 1991, mwandishi mmoja wa gazeti aliniuliza hivi:

“Watu hawa wote wametoka wapi? Nilifikiri kuwa Mashahidi hawako katika Muungano wa Sovieti, ghafula naona maelfu!”

“Hatukutokea ghafula kwa usiku mmoja,” nikamwambia. “Tumekuwa tukimtumikia Yehova huku kwa miaka mingi.”

“Mnatumia mbinu gani kuwavutia vijana wengi hivi katika dini yenu?” akataka kujua.

“Yafaa uwaulize vijana wenyewe swali hilo. Acha wakueleze sababu yao ya kutaka kumtumikia Yehova.”

“Tayari nimewauliza,” yule mwandishi akasema. “Wamenieleza kwamba wanafurahia kufanya hivyo.”

“Basi hiyo ndiyo sababu,” nikasema. “Iwapo hivyo ndivyo vijana wetu wanavyosema, basi hamna jingine.”

Si vijana tu wanaofurahia kumtumikia Yehova. Mimi na Tamara tumekuwa tukimtumikia Yehova kwa jumla ya miaka zaidi ya 80, na hatungependa kuacha imani yetu kwa sababu ya chochote. Ingawa sisi ni Mashahidi wa Yehova, tungali tunapatwa na matatizo. Tunafahamu kwamba maadamu mfumo huu wa kale ungalipo, kila mtu ataendelea kukabili magumu. Lakini sisi tumetayarishwa vyema kukabili magumu zaidi ya kikundi chochote kile ulimwenguni. Sisi tumeazimia kuyakabili majaribu hayo kama vile tulivyofanya wakati uliopita, kwa nguvu za Mungu wetu mweza yote, Yehova. Sisi tunahisi kama Musa alipoimba wimbo huu wa ushindi: “BWANA ni nguvu zangu, na wimbo wangu; naye amekuwa wokovu wangu.”—Kutoka 15:2.

[Picha katika ukurasa wa 22]

Nikiwa na Mashahidi wenzangu katika kambi nambari 21 ya kazi ngumu

[Picha katika ukurasa wa 22]

Filamu za picha zilizopunguzwa kabisa za “Mnara wa Mlinzi” wa Kiukrainia (ukubwa halisi)

[Picha katika ukurasa wa 23]

Nikiwa na mke wangu, Tamara

[Picha katika ukurasa wa 24, 25]

Mchoro wa msanii wa majengo ya ofisi mpya ya tawi yanayojengwa huko Lviv

[Picha katika ukurasa wa 25]

Kwa nini vijana wengi sana wanamtumikia Yehova katika Ukrainia?