Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Familia Zisizo na Baba Asanteni kwa ule mfululizo “Familia Zisizo na Baba—Kukomesha Zoea Hilo”! (Februari 8, 2000) Nilikuwa mwenye uchungu mwingi kwa ajili ya talaka niliyopata na nilitaka kupata haki zote za kumlea binti yangu. Lakini makala hizo zilinisaidia kufahamu kwamba binti yangu alihitaji kuwa na uhusiano mzuri iwezekanavyo na baba yake. Kupigania haki za malezi si njia ya kutatua tatizo hili.

L. D., Guam

Nikiwa mzazi mmoja, nimejaribu sana kumlea mvulana wangu kulingana na kanuni za Biblia. Yule aliyekuwa mume wangu ni kama wale mnaowataja kuwa “wenye ubaridi”; hapendezwi kamwe na mwanaye. Hata hivyo, nimemzoeza mwanangu kumpenda na kumheshimu baba yake, kama makala yenu ilivyodokeza. Nilitiwa moyo sana kujua kwamba ninafanya lililo sawa.

R. S., Brazili

Wazazi wangu walitalikiana nikiwa na umri wa miaka mitano. Baba yetu hakupendezwa nasi tukiwa watoto. Nyakati nyingine mimi huona afadhali nisingalimjua kamwe kuliko kuona ubaridi huo wake. Kupitia fadhili za Yehova, nilianza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova nikiwa mtoto mdogo. Kujua kweli za Biblia kumenisaidia kukabili uchungu wa kuachwa na baba.

C. B., Puerto Riko

Kwa miaka ipatayo saba sasa, nimekuwa nikiwalea wanangu watatu nikiwa peke yangu, na wakati mwingine hali imekuwa ngumu. Kwa mfano, pindi nyingine wavulana hao hawanisikilizi. Lakini nawapenda kwa moyo wangu wote, nami humshukuru Yehova kwa ajili yao. Bidii yangu si ya bure, kwa kuwa yule mkubwa alibatizwa karibuni. Makala kama hii hunitia nguvu kuendelea. Nitazisoma kwa kawaida.

N. B., Kanada

Baba yangu aliondoka nyumbani nilipokuwa na umri wa miaka sita. Sasa nina umri wa miaka 21, na nimeanza kuona athari ya tendo hilo. Nimeogopa sana kuolewa, nikiwaza kwamba mwanamume ataniacha tu hatimaye. Nilihisi pia ningemsumbua huyo mwanamume kwa kuwa sijui namna familia nzuri inavyopaswa kuwa. Hata hivyo, makala hiyo ilinitia moyo sana. Ilinisaidia kuona kwamba inawezekana siku moja niwe mke mwenye usawaziko, mwaminifu, na mwenye upendo.

E.V.W., Marekani

Matatizo Yanayotatiza Urafiki Mara nyingi nimetaka kuwaandikia, lakini bado sijafaulu. Nimemaliza tu kusoma makala “Vijana Huuliza . . . Kwa Nini Rafiki Yangu Aliniumiza?” (Februari 22, 2000) Tatizo kubwa lilitokea kati yangu na rafiki yangu wa karibu, nikaanza kumchukia. Makala hiyo ilifika kwa wakati unaofaa.

C. V., Italia

Niliumizwa na mmojawapo wa marafiki wangu. Makala hiyo ilinisaidia kuona kwamba mradi sisi si wakamilifu, nyakati nyingine tunakosana. Nilifanya kama makala ilivyosema na kunyoosha mambo kati yetu.

N. T., Trinidad

Nina umri wa miaka 18 na ninao marafiki wawili wakubwa. Mmoja wao ni mwenye umri mkubwa zaidi yangu na yule mwingine ni mchanga kwa miaka miwili. Kwa kweli, kumekuwa na matatizo kati yangu na huyo mwenye umri mchanga. Makala hiyo ilifika kwa wakati unaofaa. Wakolosai 3:13 lilitukumbusha kwamba Yehova hutusamehe kwa hiari mara nyingi sana, na sisi twapaswa kuwa wenye kusameheana vivyo hivyo. Fungu la mwisho lilieleza jambo hilo wazi kabisa. Hivyo sisi sote twatamani kuwa kama rafiki anayesimuliwa katika Mithali 18:24—“aambatanaye na mtu kuliko ndugu” au dada!

W. C., Marekani