Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Imani Yajaribiwa Huko Poland

Imani Yajaribiwa Huko Poland

Imani Yajaribiwa Huko Poland

KAMA ILIVYOSIMULIWA NA JAN FERENC

NILIKUWA kijana tu wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Pili. Ninamkumbuka vizuri ndugu mmoja wa Baba aliyekuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Alitutembelea nyumbani na kutusomea Biblia. Wazazi wangu hawakupendezwa, lakini mimi, kaka yangu Józef, na dada yangu mkubwa Janina, tulipendezwa sana. Punde si punde sote tulionyesha wakfu wetu kwa Yehova kupitia ubatizo. Nilipobatizwa nilikuwa na umri wa miaka 14 tu.

Wazazi wetu walianza kusikiliza walipoona jinsi funzo la Biblia lilivyokuwa na matokeo mazuri katika maisha yetu. Baba yangu alipoelewa kwamba Biblia yakataza ibada ya sanamu, alisema hivi: “Ikiwa ndivyo Neno la Mungu linavyosema, mapadri hawajatufundisha chochote. Mwanangu, toa sanamu zote zilizo ukutani na uzitupilie mbali!” Yapata miaka miwili baadaye, wazazi wangu walibatizwa. Walimtumikia Yehova kwa uaminifu hadi kifo.

Taabu Tulizokabili

Baada ya vita kukoma, Mashahidi wa Yehova walikabili nyakati ngumu. Kwa mfano, ofisi iliyo Lodz ilivamiwa na askari wa Idara ya Usalama, na wale ambao walifanya kazi pale walikamatwa. Mashariki mwa Poland, wapiganaji wa kuvizia wa Majeshi ya Taifa waliochochewa na makasisi wa Kanisa Katoliki waliwashambulia kikatili Mashahidi wa Yehova. *

Yapata wakati huo pia, serikali ya Kikomunisti ilifuta kibali cha kufanya makusanyiko ilichokuwa imetupa awali, na ikajaribu kusimamisha makusanyiko yaliyokuwa yakiendelea. Hata hivyo, upinzani ulioongezeka ulitufanya kuazimia kwa dhati zaidi kuendelea kuhubiri Ufalme wa Mungu. Mnamo mwaka wa 1949 kulikuwa Mashahidi zaidi ya 14,000 katika Poland.

Punde si punde, nikawa painia, mhudumu wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova. Mgawo wangu wa kwanza ulikuwa umbali wa kilometa 500 hivi kutoka nyumbani. Hata hivyo, hatimaye niliwekwa kuwa mwangalizi asafiriye katika eneo lililo mashariki ya Lublin, karibu na mahali walipoishi wazazi wangu.

Kukamatwa na Kunyanyaswa

Mnamo Juni 1950, nilikamatwa na kushtakiwa na serikali ya Kikomunisti kwamba nilifanyia Marekani upelelezi. Nilitupwa katika chumba cha chini ya ardhi chenye unyevunyevu. Usiku nilitolewa ili kuhojiwa na ofisa mmoja mwenye kufanya uchunguzi. “Shirika la kidini ambalo unashirikiana nalo ni farakano na ni adui ya Serikali yetu,” akaniambia. “Ofisi yenu inafanyia kazi shirika la ujasusi la Marekani. Twaweza kuthibitisha jambo hilo! Ndugu zako tayari wamekubali kwamba wamesafiri sehemu zote za nchi na kukusanya habari kuhusu ngome na viwanda vya majeshi yetu.”

Bila shaka, mashtaka hayo yote yalikuwa ya uwongo. Hata hivyo, ofisa huyo alinishauri nitie sahihi hati ya kuacha kile alichokiita “tengenezo lenu lenye fedheha.” Alijaribu tena na tena kunishawishi nitie sahihi. Hata alijaribu kunishawishi niandike majina na anwani za Mashahidi wote niliowajua na sehemu za kugawanyia vichapo vyetu. Hakufaulu.

Baada ya hapo, maofisa walinipiga kwa rungu hadi nikapoteza fahamu. Kisha, wakanilowesha maji ili nirudiwe na fahamu, wakaendelea kunihoji. Usiku uliofuata nilipigwa visiginoni kikatili. Nilisali kwa Mungu kwa sauti anipe nguvu ya kuvumilia. Nahisi alifanya hivyo. Mahojiano hayo ya usiku yalifanywa kwa ukawaida kwa muda wa mwaka mmoja hivi.

Niliachiliwa huru katika mwezi wa Aprili 1951, lakini Mashahidi wengi bado walikuwa gerezani. Nilikwenda kumwona Shahidi mwenye daraka na kuomba mgawo mpya. “Huogopi kukamatwa tena?” akaniuliza. “Nimeazimia kwa uthabiti hata zaidi kufanya kazi mahali penye uhitaji mkubwa zaidi,” nikamjibu. Niliendelea na kazi yangu nikiwa mwangalizi asafiriye, na baadaye nilipewa kazi ya kupanga uchapishaji na ugawanyaji wa vichapo vyetu katika Poland.

Wakati huo, tulitumia mashine za kale za kunakili na mabamba ya nta ya kupigia chapa ili kufanyiza nakala za Mnara wa Mlinzi. Hali ya uchapishaji wetu ilikuwa duni, na tulilazimika kununua karatasi kwa bei kubwa sana kwa sababu ya upungufu wa karatasi wakati huo. Uchapishaji huo ulihitaji kufanywa mahali pa siri, kama vile katika ghala za nafaka, vyumba vya chini ya ardhi, au darini. Wale waliopatikana walihukumiwa kufungwa gerezani.

Nakumbuka kisima kimoja kikavu tulichotumia. Katika ukuta wake, meta 10.7 chini ya ardhi, kulikuwapo mlango wa kuingilia chumba kidogo ambamo tulifanyiza nakala za magazeti. Ilitubidi kuteremshwa kwa kamba ili kufika humo. Siku moja, nilipokuwa nikiteremshwa kisimani katika ndoo kubwa ya mbao, kamba ilikatika ghafula. Nilianguka hadi chini na nikavunjika mguu. Baada ya kutoka hospitalini, niliendelea kufanyiza nakala za magazeti kwa kutumia mashine hiyo ya kunakili.

Yapata wakati huo nilikutana na Danuta, mhudumu painia mwenye bidii. Tulifunga ndoa mwaka wa 1956, na kwa muda wa miaka minne, tulitumika pamoja katika huduma katikati mwa Poland. Kufikia mwaka wa 1960 tulikuwa na watoto wawili, tukaamua kwamba Danuta aache huduma ya wakati wote ili kuwatunza. Muda si muda, nilikamatwa tena, na wakati huo nilifungiwa katika chumba kilichojaa panya. Baada ya miezi saba nilihukumiwa kifungo cha miaka miwili.

Kufungwa na Kuachiliwa Kutoka Gerezani

Gereza la Bydgoszcz lilikuwa na wafungwa zaidi ya 300, na nilitoa sala kwa Yehova nipate fursa ya kuwaeleza wale wenye mioyo minyofu ujumbe wa Ufalme. Nilizungumza na msimamizi wa gereza, na kupendekeza kwamba nifanye kazi ya kinyozi. Kwa kushangaza, alikubali. Punde si punde nilikuwa nikiwanyoa wafungwa ndevu na nywele, na kuwatolea ushahidi walioelekea kupendezwa.

Muda si muda, mfungwa ambaye nilifanya naye kazi ya kinyozi alianza kutenda kwa kupatana na mazungumzo yetu. Hata alianza kuwaambia wengine mambo aliyojifunza kutoka kwa Biblia. Punde si punde, msimamizi wa gereza alituamuru tusieneze tena zile alizoziita “propaganda za kupinga Serikali.” Kinyozi mwenzangu alisimama imara. Alieleza hivi: “Nilikuwa mwizi, sasa siibi. Nilikuwa mraibu wa nikotini, sasa sivuti sigareti. Sasa maisha yangu yana kusudi, nami nataka kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova.”

Nilipoachiliwa huru, nilitumwa Poznan kusimamia “tanuri ya kuoka mikate,” kama tulivyoviita viwanda vyetu vya siri vya uchapishaji. Kufikia mwisho wa miaka ya 1950, uchapishaji wetu ulikuwa umeboreka zaidi. Tulijifunza jinsi ya kupunguza ukubwa wa kurasa kwa kutumia kamera—maendeleo makubwa sana katika uchapishaji wetu—pamoja na kutumia matbaa aina ya Rotaprint. Mnamo mwaka wa 1960 tulianza pia kuchapisha na kujalidi vitabu.

Muda mfupi baadaye, jirani mmoja aliripoti utendaji wetu, nami nikakamatwa tena. Baada ya kuachiliwa mnamo mwaka wa 1962, nilitumwa kutumikia Szczecin pamoja na ndugu wengine kadhaa. Lakini kabla ya kuondoka, tulipata maagizo ya kwenda Kielce, kutoka kwa ndugu ambao tuliamini ni ndugu Wakristo waaminifu. Hata hivyo, tulikamatwa huko, nami nikahukumiwa kifungo cha mwaka mmoja na nusu tena. Tulikuwa tumesalitiwa na walaghai kutanikoni. Baada ya muda, waligunduliwa na kuondolewa miongoni mwetu.

Hatimaye, nilipoachiliwa huru, niliwekwa rasmi kuwa msimamizi wa uchapishaji wetu wote katika Poland. Mnamo mwaka wa 1974, baada ya miaka kumi ya kufanya kazi bila kugunduliwa, nilifuatwa na kukamatwa huko Opole. Baada ya hapo nilipelekwa gerezani Zabrze. “Kazi yako ya askofu imekwisha,” niliambiwa na msimamizi wa gereza. “Ukiendelea kueneza propaganda yako, utapata kifungo cha upweke.”

Kuhubiri Gerezani

Bila shaka, kazi yangu nikiwa mhudumu haikuwa imekwisha. Nilianzisha funzo la Biblia pamoja na wafungwa wenzangu wawili. Hatimaye, walifanya maendeleo hivi kwamba niliwabatiza katika beseni kubwa ya bafu humo gerezani.

Wafungwa wengine pia walipendezwa na kuhubiri kwetu, na mnamo mwezi wa Aprili 1977, tulikutana ili kuadhimisha Ukumbusho wa kifo cha Kristo. (Luka 22:19) Miezi miwili baadaye, mnamo Juni 1977, niliachiliwa huru na sikukamatwa tena.

Wakati huo uhasama wa serikali kuelekea kazi yetu ulikuwa umepungua. Bila shaka, ziara za ndugu wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova zilisaidia sana. Mnamo mwaka wa 1977, ndugu watatu wa Baraza Linaloongoza walizungumza na waangalizi, mapainia, na Mashahidi wa muda mrefu katika majiji mbalimbali. Mwaka uliofuata, ndugu wawili kati yao walifanya ziara ya hisani kwenye Idara ya Mambo ya Dini. Hata hivyo, kazi yetu ilikuwa imepigwa marufuku hadi mwaka wa 1989. Kwa sasa, kuna Mashahidi watendaji 124,000 katika Poland.

Kwa sababu ya afya mbaya, Danuta hajaweza kusafiri nami miaka ya karibuni, hata hivyo ananitia moyo, na anataka niendelee kutembelea makutaniko. Nitamshukuru daima kwa msaada wake wakati wa vifungo vyangu vingi vya gereza.

Kwa hakika, uamuzi wa kumtumikia Yehova Mungu nilioufanya miaka 50 iliyopita ulifaa. Nimefurahi mno kumtumikia kwa moyo wote. Mimi na mke wangu tumeona ukweli wa maneno ya Isaya 40:29 katika maisha yetu: “[Yehova] huwapa nguvu wazimiao, humwongezea nguvu yeye asiyekuwa na uwezo.”

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Ona kitabu cha 1994 Yearbook of Jehovah’s Witnesses, ukurasa wa 213-222.

[Picha katika ukurasa wa 20]

Tulitumia mashine ya kunakili na baadaye tukatumia matbaa aina ya Rotaprint kuchapisha vichapo

[Picha katika ukurasa wa 21]

Nikiwa na mke wangu Danuta