Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Maisha Yako Yaongozwe na Unajimu?

Je, Maisha Yako Yaongozwe na Unajimu?

Maoni ya Biblia

Je, Maisha Yako Yaongozwe na Unajimu?

“WATU WENGI, WAZIMA NA VIJANA HUTAFUTA KUJUA MAMBO YA WAKATI WAO UJAO KUPITIA UTABIRI WA NYOTA.”—PAPA JOHN PAUL WA PILI.

KULINGANA na uchunguzi mmoja, Mmarekani 1 kati ya 4 hutumia unajimu anapofanya maamuzi. Hata hivyo, kutafuta ushauri wa nyota za unajimu bila shaka kumeenea kotekote ulimwenguni. Kote ulimwenguni, watu hutafuta ushauri wa nyota za unajimu kuhusu mambo ya kifedha, mipango ya safari, kazi-maisha, kuweka tarehe ya kufunga ndoa, na harakati za kijeshi. Imedaiwa kwamba nyota ya mtu inaweza kutambulisha wenzi watakaofaana katika ndoa na hata kutoa habari kuhusu wenzi ambao hawatafaana katika ndoa. Iwe ni katika Mashariki au Magharibi, unajimu umevutia mamilioni ya watu. Lakini unajimu ulianzia wapi?

Historia Yake

Aina mbalimbali za unajimu zilipatikana katika tamaduni za kale sana. Hata Biblia husema juu ya “jeshi lote la mbinguni.” (2 Wafalme 23:5) Inaonekana kwamba unajimu ulitumiwa nyakati za kale na Wahindu, Wachina, Wamisri, Wagiriki, na watu wengine. Hata hivyo, marejezo ya kale zaidi ya nyota za unajimu yalipatikana katika Babiloni ya kale.

Wababiloni waliendeleza unajimu ili kutafuta habari ya wakati ujao. Walitazama miendo ya nyota na sayari na kuchora chati na jedwali kwa uangalifu sana. Mambo ya wanadamu na ya dunia yalibashiriwa kutokana na chati na jedwali hizo. Mara nyingi maamuzi ya kisiasa au ya kijeshi yalifanywa baada tu ya kushauriana na wanajimu. Kwa sababu hiyo, jamii ya kikuhani yenye kudai kuwa na hekima ya pekee na nguvu ipitayo ya kibinadamu ikaja kuwa yenye uvutano mkubwa. Kwa hakika, mahekalu yote makubwa katika Babiloni yalikuwa na mahali pa kuangalilia nyota na sayari.

Leo nyota za unajimu ni zenye uvutano mkubwa katika maisha ya watu wengi. Hata watu wenye kudai kwamba hawaamini nyota za unajimu, huenda wakachunguza mambo hayo mara kwa mara ili wajifurahishe au kutokana na udadisi. Ni kweli kwamba wanajimu wamebashiri mambo fulani na yakatimia. Je, hilo lamaanisha kwamba kuchunguza nyota ni kwenye mafaa? Kwa kweli, watumishi wa Mungu wa kale walikuwa na maoni gani juu ya unajimu?

Hatari Zilizofichika

Tofauti na Wababiloni, Wayahudi waaminifu hawakuhusika na unajimu—kukiwa na sababu nzuri. Mungu alikuwa amewaonya wazi hivi: “Asionekane kwako . . . mtu atazamaye bao, wala mtu atazamaye nyakati mbaya, wala mwenye kubashiri, wala msihiri, wala mtu alogaye kwa kupiga mafundo, wala mtu apandishaye pepo, wala mchawi, wala mtu awaombaye wafu. Kwa maana mtu atendaye hayo ni chukizo kwa BWANA.” *Kumbukumbu la Torati 18:10-12, italiki ni zetu.

Watumishi wa Mungu walichukua msimamo thabiti dhidi ya unajimu. Kwa mfano, Mfalme Yosia mwaminifu ‘aliwaondosha . . . waliomfukizia uvumba Baali, na jua, na mwezi, na sayari, na jeshi lote la mbinguni.’ Matendo hayo ya Yosia yalisemwa kuwa “mema machoni pa BWANA,” na kwa ajili ya hayo alibarikiwa na Mungu. (2 Wafalme 22:2; 23:5) Lakini huenda watu wengine wakauliza, ‘Si angalau baadhi ya matabiri ya wanajimu huthibitika kuwa ya kweli?’

Katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, tunasoma juu ya msichana ambaye “alikuwa na kawaida ya kuwapatia mabwana-wakubwa wake faida nyingi kwa kufanya ufundi wa kutabiri.” Yaonekana kwamba, baadhi ya matabiri ya msichana huyo yalitimia, kwa kuwa mabwana-wakubwa wake walipata faida kutokana na uwezo huo wake wa kutabiri. Lakini chanzo cha uwezo wa msichana huyo wa kubashiri mambo ya wakati ujao kilikuwa nini? Biblia yaeleza kwamba aliongozwa na “roho mwovu wa uaguzi.”—Matendo 16:16.

Biblia yasema kwamba “ulimwengu wote unakaa katika nguvu ya mwovu,” Shetani Ibilisi. (1 Yohana 5:19) Kwa kuongoza mambo kwa hila ili matabiri fulani yatimie, Shetani na roho waovu wamenasa akili za mamilioni ya watu.

Ukweli ulio wazi ni kwamba unajimu ni mojawapo ya “mbinu za Ibilisi,” anazotumia kuwaongoza na kuwavuta watu ili kutimiza kusudi lake. Ndiposa, haishangazi kwamba Biblia huwahimiza sana Wakristo ‘wasimame imara’ dhidi ya mbinu zenye hila za Shetani—ukiwemo unajimu. (Waefeso 6:11) Je, yamaanisha basi kwamba hatuna mwongozo wowote kuhusu mambo ya wakati ujao?

Biblia—Mwongozo Wenye Kutegemeka

Mamilioni ya watu wameiona Biblia kuwa mwongozo wenye kutegemeka wanapofanya maamuzi yao. Kuhusu jambo hilo mtunga-zaburi Daudi alisema kwamba “ushuhuda wa BWANA ni amini, humtia mjinga hekima.” (Zaburi 19:7; 119:105) Hilo halimaanishi kwamba Biblia hueleza kihususa jambo la kufanya katika kila hali. Hata hivyo, Neno la Mungu lina kanuni ziwezazo kuzoeza nguvu zetu za ufahamu. Hivyo, tutaweza kutofautisha lililo sahihi na lililo kosa na kutusaidia kufanya maamuzi yenye hekima.—Waebrania 5:14.

Hivyo, ni kwa sababu nzuri kwamba Wakristo wa kweli hawachunguzi nyota za unajimu, haidhuru kwa kujifurahisha au kwa kudadisi. Badala yake, wanatii kwa hekima maonyo kutoka kwa Neno la Mungu dhidi ya uvutano wowote kutoka kwa roho waovu, kutia ndani uvutano wowote wenye hila. Kwa kuruhusu uvutano wa Biblia badala ya uvutano wa unajimu uathiri maisha yako, waweza kubarikiwa na Mungu milele.—Zaburi 37:29, 38.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 10 Ubashiri hutia ndani mambo yote yanayohusu kutafuta habari, hasa kuhusu wakati ujao kupitia nguvu za kifumbo.

[Picha katika ukurasa wa 26]

Nyota za unajimu za Mashariki

[Picha katika ukurasa wa 26]

Nyota za unajimu za Magharibi