Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Mhubiri Aliye Mlemavu Sikuweza kujizuia kulia machozi niliposoma simulizi la Konstantin Morozov katika makala “Wakati Ujao Wenye Tumaini Licha ya Udhaifu.” (Februari 22, 2000) Mimi ni mama nisiye na mwenzi na nina watoto wawili ninaopaswa kulea. Hilo si jambo rahisi, na nyakati nyingine mimi huona matatizo yangu hayatakoma kamwe. Hata hivyo, hayo si kitu yakilinganishwa na hali anayokabili Konstantin!

I., Urusi

Mimi ni mweneza-evanjeli wa wakati wote. Ugonjwa umedhoofisha macho yangu na siwezi kusoma vizuri. Daima nimekuwa msomaji mwenye bidii, na nyakati nyingine mimi hushuka moyo na kukata tamaa. Ninapomfikiria Konstantin, nahisi kwamba sina sababu ya kulalamika. Amekabiliana na matatizo makubwa sana na anatumikia akiwa mweneza-evanjeli wa wakati wote. Yehova huandaa uwezo ulioje!

W. W., India

Nikiwa na umri wa miaka 16 nilipooza kutoka kiunoni hadi miguuni. Na kama Konstantin, nakabili matatizo kila siku. Hata hivyo, makala hiyo ilithibitisha kwamba inawezekana mtu mlemavu kuwa na mahali pake panapomfaa katika jamii na kuabudu Mungu. Ingawa masikio yangu yamekuwa mazito na macho yangu yamedhoofika, mara kwa mara mimi huketi kwenye kiti kidogo nikiegemea ukuta karibu na barabara na kuhubiri nikiwa peke yangu. Nampongeza Konstantin kwa ajili ya bidii na ujitoaji wake.

D. F., Côte d’Ivoire

Utumwa wa Kisasa Katika ule mfululizo wa makala zenye kugusa moyo sana “Utumwa wa Kisasa—Mwisho Wake Wakaribia!” (Machi 8, 2000), habari hii yapatikana: “Hakuna mtu awezaye kuwa Mkristo wa kweli na ashiriki kutumia vibaya na kuonea wanadamu wenzake.” Mkristo apaswa kufanya nini ili kuepuka kuchangia hali hiyo yenye kuchukiza sana? Katika nchi za Magharibi ni vigumu sana kununua bidhaa ambazo hazikutengenezwa katika mazingira ya kutiliwa shaka.

K. H., Marekani

Makala hiyo ilikuwa ikizungumzia kutumia watu vibaya moja kwa moja kunakofanywa na wenye viwanda na watu wengine. Hatukumaanisha kwamba Mkristo atumie muda wake mwingi akijaribu kuchunguza chanzo cha kila bidhaa anayonunua. Lakini ikiwa inajulikana wazi kwamba bidhaa fulani imetengenezwa kwa kazi ya utumwa, basi kila Mkristo apaswa kuamua kibinafsi kununua au kutonunua bidhaa hiyo. Kama ilivyo katika mambo yote, Mkristo ahitaji kuwa na dhamiri njema mbele za Mungu katika jambo hili. (1 Petro 3:16)—Mhariri.

Mimi ni msichana mwenye umri wa miaka 16, na niliguswa moyo sana na makala yenu. Ninawafahamu wasichana fulani wachanga wanaoteseka kutokana na utumwa wa kisasa. Wanafanya kazi kwa bidii katika nyumba za watu ambao wamewapa makao. Lakini hawapati elimu yoyote—au kuonyeshwa shauku. Nilifurahi sana kusoma katika Biblia kwamba hivi karibuni Yehova atawaweka huru wote wanaoonewa.

A. O., Burkina Faso

Imani Leo nilisoma ile makala ya “Maoni ya Biblia: Imani ya Kweli—Ni Nini?” (Machi 8, 2000) Ilionyesha kwa njia muafaka kwamba, imani ya kweli si kuitikadi tu mambo bila sababu. Magazeti mengi huwa na matangazo ya kibiashara chungu nzima na makala chache tu zenye kuelimisha au zenye kujenga. Hatupaswi kamwe kuchukua mambo mnayochapisha kivivi hivi.

E. S., Italia

Vidio ya Noa Sina budi kusema jinsi nilivyothamini ile makala “Noah—He Walked With God—Jinsi Vidio Hiyo Ilivyotayarishwa.” (Machi 8, 2000) Mwana wetu mwenye umri wa miaka miwili na nusu amekuwa akitazama vidio hiyo kabla ya kuanza kutembea. Yeye huitazama tena na tena na kuniomba nirudie sehemu fulani ili aweze kuzitazama mara nyingine. Inapendeza kama nini kuwa na vyombo ambavyo vinakazia upendo kwa Yehova ndani ya watoto wetu!

M.V. G., Marekani