Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Baba Alituacha?

Kwa Nini Baba Alituacha?

Vijana Huuliza . . .

Kwa Nini Baba Alituacha?

“Sikufahamu kamwe sababu baba yetu alituacha. Nililojua tu ni mambo yale niliyoambiwa na mama yangu.”—James. *

BABA anapofunganya virago na kwenda zake, huacha familia ikiwa na uchungu mwingi na huzuni sana. “Nilifadhaika sana ndoa ya wazazi wangu ilipovunjika,” asema James mwenye umri wa miaka 14 aliyenukuliwa mwanzoni. Baba anapotoweka bila kusema jambo lolote na kukata mawasiliano kabisa, huenda watoto wake wakapambana na hisia za kujilaumu, kukataliwa, na uchungu wa moyo kwa miaka mingi. *

Ikiwa baba yako ametoweka, huenda ukawa unajua sababu yenye kuumiza ya yeye kufanya hivyo. “Baba yangu alituacha kwa sababu ya mwanamke mwingine,” kijana aitwaye Michael akasema. “Nilimwona baba siku moja akiwa pamoja na huyo mwanamke, nilikasirika sana. Nilihisi kwamba baba ametusaliti.” Lakini, huenda nyakati nyingine kuondoka kwake kukawa kwenye mafaa. Melissa, ambaye baba yake ni mraibu wa kileo, asema hivi: “Ikiwa angeendelea kukaa nyumbani, maisha yetu yangekuwa magumu sana.”

Ingawa hivyo, watoto wengi hawafahamu sababu zilizomfanya baba yao kutoweka, na hilo huwaumiza hata zaidi. Huenda ikawa ulijua kuwa wazazi wako walikuwa na matatizo, lakini huenda hukuwazia kamwe kwamba wangetalikiana. Robert akumbuka hivi: “Baba yangu alipoondoka nyumbani, sikujua mambo yote yaliyokuwa yakifanyika. Nilijua tu kwamba walikuwa na matatizo mengi kwa sababu walikuwa wakizozana daima.”

Kwa nini baadhi ya akina baba hutoweka nyumbani? Ikiwa baba yako ametoweka nyumbani, je, wapaswa kuhisi kwamba umekataliwa kibinafsi? Na sababu gani huenda wazazi wako wasikueleze mambo yote kuhusu hali yao? Je, wanapaswa kukujulisha?

Sababu ya Wao Kuwa Kimya

Hakuna sababu yenye kupendeza inayofanya baba kutoweka nyumbani. Mara nyingi, sababu ni uzinzi—dhambi ambayo kwa kawaida hufichwa sana isijulikane na washiriki wengine wa familia. Mara tu mke anapogundua dhambi hiyo, huenda akaamua kumtaliki mume wake. Huenda hata akamwomba aondoke kabla ya kuwasilisha talaka mahakamani. Watoto huenda wasijue kamwe kinachotendeka.

Ingawa hivyo, jaribu kuelewa kwa nini mama yako anasita kukujulisha waziwazi kilichotukia. Huenda akawa anahisi kwamba iwapo atafunua ukosefu wa uaminifu wa baba yako hilo litazidisha tu maumivu. Elewa pia kwamba mwanamke huumia sana anapogundua mume wake ni mzinzi. (Malaki 2:13, 14) Kwa hivyo, ikiwa uzinzi ndiyo sababu ya kuvunjika kwa ndoa ya wazazi wako, usishangae iwapo mama yako aona vigumu kuzungumzia jambo hilo kwa sababu ya maumivu aliyo nayo.

Vipi baba yako? Kwa hakika, iwapo amekosa uaminifu kuelekea mama yako, haielekei kwamba atakueleza jambo hilo. Baadhi ya wanaume huhisi aibu sana kwa sababu ya mwenendo wao mbaya hivi kwamba hushindwa hata kukutana ana kwa ana na watoto wao! Licha ya tendo lao la aibu, akina baba walio wengi huendelea kuwapenda watoto wao na huenda wakajaribu kuanzisha tena uhusiano pamoja nao.

Katika visa fulani, baba hutoweka nyumbani kwa sababu ya ukosefu wa adili wa mke wake, lakini bado hujaribu sana kudumisha uhusiano wa karibu pamoja na watoto wake. Katika visa vingine, ndoa haivunjiki kwa sababu ya uzinzi tu, bali ni tokeo la mizozano ya miaka mingi. * (Mithali 18:24) Na kwa sababu zogo hilo halikuwa likifanywa peupe, huenda usijue kiini chake kilikuwa nini.

Biblia yasema hivi katika Mithali 25:9: “Ujitetee na mwenzako peke yake; bali usiifunue siri ya mtu mwingine.” Nyakati nyingine, zogo katika ndoa huhusisha mambo ya kibinafsi yaliyo ya siri. Amini usiamini, huenda ikawa vyema kwako kutosikia mambo hayo. Isitoshe, kufunua “siri” mara nyingi hufanya hali kuwa mbaya hata zaidi. Huenda ukataka kuunga mkono upande mmoja—ukazidisha mtengano katika familia hata zaidi. Kwa hivyo, huenda ikawa afadhali wasikuambie sababu za ugomvi wao.

Jitahidi Kushinda Uchungu wa Moyo kwa Kuwa na Busara

Ingawa hivyo, ni vigumu kuepuka kuwa na hasira na uchungu wa moyo ikiwa baba ametoweka nyumbani na wewe huwezi kujibu swali hili, Kwa nini? Hata hivyo, kwenye Mithali 19:11, Biblia husema hivi: “Busara ya mtu huiahirisha [wala haimalizi kabisa] hasira yake.” Wala huhitaji kujua kila kitu ili uwe na busara.

Kwa mfano, Biblia hutusaidia kujua kwamba wazazi wetu si wakamilifu. Inasema hivi: “Kwa maana wote wamefanya dhambi na hupungukiwa na utukufu wa Mungu.” (Waroma 3:23) Kukubali ukweli wa maneno hayo kutakuwezesha kuwa na maoni yanayofaa kuhusu makosa ya wazazi wako. Kwa mfano, ikiwa baba yako amevunja nadhiri zake za ndoa, hilo ni kosa zito sana—ambalo atatoa hesabu mbele za Mungu. (Waebrania 13:4) Lakini hilo halimaanishi kwamba amekukataa wewe au hakupendi.

Wenzi wote wa ndoa hupatwa “na dhiki katika mwili wao.” (1 Wakorintho 7:28) Na ingawa hawapaswi kutenda hivyo, wanaume na wanawake fulani huruhusu mikazo ya ulimwengu huu wenye matatizo iwaingize katika kosa. Robert akumbuka hivi: “Baba alitaka tuwe na maisha bora. Hivyo, akahamisha familia yake hadi kwenye eneo alilodhani angeweza kuchuma pesa nyingi zaidi na hivyo aweze kutuandalia nyumba nzuri na familia iwe yenye furaha.” Lakini punde si punde mipango aliyokusudia baba yake kwa moyo mweupe ya kutaka familia yake iwe na maisha mazuri iliharibika. Robert asema hivi: “Baba akawa mvivu kuhudhuria mikutano ya Kikristo. Kisha akapoteza kazi yake ya kuajiriwa. Baadaye akaanza kumdhulumu mama pamoja na dada yangu.” Punde hali ikawa mbaya kufikia hatua ya baba na mama kutalikiana.

Robert angeweza kulemewa na uchungu wa moyoni kwa sababu ya makosa ya baba yake. Lakini kuelewa hali ya baba yake kumepunguza hasira yake. Na ingawa kuvunjika kwa ndoa ya wazazi wake kulikuwa pigo kubwa, Robert amejifunza somo muhimu kutokana na jambo hilo. Robert anasema hivi: “Nitakapokuwa na familia yangu mwenyewe, nitatanguliza mambo ya kiroho.”

Michael, aliyetajwa mwanzoni, amepiga vita dhidi ya uchungu wa moyo. “Nilitaka kumwumiza baba yangu kwa sababu ya mambo aliyotutendea,” yeye akiri. Lakini alidumisha uhusiano pamoja na baba yake. Kadiri wakati ulivyopita, Michael aliweza kushinda hasira yake na kusonga mbele na maisha yake.

Wewe pia huenda ukajaribu kudumisha uhusiano wa kawaida pamoja na baba yako kadiri hali zinavyoruhusu. Bila shaka, huenda amekuumiza wewe na mama yako pia. Lakini huenda ikawa hujui ukweli wote wa mambo. Na hata kama unajua yeye ndiye mkosaji, bado yeye ni baba yako. Una wajibu wa kumheshimu angalau kwa kiasi fulani. (Waefeso 6:1-3) Epuka “hasira na hasira ya kisasi na kupiga kelele na usemi wenye kuudhi” unaposhughulika naye. (Waefeso 4:31) Inapowezekana, epuka kuingilia migogoro ya kibinafsi katika ndoa ya wazazi wako. Kwa kuwahakikishia wazazi wako unawapenda, huenda ukafurahia uhusiano mzuri pamoja nao.

Si Kosa Lako

Baba yako anapotoweka nyumbani huenda hilo likawa mojawapo ya mambo yenye kuumiza zaidi maishani mwako. Na hata ikiwa hutaweza kamwe kujua sababu zote zilizofanya baba atoweke, huhitaji kuhisi kwamba lilikuwa kosa lako. Kwa hakika, huenda ukahisi kwamba amekukataa wewe binafsi. Lakini kwa kawaida watoto hawasababishi ndoa kuvunjika. Wazazi wako waliweka nadhiri mbele za Mungu kuishi pamoja. Ni jukumu lao—wala si lako—kutimiza nadhiri hiyo.—Mhubiri 5:4-6.

Iwapo bado unahisi kutatanishwa, ukiwa mwenye hatia, kuhisi kwamba ulisababisha hali hiyo, kwa nini usijaribu kuzungumza pamoja na wazazi wako? Huenda wakakubali kusema nawe na kukupa kitia-moyo unachohitaji. James aliyetajwa mwanzoni akiri hivi: “Nilifikiri daima kuwa ni mimi niliyesababisha hali hiyo, hadi mama na baba yangu walipozungumza nami kinaganaga.” Nancy ambaye ni mchanga alijilaumu pia ndoa ya wazazi wake ilipovunjika. Baada ya kuzungumza pamoja na mama yake mara kadhaa, Nancy alifikia kauli hii: “Watoto hawapaswi kujilaumu kwa ajili ya matendo ya wazazi wao.” Naam, kuwaacha wazazi wako ‘wachukue mzigo wao wenyewe’ kwaweza kukusaidia usilemewe na hisia-moyo. (Wagalatia 6:5) Hata hivyo, utakabilianaje na hali ya kuishi bila baba? Makala ya wakati ujao ya mfululizo huu itaandaa baadhi ya majibu.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Baadhi ya majina yamebadilishwa.

^ fu. 4 Ona mfululizo wa makala kuu “Familia Zisizo na Baba—Kukomesha Zoea Hilo,” kwenye toleo la Amkeni! la Februari 8, 2000.

^ fu. 12 Hata hivyo, Biblia husema wazi kwamba uasherati ndiyo sababu pekee ya Kimaandiko ya kuvunja ndoa na kuweka mtu huru kufunga ndoa na mtu mwingine.—Mathayo 19:9.

[Picha katika ukurasa wa 15]

Usijilaumu kwa ajili ya matatizo katika ndoa ya wazazi wako