Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Sayansi Yaweza Kutokeza Uhai Udumuo Milele?

Je, Sayansi Yaweza Kutokeza Uhai Udumuo Milele?

Maoni ya Biblia

Je, Sayansi Yaweza Kutokeza Uhai Udumuo Milele?

MIAKA mingi iliyopita, swali hilo lingeonwa kuwa la kipumbavu. Lakini, leo, watu fulani wanafikiria kwa uzito uwezekano wa jambo hilo. Tayari, wanasayansi wameweza kurudufisha muda wa kawaida wa kuishi wa nzi wa matunda na minyoo wakitumia mbinu ambazo watu fulani wanaona zaweza kutumika kwa wanadamu.

Uchunguzi umeonyesha kwamba chembe za kawaida za mwanadamu zaweza kufa nazo hujigawanya kwa kipindi. Baadaye huacha kujigawanya. Utaratibu huo umelinganishwa na saa ya silika inayodhibiti wakati wa watu kuzeeka na wakati wa kufa. Wanasayansi sasa wanatafuta mbinu ya kurekebisha saa hiyo.

Nadharia moja inayopendwa na wengi husema kwamba habari kuhusu kuzeeka hupatikana kwenye ncha za kila ukanda wa DNA, sehemu iitwayo telomere. Sehemu hizo zimelinganishwa na plastiki zilizo kwenye ncha za kamba za viatu, ambazo zimekusudiwa kuzuia kamba isifumuke. Wanasayansi wameona kwamba kila mara chembe fulani zigawanyikapo, sehemu hizo za telomere huzidi kuwa fupi kama fataki yenye kuchomeka. Hatimaye, yaonekana telomere hufupika hadi kufikia mwisho wa chembe kugawanyika. Hata hivyo, kunapokuwa na aina fulani ya kimeng’enya, telomere huacha kufupika. Na hivyo kulingana na nadharia hiyo, hilo linaweza kufanya chembe ziendelee kujigawanya daima. Ofisa wa kampuni moja inayohusika katika shughuli hii alisema: “Hii ndiyo mara ya kwanza tunapoweza kuwazia kutokufa kwa mwanadamu.” Hata hivyo, si wanasayansi wote ambao hukubaliana na wazo hilo.

Kifo Kilivyotokea

Bila shaka, watu wenye imani katika Biblia wameamini kwa milenia nyingi uwezekano wa uhai udumuo milele kwa wanadamu. Hawawatumaini wanasayansi wa kibinadamu bali Mwanasayansi Mkuu, aliyeviumba vitu vyote vilivyo hai, Yehova Mungu.—Zaburi 104:24, 25.

Biblia huonyesha kwamba Muumba hakukusudia mwanadamu afe. Wenzi wa kwanza wa kibinadamu waliumbwa kwa mfano wa Mungu na kuwekwa katika bustani ya paradiso. Walikuwa wakamilifu, bila kasoro iwayo yote katika akili au miili yao. Walikuwa na tazamio la kuishi milele duniani. Hilo lilikuwa kusudi la Mungu kuwaelekea. Aliwaagiza wazae watoto na kupanua paradiso hatua kwa hatua hadi ienee kote duniani.—Mwanzo 1:27, 28; 2:8, 9, 15.

Kama inavyoonyeshwa katika Mwanzo sura ya 3, Adamu, huku akijua kwamba adhabu ni kifo, alimwasi Mungu kimakusudi. Zaidi ya hayo, kwa kufuatia mwendo wa kutotii, aliwaletea dhambi na kifo watoto wake ambao hawakuwa wamezaliwa. Mtume Paulo alisema hivi kuhusu hilo: “Kupitia mtu mmoja dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi, na hivyo kifo kikasambaa kwa watu wote kwa sababu wote walikuwa wamefanya dhambi.” (Waroma 5:12) Yaani, kwa sababu Adamu alifanya dhambi, mwili wake ulipoteza ukamilifu. Alizeeka hatua kwa hatua na hatimaye akafa. Watoto wake walirithi kasoro hiyo.

Hivyo, wanadamu hufa kwa sababu ya uasi wa Adamu na hukumu ya Mungu iliyofuata. Wanadamu hawatafaulu kubatilisha hukumu hiyo. Ingawa sayansi imepiga hatua kubwa za kitiba, maneno ya Musa yaliyopuliziwa, yaliyoandikwa miaka 3,500 iliyopita yangali kweli: “Siku za miaka yetu ni miaka sabini, na ikiwa tuna nguvu miaka themanini; na kiburi chake ni taabu na ubatili, maana chapita upesi tukatokomea mara.”—Zaburi 90:10.

Uandalizi wa Yehova kwa Ajili ya Uhai Udumuo Milele

Jambo la kufurahisha ni kwamba kuna tumaini! Ingawa kwa sasa wanadamu wote hatimaye hufa, si mapenzi ya Yehova hali hiyo iendelee milele. Ingawa Adamu na Hawa walistahili kifo, Mungu alijua kwamba kungekuwako na wengi miongoni mwa watoto wao ambao hawakuwa wamezaliwa ambao wangekubali kwa uthamini uongozi wake wenye upendo. Kwa watu hao, yeye aliwaandalia uhai udumuo milele hapa duniani. Mtunga-zaburi aliandika hivi: “Wenye haki watairithi nchi, nao watakaa humo milele.” (Zaburi 37:29) Lakini hilo litatimizwaje?

Hilo halitatimizwa kupitia wanadamu kufumbua siri za DNA. Badala yake, uhai udumuo milele ni zawadi kutoka kwa Yehova kwa wale wanaodhihirisha imani katika yeye. Akitambua kwamba watoto wa Adamu na Hawa walihitaji kuokolewa, alitokeza njia ya wao kupata uhai udumuo milele—dhabihu ya fidia ya Yesu Kristo. Yesu alirejezea uandalizi huo aliposema hivi: “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akatoa Mwana mzaliwa-pekee wake, ili kila mtu anayedhihirisha imani katika yeye asipate kuangamizwa bali awe na uhai udumuo milele.”—Yohana 3:16.

Kama Adamu, Yesu alikuwa mwanadamu mkamilifu. Tofauti na Adamu, Yesu alimtii Mungu kikamilifu. Kwa hivyo, Yesu aliweza kudhabihu uhai wake mkamilifu wa kibinadamu ili kulipia dhambi ya Adamu. Kupitia tendo hilo la upendo, lililosawazisha mizani ya haki, watoto wa Adamu wangeweza kukombolewa kutoka hukumu ya kifo. Kwa sababu hiyo, wote wanaodhihirisha imani katika Yesu watapokea zawadi ya Mungu ya uhai udumuo milele.—Waroma 5:18, 19; 1 Timotheo 2:5, 6.

Ikiwa wanadamu wangeweza kushinda kutokamilika na kujiletea uhai udumuo milele, hakungekuwa na uhitaji wa fidia. Biblia hushauri hivi kwa hekima: “Msiwatumainie wakuu, wala binadamu ambaye hakuna wokovu kwake. Pumzi yake hutoka, huurudia udongo wake, siku hiyo mawazo yake yapotea. Heri ambaye Mungu wa Yakobo ni msaada wake, na tumaini lake ni kwa BWANA, Mungu wake, aliyezifanya mbingu na nchi, bahari na vitu vyote vilivyomo. Huishika kweli milele.”—Zaburi 146:3-6.

Uhai udumuo milele hautatokezwa na utafiti wa kisayansi bali na Yehova. Lolote Mungu akusudialo, aweza kulifanya na atalitimiza. “Kwa Mungu hakuna tangazo lolote litakalokuwa lisilowezekana.”—Luka 1:37.

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 18]

© Charles Orrico/SuperStock, Inc.