Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Suluhisho Hatimaye!

Suluhisho Hatimaye!

Suluhisho Hatimaye!

WAZIA ulimwengu ambamo kila mtoto anathaminiwa kwelikweli, anapendwa kikweli, naye amebarikiwa kuwa na wazazi wenye kujali, na wenye upendo ambao wanatamani kwa moyo wote kumwandalia mtoto wao mwelekezo na mwongozo bora iwezekanavyo. Wazia ulimwengu ambamo kila mtoto ana afya nzuri kimwili na kiakili, ulimwengu usio na mtoto wa mitaani hata mmoja, na usio na watoto wasiofurahia tena maisha yao ya utotoni kwa kuwa hali ya kiuchumi imewalazimu kuajiriwa!

Je, ni wenye kutamanika? Bila shaka. Je, ni jambo la kuaminika? Mashahidi wa Yehova wafikiri hivyo, kukiwa na sababu mbili.

Wazazi Wanaweza Kusuluhisha Matatizo kwa Kiasi Fulani

Bila tashwishi yoyote utakubali kwamba watu wazima wana uwezo wa kusuluhisha—nyakati nyingine hata kuzuia—baadhi ya matatizo ya watoto. Bila shaka inawezekana, mradi tu hao watu wazima wana nia ya kufanya hivyo. Naam, wazazi wenyewe wana ufunguo mmoja wa kusuluhisha matatizo hayo.

Kwa kielelezo, watu wazima wanaofuata shauri la Biblia la kwamba “mke hapaswi kuondoka kwa mume wake . . . na mume hapaswi kumwacha mke wake” hawana watoto wanaoteseka kwa sababu ya kuishi katika familia zilizovunjwa na talaka au kutengana.—1 Wakorintho 7:10, 11.

Watu wazima walio tayari kufuata shauri la Biblia ‘kujiendesha kwa adabu, si katika sherehe zenye makelele ya ulevi,’ hawana watoto wanaoteswa na mkazo unaowapata wale walio na wazazi walevi au waraibu wa dawa za kulevya.—Waroma 13:13; Waefeso 5:18.

Watu wazima walio tayari kufuata shauri la Biblia la ‘kujiepusha na uasherati’ hupunguza hatari ya watoto wao kukua wakihisi hawathaminiwi, labda katika familia yenye mzazi mmoja.—1 Wathesalonike 4:3; Mathayo 19:9.

Watu wazima walio tayari kufuata shauri la Biblia la, “Msiwe mkichochea watoto wenu wakasirike, ili wasishuke moyo,” na “kuwapenda watoto wao” hawatakuwa na watoto wanaoumia kimwili au kiakili kwa sababu ya kutendewa vibaya kwa njia yoyote.—Wakolosai 3:21; Tito 2:4.

Kwa muhtasari, ikiwa watu wote wazima wangekuwa tayari kufuata shauri hili la Biblia lililotolewa na Yesu, “Mambo yote mtakayo watu wawafanyie nyinyi, lazima mwafanyie wao pia hivyohivyo,” je, kungekuwako na mamilioni ya watoto wasiothaminiwa na wasiopendwa?—Mathayo 7:12.

Jambo la kufurahisha ni kwamba kuna watu wengi wazima walio tayari kutekeleza mashauri yote hayo yaliyotajwa. Lakini, inasikitisha kwa sababu si watu wote wanaofanya hivyo, na hicho ndicho kiini cha tatizo. Na hata wale walio tayari kufuata mashauri hayo hukuta kwamba mara nyingi jitihada zao hutatanishwa na kukosa ukamilifu kwa kibinadamu na mambo mengine wasiyoweza kudhibiti. Wanadamu wanaweza kusuluhisha matatizo ya watoto kwa kiasi fulani, lakini ni dhahiri kwamba hawawezi kusuluhisha kikamili matatizo hayo.

Serikali ya Kimungu Itakayoleta Suluhisho Kamilifu

Mwandishi John Ruskin, aliyetajwa katika makala iliyotangulia, aliitikadi kwa uthabiti kwamba “wajibu wa msingi wa Serikali ni kuhakikisha kwamba kila mtoto anayezaliwa humo atakuwa na makao mazuri, mavazi, atalishwa ifaavyo, na kuelimishwa, hadi afikiapo umri wa kujiamulia.” Hata hivyo, Ruskin alikiri kwamba “ili [kutekeleza] wajibu huo ni sharti Serikali iwe na mamlaka juu ya raia ambao kwa leo ni ndoto kwetu kuwazia.”

Ni serikali yenye utegemezo wa kimungu tu inayoweza kuwa na mamlaka bora aliyotaja Ruskin. Na serikali ya aina hiyo imeahidiwa—ile iliyotajwa na Yesu kwenye Mathayo 6:9, 10. Serikali hiyo iliyobuniwa na Mungu ikisha chukua hatamu kamili ya mambo duniani, itatawala watu wote—itawaandalia makao, mavazi, chakula, na kuwaelimisha raia wake wote, kutia ndani watoto. (Isaya 65:17-25) Lakini serikali hiyo kamilifu itatimiza mengi zaidi.

Chini ya Ufalme wa Mungu wanadamu watawezeshwa kulea watoto kwa njia iliyosawazika. (Ayubu 33:24-26) Watoto watalelewa kwa minajili ya kusitawisha amani na udugu wa ulimwenguni, lengo lililo katika Azimio la UM la Haki za Mtoto. (Zaburi 46:8, 9) Hakutakuwapo tena kamwe na uhitaji wa Mwaka wa Kimataifa wa Mtoto wala Mkataba wa Haki za Mtoto.

Kuwarejeshea afya kamilifu wazazi na watoto walemavu kutakuwa kazi rahisi sana kwa Kristo Yesu, Mfalme wa serikali hiyo ya kimbingu. Miujiza ya uponyaji aliyofanya alipokuwa duniani hutuhakikishia hilo. (Luka 6:17-19; Yohana 5:3-9; 9:1-7) Kadhalika Yesu hatashindwa kufufua watoto waliokufa na wazazi waliokufa!—Mathayo 9:18-25.

Ni shangwe iliyoje kujua kwamba wakati wa Mungu kutenda kwa niaba ya watoto walio duniani u karibu!

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 12]

Msaada kwa Vijana

Mashahidi wa Yehova hupendezwa sana kuwasaidia vijana kuepuka matatizo na kuwaonyesha njia bora ya kukabiliana na matatizo ambayo hayawezi kuepukika. Ndiyo sababu kwa miaka mingi wamechapisha vichapo kadhaa vinavyokusudiwa kushughulikia mahitaji ya vijana—kuanzia wale wasiofikia umri wa kwenda shuleni hadi kwa matineja. Vichapo hivyo vyatia ndani Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia na kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi na vilevile vidio yenye kichwa Young People Ask—How Can I Make Real Friends? Waweza kupokea vifaa hivyo kutoka kwa Mashahidi wa Yehova wanaoishi karibu nawe au kwa kuwaandikia wachapishaji wa gazeti hili.

Kwa habari ya watoto wao wenyewe, Mashahidi wa Yehova huwaonyesha kwamba wanathaminiwa na wanapendwa kwa kuzungumza nao kwa ukawaida kuhusu matatizo wanayokabili. Kwa kawaida wazazi hutumia habari nzuri iliyo kwenye vifaa vya kujifunzia vilivyotajwa hapo juu kuwa msingi wa programu ya kawaida, yenye kuendelea ya kuwazoeza vijana. Huenda ukapenda kufuata utaratibu huo kuwasaidia watoto wako.