Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutoka kifo cha polepole hadi maisha yenye Furaha

Kutoka kifo cha polepole hadi maisha yenye Furaha

Kutoka kifo cha polepole hadi maisha yenye Furaha

KAMA ILIVYOSIMULIWA NA DIAMÁNTI DATSERIS

‘Naweza kufa wakati wowote.’ Wazo hilo lilikuwa akilini mwangu daima nilipokuwa nimelala kwenye kitanda hospitalini huku damu ikitona polepole katika mishipa yangu. Kwa zaidi ya miaka 20, niliambiwa kwamba ni sharti nitiwe damu mishipani ili niendelee kuishi—ikiwa kwa kweli huko kungeitwa kuishi.

PUNDE baada ya kuzaliwa mwaka wa 1969 huko Ierápetra, kwenye kisiwa cha Ugiriki cha Krete, wazazi wangu walipokea habari zenye kusikitisha sana. Madaktari walisema kwamba mtoto wao msichana alikuwa na maradhi ya upungufu wa damu yanayoitwa beta-thalassemia, au Cooley. Maradhi hatari sana ya beta-thalassemia hurithiwa, nayo huwashika mara nyingi Wagiriki, Waitalia, wenyeji wa Mashariki ya Kati, Asia Kusini, au wa asili ya Afrika.

Madaktari waliwaeleza wazazi wangu kwamba mtu anapougua maradhi hayo, chembe nyekundu za mwili hazitengenezi himoglobini ya kutosha, protini ambayo husafirisha oksijeni kwenye chembe. Kama tokeo, chembe zangu hazipati oksijeni ya kutosha. Chembe nyekundu hukaa katika damu yangu kwa muda mfupi tu kwa sababu ini langu na wengu huziharibu na kuziondolea mbali. Viungo hivyo ndivyo vinavyoharibu chembe nyekundu zenye kasoro au zilizochakaa.

Wazazi wangu waliambiwa kwamba tiba pekee ijulikanayo ya thalassemia ni kutiwa damu mishipani kwa ukawaida na kuondolewa kwa madini ya chuma yanayorundikana mwilini. Hata hivyo, madaktari walieleza kwamba tiba ya kutiwa damu mishipani huambatana na mrundikano unaoendelea wa madini ya chuma katika moyo na ini, na hilo laweza kufisha. Kutiwa damu mishipani—tiba ambayo huzuia wagonjwa kufa katika miaka kumi ya kwanza ya maisha yao—kwa kawaida huchangia sehemu kubwa ya sumu inayotokana na madini ya chuma ambayo huwa hatari sana baadaye. Wagonjwa wenye maradhi ya thalassemia wanaotiwa damu mara nyingi, kama mimi, kwa kawaida hufa kutokana na kasoro ya moyo kabla ya kufikia umri wa miaka 30.

Kuishi na “Taraja la Kifo”

Tangu nilipokuwa mtoto mchanga, kifo kilinikodolea macho. Siwezi kueleza jinsi ilivyo vigumu kuishi na taraja hilo lenye kuogofya. Sikuwa na mipango yoyote ya wakati ujao wala sikutumaini kuishi maisha ya kawaida. Nilihisi kwamba maradhi yangu ya thalassemia yalikuwa kama bomu lililotegwa tayari kulipuka.

Wazazi wangu walitahadhari sana kwa sababu walihangaikia afya yangu. Nililelewa na masharti chungu nzima ya mambo ya “kuepuka” na sheria nyingine: “Usikimbie!” “Usisisimke!” “Uwe mwangalifu!”

Hali yangu ilimfanya mama yangu aliyekuwa mfuasi wa Kanisa Othodoksi la Ugiriki awe mtu wa kidini sana. Kwa moyo mnyoofu alitafuta msaada kutoka kwa sanamu za kidini. Ili kuboresha hali yangu, alikuwa akinipeleka kwa makao ya watawa yaliyo mbali sana yaliyojulikana kwa uponyaji wa imani kisha akanipa hirizi mbalimbali. Alitumia fedha nyingi katika mambo hayo—lakini hakufanikiwa.

Nilimwamini na kumpenda Mungu, japo sikujua jinsi ya kumwabudu. Nilipokata tamaa, ningesali hivi kwa machozi: “Mungu, iwapo kweli upo nawe wanipenda, tafadhali nisaidie.”

Jitihada ya Kutafuta Faraja

Nilipoendelea kukua, afya yangu ilizorota kasi, hasa kwa sababu ya mrundikano wa madini ya chuma katika damu yangu. Ili kutibu hali yangu, nilitumia kifaa kinachopunguza madini hayo katika damu. Kila usiku nililazimika kudunga sindano katika ngozi yangu ya tumbo ili kuruhusu msombo fulani unaopunguza madini ya chuma upenye mwilini mwangu usiku kucha. Kila usiku nilivumilia zoea hilo lenye kuumiza sana. Mara nyingi niliposhindwa kulala usiku, nilitamani kufa. Nilihisi kwamba Mungu alikuwa amepuuza maombi yangu ya msaada.

Nilipokuwa na umri wa miaka 16, nilianza kushirikiana na kikundi cha vijana waliokuwa waraibu wa muziki mchafu wenye mdundo mzito. Katika jitihada yangu ya kutafuta faraja, nilijiliwaza kidogo kwa muziki huo uliokuwa ukitukuza ukatili, jeuri mbaya sana, na Ibada ya Shetani. Kwa vyovyote vile, kwa kuwa uovu ulienea kote kunizunguka, nilikubali dhana ya kwamba mtu fulani mwovu mwenye mamlaka alikuwa akidhibiti ulimwengu wote. Lakini muda si muda, nilianza kuathiriwa na dawa za kulevya na Ibada ya Shetani. Marafiki wangu walikuwa wakiwaepa polisi daima.

Kutiwa damu mishipani pasipo kikomo kuliacha makovu mwilini mwangu. Mrundikano wa madini ya chuma ulitia miviringo myeusi chini ya macho yangu na kufanya ngozi yangu kuwa na rangi ya manjano. Sura yangu haikuboreshwa na mavazi yangu—mavazi meusi na jaketi la ngozi, lililotiwa njumu na kupambwa kwa mafuvu ya vichwa, mtindo uliopendwa na marafiki wangu. Angalau sikutumia dawa za kulevya.

Nilipozidi kusikiliza muziki mchafu wenye mdundo mzito na maneno yake yaliyokazia kifo, dawa za kulevya, roho waovu, uwasiliani-roho, na damu, nilihisi kwamba Shetani alikuwa ameninasa. Usiku nilishuka moyo na kulia mara nyingi. Wakati huo nilipokuwa nimevunjika moyo sana maishani ndipo mwanga wa tumaini uliponiangazia.

Maisha Yangu Yabadilika Kabisa

Siku moja, nilipokuwa na umri wa miaka 20, rafiki mmoja alinipa kitabu alichokuwa ameachiwa na Mashahidi wa Yehova. Kiliitwa Biblia—Neno la Mungu au la Binadamu? * Hakupendezwa kikweli na kitabu hicho, lakini nilipokipitia-pitia, kilinivutia sana. Kilionyesha wazi kwamba kanuni za Biblia zinaweza kuboresha maisha ya mtu. Pia nilivutiwa kujifunza kuhusu mnyanyaso wa Wakristo wa mapema na utayari wao wa kudhabihu uhai wao kwa sababu ya itikadi zao. Nilipomaliza kusoma kitabu hicho, nilitaka kuwaambia wengine mambo hayo. Ndipo nilipokutana na Manolis, mwanamume aliyemjua Yehova na ujumbe wa Biblia kwa sababu watu wake kadhaa wa ukoo walikuwa Mashahidi wa Yehova. Niliandamana naye hadi mahali pa karibu pa mikutano ya Mashahidi wa Yehova, na katika kiangazi cha mwaka wa 1990, nilianza kujifunza nao Biblia.

Kupitia funzo langu la Biblia, nilijifunza kwamba Muumba wetu anatujali kwelikweli na kwamba hasababishi magonjwa na maumivu yanayotesa wengi wetu. (1 Petro 5:7) Nilijifunza kwamba ni Shetani aliyeleta dhambi na kifo ulimwenguni na kwamba hivi karibuni Yehova ataharibu kazi za Shetani kwa kuondoa mfumo huu wa kale wa mambo na kuweka mahali pake ulimwengu mpya mkamilifu. (Waebrania 2:14) Katika hali za paradiso, watu wanaomhofu Mungu watarejeshwa kwa ukamilifu wa kibinadamu. Kisha, hakuna mtu atakayesema, “Mimi mgonjwa.”—Isaya 33:24.

Nilijifunza pia kwamba Biblia hutuambia ‘tujiepushe na damu.’ (Matendo 15:20, 29; Mwanzo 9:4) Dhamiri yangu ilipoanza kufinyangwa na kuzoezwa na viwango na kanuni bora zaidi za Biblia, nilichochewa kufanya uamuzi wa kibinafsi kuhusu kutiwa damu mishipani. Niliamua kwamba sitakubali kutiwa damu tena.

Kwa zaidi ya miaka 20, nilishawishiwa kuamini kwamba ni sharti nitiwe damu mishipani kwa ukawaida ili niendelee kuishi. Je, ningekuwa najiletea kifo kwa kutii amri ya Biblia? Wazazi wangu wangeonaje kukataa kwangu damu? Je, madaktari wangu na wanatiba wengine wangejaribu kunishinikiza?

Kufanya Maamuzi Muhimu Sana

Nilimtupia Yehova mahangaiko yangu yote kwa kusali kwa bidii. (Zaburi 55:22) Niliamua pia kutafuta matibabu mengine. Baada ya kusoma sana, niligundua kwamba badala ya kutiwa damu mishipani ningeweza kula mlo maalumu wenye madini ya chuma na vitamini nyingi. Zaidi ya yote, niliazimia kuishi kupatana na sheria ya Mungu kama inavyoonyeshwa katika Biblia.

Haishangazi kwamba wazazi wangu walikasirika sana. Tangu nilipokuwa mtoto mchanga walifanya yote waliyoweza ili niwe hai, na sasa nilikuwa nikikataa kutiwa damu mishipani! Ingawa hivyo, hatimaye walisema kwamba wangeheshimu uamuzi wangu binafsi kuhusu suala hilo.

Kisha nikawaeleza wanatiba hospitalini msimamo wangu wa kidini, pamoja na kuwaeleza kwamba ningejitahidi vilivyo kupata matibabu ya badala kuliko kutiwa damu mishipani. Madaktari walikubali shingo upande kutii uamuzi wangu.

Nilipokuwa nikitiwa damu mishipani hapo awali, nilikuwa nimefanya urafiki na vijana wengine wenye maradhi ya thalassemia. Sasa walishtuliwa na msimamo wangu kuhusu damu. Mmoja wao aliniambia kwa kejeli kwamba karibuni “nitabebwa na watu wanne kwa machela”—ni msemo wa Kigiriki unaomaanisha kwamba ningekufa. Jambo la kuhuzunisha ni kwamba baadaye alikuwa miongoni mwa wagonjwa watano waliokufa kwa sababu ya kutiwa mishipani damu iliyoambukizwa!

Tangu Agosti 1991, sijatiwa damu mishipani. Kinyume kabisa cha matarajio yote, niko hai nikiwa na afya ya kadiri. Kwa kula chakula chenye vitamini nyingi na madini ya chuma, nimeweza kudumisha afya njema kiasi, licha ya matatizo yanayozuka mara kwa mara na hali ngumu za kudumu zinazosababishwa na maradhi yangu ya thalassemia.

Lakini, jambo la kupendeza kuliko yote ni kwamba maisha yangu yana kusudi, yameboreshwa na uhusiano wa karibu pamoja na Muumba wangu, Yehova Mungu. Mnamo Julai 1992, nilionyesha wakfu wangu kwa Yehova kwa ubatizo wa maji. Manolis, yule rafiki yangu mpendwa aliyenijulisha kwa kutaniko la Kikristo la Mashahidi wa Yehova lenye kutoa utegemezo muhimu, alibatizwa siku hiyohiyo. Miezi 18 hivi baadaye, tulifunga ndoa. Baadaye, nilikuwa na shangwe ya kumwona mama yangu na dada yangu wakibatizwa na kuwa watumishi wa Yehova. Maoni ya baba yangu kuelekea Mashahidi wa Yehova yamebadilika, na mara kwa mara yeye huhudhuria mikutano ya kutaniko.

Nimejifunza kwamba ingawa kifo ni adui, si adui wa kuogopwa. (Zaburi 23:4) Kama tukiishi au tukifa, ni kwa Yehova. Uhai wetu u mikononi mwake. (Waroma 14:8) Nitamshukuru daima kwa kuniokoa kutokana na maisha yenye taraja la kifo cha polepole tu. Kwa kweli, ameniongoza kwenye tumaini la uhai wa milele!—Ufunuo 21:1-4.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 18 Kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

[Picha katika ukurasa wa 21]

Nilijitahidi sana kutafuta faraja

[Picha katika ukurasa wa 22]

Nikiwa na mume wangu, Manolis