Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ndoa Yako-Yaweza Kuokolewa

Ndoa Yako-Yaweza Kuokolewa

Ndoa Yako-Yaweza Kuokolewa

Biblia ina mashauri chungu nzima yenye kutumika yawezayo kuwanufaisha waume na wake. Jambo hilo halishangazi hata kidogo, kwa sababu Yule aliyevuvia Biblia ndiye Mwanzilishi wa mpango wa ndoa.

BIBLIA ina maoni halisi juu ya ndoa. Inakiri kwamba mume na mke watakuwa na “dhiki” au kulingana na Biblia Habari Njema, “matatizo.” (1 Wakorintho 7:28) Hata hivyo, Biblia pia husema kwamba ndoa yaweza na yapasa kuleta shangwe, hata kufurahiana. (Mithali 5:18, 19) Mawazo hayo mawili hayapingani. Yanaonyesha tu kwamba licha ya matatizo mazito, wenzi wa ndoa wanaweza kuwa na uhusiano wa karibu na wenye upendo.

Je, ndoa yako imekosa uhusiano kama huo? Je, matatizo na kukata tamaa yameharibu ukaribu na shangwe mliyokuwa nayo hapo mwanzoni? Hata ikiwa ndoa yako imekosa upendo kwa miaka mingi, hali inaweza kurudi kama ilivyokuwa hapo mwanzoni. Bila shaka, unahitaji kuona mambo kwa njia halisi. Hakuna mwanamume na mwanamke wasio na ukamilifu wawezao kuwa na ndoa kamilifu. Hata hivyo, kuna hatua unazoweza kuchukua ili kubadilisha hali zinazoharibu ndoa.

Unaposoma habari hii jaribu kuona mambo yanayohusu hasa ndoa yako. Badala ya kukazia fikira udhaifu wa mwenzi wako, teua madokezo machache ambayo wewe unaweza kufanyia kazi, halafu tumia mashauri hayo ya Kimaandiko. Huenda ukagundua kwamba ndoa yako yaweza kuokolewa kuliko ulivyodhani awali.

Tutaanza kwa kuzungumzia mtazamo kwa sababu maoni yako kuhusu uwajibikaji na hisia zako kuelekea mwenzi wako wa ndoa ni ya muhimu sana.

Maoni Yako Kuhusu Uwajibikaji

Kuazimia kuwa pamoja kwa muda mrefu ni kwa maana iwapo unataka kuboresha ndoa yako. Kwa vyovyote, Mungu alibuni mpango wa ndoa kuunganisha watu wawili wasitengane kamwe. (Mwanzo 2:24; Mathayo 19:4, 5) Kwa sababu hiyo, uhusiano wako na mwenzi wako wa ndoa haulingani na kazi ambayo unaweza kuacha au chumba unachoweza kuhama kwa kuvunja mapatano ya kulipa kodi. Badala ya hivyo, mlipokuwa mkifunga ndoa mliweka nadhiri ya kushikamana pamoja, hata hali iweje. Uwajibikaji wenye kina unapatana na maneno yaliyosemwa na Yesu Kristo yapata miaka 2,000 iliyopita: “Kile ambacho Mungu amefunga nira pamoja msiache mtu yeyote akitenganishe.”—Mathayo 19:6.

Watu fulani huenda wakasema, ‘Bado, tunaishi pamoja. Je, hilo halionyeshi kwamba tumewajibika?’ Labda. Hata hivyo, kama ilivyotajwa mwanzoni mwa mfululizo huu, wenzi fulani wanaishi pamoja wakiwa na matatizo chungu nzima, wakiwa wamenaswa katika ndoa isiyo na upendo. Lengo lako ni kufanya ndoa yako iwe na furaha, si yenye kuvumilika tu. Uwajibikaji wapasa kuambatana na uaminifu katika mpango wa ndoa na kwa yule mtu ambaye umeahidi kumpenda na kumtunza.—Waefeso 5:33.

Mambo unayomwambia mwenzi wako hufunua kadiri ya uwajibikaji wako. Kwa mfano, wakati wa mabishano makali, waume na wake fulani husema hivi bila kufikiri: “Nitakuacha!” au “Nitatafuta mtu mwingine anayenithamini!” Ingawa huenda usifanye hivyo, maneno kama hayo humomonyoa uwajibikaji kwa kudokeza kwamba mnaweza kuachana wakati wowote na kwamba mwenye kusema hivyo yuko tayari daima kuondoka.

Ili kurejesha upendo katika ndoa yenu, komeni kutoa vitisho kama hivyo mnapoongea. Kwa vyovyote, je, unaweza kupamba chumba ukijua kwamba unaweza kuhama wakati wowote? Kwa sababu gani, basi, umtazamie mwenzi wako kujitahidi kuboresha ndoa iliyo katika hatari ya kuvunjika? Azimia kujikakamua kwa moyo wote kutafuta suluhisho.

Mke mmoja alifanya hivyo baada ya kuvurugana kwa muda fulani na mume wake. “Licha ya kutopendezwa naye mara kwa mara, sikufikiria kuvunja uhusiano wetu,” yeye asema. “Tulitarajia kunyoosha mambo kwa vyovyote. Na sasa, baada ya miaka miwili iliyojaa misukosuko, naweza kusema kwa moyo mweupe kwamba tunafurahia uhusiano wetu tena.”

Naam, uwajibikaji ni wa pande zote—si kuishi tu pamoja bali kujitahidi mkiwa na lengo moja. Hata hivyo, huenda ukahisi kwamba pindi hii ndoa yenu imeunganishwa na wajibu tu. Ikiwa hali yako iko hivyo, usikate tamaa. Huenda ikawa kwamba upendo waweza kurudishwa tena. Vipi?

Kumheshimu Mwenzi Wako wa Ndoa

Biblia yasema hivi: “Acheni ndoa iwe yenye kuheshimika miongoni mwa wote.” (Waebrania 13:4; Waroma 12:10) Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “kuheshimika” limefasiliwa kwingineko katika Biblia kama “-enye kupendwa”, “-enye kustahiwa,” na “-enye thamani.” Ikiwa tunathamini kitu sana huwa tunafanya juhudi kukitunza. Labda umepata kuona jinsi mwanamume mwenye gari jipya lenye gharama sana anavyolitunza. Yeye huliweka gari lake la thamani likiwa safi na katika hali nzuri. Gari hilo likikwaruzwa yeye huhuzunika sana! Watu wengine hutunza afya yao kwa njia iyo hiyo. Kwa nini? Kwa sababu wanapendezwa na hali yao njema, na hivyo wanatunza afya yao.

Tunza na kulinda ndoa yako vivyo hivyo. Biblia husema kwamba upendo “hutumaini mambo yote.” (1 Wakorintho 13:7) Badala ya kulemewa na maoni hasi—labda kwa kukata tamaa na kusema, “Hatukuwa na upendo wa kweli,” “Tulifunga ndoa tukiwa wachanga mno,” au “Hatukujua tulichokuwa tukifanya” —kwa nini usitarajie mema na kujitahidi uwezavyo kuboresha hali, kisha usubiri uone matokeo? “Nimewasikia wateja wangu wengi wakisema, ‘Nimeshindwa kabisa!’” asema mshauri mmoja wa maisha ya ndoa. “Badala ya wao kuchanganua uhusiano wao na kuona sehemu zinazohitaji kuboreshwa, wao huvunjilia mbali ndoa yao haraka-haraka, na kutupilia mbali sifa nzuri wanazoshiriki pamoja, mambo muhimu waliyopata kushiriki pamoja, na matumaini yoyote ya wakati ujao.”

Ni mambo gani umeshiriki pamoja na mwenzi wako? Licha ya matatizo yaliyo katika uhusiano wenu, angalau unaweza kukumbuka pindi zenye furaha, miradi mliyotimiza, na hata magumu mliyokabili mkiwa pamoja. Tafakari mambo hayo, na uonyeshe kwamba unaheshimu ndoa yako na mwenzi wako wa ndoa kwa kujitahidi kwa moyo mweupe kuboresha uhusiano wenu. Biblia huonyesha kwamba Yehova Mungu hupendezwa sana na jinsi wenzi wa ndoa wanavyotendeana. Kwa mfano, katika siku za nabii Malaki, Yehova aliwakemea waume Waisraeli waliowatendea wake zao hiana kwa kuwataliki kwa sababu zisizo na maana. (Malaki 2:13-16) Wakristo wanataka ndoa yao imletee Yehova Mungu heshima.

Ugomvi—Hali Hiyo Ni Mbaya Kadiri Gani?

Sababu kuu ya kuwa na ndoa isiyo na upendo ni kushindwa kwa mume na mke kudhibiti ugomvi. Kwa kuwa hakuna watu wawili wanaofanana kabisa, ndoa zote zitakuwa na pindi za kutoelewana. Lakini wenzi wa ndoa wanaogombana daima hukuta upendo wao umepoa baada ya miaka fulani. Huenda hata wakakata kauli hivi, ‘Sisi hatupatani kwa vyovyote. Daima tunagombana!’

Hata hivyo, ugomvi haupasi kuvunja ndoa. Swali ni, Ugomvi ushughulikiweje? Katika ndoa zenye kufanikiwa, mume na mke wamejifunza kuzungumzia matatizo yao bila kuwa kama wale ambao daktari mmoja aliwaita, “maadui wa karibu sana.”

“Uwezo wa Ulimi”

Je, wewe na mwenzi wako mnajua namna ya kuzungumzia matatizo yenu? Nyote mwapaswa kuwa na nia ya kuzungumzia matatizo pamoja. Kwa kweli, huo ni ustadi—unaoweza kuwa mgumu kujifunza. Kwa nini? Mara kwa mara sote ‘hujikwaa katika neno’ kwa sababu sisi si wakamilifu. (Yakobo 3:2) Isitoshe, watu wengine pia walilelewa na wazazi wenye kufoka kwa hasira kwa ukawaida. Tangu utotoni, kwa njia fulani walilelewa wakijua kwamba kufoka kwa hasira na usemi wenye matusi ni mambo ya kawaida. Mvulana aliyelelewa katika mazingira kama hayo huenda akawa “mtu wa hasira” na “mwenye ghadhabu” anapokuwa mtu mzima. (Mithali 29:22) Vilevile, msichana mwenye malezi kama hayo anaweza kuwa ‘mwanamke mgomvi na mchokozi.’ (Mithali 21:19) Ni vigumu kubatilisha kufikiri na kuchangamana ambako kumekita mizizi. *

Hivyo basi, kudhibiti ugomvi hutaka kujifunza mbinu mpya za kujieleza. Hilo ni jambo zito, kwa sababu mithali moja ya Biblia husema hivi: “Mauti na uzima huwa katika uwezo wa ulimi.” (Mithali 18:21) Naam, huenda likaonwa kuwa jambo ndogo, lakini usemi wako kuelekea mwenzi wako unaweza kuharibu au kuufufua uhusiano wenu. “Kuna anenaye bila kufikiri, kama kuchoma kwa upanga,” yasema mithali nyingine ya Biblia, “bali ulimi wa mwenye haki ni afya.”—Mithali 12:18.

Hata ijapokuwa mwenzi wako ndiye anayeonekana kuwa mwenye makosa kwenye ugomvi huo, fikiria unayosema. Je, maneno yako yanaumiza, au yanatuliza? Je, maneno yako huchochea au hutuliza hasira? “Neno liumizalo huchochea ghadhabu,” yasema Biblia. Kinyume cha hilo, “jawabu la upole hugeuza hasira.” (Mithali 15:1) Maneno yenye kuumiza—hata yakisemwa kwa upole—yatachochea hasira.

Bila shaka, iwapo kuna jambo linalokukera, una haki ya kujieleza. (Mwanzo 21:9-12) Lakini waweza kulieleza bila kejeli, matusi, na madharau. Jiwekee mipaka imara—kuhusu mambo ambayo utaazimia kutomwambia mwenzi wako, kama vile “Nakuchukia” au “Laiti hatungeoana.” Na ingawa mtume Mkristo Paulo hakuwa akizungumzia hususa juu ya ndoa, ni hekima kutohusika katika yale aliyoita “mashindano juu ya maneno” na “mabishano makali sana juu ya mambo madogo-madogo.” * (1 Timotheo 6:4, 5) Ikiwa mwenzi wako hutumia mbinu hizo, usimwige. Kwa kadiri inavyokutegemea wewe, fuatia amani.—Waroma 12:17, 18; Wafilipi 2:14.

Ni kweli kwamba wakati wa ugomvi mkali, ni vigumu kudhibiti usemi. Yakobo, mwandikaji wa Biblia asema kwamba “ulimi ni moto. Hakuna hata mmoja kati ya wanadamu awezaye kuufuga. Ni kitu kisichotawalika chenye ubaya, umejaa sumu yenye kuleta kifo.” (Yakobo 3:6, 8) Basi, utafanyaje hasira inapoanza kupanda? Utazungumzaje na mwenzi wako ili kutuliza ugomvi badala ya kuuchochea?

Kutuliza Ugomvi Mkali

Watu fulani wamegundua wanaweza kutuliza hasira kwa urahisi wakikazia fikira hisia zao na kutatua mambo yanayohusika badala ya kukazia matendo ya mwenzi wao. Kwa mfano, kusema “Mimi nahisi nimeumizwa na mambo uliyosema” kuna matokeo mazuri kuliko kusema “Unaniudhi” au “Unajua hupaswi kusema hivyo.” Bila shaka, unapoeleza hisia zako, sauti yako haipasi kuonyesha uchungu au madharau. Kusudi lako lapasa kuwa kuzungumzia tatizo wala si kushambulia mwenzako.—Mwanzo 27:46–28:1.

Kwa kuongezea, kumbuka nyakati zote kwamba kuna “wakati wa kunyamaza, na wakati wa kunena.” (Mhubiri 3:7) Watu wawili wanaposema wakati uleule, hakuna anayesikiliza, na hakuna manufaa yoyote yanayopatikana. Kwa hiyo, zamu yako ya kusikiliza ikiwadia, uwe “mwepesi sana juu ya kusikia, wa polepole juu ya kusema.” La maana pia, uwe “wa polepole juu ya hasira ya kisasi.” (Yakobo 1:19) Usiweke maanani kila neno la kuudhi asemalo mwenzi wako; wala “usifanye haraka kukasirika rohoni mwako.” (Mhubiri 7:9) Badala yake, jitahidi kufahamu sababu ya yeye kusema hivyo. “Busara ya mtu huiahirisha hasira yake” yasema Biblia, “nayo ni fahari yake kusamehe makosa.” (Mithali 19:11) Busara inaweza kumsaidia mume au mke kutafuta kiini cha ugomvi.

Kwa mfano, mke anapolalamika kwamba mume hapati wakati wa kuwa pamoja naye kwa kawaida halalamiki juu ya wakati tu. Huenda ikawa anahisi hakuna anayemjali au hathaminiwi. Vivyo hivyo, mume anayelalamika kwa kuwa mke alinunua kitu kisichopangiwa huenda asiwe analalamikia matumizi mabaya ya pesa. Bali huenda ikawa analalamika kwamba hakuhusishwa katika uamuzi huo. Mume au mke mwenye busara atachunguza ili kubaini kiini cha tatizo.—Mithali 16:23.

Je, jambo hilo ni gumu sana? Bila shaka! Nyakati fulani, licha ya juhudi zote, maneno makali yatasemwa na hamaki kuwaka. Unapoona dalili hizo, huenda ukahitaji kutumia shauri la Mithali 17:14: “Acheni ugomvi kabla haujafurika.” Afadhali kuahirisha mazungumzo hayo hadi hisia ziwe zimetulia. Ikiwa mmeshindwa kuzungumza kwa utulivu, basi huenda ikafaa kuwe na rafiki mkomavu awasaidie kutatua ugomvi wenu. *

Dumisha Mtazamo Halisi

Usivunjike moyo iwapo maisha yako ya ndoa ni tofauti na ulivyodhani wakati wa uchumba. Kikundi kimoja cha wataalamu chasema hivi: “Kwa watu wengi maisha ya ndoa si raha mstarehe nyakati zote. Kuna pindi ya raha na ya huzuni.”

Naam, maisha ya ndoa huenda yasiwe kama yanavyosimuliwa katika riwaya za mahaba, wala hayapasi kuwa yenye huzuni. Ingawa kutakuwako na pindi zenye magumu baina yako na mwenzi wako, kutakuwako pia na pindi za kusahau matatizo yenu na kufurahia tu kuwa pamoja, kuwa na ushirika wenye uchangamfu, na kuzungumza pamoja kama marafiki. (Waefeso 4:2; Wakolosai 3:13) Pindi kama hizo zinaweza kutumika kuamsha tena upendo uliofifia.

Kumbuka, watu wawili wasio wakamilifu hawawezi kuwa na ndoa kamilifu. Lakini wanaweza kuwa na kadiri fulani ya furaha. Kwa kweli, hata matatizo yakiwepo, uhusiano baina yako na mwenzi wako wa ndoa waweza kuwapa uradhi kikweli. Jambo moja ni hakika: Ikiwa wewe na mwenzi wako wa ndoa mtajitahidi na kuwa tayari kunyumbulika na kutafuta faida ya yule mwingine, kuna matumaini kwamba ndoa yenu yaweza kuokolewa.—1 Wakorintho 10:24.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 22 Malezi si udhuru wa kumfokea mwenzi wako wa ndoa. Hata hivyo, malezi yanatoa sababu kwa nini tabia hiyo imekita mizizi sana na kuwa vigumu kuishinda.

^ fu. 25 Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “mabishano makali sana juu ya mambo madogo-madogo” laweza pia kurejezea “kuudhiana kwa vijambo vidogo.”

^ fu. 31 Mashahidi wa Yehova wana msaada wa wazee wa kutaniko. Na ingawa hawajihusishi na mambo ya kibinafsi ya wenzi waliooana, wazee wanaweza kuwa msaada mkubwa kwa wenzi wenye matatizo.—Yakobo 5:14, 15.

[Blabu katika ukurasa wa 12]

Je, maneno yako yanaumiza, au yanatuliza?

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 10]

TUPA MPIRA KWA UANANA

Biblia yasema hivi: “Acheni tamko lenu liwe na upendezi sikuzote, lenye kukolezwa chumvi, ili kujua jinsi mpaswavyo kumpa jibu kila mmoja.” (Wakolosai 4:6) Bila shaka hilo lafaa katika ndoa! Kwa kielelezo: Katika mchezo wa kutupiana mpira, unatupa mpira kwa njia ambayo mwenzako aweza kuudaka kwa urahisi. Huvurumishi mpira kwa nguvu sana na kumwumiza mwenzio. Tumia kanuni hiyohiyo unapozungumza na mwenzi wako wa ndoa. Kumtupia maneno makali huumiza tu. Badala yake, sema kwa upole—kwa upendezi—ili mwenzi wako aweze kufahamu maoni yako.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 11]

ZUNGUMZIA YALIYOPITA!

Soma barua na kadi za wakati uliopita. Tazama picha. Jiulize, ‘Ni nini kilichonivuta kwa mwenzi wangu? Ni sifa zipi zilizonivutia zaidi? Tulishiriki mambo gani pamoja? Tulifurahishwa na mambo gani?’ Kisha zungumzia mambo hayo yaliyopita pamoja na mwenzi wako wa ndoa. Mazungumzo yenye kuanza na taarifa “Unakumbuka wakati. . . ?” huenda yakatokeza fursa ya kuamsha hisia mlizokuwa nazo wakati uliopita.

[Sanduku katika ukurasa wa 12]

MWENZI MPYA, MATATIZO YALEYALE

Wenzi fulani wa ndoa ambao wamenaswa katika ndoa isiyo na upendo hutamani kuanza upya na mwenzi mpya. Lakini Biblia hulaumu uzinzi, ikisema kwamba mtu anayetenda dhambi hiyo “hana akili kabisa” na kwamba “hujiangamiza yeye mwenyewe.” (Mithali 6:32, BHN) Hatimaye, mzinzi huyo asiyetubu hupoteza kibali cha Mungu—uangamizi ulio mbaya zaidi.—Waebrania 13:4.

Upumbavu wa mwenendo wa uzinzi hudhihirishwa katika njia nyinginezo. Kwanza, mtu huyo mzinzi anayechukua mwenzi mwingine yaelekea atakabili matatizo yaleyale yaliyotatiza ndoa yake ya kwanza. Dakt. Diane Medved, anataja jambo jingine muhimu: Yeye anasema, “Jambo la kwanza ambalo mwenzi wako mpya alijifunza kukuhusu ni kwamba wewe uko tayari kuvunja uaminifu. Yeye anajua kwamba unaweza kumdanganya mtu ambaye umeahidi kuishi naye. Kwamba wewe una tabia ya kujitetea. Kwamba unaweza kukengeushwa na kusahau ahadi yako. Kwamba kutosheleza tamaa zako za mwili au kiburi ni tanzi kwako. . . . Huyu mwenzi mpya ana uhakika gani kwamba hutapendezwa na mtu mwingine na kuondoka tena?”

[Sanduku katika ukurasa wa 14]

HEKIMA KUTOKA MITHALI ZA BIBLIA

Mithali 10:19: “Katika wingi wa maneno hapakosi kuwa na maovu; bali yeye azuiaye midomo yake hufanya akili.”

Unapokuwa na hasira, huenda ukasema mambo usiyokusudia—na kujuta baadaye.

Mithali 15:18: “Mtu wa hasira huchochea ugomvi; bali asiye mwepesi wa hasira hutuliza mashindano.”

Shutuma zenye kuumiza yaelekea zitamfanya mwenzi wako ajitetee, ilhali kusikiliza kwa subira kutawasaidia nyote kutafuta suluhisho.

Mithali 17:27: “Azuiaye maneno yake ni mwenye maarifa; na mwenye roho ya utulivu ana busara.”

Unapohisi hasira yako ikipanda, afadhali kunyamaza ili kuzuia ugomvi mkali.

Mithali 29:11: “Mpumbavu hudhihirisha hasira yake yote; bali mwenye hekima huizuia na kuituliza.”

Kujidhibiti ni kwa maana. Kuropoka kwa hasira maneno yenye kuumiza kutafanya mwenzi wako ajitenge nawe.