Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Vipi Ikiwa Wazazi Wangu Wanafikiri Mimi Ni Mchanga Mno Kuweka Miadi ya Kijinsia?

Vipi Ikiwa Wazazi Wangu Wanafikiri Mimi Ni Mchanga Mno Kuweka Miadi ya Kijinsia?

Vijana Huuliza . . .

Vipi Ikiwa Wazazi Wangu Wanafikiri Mimi Ni Mchanga Mno Kuweka Miadi ya Kijinsia?

“Mama, maoni yako ni ya kikale. Hatuishi katika miaka ya 1950. Kila mtu anaweka miadi ya kijinsia! Mimi si msichana mchanga tena.”—Janie * mwenye umri wa miaka 16.

INAWEZA kutamausha kuambiwa kwamba huko tayari kuweka miadi ya kijinsia. “Nataka kufuata shauri la Biblia na kuwaheshimu baba na mama, lakini naona wamekosea. Naona vigumu kusema nao kuhusu jambo hili,” asema kijana mmoja. Sawa na kijana huyu, huenda ukahisi wazazi wako hawasababu ifaavyo na hawaelewi hisia zako. Labda umekutana na mtu fulani ambaye umempenda sana nawe wataka kufahamiana naye zaidi. Au labda unahisi kwamba kuweka miadi ya kijinsia kutafanya ufaane zaidi na marika zako. “Mkazo upo,” asema Michelle. “Usipoweka miadi ya kijinsia, wanashule wenzako wanakuona kana kwamba una kasoro.”

Mshauri mmoja wa familia alisema hivi kuhusu miadi ya kijinsia: “Hakuna jambo linalowafanya wazazi waonekane kuwa wasiokubali sababu kama hili.” Je, kule kuonekana kwa wazazi wako kuwa wasiokubali sababu, kwamaanisha wako hivyo hasa? Kwa vyovyote, wazazi wako wamepewa na Mungu daraka la kukufundisha, kukuzoeza, kukulinda, na kukupa mwongozo. (Kumbukumbu la Torati 6:6, 7) Je, inawezekana kuwa wazazi wako wana sababu halali za kuhangaikia hali yako? “Naona hatari mbele, na ni yenye kuogofya kweli-kweli,” asema mzazi mmoja. Kwa nini wazazi wengi wanahofia watoto wao kuanza kuweka miadi ya kijinsia wakiwa wangali wachanga?

Hisia Hatari

“Wazazi wangu wanafanya ionekane kana kwamba ni makosa kumpenda mtu fulani,” Beth mwenye umri wa miaka 14 alalamika. Hata hivyo, ikiwa wazazi wako ni Wakristo, wanaelewa vyema kwamba Mungu aliumba watu wa jinsia tofauti wakiwa na uwezo wa kuvutiana. (Mwanzo 2:18-23) Wanaelewa kwamba mvuto huo ni wa asili, na kwamba unapatana na kusudi la Muumba kwa wanadamu la ‘kujaza nchi.’—Mwanzo 1:28.

Zaidi ya hilo, wazazi wako wanafahamu jinsi hisia za ngono zilivyo na nguvu wakati wa “mchanuko wa ujana.” (1 Wakorintho 7:36) Pia wanafahamu kwamba huna uzoefu mkubwa wa kudhibiti hisia hizo. Ikiwa utatumia wakati wako mwingi na mtu wa jinsia tofauti ana kwa ana, kwa simu, au hata kupitia barua au E-mail, bila shaka uvutio utaongezeka. ‘Kuna kosa gani hilo likitukia?’ huenda ukauliza. Una njia gani halali ya kutosheleza hisia hizo? Je, umejiandaa kutosheleza hisia hizo kwa njia ifaayo, yaani katika ndoa? Huenda sivyo.

Hivyo, kuweka miadi ya kijinsia mapema katika maisha ni hatari sana. Biblia huonya hivi: “Je! waweza kuweka moto kifuani na nguo zako zisiungue?” (Mithali 6:27, Biblia Habari Njema) Mara nyingi, kuweka miadi ya kijinsia mapema mno maishani huongoza kwenye ngono ya kabla ya ndoa, uwezekano wa vijana kupata mimba haramu na kupatwa na magonjwa yenye kuambukizwa kingono. (1 Wathesalonike 4:4-6) Kwa mfano, kijana Tammy aliwaona wazazi wake kuwa wenye uonevu walipomkataza kuweka miadi ya kijinsia. Kwa hiyo, akaanza kuweka miadi ya kijinsia kisiri pamoja na mwanashule mwenzake. Punde si punde, Tammy akashika mimba—maisha yake yakabadilika. Sasa yeye anakiri hivi: “Kuweka miadi ya kijinsia si jambo bora kama inavyodaiwa.”

Lakini, vipi vijana wakiamua kuweka mipaka katika uhusiano wao? Licha ya hivyo, bado kuna hatari ya kuamsha hisia za mahaba kabla ya wakati ufaao. (Wimbo Ulio Bora 2:7) Kuamsha hisia ziwezazo kutoshelezwa tu miaka mingi ijayo kwaweza kutamausha na kusononesha.

Mambo mengine ya kutafakari ni: Je, kweli wewe una uzoefu wa kutosha maishani wa kujua unalopaswa kuangalia katika mtu atakayekuwa mwenzi wa ndoa? (Mithali 1:4) Kwa upande mwingine, je, umesitawisha sifa na ujuzi wa kuwa mume au mke wa kupendeka na kustahiwa kikweli? Je, kwa kweli umesitawisha saburi na ujasiri unaohitajika ili kuwa na uhusiano wenye kudumu? Haishangazi kwamba mahusiano mengi ya kimahaba ya vijana hukatika kwa uchungu baada ya muda mfupi tu. Ni nadra mahusiano hayo kuwa ndoa ya kudumu.

Monica mwenye umri wa miaka 18 alieleza hivi kwa ufupi: “Marafiki wangu wote shuleni waliniambia kuhusu uhusiano wao na marafiki wa kiume. Lakini, ama waliolewa wakiwa wachanga mno ama walipata kuumizwa na kuvunjika kwa uhusiano huo kwa sababu hawakuwa tayari kuolewa.” Kijana aitwaye Brandon pia asema hivi: “Inatamausha sana unapong’amua kwamba hauko tayari kufunga ndoa na mtu fulani na unahisi kana kwamba tayari umekwisha ahidi kufanya hivyo kwa sababu unaweka naye miadi ya kijinsia. Unaweza kuvunjaje uhusiano huo bila kumuumiza yule mwingine?”

Kwa hakika, wazazi wako wanajaribu kukulinda usipatwe na maumivu na mtamauko wa jinsi hiyo wanaposisitiza kwamba usiweke miadi ya kijinsia hadi utakapokuwa umekomaa vya kutosha kuchukua wajibu wa ndoa. Kwa kweli, maoni yao yanapatana na shauri lililopuliziwa la Mhubiri 11:10: “Ondoa majonzi moyoni mwako, nawe uuondoe ubaya mwilini mwako.”

‘Kupanuka’

Hilo halimaanishi kwamba huwezi kuchangamana na watu wa jinsia tofauti. Lakini mbona upendezwe na mtu mmoja tu? Kinyume cha hilo, Biblia inatutia moyo ‘tupanuke’ katika mashirika yetu. (2 Wakorintho 6:12, 13) Hilo ni shauri linalofaa vijana. Njia moja ya kutimiza hilo ni kuwa katika vikundi vyenye watu wa jinsia zote mbili. “Nafikiri inaburudisha zaidi,” asema Tammy. “Ni bora kuwa na marafiki wengi.” Monica asema hivi: “Ushirika wa kikundi unafaa sana kwa sababu unapata fursa ya kuwa na watu wenye nyutu tofauti na pia utakuchochea utake kukutana na watu wengi zaidi.”

Wazazi wako huenda pia wakakusaidia kupanga pindi nzuri za kushirikiana na vijana wengine. Anne, mama mwenye watoto wawili, asema hivi: “Sikuzote tunahakikisha kwamba watoto wanafurahia kuwa nyumbani. Huwa tunawaalika marafiki wao na kuwaandalia vyakula vyepesi kisha tunawaacha wacheze. Kwa kufanya hivyo, watoto wetu hawahisi kwamba wanahitaji kwenda kwingineko ili kujifurahisha.”

Bila shaka, hata kwenye kikundi bado unahitaji kuwa mwangalifu kutomwonyesha mtu mmoja upendezi wa pekee. Vijana fulani husababu kwamba kuonyesha mtu wa jinsia tofauti upendezi wa pekee wakiwa kwenye kikundi, haimaanishi wanaweka miadi ya kijinsia. Epuka kujidanganya hivyo. (Zaburi 36:2) Ikiwa kila mara unajikuta na mtu yuleyule wa jinsia tofauti unapokuwa katika kikundi, ni hali moja na kuweka miadi ya kijinsia. * Jaribu kutumia hekima katika uhusiano wako na watu wa jinsia tofauti.—1 Timotheo 5:2.

Manufaa ya Kusubiri

Inaumiza kuambiwa kwamba wewe ni mchanga mno kuweka miadi ya kijinsia. Lakini wazazi wako hawana nia ya kukuumiza. Kinyume cha hilo, wanajaribu wawezavyo kukusaidia na kukulinda. Kwa hiyo, badala ya kuutumainia moyo wako na kuyapa kisogo mashauri yao, kwa nini usinufaike na uzoefu wao? Kwa mfano, kwa nini usiwaombe msaada ukijikuta umekanganywa na mtu wa jinsia tofauti? Mithali 28:26 hutukumbusha hivi: “Mwenye kujitumainia moyo wake ni mjinga.” Kijana aitwaye Connie asema hivi: “Mvulana anapopendezwa nami, mimi huzungumzia jambo hilo na mama yangu ili kukinza mkazo wa kuweka miadi ya kijinsia. Yeye husimulia mambo yaliyowakumba rafiki zake na washiriki wa familia yake hapo awali. Hilo hunisaidia sana.”

Kusubiri kwa muda kabla ya kuweka miadi ya kijinsia hakutazuia ukuzi wako wa kihisia wala kukunyima uhuru. Kwa kuwa huna daraka la uchumba na ndoa linalowakabili watu wazima, una uhuru wa ‘kuufurahia ujana wako.’ (Mhubiri 11:9) Kusubiri kutakupa pia fursa ya kusitawisha utu wako, kukomaa kiakili na jambo la muhimu hata zaidi, kuboresha hali yako ya kiroho. (Maombolezo 3:26, 27) Ni kama alivyosema kijana mmoja Mkristo kwamba, “unahitaji kuwajibika kwa Yehova kwanza kabla ya kuwajibika kwa mtu mwingine yeyote.”

Unapoendelea kukua na ukomavu wako kuonekana wazi kwa kila mtu, wazazi wako watakuwa na maoni tofauti kukuelekea. (1 Timotheo 4:15) Na utakapokuwa tayari kikweli kuweka miadi ya kijinsia, bila shaka utafanya hivyo ukiwa na kibali chao.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Majina yamebadilishwa.

^ fu. 17 Kwa habari zaidi, ona kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, ukurasa wa 232-233, kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

[Picha katika ukurasa 20]

Kutumia wakati wako mwingi na mtu wa jinsia tofauti. . .

. . . kwa kawaida kutaamsha hisia za mahaba

[Picha katika ukurasa 21]

Badala ya kupendezwa na mtu mmoja tu, panuka katika mashirika yako