Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Ndoa Iwe Muungano wa Maisha?

Je, Ndoa Iwe Muungano wa Maisha?

Maoni ya Biblia

Je, Ndoa Iwe Muungano wa Maisha?

HATA kwa nini swali hilo liulizwe? Tukinukuu viapo vya ndoa vya nchi za Magharibi, je, ndoa si “kwa mema au kwa mabaya” na “hadi kifo kitutenganishe”? Naam, mara nyingi viapo vya ndoa husema kwamba bibi na bwana-arusi wanaingia katika kifungo cha uwajibikaji cha maisha. Lakini wengi hawajioni tena kuwa wamefungwa na ahadi hizo zenye uzito. Idadi kubwa ya wenzi wa ndoa wanatengana—wengine baada ya miezi michache, na wengine baada ya miongo mingi. Kwa nini heshima kwa ndoa imedidimia sana? Biblia hutoa jibu.

Tafadhali fungua 2 Timotheo 3:1-3, na ulinganishe andiko hilo na yale unayoona ulimwenguni leo. Kwa sehemu, mistari hiyo yasema hivi: “Katika siku za mwisho nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo zitakuwa hapa. Kwa maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wapenda-fedha, . . . wasio na shukrani, wasio waaminifu-washikamanifu, wasio na shauku ya kiasili, wasiotaka upatano wowote, . . . wasio na hali ya kujidhibiti.” Unabii huu wavutia kwa usahihi wake. Mitazamo hiyo imeharibu na kudhoofisha uhusiano wa ndoa ulimwenguni pote, jambo linalothibitishwa na idadi kubwa sana ya talaka.

Kwa wazi, watu wengi hawaheshimu tena ndoa. Kwa sababu hiyo, twaweza kuuliza hivi: Je, ndoa yapasa kuchukuliwa kwa uzito? Je, kweli ndoa ni takatifu? Wakristo waoneje kifungo cha ndoa? Biblia hutoa msaada gani kwa wenzi wa ndoa leo?

Je, Maoni ya Mungu Yamebadilika?

Mwanzoni, Mungu hakusema kwamba vifungo vya ndoa vilikuwa vya muda tu. Kuwaunganisha mwanamume na mwanamke wa kwanza kwasimuliwa kwenye Mwanzo 2:21-24, na hapo hapataji uchaguzi mwingine wa talaka au mtengano. Badala yake, mstari wa 24 husema: “Mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye ataambatana na mkewe, nao watakuwa mwili mmoja.” Andiko hilo lamaanisha nini?

Hebu fikiria mwili wa binadamu, jinsi ambavyo tishu zilizofumana pamoja bila kushonwa na jinsi mifupa inavyokutana katika viungo imara, bila msuguano. Huo ni Muungano ulioje! Muungano unaodumu kwelikweli! Lakini kunakuwa na maumivu makali kama nini wakati mwili huu usio na kifani unapoumizwa vibaya sana! Kwa hiyo, kwenye Mwanzo 2:24, msemo “mwili mmoja” hukazia ukaribu na kudumu kwa muungano wa ndoa. Pia hutoa onyo lililo wazi la maumivu makali muungano huo unapovunjwa.

Ijapokuwa mielekeo yenye kubadilika katika milenia ambazo zimepita imebadilisha maoni ya wanadamu tena na tena, Mungu angali anaona ndoa kuwa kifungo cha uwajibikaji cha maisha. Yapata miaka 2,400 iliyopita, wanaume fulani Wayahudi walijiamulia kuwaacha wake zao wa kwanza na kuoa wanawake wachanga. Mungu alilaani zoea hilo, akitangaza hivi kupitia nabii wake Malaki: “Jihadharini roho zenu; mtu awaye yote asimtende mke wa ujana wake mambo ya hiana. Maana mimi nakuchukia kuachana [“talaka,” NW], asema BWANA, Mungu wa Israeli.”—Malaki 2:15, 16.

Zaidi ya karne nne baadaye, Yesu alithibitisha tena maoni ya Mungu ya awali kuhusu ndoa aliponukuu Mwanzo 2:24 kisha akaagiza hivi: “Kile ambacho Mungu amefunga nira pamoja msiache mtu yeyote akitenganishe.” (Mathayo 19:5, 6) Miaka kadhaa baadaye, mtume Paulo aliagiza kwamba “mke hapaswi kuondoka kwa mume wake” na kwamba “mume hapaswi kumwacha mke wake.” (1 Wakorintho 7:10, 11) Maandiko haya yanaonyesha kwa usahihi maoni ya Mungu kuhusu ndoa.

Je, Biblia huruhusu kuvunjwa kwa ndoa? Ndiyo, ndoa hukoma mwenzi wa ndoa anapokufa. (1 Wakorintho 7:39) Pia uzinzi waweza kuwa sababu ya kukomesha ndoa, mwenzi asiye na hatia akiamua hivyo. (Mathayo 19:9) La sivyo, Biblia hutia moyo wenzi wa ndoa waendelee kuishi pamoja.

Jinsi ya Kufanya Ndoa Idumu

Mungu anataka ndoa idumu, isiwe mahali pa kuvumiliana tu, bali iwe mwendo wa furaha. Yeye hutaka mume na mke watatue matatizo yao na wafurahi kuwa pamoja. Neno lake hutoa mwongozo wa ndoa yenye furaha, ya kudumu. Tafadhali ona maandiko yafuatayo.

Waefeso 4:26: “Msiache jua litue mkiwa katika hali ya kuchokozeka.” * Mwanamume mmoja mwenye ndoa yenye furaha anaamini kwamba andiko hili humsaidia yeye na mke wake watatue kutoelewana bila kukawia. “Ikiwa huwezi kulala baada ya kutoelewana, mambo hayako sawa. Huwezi kuruhusu tatizo liendelee,” yeye anasema. Nyakati nyingine yeye na mke wake wamezungumzia matatizo yao hadi usiku. Lakini hufanikiwa. Aongeza kusema: “Kutumia kanuni za Biblia kumeleta matokeo mazuri ajabu.” Kwa kufanya hivyo, mwanamume huyo na mke wake wamefurahia maisha ya ndoa yenye furaha kwa miaka 42.

Wakolosai 3:13: “Endeleeni kuchukuliana mtu na mwenzake na kusameheana kwa hiari mtu na mwenzake.” Mume mmoja asimulia jinsi ambavyo yeye na mke wake wamefanya hivyo: “Wenzi wa ndoa wanaweza kuchokozana bila kufanya kosa lolote, kwa kuwa kila mtu ana upungufu na mazoea ambayo huwaudhi watu wengine. Sisi huchukuliana kwa kutoruhusu mambo hayo yatutenganishe.” Bila shaka kufikiri huko kumesaidia wenzi hao wakati wa miaka yao 54 ya ndoa!

Kutumia kanuni hizo za Kimaandiko huimarisha kifungo kinachounganisha waume na wake. Hivyo, ndoa yao yaweza kuwa yenye shangwe, yenye kuridhisha, na ya maisha.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 14 Kulingana na saa za Mashariki ya Kati ya karne ya kwanza, siku huisha jua linaposhuka. Kwa hiyo Paulo alikuwa akiwatia moyo wasomaji wafanye amani na wengine kabla kila siku kwisha.