Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kukabiliana kwa Shangwe na Ulimwengu Wenye Hekaheka

Kukabiliana kwa Shangwe na Ulimwengu Wenye Hekaheka

Kukabiliana kwa Shangwe na Ulimwengu Wenye Hekaheka

Watu Wengi Hukabiliana Na Mikazo Ya Maisha, Lakini Ni Wachache Wanaofanya Hivyo Kwa Shangwe. Hilo Lahitaji Hekima Ya Pekee.

KIKIKIRI ukweli huo, kitabu The 24-Hour Society chasema hivi: “Tunahitaji kusitawisha hekima ya kulinda utu na mahitaji ya binadamu katika ulimwengu wa kitekinolojia tuliobuni.”

Kwa kupendeza, hekima yenye kutumika inapatikana kwa urahisi katika kitabu ambacho kimeenezwa sana ulimwenguni—Neno la Mungu, Biblia. Biblia imepuliziwa na Mtu anayefahamu kikamili mahitaji na utu wa binadamu, ina kanuni ambazo zimetumika kwa mafanikio kwa muda mrefu. Kutumia kanuni hizo kutakusaidia kudhibiti zaidi maisha yako, na utapata pia kiasi fulani cha shangwe unapoendelea kukabiliana na hekaheka za ulimwengu wa leo.—Isaya 48:18; 2 Timotheo 3:16.

Kanuni hizo hutumika katika maeneo matatu. Kwanza, zaonyesha mambo unayopaswa kufanyia marekebisho. Pili, zaweza kukusaidia kuchanganua mambo ya kutangulizwa. Tatu, zinasitawisha mtazamo wa kiroho ulio bora kuliko mtazamo wa kimwili tu kuelekea maisha. Acheni sasa tuchanganue maeneo hayo matatu.

Ishi Maisha Sahili na Yenye Utaratibu

Jiwazie ukienda kupiga kambi kwa siku kadhaa. Kwa sababu unataka kustarehe ifaavyo, unachukua hema kubwa lenye kila aina ya vifaa. Pia kwenye trela ya gari lako unapakia fanicha, vifaa vya jikoni, friji, jenereta ndogo, taa, televisheni na vitu vingine vingi kutia ndani chakula. Hata hivyo, kupanga vitu hivyo vyote kwachukua wakati wako mwingi! Kisha baada ya likizo yako fupi, inakubidi kutumia wakati mwingi tena kuvipakia garini—na kuvipanga tena ufikapo nyumbani. Unapochanganua mambo unagundua kwamba hukuwa na wakati wa kutosha kufurahia kupiga kambi! Unajiuliza kama likizo hiyo ilikuwa na manufaa yoyote.

Kwa mamilioni ya watu leo, maisha yanafanana kwa kiasi fulani na safari hiyo ya kupiga kambi. Wanatumia wakati wao mwingi wakirundika na kudumisha vitu vya kimwili visivyohesabika ambavyo ulimwengu unataka kutusadikisha kwamba ni lazima tuwe navyo ili kuwa na furaha. Kinyume cha hilo, Yesu Kristo alisema hivi: “Hata wakati mtu ana wingi uhai wake hautokani na vitu alivyo navyo.” (Luka 12:15) Naam, ubora wa maisha hautegemei utajiri. Kwa kweli, mali huongeza mikazo na mahangaiko maishani. “Kushiba kwake tajiri hakumwachi kulala usingizi,” lasema andiko la Mhubiri 5:12.

Kwa hiyo, chunguza kwa uangalifu kila kitu ulicho nacho, kisha ujiulize, ‘Je, kitu hiki kinahitajika kikweli au ni mrundamano usiofaa? Je, kinachangia hali njema ya maisha yangu au kinapoteza wakati wangu muhimu?’ Utangulizi wa kitabu Why Am I So Tired?, kilichoandikwa na Leonie McMahon, unasema hivi: “Vifaa vilivyobuniwa kwa madhumuni ya kupunguza kazi za nyumbani, vimemlazimu mke wa nyumbani kutafuta kazi ili kuvinunua na kugharamia kuvirekebisha.”

Unapofanya maisha yako yawe sahili, unakuwa na wakati mwingi na familia yako, rafiki zako na wakati wa kufanya mambo yako ya kibinafsi. Wakati huo ni chanzo muhimu sana cha furaha. Usiwe kamwe miongoni mwa watu wanaotambua kwa kuchelewa mno maishani kwamba rafiki na familia ni wa muhimu zaidi—na wenye kupendeza—kuliko pesa na vitu. Watu tu ndio wanaoweza kukupenda. Ingawa akaunti za benki, hisa, kompyuta, televisheni, na vifaa vingine vina umuhimu wake, vyote hivyo ni sehemu tu ya maisha wala si kiini chake. Watu wanaotanguliza vitu hivyo hudunisha maisha yao na hatimaye wanakosa uradhi au hata kuhuzunika.—1 Timotheo 6:6-10.

Tunza Wakati na Panga Mambo ya Kutangulizwa

Nyakati nyingine kutunza wakati kwalingana na kupanga bajeti. Ikiwa unajaribu kufanya mambo mengi mno katika wakati mchache ulionao, basi huishi kulingana na wakati ulionao. Mtindo huo wa maisha hatimaye hukatisha tamaa, huleta mikazo na uchovu. Hivyo, jifunze kupanga mambo ya kutangulizwa.

Kwanza, changanua mambo muhimu, kisha panga wakati wa kutosha kufanya mambo hayo. Kwa Wakristo, sikuzote mambo ya kiroho hutangulizwa maishani. (Mathayo 6:31-34) Iwapo mambo muhimu yanafanywa mbiombio au kushughulikiwa kijuujuu, matatizo mazito huzuka baadaye. Kwa sababu hiyo, huenda ikakulazimu kuondolea mbali lolote linalochukua wakati na lenye manufaa haba.

Unapopanga mambo ya kutangulizwa, panga pindi fupi za faragha—pindi za kutafakari mambo yenye kujenga na kujiimarisha tena. “Pindi nzuri ya faragha,” lasema jarida la Psychology Today, ni “burudisho muhimu katika ulimwengu wa leo wenye hekaheka chungu nzima. . . . Pindi za faragha humchochea mtu kuishi.” Watu wasio na pindi ya kutafakari huenda wakayaona maisha kivivi hivi.

Kiasi na Hali ya Kiroho

Kiasi na hali ya kiroho ni sifa mbili bora sana katika maisha yenye furaha na usawaziko. Kuwa na kiasi ni muhimu sana kwa kuwa kutakusaidia kuepuka kutwaa kazi au madaraka zaidi ya uwezo wako. Iwapo u mwenye kiasi, utafahamu wakati wa kukataa kazi ya ziada au shughuli nyinginezo zitakazovuruga utendaji mwingine muhimu zaidi. Watu wenye kiasi hawatamani ufanisi au kazi za wengine; wao huelekea kuridhika na walicho nacho. Sifa halisi ya kiasi, pia hudhihirisha hali ya kiroho, ambayo ni ufunguo mwingine muhimu wa kudhibiti maisha yetu zaidi.—Mika 6:8; 1 Yohana 2:15-17.

Hali ya kiroho inayotegemea ujuzi sahihi wa Biblia hukufanya uwe mtambuzi na mwenye busara zaidi—mtu asiyepumbazwa na maoni duni ya kilimwengu juu ya ufanisi. Utazingatia moyoni shauri lenye hekima la 1 Wakorintho 7:31: “[Acheni] wale wanaoutumia ulimwengu [wawe] kama wale wasioutumia kwa ukamili; kwa maana mandhari ya ulimwengu huu inabadilika.” Wakristo ‘hutumia ulimwengu’ wanapokidhi mahitaji yao ya kimwili na ya familia zao, lakini hawaruhusu ulimwengu huu uwameze. Wanafahamu kwamba ulimwengu hauna himaya halisi na kwamba karibuni utatokomea mbali, kwamba ufanisi wa kweli—himaya na uhai udumuo milele katika dunia paradiso—hutegemea msimamo mzuri pamoja na Mungu. (Zaburi 1:1-3; 37:11, 29) Kwa hiyo tii onyo hili la upole la Yesu na uwe na hekima kwa kujiwekea “akiba ya hazina mbinguni, ambako wala nondo wala kutu haili kabisa, na ambako wezi hawavunji na kuiba.”—Mathayo 6:20.

Epuka Mahangaiko na Pata Amani ya Kweli

Mfumo uliopo wa mambo unapokaribia kikomo, bila shaka mikazo na mambo yanayochukua wakati wako yatazidi kuongezeka. Hivyo, ni muhimu kama nini kwamba ujitahidi sana kufuata shauri hili la Biblia: ‘Usihangaikie kitu chochote, bali katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na utoaji-shukrani acha maombi yako ya bidii yajulishwe kwa Mungu; na amani ya Mungu izidiyo fikira yote kwa ubora italinda moyo wako na nguvu zako za akili kwa njia ya Kristo Yesu.’ Mtu yeyote mwenye mtazamo wa kilimwengu, asiyethamini sala hawezi kuwa na amani hiyo.—Wafilipi 4:6, 7.

Isitoshe, Yehova atafanya mengi zaidi ya kukupa amani ya akili. Atakusaidia kubeba mzigo wako wa daraka kila siku ‘ukitupa hangaiko lako lote juu yake.’ (1 Petro 5:7; Zaburi 68:19) Hivyo, ni busara kumsikiliza Mungu kila siku kwa kusoma sehemu fulani ya Neno lake. Je, ni nani awezaye kukupa shauri bora kuliko Muumba wako? (Zaburi 119:99, 100, 105) Naam, mambo yaliyoonwa yanathibitisha kwamba watu wanaomtanguliza Mungu katika maisha yao wanapata msaada wa kukabiliana kwa shangwe na ulimwengu wa leo wenye hekaheka.—Mithali 1:33; 3:5, 6.

[Blabu katika ukurasa wa 11]

Panga mambo ya kutangulizwa, kutia ndani kutimiza uhitaji wako wa faragha na wa mambo ya kiroho

[Picha katika ukurasa 9]

Je, waweza kufanya maisha yako kuwa sahili, yenye taratibu?

[Picha katika ukurasa 10]

Je, unatanguliza watu au mali?