Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Cheche za Mnururisho Suala Linalohangaisha

Cheche za Mnururisho Suala Linalohangaisha

Cheche za Mnururisho Suala Linalohangaisha

BAADA ya majaribio ya silaha za nyuklia katika miaka ya 1950, strontium 90 (Sr90), cheche inayotokana na umenyukaji wa nyuklia, iligunduliwa katika meno ya watoto, laripoti gazeti la Globe and Mail la Kanada. Wakati huo, ilionwa kuwa kisababishi cha kansa katika watoto.

Sasa, miongo mingi baadaye, wanasayansi wanaohusika na Mradi wa Marekani wa Mnururisho na Afya ya Umma wanahangaishwa na suala hilo tena. Dakt. Janet Sherman, mtaalamu wa tiba ya sehemu za ndani za mwili anayeshiriki kwenye mradi huo, aeleza kwamba “viwango vya Sr90 katika meno ya watoto waliozaliwa tangu mwaka wa 1990 vinalingana na viwango vilivyokuwapo wakati ambapo silaha za nyuklia zilikuwa zikijaribiwa hewani.”

Cheche ya Sr90 inatoka wapi? Baadhi ya wanasayansi wanalaumu milipuko ya nyuklia ya wakati uliopita, minururisho kutoka kwa viwanda vya nyuklia vinavyofanya kazi, au majaribio ya mabomu yaliyofanywa miaka mingi iliyopita kuwa visababishi vya cheche hizo. * Haidhuru chanzo chake, wanadamu hupata Sr90 kwa kula mimea iliyotiwa sumu na kunywa maziwa ya ng’ombe ambao wamekula nyasi yenye sumu. Kwa kuwa Sr90 ina dutu sawa na kalisi, mwili wa mwanadamu huhifadhi cheche hizo nururishi mifupani, na hivyo hukabili hatari kubwa ya kuugua kansa ya mifupa na kansa ya damu.

Gazeti la Globe lahangaikia pia hatari ya mnururisho kwa vizazi vijavyo. Gazeti hilo laeleza kwamba “[mabaki ya nyuklia] yanapoondolewa kwenye kimenyushaji, huwa na mnururisho unaozidi ule wa mwanzoni kwa takriban mara milioni moja. Mabaki ya fueli iliyotumiwa karibuni huwa hatari sana hivi kwamba mtu anayesimama umbali wa meta moja tu aweza kufa kutokana na sumu ya mnururisho baada ya muda wa saa moja.”

Kwa kuwa tisho la cheche za mnururisho linawakabili wanadamu, je, ni jambo la akili kutarajia wakati ujao salama? Dunia na viumbe waliomo walipoumbwa, Biblia hutuambia kwamba kila kitu kilikuwa “chema sana.” (Mwanzo 1:31) Tunaweza kuwa na uhakika kwa ahadi ya Biblia ya kwamba hivi karibuni sayari yetu itakuwa paradiso. Chakula na maji yaliyochafuliwa na mnururisho hayatakuwapo tena.—Zaburi 65:9-13; Ufunuo 21:1-4.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Baada ya mlipuko wa mtambo wa nguvu za nyuklia huko Chernobyl, Ukrainia mnamo mwaka wa 1986, viwango vya Sr90 katika meno ya watoto wachanga nchini Ujerumani viliongezeka mara kumi.

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 31]

Picha: U. S. Department of Energy photograph