Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Ponografia Kwenye Internet Nilipopokea toleo la Juni 8, 2000, lenye mfululizo “Ponografia Kwenye Internet—Yaweza Kuleta Madhara Gani?” Lo, niliguswa moyo sana! Mwezi mmoja hivi mapema, nilimfumania mume wangu akitazama ponografia kwenye kompyuta, alikuwa ameweka programu hiyo siku hiyohiyo. Nilifungua mlango ghafula na kumkuta akitazama picha chafu. Ni vigumu kueleza jinsi jambo hilo lilivyoathiri uhusiano wetu. Anasema anajuta, lakini amedhalilisha ndoa yetu.

L. K., Marekani

Ningependa kushukuru kwa ajili ya makala hizo. Nimekuwa nikipambana na tatizo la kutazama ponografia kwa muda unaokaribia miaka minane. Hivi majuzi nilisali na kuazimia kuacha uraibu wangu wa kutazama ponografia. Siku hiyohiyo nilipokea makala hizo.

L. M., Marekani

Miezi michache iliyopita, nilifungua bila kutaka kituo chenye ponografia kwenye Internet. Nilianza kufungua kwa ukawaida vituo vingine vichafu zaidi katika Internet. Tokeo ni kwamba nimepoteza furaha na hamu ya mambo ya kiroho huku nikijitenga na wengine. Ni rahisi sana kuwa mraibu wa kutazama picha hizo. Lakini sasa nitafanya kila niwezalo kuacha uraibu huo.

M. G., Marekani

Tai Ningependa kushukuru sana kwa ajili ya makala yenye kusisimua ya “Tai za Zamani na za Sasa.” (Juni 8, 2000) Mimi ni mama mwenye watoto watatu na ninawafunza kumpenda Yehova. Kijana wangu mkubwa ana umri wa miaka 13, na sote hatukujua kufunga tai ili aweze kutoa hotuba yake kwenye Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Mume wangu ambaye si mwamini, hajawahi kuvaa tai. Asanteni sana kwa kutufunza kufunga tai kwa njia sahili.

M. B., Marekani

Nina umri wa miaka 11 na ingawa huenda ikashangaza, picha hizo zilinifunza jinsi ya kufunga tai. Sasa naweza kuvaa tai zangu zote!

A. P., Italia

Mageuzi Mambo fulani yenye kuzuia mjadala mnyoofu kuhusu mageuzi yalidokezwa katika makala, “Je, Mageuzi Hupatana na Akili?” (Juni 8, 2000) Mwasema hivi: “Je, haishangazi kwamba buibui amebuni mbinu ya utengenezaji bidhaa iliyo tata zaidi kwa mwanadamu kuweza kuelewa?” Hilo si jambo la kushangaza kwa kuwa wanasayansi hawajui kila jambo.

C. W., Australia

Namna buibui anavyotengeneza hariri inahusisha mbinu tata sana ambazo wanasayansi wameshindwa kuzifahamu hata baada ya kufanya uchunguzi kwa miongo mingi. Licha ya hayo, wanasayansi wanaendelea kusisitiza kwa kiburi kwamba yote hayo yalitokana na mageuzi. Tunaamini kwamba jambo hilo na mifano mingine kama hiyo hudhihirisha kimsingi kuwa fundisho la mageuzi halipatani na akili na huonyesha kwamba itikadi katika nadharia hiyo inapatana zaidi na imani isiyo na msingi kuliko sayansi.—Mhariri.

Sijawahi kamwe kusoma hoja yenye nguvu ambayo daima nimehisi kwamba inapinga vikali mageuzi kama hoja hii: Wazazi wetu wa kale (haidhuru wengine wanafikiri walikuwa nani) waliwezaje kujigawanya kwa jinsia mbili tofauti? Kusema kwamba kujigawanya huko kulitukia kwa muda wa mamilioni ya miaka hakutoi kabisa jibu kwa sababu wa kike hapati mimba hatua kwa hatua.

H. R., Marekani

Msomaji wetu atoa hoja sahihi ambayo tulizungumzia kwenye makala, “Je, Msingi wa Mageuzi Wakosekana?” katika toleo letu la Mei 8, 1997. Tuliandika hivi: “Tunatazamiwa kuamini kwamba kwa nasibu mageuzi pia yalitokeza wa kiume na wa kike kwa wakati uleule ili spishi mpya iendelezwe. Na kufanya jambo hilo hata lisiwezekane zaidi, ni lazima pia tuamini kwamba wa kiume na wa kike hawakupitia mageuzi wakati uleule tu bali pia mahali palepale! Kama hawangekuja pamoja basi kuzaana hakungekuwapo!”—Mhariri.