Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Tuhudhurie Mikutano ya Kikristo?

Je, Tuhudhurie Mikutano ya Kikristo?

Maoni ya Biblia

Je, Tuhudhurie Mikutano ya Kikristo?

“NILIKUWA nikienda kanisani, lakini sasa siendi.” “Nafikiri unaweza kumwabudu Mungu popote pale, si kanisani tu.” “Namwamini Mungu na Biblia, lakini siamini kwamba ni lazima niende kanisani.” Je, umewahi kusikia maelezo kama hayo? Watu wengi sana leo husema hivyo, hasa katika nchi za Magharibi. Watu waliokuwa na zoea la kwenda kanisani sasa hawafikiri kwamba ni jambo la lazima. Biblia inasema nini kuhusu kwenda kanisani?

Maneno “kanisa” na “makanisa” yameandikwa zaidi ya mara 110 katika Biblia ya King James Version. Tafsiri nyingine pia hutumia maneno hayo. Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “kanisa” humaanisha kihalisi “mwito,” au, kwa maneno mengine, mkusanyiko wa watu. Kwa mfano, Matendo 7:38, katika Biblia ya Union Version, yasema kwamba Musa alikuwa “katika kanisa jangwani,” yaani, miongoni mwa mkusanyiko wa taifa la Israeli. Katika sehemu nyingine Maandiko yanasema kwamba ‘kulitukia adha kuu ya kanisa,” yakirejezea jamii ya Wakristo katika Yerusalemu. (Matendo 8:1, UV) Katika mojawapo ya barua zake, Paulo asalimu “kanisa lililo katika nyumba [ya Filemoni],” kutaniko lililokutanikia humo.—Filemoni 2, UV.

Ni dhahiri kwamba neno “kanisa” kama litumiwavyo kwenye Biblia halirejezei mahali pa ibada, bali kikundi cha waabudu. Akikiri hilo, Clement wa Alexandria, mwalimu wa dini wa karne ya pili, aliandika hivi: “Kanisa ni kutaniko la wateule wala si mahali pao.” Lakini, je, ni lazima Wakristo wakutanikie mahali au kwenye jengo hususa ili ibada yao ikubaliwe na Mungu?

Ibada Katika Taifa la Israeli

Sheria ya Musa iliamuru kwamba wanaume wote Wayahudi wahudhurie misherehekeo mitatu ya kila mwaka mahali fulani hususa. Wanawake wengi na watoto walihudhuria pia. (Kumbukumbu la Torati 16:16; Luka 2:41-44) Kwenye pindi fulani makuhani na Walawi walifundisha umati uliokusanyika, na kusoma Sheria ya Mungu. ‘Walieleza maana yake, na watu wakafahamu yaliyosomwa.’ (Nehemia 8:8) Katika miaka ya Sabato, Mungu aliagiza hivi: “Wakusanye watu, wanaume na wanawake na watoto, na mgeni wako aliyemo malangoni mwako wapate kusikia na kujifunza, na kumcha BWANA, Mungu wenu, na kuangalia kutenda maneno yote ya torati hii.”—Kumbukumbu la Torati 31:12.

Mtu angeweza tu kumtolea Mungu dhabihu na kupokea maagizo kutoka kwa makuhani kwenye hekalu huko Yerusalemu. (Kumbukumbu la Torati 12:5-7; 2 Mambo ya Nyakati 7:12) Baada ya muda, majengo mengine ya ibada yalijengwa katika Israeli—Masinagogi. Yalitumiwa kwa ajili ya usomaji wa Maandiko na sala. Hata hivyo, hekalu lililokuwa Yerusalemu lilikuwa kitovu cha ibada. Hilo lathibitishwa na yale yanayoripotiwa na mwandikaji wa Biblia aitwaye Luka. Anamtaja mwanamke mkongwe aitwaye Anna, ambaye “alikuwa hakosi kamwe kuwa katika hekalu, akitoa utumishi mtakatifu usiku na mchana kwa mifungo na dua.” (Luka 2:36, 37) Jambo muhimu maishani mwa Anna lilikuwa kutoa ibada ya kweli pamoja na waabudu wengine. Wayahudi wengine wacha-Mungu waliishi vivyo hivyo.

Ibada ya Kweli Baada ya Kifo cha Kristo

Baada ya kifo cha Yesu, wafuasi wake hawakuwa tena chini ya Sheria ya Musa, wala hawakuhitajiwa kuabudu hekaluni. (Wagalatia 3:23-25) Lakini bado waliendelea kukutana ili kusali na kujifunza Neno la Mungu. Hawakuwa na majengo ya kifahari, badala yake walikutanikia kwenye nyumba za kibinafsi na sehemu za umma. (Matendo 2:1, 2; 12:12; 19:9; Waroma 16:4, 5) Mikutano hiyo ya Kikristo ya karne ya kwanza haikuwa na mambo ya kidesturi wala majisifu, ilikuwa sahili na yenye kupendeza.

Licha ya hali mbaya za kiadili katika Milki ya Roma, kanuni za Biblia zilizofundishwa kwenye mikutano hiyo zilikuwa zenye kutokeza sana. Watu fulani waliohudhuria kwa mara ya kwanza waliweza tu kusema hivi kwa mshangao: “Mungu kwa kweli yumo miongoni mwenu.” (1 Wakorintho 14:24, 25) Naam, Mungu alikuwa kwelikweli miongoni mwao. “Kwa hiyo, kwa kweli, makutaniko [“makanisa,” UV] yakaendelea kufanywa imara katika imani na kuongezeka idadi siku baada ya siku.”—Matendo 16:5.

Je, Mkristo wa wakati huo angeweza kupata kibali cha Mungu kwa kuabudu katika mahekalu ya kipagani au kuabudu akiwa peke yake? Biblia inatoa mwongozo dhahiri kuhusu jambo hilo: Waabudu wenye kibali cha Mungu walihitaji kuwa sehemu ya kanisa pekee la kweli, au kutaniko, “mwili mmoja” wa waabudu wa kweli. Hao walikuwa wanafunzi wa Yesu, walioitwa Wakristo.—Waefeso 4:4, 5; Matendo 11:26.

Vipi Leo?

Badala ya kutuhimiza tuabudu kanisani, Biblia hutuhimiza tuabudu na kanisa, “kutaniko la Mungu aliye hai,” yaani, watu ambao ‘wanaabudu kwa roho na kweli.’ (1 Timotheo 3:15; Yohana 4:24) Mikutano ya kidini inayokubaliwa na Mungu ni sharti ifundishe watu “matendo matakatifu ya mwenendo na vitendo vya ujitoaji-kimungu.” (2 Petro 3:11) Inahitaji kuwasaidia wahudhuriaji wawe Wakristo wakomavu, ambao wanaweza “kutofautisha lililo sahihi na lililo kosa pia.”—Waebrania 5:14.

Mashahidi wa Yehova hujitahidi kufuata kielelezo cha Wakristo wa karne ya kwanza. Makutaniko zaidi ya 91,400 ulimwenguni pote hukutanika kwa ukawaida katika Majumba ya Ufalme, nyumba za kibinafsi, na sehemu nyinginezo ili kujifunza Biblia na kuhimizana. Hilo lapatana na maneno ya mtume Paulo: “Acheni tufikiriane ili kuchocheana kwenye upendo na kazi zilizo bora, si kuachilia mbali kukusanyika pamoja sisi wenyewe.”—Waebrania 10:24, 25.