Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Naweza Kumkataaje?

Naweza Kumkataaje?

Vijana Huuliza . . .

Naweza Kumkataaje?

“Kiangazi hiki ndugu mmoja katika kutaniko letu alinipenda sana. Kwa kweli sikuwa nimempenda vile. Tatizo ni kwamba, sikujua jinsi ya kumkataa bila kumuumiza hisia zake.”—Elizabeth. *

“JE, TWAWEZA kufahamiana vizuri zaidi?” Je, mwanamume kijana amepata kukuuliza swali hilo? Ukiwa mwanamke kijana, * huenda ikawa ulifurahi na kupendezwa sana—hata ukasisimuka! Kwa upande mwingine, huenda ikawa ulivurugika hivi kwamba hukujua la kusema.

Mtu anapoonyesha kupendezwa nawe kimahaba, inaweza kutokeza vurugu ya hisia mbalimbali. Ni kweli hasa ikiwa una umri mkubwa wa kutosha kuoa au kuolewa na hivyo uko tayari kwa uhusiano huo! * Hata hivyo, jinsi utakavyoitikia itategemea kwa kadiri kubwa yule anayekuuliza swali hilo. Ikiwa ni mtu aliyekomaa kihisia-moyo na unavutiwa naye, huenda jibu lako likawa rahisi. Lakini vipi ikiwa kwa wazi hana sifa zinazomfanya awe mwenzi anayefaa? Au vipi ikiwa zijapokuwa sifa zake nzuri, hupendezwi naye kimahaba?

Pia, fikiria hali ya mwanamke kijana ambaye amekuwa akiweka miadi ya kijinsia na mtu kwa muda fulani lakini amekuja kutambua kwamba hataki kuishi maisha yake yote na mtu huyo. Badala ya kuvunja uhusiano huo, anaendelea kufanya urafiki naye. “Naweza kumkataaje?” auliza.

Unapokosa Kupendezwa na Mtu Kimahaba

Huko nyuma nyakati za wazee wa ukoo wa kale, yamkini watu walioa na kuolewa na watu ambao wazazi wao waliwachagulia. (Mwanzo 24:2-4, 8) Katika nchi za Magharibi, Wakristo wengi wako huru kuchagua mwenzi wao wa ndoa. Biblia ina sharti moja—kwamba Mkristo aolewe “katika Bwana tu.”—1 Wakorintho 7:39.

Je, hilo lamaanisha kwamba wapaswa kuolewa na mwamini yeyote anayependezwa nawe kimahaba au ambaye umeweka miadi ya kijinsia naye kwa muda mfupi? Fikiria mfano wa Biblia wa msichana wa mashambani kutoka kijiji cha Mashariki ya Kati cha Shunemu. Solomoni, mfalme wake, alimwona naye akampenda sana. Hata hivyo, alipojaribu kufuatilia urafiki naye, msichana huyo hakumkataa tu bali pia aliwasihi wanawake wa makazi ya kifalme hivi: “Msiyachochee mapenzi, wala kuyaamsha, hata yatakapoona vema yenyewe.” (Wimbo Ulio Bora 2:7) Msichana huyo mwenye hekima hakutaka wengine wajaribu kumkaza afanye maamuzi kwa sababu ya hisia tu. Hakupendezwa kimahaba hata kidogo na Solomoni, kwa kuwa alikuwa anampenda sana mchungaji wa hali ya chini.

Hilo lafundisha somo la maana kwa wale wanaofikiria ndoa leo: Huwezi kuwa na upendo wa kimahaba kwa mtu yeyote tu. Kwa hiyo hata baada ya kuweka miadi ya kijinsia na mtu mwingine kwa muda fulani, mwanamke kijana huenda akaona kwamba hapendezwi naye kimahaba. Labda anahisi hivyo kwa kuwa anaona udhaifu fulani katika utu wa mtu huyo. Au labda havutiwi naye. Lingekuwa jambo la upumbavu kupuuza hisia hizo. Kuzipuuza tu huenda kusizifanye ziishe. * “Nilikuwa na mashaka sana akilini mwangu kumhusu,” asema Tamara kuhusu mwanamume kijana aliyekuwa rafiki yake. “Si mashaka madogo tu bali mashaka ambayo yalinisumbua sana kufikia kuhisi nimekazwa na kuwa mwenye wasiwasi nilipokuwa naye.” Baadaye alitambua kuwa kwa sababu ya mashaka hayo, ilikuwa afadhali avunje uhusiano huo.

Sababu Inayofanya Iwe Vigumu Kumkataa

Hata hivyo, kumkataa mwanamume kijana kwaweza kuwa jambo gumu sana. Kama Elizabeth, aliyetajwa mwanzoni, huenda ukaogopa kumwumiza. Twapaswa kuwa wepesi kujali hisia za wengine. Biblia hutia moyo Wakristo ‘wajivike shauku nyororo za huruma’ na wawatendee wengine kama vile ambavyo wangependa kutendewa. (Wakolosai 3:12; Mathayo 7:12) Ingawa hivyo, je, hilo lamaanisha kwamba uendelee kujifanya unapendezwa naye ili usimtamaushe au kumwumiza huyu mwanamume kijana? Bila shaka hatimaye atapata kujua jinsi unavyohisi, na ukikosa kuwa mnyofu na kuahirisha kumjulisha jinsi unavyohisi, utakuwa unaongezea uchungu tu. Jambo baya zaidi lingekuwa kuolewa na huyo mwanamume kijana kwa sababu tu unamhurumia. Huruma si msingi mzuri wa kuanzishia ndoa.

Ingawa hivyo, labda, unasumbuliwa na wazo la kwamba, ‘Nisipoolewa naye, huenda nisipate mwingine.’ Kama makala moja katika gazeti Teen inavyosema, huenda msichana akasababu hivi: “Si ‘yule niliyetaka,’ lakini angalau nimepata mtu wa kunioa—na kwa hakika sitaki kuwa peke yangu.” Kwa wazi, kutamani mwandamani ni jambo lenye uvutano mkubwa. Hata hivyo, tamaa hiyo haitimizwi tu kwa kufunga ndoa na mtu yeyote. Hutia ndani kupata mtu ambaye unaweza kumpenda kikweli na ambaye ana uwezo wa kutimiza madaraka ya Kimaandiko kuhusu ndoa. (Waefeso 5:33) Kwa hiyo usiwe na haraka ya kuamua! Wengi wamekuja kujuta kuolewa haraka haraka.

Mwishowe, huenda wengine wakaendelea kuweka miadi ya kijinsia hata kama ni wazi kwamba tabia ya huyo mwanamume kijana ina kasoro kubwa. ‘Nikimpa wakati zaidi, huenda akabadilika,’ ndivyo wanavyosababu. Je, kweli huko ni kusababu kuzuri? Isitoshe, tabia mbaya na mwenendo usiofaa mara nyingi huwa umeimarika na ni mgumu sana kubadili. Na hata akifanya mabadiliko ya ghafula na makubwa, je, kweli waweza kuwa na uhakika kwamba mabadiliko hayo ni ya daima? Akiwa katika hali hiyo mwanamke kijana aitwaye Karen aliamua kwa hekima kuvunja uhusiano wa kimahaba na mwanamume mmoja kijana alipotambua kwamba hawakuwa na miradi iliyolingana. “Lilikuwa jambo gumu,” akubali, “kwa kuwa nilivutiwa naye. Lakini nilijua kwamba ilikuwa muhimu kufanya hivyo.”

Shughulikia Hali Hiyo kwa Uangalifu

Kwa wazi, kumkataa mtu si jambo rahisi. Kama kifurushi chenye chombo dhaifu ndani yake, hali hiyo yapasa kushughulikiwa kwa uangalifu. Yafuatayo ni madokezo machache ambayo huenda yakakusaidia.

Zungumzia jambo hilo na wazazi wako au mtu mwingine mkomavu kutanikoni. Huenda wakaweza kukusaidia uone kama matazamio yako labda si halisi.

Sema kwa njia inayoeleweka na iliyo wazi. Usimwache na mashaka akilini mwake kuhusu hisia zako. Kusema tu, “La” kutavunja moyo wanaotaka kutafuta uchumba. Ikiwezekana, eleza kukataa kwako katika maneno imara kama vile, “Nasikitika, sipendezwi.” Uwe mwangalifu usitoe wazo la kwamba huenda ukabadili maoni yako akisisitiza kidogo. Kumweleza wazi kwamba huvutiwi naye kimahaba hakupaswi kumfanya achanganyikiwe kimawazo bali kwapaswa kumfanya ashinde kwa urahisi mtamauko huo.

Tumia unyofu na busara. Mithali 12:18 husema: “Kuna anenaye bila kufikiri, kama kuchoma kwa upanga.” Ijapokuwa ni jambo la maana kusema waziwazi, Biblia husema kwamba usemi wetu lazima ‘upendeze, ukolezwe chumvi.’—Wakolosai 4:6.

Shikilia uamuzi wako. Marafiki wenye kukutakia mema, ambao yaelekea hawajui sana sababu zilizokufanya ufanye uamuzi wako, wanaweza kukukaza ufikirie kurudia uhusiano wenu. Lakini mwishowe ni wewe utakayepatwa na matokeo ya uamuzi wako—si marafiki wako wenye kukutakia mema.

Tenda kupatana na maneno yako. Hapo awali nyote wawili mlikuwa marafiki sana, na ni jambo la kawaida kutamani kwamba mwendelee kuwa marafiki. Lakini kwa kawaida hilo si jambo linalofaa wala linalowezekana. Hisia zake kwako zimekuwa za kimahaba. Je, inawezekana kufikiri kwamba anaweza tu kupuuza hisia hizo kisha asingizie hakuna jambo ambalo limetokea? Kwa hiyo ijapokuwa ni wazi kwamba ni vizuri mchangamkiane, kuongea kupitia simu kwa ukawaida au kuwa pamoja kwa muda mrefu katika hali za kirafiki yamkini kutaongeza maumivu yake. Hilo lingeweza kuwa kuchezea hisia zake, na hilo halitakuwa jambo la fadhili kwako kufanya.

Mtume Paulo alisihi Wakristo ‘waseme kweli’ mmoja na mwenzake. (Waefeso 4:25) Huenda likawa jambo gumu kufanya hivyo, lakini huenda ikawasaidia nyinyi nyote kuendelea na maisha yenu.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Baadhi ya majina yamebadilishwa.

^ fu. 4 Ijapokuwa makala hii inaelekezewa wanawake vijana, kanuni hizohizo zatumika kwa wanaume vijana pia.

^ fu. 5 Hatari za kuweka miadi ya kijinsia ukiwa mchanga mno zilizungumziwa katika toleo letu la Januari 22, 2001.

^ fu. 10 Ona makala “Vijana Huuliza . . . Je! Inatupasa Tuvunje Uhusiano?” inayopatikana katika toleo la Amkeni! Septemba 8, 1989.

[Picha katika ukurasa wa 13]

Huwezi kuwa na upendo wa kimahaba kwa mtu yeyote tu

[Picha katika ukurasa wa 14]

Sema kwa njia inayoeleweka na iliyo wazi unapoelezea hisia zako