Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Shabaha ya Mashambulizi ya Sovieti

Shabaha ya Mashambulizi ya Sovieti

Shabaha ya Mashambulizi ya Sovieti

LICHA ya maelewano yaliyokuwapo kati ya serikali na Kanisa Othodoksi la Urusi ili kushinda Vita ya Ulimwengu ya Pili, Muungano wa Sovieti uliendelea kukandamiza shughuli za kanisa. Kwa hiyo, kama vile kitabu The Sword and the Shield, kilichoandikwa mwaka wa 1999 chenye historia ya KGB (Halmashauri ya Usalama wa Kitaifa ya Sovieti), kilivyosema, “shirika la KGB lilihangaishwa hasa na shughuli za ‘uchochezi’ za Wakristo ambao halikuweza kuwadhibiti moja kwa moja.” Ni dini zipi hizo?

Dini kubwa zaidi ilikuwa Kanisa Katoliki la Ugiriki la Ukrainia, ambalo sasa laitwa Kanisa Katoliki la Ukrainia. Lilikuwa na wafuasi wapatao 4,000,000. Kulingana na kichapo The Sword and the Shield, “maaskofu wanane kati ya maaskofu wake kumi, na maelfu ya makasisi na waumini, walikufa katika kambi za kazi ngumu huko Siberia kwa sababu ya imani yao.” Shirika la KGB lilichukia pia makanisa ya Kiprotestanti yasiyosajiliwa, ambayo pia hayakudhibitiwa na Serikali. Mwishoni mwa miaka ya 1950, shirika la KGB lilikadiria kwamba vikundi hivyo vya Kiprotestanti vilikuwa na jumla ya washiriki 100,000.

Shirika la KGB liliwaona Mashahidi wa Yehova kuwa kikundi cha Kiprotestanti, kilichokadiriwa kuwa na washiriki wapatao 20,000 katika Muungano wa Sovieti mnamo mwaka wa 1968. Mashahidi walikuwa wachache sana mwanzoni mwa Vita ya Ulimwengu ya Pili mwaka wa 1939. Hawakujulikana sana. Lakini hali ilibadilika sana wakati maelfu ya Mashahidi walipotokea ghafula katika Muungano wa Sovieti. Hilo lilitukiaje?

Mwanzo wa Ongezeko Kubwa

Walter Kolarz ataja sababu mbili za ongezeko hilo kubwa katika kitabu chake Religion in the Soviet Union, kilichochapishwa mwaka wa 1961. Alisema sababu moja ni kwamba “maeneo yaliyotwaliwa na Muungano wa Sovieti mwaka wa 1939-1940”—Latvia, Lithuania, Estonia, na Moldavia—yalikuwa na “vikundi [vingi] vyenye bidii vya Mashahidi wa Yehova.” Isitoshe, Muungano wa Sovieti ulitwaa maeneo fulani mashariki mwa Poland na Chekoslovakia, yaliyokuwa na Mashahidi zaidi ya elfu moja, na kuyafanya kuwa sehemu ya Ukrainia. Kwa hivyo, Mashahidi hao wote walihamishwa ghafula hadi kwenye Muungano wa Sovieti.

Jambo jingine lililochangia ongezeko zaidi, “amini usiamini,” akaandika Kolarz, lilikuwa “kambi za mateso za Ujerumani.” Wanazi waliwatia gerezani maelfu ya Mashahidi kwa sababu ya kukataa kumwunga mkono Hitler na harakati zake za vita. Kolarz alieleza kwamba wafungwa Warusi waliokuwa kwenye kambi hizo “walivutiwa na ujasiri na ushikamanifu wa ‘Mashahidi’ na huenda hilo liliwafanya wapendezwe na mafundisho yao.” Tokeo ni kwamba vijana wengi Warusi waliokuwa kwenye kambi hizo walirejea kwenye Muungano wa Sovieti wakiwa wamemwamini Yehova Mungu na makusudi yake mazuri kwa dunia.—Zaburi 37:29; Ufunuo 21:3, 4.

Sababu hizo zilichangia kuongezeka kasi kwa maelfu ya Mashahidi katika Muungano wa Sovieti. Kufikia mapema mwaka wa 1946, kulikuwa na Mashahidi wapatao 1,600, nao walizidi 8,000 mwishoni mwa miaka ya 1940. Wapelelezi wa KGB walihofia ongezeko hilo, na kama ilivyotajwa awali, walihangaishwa hasa na “shughuli za Wakristo ambao hawakuwa chini ya udhibiti wao.”

Mashambulizi Yaanzishwa

Punde si punde serikali ya Sovieti ilianza kuwashambulia Mashahidi waliokuwa wakihubiri kwa bidii katika Muungano wa Sovieti. Huko Estonia mashambulizi yalianza mwezi wa Agosti mwaka wa 1948 wakati wasimamizi watano wa kazi hiyo walipokamatwa na kufungwa gerezani. “Muda si muda ikawa dhahiri kwamba wapelelezi wa KGB walinuia kuwakamata Mashahidi wote,” akasema Lembit Toom, Shahidi wa Estonia. Mashahidi wote katika Muungano wa Sovieti walikabili hali hiyohiyo.

Viongozi wa Sovieti waliwataja Mashahidi kuwa wahalifu wabaya sana na kwamba wao ni tisho kwa Serikali ya Sovieti isiyoamini kuwapo kwa Mungu. Kwa hiyo, walisakwa kila mahali, wakakamatwa, na kufungwa gerezani. Kichapo The Sword and the Shield kilisema hivi: “Wasiwasi mkubwa ambao maofisa wakuu wa KGB walikuwa nao kuelekea Mashahidi wa Yehova unaonyesha waziwazi jinsi walivyowachukia watu waliokuwa na maoni tofauti.”

Wasiwasi wao ulidhihirishwa wakati waliposhambulia Mashahidi mnamo mwezi wa Aprili 1951. Miaka miwili tu iliyopita, mnamo mwaka wa 1999, Profesa Sergei Ivanenko, msomi Mrusi anayeheshimiwa, alisema katika kitabu chake The People Who Are Never Without Their Bibles kwamba mapema mwezi wa Aprili 1951, “familia zaidi ya 5,000 za Mashahidi wa Yehova kutoka jamhuri za Sovieti za Ukrainia, Belorusia, Moldavia, na Baltiki zilihamishwa hadi ‘makao ya kudumu’ huko Siberia, Mashariki ya Mbali, na Kazakhstan.”

Tukio Linalostahili Kukumbukwa

Hebu wazia jitihada zilizohusika katika shambulizi hilo—kukusanya maelfu ya familia za Mashahidi kutoka kwenye eneo kubwa hivyo kwa siku moja tu? Wazia kukusanya mamia, ama maelfu ya watu, ili wafanye kazi ya kutambulisha Mashahidi, kisha kuvamia ghafula nyumba zao zote usiku mmoja. Halafu, kulikuwa na kazi ya kupakia watu kwenye mikokoteni, magari yanayokokotwa na wanyama, na magari mengine. Kisha kuwapeleka kwenye vituo vya magari ya moshi, na kuwapakia kwenye mabehewa ya mizigo.

Fikiria pia mateso yao. Je, waweza kuwazia pia jinsi walivyolazimishwa kusafiri kwa maelfu ya kilometa—kwa muda wa majuma matatu au zaidi, huku wakiwa kwenye mabehewa machafu, yaliyosongamana watu ambayo hayakuwa na vyoo ila ndoo ya kujisaidia tu? Jaribu kuwazia ukiachwa tu kwenye nyika ya Siberia. Nawe wafahamu kwamba si rahisi kuishi kwenye mazingira hayo magumu.

Mwezi huu ni ukumbusho wa miaka 50 tangu kuhamishwa kwa Mashahidi wa Yehova mnamo Aprili mwaka wa 1951. Masimulizi ya wale waliookoka ambayo yamerekodiwa kwenye ukanda wa vidio yanaonyesha jinsi walivyodumisha uaminifu licha ya kuteswa kwa miaka mingi. Masimulizi hayo yaonyesha kwamba jitihada za kuzuia watu kumwabudu Mungu haziwezi kufaulu. Hata Wakristo wa karne ya kwanza hawakuacha licha ya vizuizi.

Matokeo ya Uhamisho Huo

Serikali ya Sovieti iligundua upesi kwamba kuzuia Mashahidi kumwabudu Yehova hakukuwa kazi rahisi kama ilivyodhaniwa. Bila kujali malalamiko makali ya askari, Mashahidi walimwimbia Yehova sifa walipokuwa wakipelekwa uhamishoni. Waliangika ishara zilizosema hivi kwenye mabehewa yaliyowabeba: “Mashahidi wa Yehova Garini.” Shahidi mmoja alieleza hivi: “Tulipokuwa njiani tulikutana na magari mengine ya moshi vituoni, yaliyobeba wahamishwa, nasi tuliona ishara zilizoangikwa kwenye mabehewa.” Tulitiwa moyo kama nini!

Kwa hiyo badala ya kuvunjika moyo, wale waliokuwa wakihamishwa walidhihirisha roho kama ya mitume wa Yesu. Biblia yasema kwamba baada ya kupigwa viboko na kuagizwa wakome kuhubiri, ‘waliendelea bila kuacha kufundisha na kutangaza habari njema juu ya Kristo.’ (Matendo 5:40-42) Kwa kweli, ni kama Kolarz alivyosema kuhusu uhamisho huo, “haukuwa mwisho wa ‘Mashahidi’ nchini Urusi, ila ulikuwa mwanzo tu wa kazi yao ya kuwahubiria wengi. Hata walijaribu kuwahubiria watu vituoni wakiwa njiani kuelekea uhamishoni.”

Mashahidi walipowasili sehemu mbalimbali, walisifiwa kuwa wafanyakazi watiifu na wenye bidii. Lakini, kama mitume wa Kristo, ni kana kwamba waliwaambia wale waliowanyanyasa: ‘Hatuwezi kukoma kusema juu ya Mungu wetu.’ (Matendo 4:20) Wengi walisikiliza mafundisho ya Mashahidi na kujiunga nao kumtumikia Mungu.

Kolarz aeleza matokeo: “Serikali ya Sovieti ilipowahamisha ilisaidia sana kusambazwa kwa dini yao. ‘Mashahidi’ walihamishwa kutoka kwenye vijiji vyao vilivyojitenga [katika jamhuri za magharibi mwa Sovieti] na kupelekwa sehemu mbalimbali zenye watu wengi, kwenye kambi za mateso au za kazi ngumu.”

Jitihada za Kukabiliana na Ongezeko

Viongozi wa Sovieti walijaribu mbinu mbalimbali ili kukomesha kazi ya Mashahidi wa Yehova. Walianzisha mpango madhubuti wa kueneza habari za uwongo kuhusu Mashahidi, kwa kuwa mnyanyaso mkali haukufaulu. Walitumia vitabu, filamu, na vipindi vya redio. Wapelelezi waliozoezwa wa KGB walijiunga na makutaniko kisirisiri.

Habari za uwongo zilizoenezwa kote ziliwafanya watu wengi wahofu na kutowaamini Mashahidi bila sababu, hilo lathibitishwa na makala moja katika kitabu Reader’s Digest cha Agosti 1982, Chapa ya Kanada. Makala hiyo iliandikwa na Vladimir Bukovsky, Mrusi aliyeruhusiwa kuhamia Uingereza mwaka wa 1976. Aliandika hivi: “Jioni moja niliona ubao kwenye jengo moja jijini London uliotangaza hivi: MASHAHIDI WA YEHOVA . . . Sikuweza kuendelea kusoma, nilipigwa na bumbuazi na kushtuka sana.”

Vladimir aeleza kilichomfanya ahofu: “Haya ndiyo madhehebu ambayo wenye mamlaka nchini mwetu huita mahayawani katili ili kuwaogopesha watoto . . . Katika Muungano wa Sovieti, ‘Mashahidi’ wako gerezani na kwenye kambi za mateso tu. Na sasa nilisimama mbele ya jengo na kutazama ubao wenye jina lao. Je, kweli mtu yeyote angeweza kuwatembelea tu kirafiki?” akauliza. Ili kukazia sababu iliyomfanya ahofu, Vladimir alimalizia kwa kusema hivi: “‘Mashahidi’ wanasakwa sana katika nchi yetu kama vile wahuni wa Mafia wanavyosakwa Uingereza, nao hawaeleweki hata kidogo.”

Lakini Mashahidi walivumilia na kuongezeka sana licha ya mnyanyaso mkali na uenezaji wa habari za uwongo kuwahusu. Vitabu vya Sovieti kama vile The Truths About Jehovah’s Witnesses, kilichochapishwa kwa nakala 100,000 za Kirusi, katika mwaka wa 1978, kilidokeza kwamba habari za uwongo zinazokashifu Mashahidi zinahitaji kuenezwa kwa mapana na marefu. Mtungaji wa kitabu hicho, V. V. Konik, ambaye alieleza jinsi Mashahidi walivyokuwa wakihubiri wajapozuiwa, alishauri hivi: “Wasovieti wanaochunguza dini wanapaswa kubuni njia bora zaidi za kukomesha mafundisho ya mashahidi wa Yehova.”

Mbona Wakawa Shabaha ya Mashambulizi?

Kwa ufupi, Mashahidi wa Yehova walikuwa shabaha kuu ya mashambulizi ya Sovieti kwa sababu waliwaiga wafuasi wa mapema wa Yesu. Katika karne ya kwanza, mitume waliagizwa ‘wasifulize kufundisha juu ya msingi wa jina [la Yesu].’ Hata hivyo, wale waliowashtaki walilalamika hivi baadaye: “Tazameni! mmejaza Yerusalemu fundisho lenu.” Mitume hawakukana kwamba walikuwa wakihubiri wajapokatazwa, badala yake walijibu hivi kwa heshima: “Lazima sisi tumtii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.”—Matendo 5:27-29.

Mashahidi wa Yehova leo huchukua kwa uzito agizo ambalo Yesu aliwapa wafuasi wake la ‘kuwahubiria watu na kutoa ushahidi kamili.’ (Matendo 10:42) Katika kitabu chake The Kremlin’s Human Dilemma, Maurice Hindus alieleza kwamba Mashahidi “walichukiwa na Moscow na kuendelea kusakwa na polisi wa Sovieti” kwa sababu “hasa ya bidii yao ya kueneza evanjeli bila kukoma.” Akaongezea hivi: “Hawawezi kukomeshwa. Wanapogandamizwa mahali fulani, wanaibuka kwingineko.”

“Nijuavyo ni kwamba,” akaandika mwanahistoria Mrusi Sergei Ivanenko, “Mashahidi wa Yehova ndiyo dini pekee katika Muungano wa Sovieti iliyopata ongezeko la watu licha ya marufuku na mnyanyaso.” Bila shaka, dini nyingine pia ziliendelea kuwapo, kutia ndani Kanisa Othodoksi la Urusi lililokuwa mashuhuri zaidi ya zote. Utapendezwa kujua jinsi makanisa mengine na Mashahidi walivyoweza kustahimili mashambulizi ya Sovieti.

[Picha katika ukurasa wa 6]

“Dini Iliyonyanyaswa Vikali Zaidi”

Kichapo A Concise Encyclopaedia of Russia cha mwaka wa 1964 kilisema kwamba Mashahidi wa Yehova “walieneza imani yao kwa bidii.” Ndiyo “dini iliyonyanyaswa vikali zaidi katika Muungano wa Sovieti.”

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 7]

FAMILIA MOJA KATI YA MAELFU—Fyodor Kalin Asimulia Kuhamishwa kwa Familia Yao

Familia yetu iliishi katika kijiji cha Vilshanitsa, magharibi mwa Ukrainia. Alfajiri na mapema Aprili 8, 1951, maofisa waliokuwa na mbwa walikuja na kutuamsha sote. Walituambia kuwa serikali ya Moscow iliamuru tuhamishwe hadi Siberia. Lakini hatungehamishwa endapo tungetia sahihi hati iliyosema kwamba sisi si Mashahidi wa Yehova tena. Familia yetu yenye watu saba, wazazi wangu na ndugu zangu, tuliazimia kwamba hatutakana imani yetu. Nilikuwa na umri wa miaka 19 wakati huo.

Ofisa mmoja alisema hivi: “Bebeni maharagwe, mahindi, unga, vyakula vilivyohifadhiwa, na kabichi—la sivyo, watoto wenu watakula nini?” Tuliruhusiwa pia kuchinja kuku kadhaa na nguruwe na kubeba nyama hiyo. Vigari viwili vya kukokotwa na farasi vililetwa, na kila kitu kikapakiwa ndani yake na kupelekwa mji wa Hriplin. Huko tulijazwa kwenye behewa la mizigo watu 40 au 50 hivi, na mlango ukafungwa.

Behewa hilo lilikuwa na mbao chache za kulalia—hazikutosha kila mtu. Kulikuwa pia na jiko lenye makaa na kuni. Tulipika kwa jiko hilo, na kutumia vifaa vya kupikia tulivyobeba. Lakini hakukuwa na choo—tulitumia ndoo tu. Kisha tulitoboa shimo sakafuni, na kuitia ndoo shimoni, halafu tukaizingira kwa mablanketi kwa ajili ya faragha.

Tulisongamana sana kwenye behewa hilo na kusafiri polepole kwa maelfu ya kilometa na kuelekea tusikojua. Mwanzoni, tulivunjika moyo kidogo. Lakini tulipata shangwe tulipoimba pamoja nyimbo za Ufalme kwa shauku sana kiasi cha kupoteza sauti. Kamanda wa jeshi alifungua mlango na kutuamrisha tunyamaze, lakini hatukuacha kuimba hadi mwisho wa wimbo. Tuliposimama kwenye vituo njiani, wengi walikuja kujua kwamba ni Mashahidi wa Yehova waliokuwa wakihamishwa. Hatimaye, baada ya kusafiri kwa siku 17 au 18 tukiwa behewani, tulishushwa Siberia karibu na Ziwa Baikal.

[Picha]

Nimesimama mstari wa nyuma, kulia

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 8]

ARMAGEDDON Filamu ya Sovieti Iliyoeneza Uwongo

Serikali ya Sovieti ilitayarisha filamu ya Armageddon ili kuharibu sifa ya Mashahidi wa Yehova. Ilikuwa hadithi ya kubuniwa ya mapenzi kati ya mvulana mmoja wa jeshi la Sovieti na msichana aliyeshawishiwa kuwa Shahidi. Mwishoni mwa filamu hiyo, dada mchanga wa msichana huyo alikufa katika aksidenti iliyosababishwa na mwangalizi mmoja Shahidi, ambaye alionyeshwa kuwa kibaraka wa shirika la upelelezi la Marekani.

Gazeti The Red Flag la Ukrainia la Mei 14, 1963 lilisema hivi kuhusu filamu hiyo iliyowaudhi watu: “Hivyo ndivyo wale wasiomwamini Mungu wanavyoeneza kwa matokeo habari za uwongo zinazosadikisha. Filamu hiyo inaweza kuonyeshwa katika vijiji vingine nchini.”

[Picha katika ukurasa wa 6]

Maelfu walisafirishwa kwa mabehewa ya mizigo hadi Siberia