Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Kweli Wahalifu Wanaweza Kurekebishwa?

Je, Kweli Wahalifu Wanaweza Kurekebishwa?

Je, Kweli Wahalifu Wanaweza Kurekebishwa?

“Hakuna mtu anayeweza kumrekebisha mwanadamu mwingine kwa lazima. Ni sharti mtu mwenyewe aamue na awe tayari kujirekebisha.”—VIVIEN STERN, KITABU A SIN AGAINST THE FUTURE—IMPRISONMENT IN THE WORLD.

NJIA bora ya kuwarekebisha kabisa wafungwa ni kuwaelimisha na kuwasaidia warekebishe maadili yao na mtazamo wao. Bila shaka, kuna watu wanyoofu ambao wanajitahidi kuwaelimisha na kuwasaidia wafungwa. Wafungwa wengi wanathamini jinsi ambavyo watu hao wanajitolea kuwasaidia.

Huenda watu fulani wakabisha kwamba mfumo wa magereza hauwezi kuboreshwa na hivyo si rahisi kwa wafungwa kurekebishwa katika mazingira hayo. Ingawa ni kweli kwamba kumfunga mtu gerezani tu hakuwezi kumfunza maadili mapya, hata hivyo, mafunzo ya Biblia yamewasaidia wafungwa fulani kurekebisha maisha yao. Hilo laonyesha kwamba mtu mmoja-mmoja anaweza kujirekebisha.

Leo, baadhi ya wafungwa wanafanya marekebisho maishani kwa msaada wa Biblia ili wawe na fikira na mwenendo ufaao. Jinsi gani? Kwa kutii shauri hili la Biblia: “Komeni kufanyizwa kulingana na mtindo wa mfumo huu wa mambo, bali mgeuzwe umbo kwa kufanya upya akili yenu, ili mpate kujithibitishia wenyewe mapenzi ya Mungu yaliyo mema na yenye kukubalika na makamilifu.” (Waroma 12:2) Hilo hutimizwaje?

Umuhimu wa Biblia

Watu wengi hufikiri kwamba dini inaweza kuwasaidia sana wafungwa watubu mwenendo mbaya waliokuwa nao hapo awali. Bila shaka, tatizo linalozuka ni kwamba mfungwa aliyerekebishwa gerezani aweza kuendelea na uhalifu mara tu aachiliwapo. Mfungwa mmoja alisema hivi: “Watu wengi hudai kwamba wamepata kumwamini Kristo gerezani—lakini wanapoachiliwa, wanamsahau Kristo kabisa!”

Mambo yaliyoonwa yanathibitisha kwamba ni lazima marekebisho halisi yatukie ndani ya moyo na akili ya mhalifu, na kwamba ni lazima atubu kwa moyo mwenendo mwovu wa awali. Elimu ya Biblia inaweza kumsaidia mtu aelewe maoni ya Mungu kuhusu uovu na sababu inayofanya uchukize. Elimu hiyo yaweza kumsaidia aone umuhimu wa kuacha kabisa mwenendo mwovu.

Mashahidi wa Yehova wanatoa elimu ya Biblia katika magereza mengi ulimwenguni pote, na wamepata matokeo mazuri sana. (Ona ukurasa wa 10.) “Kupitia Biblia tumefundishwa kuhusu kusudi la uhai na baraka ambazo wanadamu watapata wakati ujao,” akasema mfungwa mmoja, kisha akaongeza hivi: “Ni elimu bora sana!” Mfungwa mwingine alisema: “Tunatumia shauri la Mungu kufanya maamuzi. . . . Maisha yetu yamebadilika. Twajua mambo yanayohitaji kutangulizwa maishani.”

Bila shaka, si wafungwa tu wanaohitaji kurekebishwa, wala magereza. Suluhisho bora kwa matatizo yanayokabili magereza ni kutatua kiini cha tatizo hilo. Mojawapo ya kweli nzuri kabisa za Biblia ambazo zimegusa mioyo ya wafungwa wengi inaonyeshwa na ahadi hii ya Mungu: “Watenda mabaya wataharibiwa . . . Wenye haki watairithi nchi, nao watakaa humo milele.”—Zaburi 37:9, 29.

Hilo litakapotukia, viwango bora zaidi vya Mungu vitatekelezwa na serikali isiyo na ufisadi yenye upendo na iliyo thabiti, Ufalme wa Mungu wa mbinguni utakaoongozwa na Kristo. Hiyo ndiyo serikali ambayo Wakristo wamefunzwa kusali juu yake. (Mathayo 6:10) Katika ulimwengu huo mpya, kila mkazi atakuwa amefanya marekebisho kwa kujifunza sheria bora za Mungu. Kisha kwa njia isiyo na kifani, “dunia itajawa na kumjua BWANA, kama vile maji yanavyoifunika bahari.” (Isaya 11:9) Matokeo yatakuwa nini? Wakazi wenye kutii sheria wa ulimwengu huo mpya “watajifurahisha kwa wingi wa amani.”—Zaburi 37:11.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 10]

Wafungwa Wapata Fursa ya Kuwa na Tumaini

Kwa zaidi ya miaka 20, wahudumu wajitoleaji wa Mashahidi wa Yehova wamekuwa wakitoa elimu ya Biblia kwa mafanikio katika gereza kuu la Atlanta, Georgia, Marekani. Zaidi ya wafungwa 40 wamesaidiwa kuwa wahudumu waliobatizwa wa Mashahidi wa Yehova, na wafungwa wengine zaidi ya 90 wamenufaika pia kwa kujifunza Biblia kwa ukawaida.

Hivi karibuni mwandishi wa Amkeni! aliwahoji walimu kadhaa wa Biblia ambao wamejitolea kuwaelimisha wafungwa katika gereza hilo.

▪ Kwa nini elimu ya Biblia ina matokeo sana katika kuwachochea wafungwa fulani warekebishe maisha yao?

David: Wafungwa wengi ni watu ambao hawakuonyeshwa upendo, hata walipokuwa watoto. Kwa hiyo, wanapopata kujua kwamba Mungu anawapenda na wanaposali kwake kutoka moyoni na kujibiwa wanamwona kuwa halisi. Kisha mioyo yao huwachochea kumpenda.

Ray: Nilimfunza Biblia mfungwa mmoja aliyetendewa vibaya kingono utotoni. Nilipomwuliza kilichomfanya ampende Yehova, alijibu kwamba unapojifunza kweli ya Biblia, unapata kujua kwamba Yehova anakuelewa. Hilo lilimchochea kujifunza mengi kuhusu utu wa Mungu huyo mwenye upendo.

▪ Watu wengine hudai kwamba wafungwa hujiunga na dini kwa makusudi mabaya—ili kupunguziwa kifungo chao au kupitisha tu wakati. Waonaje?

Fred: Tunapojifunza na wafungwa, tunawavutia kwa kusababu nao wala si kwa kuamsha hisia zao. Sisi hujifunza tu Biblia nao. Muda si muda, wao huelewa kwamba watafunzwa Biblia, na hatujihusishi na mambo mengine. Baadhi ya wafungwa wamenijia na kuniomba niwasaidie kushughulikia kesi zao mahakamani. Mimi hukataa. Tokeo ni kwamba wale wanaojiunga na kikundi cha wanaojifunza na kuendelea ni wale wanaopendezwa kikweli kujifunza Biblia.

Nick: Jambo moja ninaloona ni marekebisho ambayo wafungwa fulani hufanya wakiwa gerezani. Baadhi yao wamekuwa wahudumu waliobatizwa na wameteswa sana na wafungwa wenzao. Wamestahimili mno. Kama Biblia haingegusa mioyo yao, hawangeweza kubaki waaminifu chini ya hali hizo.

Israel: Kwa kawaida hao ni watu wanaotaka kujifunza kuhusu Yehova kwa moyo wao wote. Wao hudhihirisha upendezi wao kwa njia yenye kugusa moyo sana. Waweza kuona kwamba wanapendezwa kwa moyo wote.

Joe: Wale ambao wamekuwa Wakristo wa kweli wamepata kuelewa sababu iliyofanya maisha yao yaharibike. Wao pia wanaelewa kwamba wanaweza kufanya marekebisho na kuwa na tumaini. Sasa wanaweza kutarajia kwa moyo wote utimizo wa ahadi za Yehova za wakati ujao.

▪ Kwa nini mfumo wa magereza peke yake hauwezi kuwarekebisha wahalifu?

Joe: Kusudi la magereza ni kuwatenga wahalifu na jamii wala si kuwarekebisha. Hicho ndicho kiini cha tatizo hilo—yaani, maoni ya wana-magereza kuwaelekea wahalifu.

Henry: Magereza hayawezi kubadili mielekeo ya wakosaji. Wengi wao huendelea kutenda uhalifu uleule mara tu waachiliwapo.

[Picha katika ukurasa wa 8, 9]

Wafungwa wengi wamesaidiwa kujifunza kweli ya Biblia