Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ninawezaje Kusitawisha Uhusiano wa Karibu Pamoja na Babu na Nyanya?

Ninawezaje Kusitawisha Uhusiano wa Karibu Pamoja na Babu na Nyanya?

Vijana Huuliza . . .

Ninawezaje Kusitawisha Uhusiano wa Karibu Pamoja na Babu na Nyanya?

“Babu zangu wanapenda kupiga hadithi. Hadithi zao hunisaidia kuelewa hisia zangu”—Joshua.

HAPO zamani, ilikuwa kawaida kwa vizazi mbalimbali vya washiriki wa familia kuishi karibu-karibu—mara nyingi katika nyumba moja. Ilikuwa kawaida kushirikiana kwa ukaribu na babu na nyanya.

Siku hizi, vijana hukaa mbali na babu na nyanya zao. Zaidi ya hayo, familia nyingi zimevunjika kwa sababu ya talaka. Gazeti la The Toronto Star liliripoti kwamba “talaka yaweza kuwaathiri pia babu na nyanya na kuwazuia wasiwaone wajukuu wao wanaowapenda.” Nyakati nyingine, tatizo huwa kwamba vijana wengi huwa na maoni mabaya kuwahusu wazee. Wanawaona kuwa washamba, wenye maoni, maadili, na mapendezi yaliyo tofauti kabisa na yao. Tokeo ni nini? Vijana wengi hawana uhusiano wa karibu pamoja na babu na nyanya zao.

Hilo lasikitisha. Kama vile makala iliyotangulia ya mfululizo huu ilivyoonyesha, kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na babu na nyanya—hasa ikiwa wanamhofu Mungu—kunanufaisha na kufurahisha. * Msichana mmoja tineja anayeitwa Rebekah asema hivi kuhusu babu na nyanya yake: “Naweza kucheka nao kila wakati.” Kijana anayeitwa Peter asema hivi pia: “Siogopi kuwaambia jinsi ninavyohisi au kuhusu miradi yangu. Nyakati nyingine mimi hujihisi huru ninapokuwa nao zaidi ya ninapokuwa na wazazi wangu. Naamini kuwa ninaweza kuzungumza na babu na nyanya yangu juu ya jambo lolote.”

Vipi wewe? Labda ulikuwa na uhusiano wa karibu na babu na nyanya zako ulipokuwa mchanga. Lakini kwa kuwa sasa wewe ni tineja, labda karibuni hujafanya mengi ili kuendeleza uhusiano huo. Ikiwa ndivyo, kanuni inayopatikana katika shauri la Biblia kwenye 2 Wakorintho 6:11-13 yaweza kufaa, yaani, ‘upanue’ shauku yako kwao. Utafanyaje hivyo?

Kuchukua Hatua ya Kwanza

‘Kupanuka’ kwamaanisha kuchukua hatua fulani. Kwani Biblia husema: “Usiwanyime watu mema yaliyo haki yao, ikiwa katika uwezo wa mkono wako kuyatenda.” (Mithali 3:27) Ulipokuwa mchanga, labda hukuwa na “uwezo” wa kufanya lolote kuhusu uhusiano wako na babu na nyanya zako. Lakini kwa kuwa sasa umekua, labda hata kuwa mtu mzima, utaona kwamba kuna hatua kadhaa unazopaswa kuchukua.

Kwa mfano, ikiwa babu na nyanya wanakaa karibu, waweza kuwatembelea kwa ukawaida. Je, itachosha? Labda, ikiwa utakaa kimya tu. Basi anzisha mazungumzo! Waweza kuzungumza kuhusu nini? Kanuni ya Biblia inayopatikana kwenye Wafilipi 2:4 yasaidia. Yatuambia ‘tufulize kuangalia, si masilahi ya kibinafsi ya mambo yenu wenyewe tu, bali pia masilahi ya kibinafsi yale ya wengine.’ Yaani, pendezwa na babu na nyanya zako. Waambie wakueleze mambo wanayopenda. Wanahisije? Wamekuwa wakifanya nini? Wanaweza kufurahia kuzungumza kuhusu mambo ya zamani. Basi waulize jinsi maisha yalivyokuwa walipokuwa vijana. Baba au mama yako alikuwaje alipokuwa kijana? Ikiwa babu na nyanya zako ni Wakristo, waulize ni nini kilichowavutia kwenye kweli za Biblia.

Babu na nyanya wanaifahamu vyema historia ya familia na wangependa sana kukuburudisha kwa hadithi zenye kupendeza. Kwa kweli, waweza kufanya pindi kama hiyo iwe yenye kufurahisha. Jaribu kuwauliza babu na nyanya zako maswali, huku labda ukiyaandika mambo mnayozungumzia au kuyarekodi kwenye kaseti au kanda ya video. Ikiwa huna hakika kuhusu maswali utakayouliza, waombe wazazi wako wakutayarishie maswali yanayofaa. Yawezekana kuwa utajifunza mengi yatakayokusaidia kuwaelewa vyema babu na nyanya zako, wazazi wako, na hata kujielewa vyema. “Babu zangu wanapenda kupiga hadithi,” aeleza Joshua. “Hadithi zao hunisaidia kuelewa hisia zangu.”

Hata hivyo, usisahau kwamba babu na nyanya zako wanapendezwa sana na maisha yako na utendaji wako. Unapowaambia unayofanya, unawahusisha katika maisha yako. Bila shaka hilo litafanya mwe na uhusiano wa karibu hata zaidi. Kijana mmoja katika nchi ya Ufaransa anayeitwa Igor asema hivi: “Mimi na nyanya yangu twapenda kunywa kahawa pamoja kwenye mkahawa, tukizungumza juu ya mambo ambayo tumefanya karibuni.”

Twaweza Kufanya Nini Pamoja?

Baada ya kuzungumza pamoja, labda mnaweza kusonga mbele na kufanya mambo pamoja. Kwa kufikiri kimbele, waweza kugundua mambo mbalimbali mnayoweza kufanya pamoja. Mwanamke kijana anayeitwa Dara asema: “Nyanya zangu wamenizoeza kupika, kuhifadhi vyakula mikebeni, kuoka, kukuza mimea, na kutunza bustani.” Amy amejiunga na babu na nyanya zake kwenye vikusanyiko vya kirafiki vya familia na hata wanapokwenda likizo. Ikitegemea umri wao, akina babu na akina nyanya wengine bado ni watendaji sana. Aaron anapenda kucheza gofu pamoja na nyanya yake. Joshua huvua samaki na kufanya kazi nyingine za nyumbani pamoja na babu zake.

Ikiwa babu na nyanya zako ni waabudu wa Yehova, laweza kuwa jambo la kufurahisha kushiriki utendaji wa ibada ya Yehova pamoja nao, kama vile kuzungumza na wengine juu ya Biblia. Igor alisafiri pamoja na nyanya yake ili kuhudhuria mkusanyiko wa kimataifa wa Mashahidi wa Yehova nchini Poland. Yeye asema, “tulishiriki pamoja jambo nisiloweza kusahau, na bado sisi hufurahia kulizungumzia.” Ni kweli kwamba si akina babu na akina nyanya wote wanaoweza kusafiri-safiri. Hata hivyo, ni jambo linalofaa kutumia wakati pamoja nao.

Urithi wa Kiroho

Katika nyakati za Biblia, mwanamke mmoja aliyeitwa Loisi alitimiza daraka muhimu kwa kumsaidia mjukuu wake, Timotheo, awe mtu wa kipekee wa Mungu. (2 Timotheo 1:5) Si ajabu kwamba, leo babu na nyanya wengi Wakristo hutimiza daraka kama hilo. Joshua asema hivi kuhusu babu na nyanya zake: “Walianza kumtumikia Yehova hata kabla sijazaliwa, basi ninawaheshimu sana, si kama babu na nyanya tu bali kama wanaoshika uaminifu-maadili.” Amy asema hivi: “Kila wakati babu na nyanya zangu husema kuwa wanatiwa moyo na wanafurahi sana kuniona nikimtumikia Yehova kwa uaminifu. Hata hivyo, mfano wao bora na bidii yao kwa ajili ya Yehova wanapotumika wakiwa mapainia [waeneza-evanjeli wa wakati wote] hunitia moyo kuendelea katika utumishi wa painia.”

Chris humwita nyanya yake “mtu aliyenitia moyo sana kujifunza na kukomaa.” Aongezea hivi: “Siwezi kusahau maneno yake kwamba ‘twapaswa kufanya lililo bora kwa ajili ya Yehova.’” Babu na nyanya ya Pedro wamemsaidia sana kufanya maendeleo ya kiroho. Yeye asema hivi: “Ujuzi wao umenisaidia sana. Sikuzote babu na nyanya yangu walinipeleka kuhubiri, nami nathamini sana jambo hilo.” Naam, kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na babu na nyanya wanaomhofu Mungu kwaweza kukusaidia kumtumikia Mungu kikamili zaidi.

Akina Babu na Akina Nyanya Wanaokaa Mbali Sana

Vipi ikiwa babu na nyanya zako wanaishi mbali sana? Ikiwezekana, jaribu kuwatembelea kwa ukawaida. Wakati ambapo huwatembelei, fanya yale uwezayo ili uwasiliane nao. Hornan huona babu na nyanya yake mara tatu tu kwa mwaka, lakini yeye asema hivi: “Mimi huwapigia simu kila Jumapili.” Dara ambaye pia huishi mbali na babu na nyanya zake, asema hivi: “Wao hupendezwa na maisha yangu, nasi hupigiana simu au kuwasiliana kwa kutumia kompyuta (E-mail) karibu kila juma.” Kuwasiliana kwa kutumia kompyuta na kupiga simu kwafaa, lakini usidharau faida za barua iliyoandikwa kwa mkono. Vijana wengi wameshangaa kugundua kwamba babu na nyanya zao wamehifadhi barua zote walizotuma tangu wawe wachanga. Barua zaweza kusomwa tena na tena—na kuthaminiwa. Basi, usisahau kuandika!

Kwa kawaida, babu na nyanya huwa na upendo wa pekee kwa wajukuu wao. (Mithali 17:6) Kuna njia nyingi za kujenga na kudumisha uhusiano wa karibu pamoja na babu na nyanya zako, iwe wanaishi karibu au wanaishi mbali. Kwa vyovyote vile, jitahidi sana kufanya hivyo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Ona makala “Vijana Huuliza . . . Kwa Nini Niwajue Vyema Babu na Nyanya?” katika toleo letu la Aprili 22, 2001.