Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Mungu Atasikiliza Sala Zangu?

Je, Mungu Atasikiliza Sala Zangu?

Vijana Huuliza . . .

Je, Mungu Atasikiliza Sala Zangu?

“Mimi husali juu ya mambo yote kwa sababu Yehova ni rafiki yangu, na ninajua kuwa atanisaidia ninapokuwa na tatizo.”—Andrea.

MSICHANA huyo Andrea, ana uhakika kuwa Mungu husikiliza sala zake. Lakini si vijana wote walio na uhakika huo. Wengine huhisi wako mbali sana na Mungu hivi kwamba hawawezi kumfikia. Pia, huenda wakajiuliza ikiwa Mungu anawajali kiasi cha kwamba atawasikiliza wanaposali.

Ni nini kinachomwezesha mtu kusali? Kwa ufupi, ni urafiki wa kweli pamoja na Mungu. Mtunga-zaburi alisali hivi: “Wakujuao jina lako wakutumaini wewe.” (Zaburi 9:10) Vipi wewe? Je, unamjua Mungu vya kutosha kuamini kuwa atasikiliza sala zako? Kabla hujasoma habari hii zaidi, tafadhali jaribu kujibu maswali yaliyo kwenye sanduku lenye kichwa “Wamjua Mungu Kadiri Gani?” Unaweza kujibu maswali mangapi?

WAMJUA MUNGU KADIRI GANI?

1. Jina la Mungu ni nani, nalo linamaanisha nini?

2. Biblia hufunua sifa zipi kuu nne za Mungu?

3. Ni nini wonyesho mkubwa wa upendo wa Mungu kwa ajili ya wanadamu?

4. Twawezaje kufurahia urafiki pamoja na Mungu?

5. Twapaswa kuwa na mtazamo gani tunaposali?

Je, unaweza kujibu angalau maswali kadhaa sasa, hata kabla ya kusoma makala yote? Basi, tayari unajua mengi kumhusu Mungu kuliko watu wengi. Hata hivyo, yamkini majibu yako yataonyesha unahitaji kutwaa ujuzi zaidi juu yake, umjue kwa undani zaidi. (Yohana 17:3) Ukiwa na lengo hilo akilini, fikiria mambo machache tu tunayofundishwa na Biblia kuhusu yule “Msikiaji wa sala.”—Zaburi 65:2, NW.

Mungu Ni Mtu Halisi

Kwanza, Biblia hutusaidia kuelewa kuwa Mungu si kani isiyo na utu. Yeye ni mtu aliye na jina, Yehova. (Zaburi 83:18) Katika Kiebrania, jina hilo humaanisha “Yeye Husababisha Iwe.” Yeye anaweza kuwa chochote anachotaka kuwa ili kutimiza kusudi lake. Nguvu zisizo na utu haziwezi kufanya hivyo! Basi unaposali, unaweza kuwa na uhakika kuwa huzungumzi na kani isiyo na utu au hewa. Unazungumza na mtu, anayeweza kusikia na kujibu sala zako.—Waefeso 3:20.

Hivyo, kijana anayeitwa Diana asema: “Ninajua kwamba Yehova hunisikia, popote nilipo.” Ili uwe na uhakika huo, Mungu apaswa kuwa halisi kwako! Biblia yasema, “amkaribiaye Mungu lazima aamini kwamba yeye yuko.”—Waebrania 11:6.

Chanzo cha Hekima na Nguvu

Mungu anaweza kutusaidia kikweli kwa sababu ana nguvu nyingi ajabu. Nguvu hizo hazina kikomo, kama zinavyoonyeshwa na ukubwa na utata wa ulimwengu. Biblia inasema kuwa Yehova anajua majina ya nyota zote—hata ingawa kuna mabilioni ya nyota! Zaidi ya hilo, yeye ndiye chanzo cha nguvu zilizo kwenye nyota hizo. (Isaya 40:25, 26) Je, hiyo haistaajabishi? Na ingawa mambo hayo yashangaza, Biblia husema kuwa “mambo haya ni fununu tu za nguvu zake”!—Ayubu 26:14, Today’s English Version.

Pia, fikiria juu ya hekima ya Yehova isiyo na kikomo. Biblia husema kuwa mawazo yake ni “mafumbo makubwa.” (Zaburi 92:5) Aliwaumba wanadamu, kwa hiyo anatuelewa zaidi ya tunavyojielewa. (Zaburi 100:3) Kwa sababu amekuwako “tangu milele hata milele,” ana ujuzi usio na kikomo. (Zaburi 90:1, 2) Hakuna kitu asichofahamu.—Isaya 40:13, 14.

Yehova hutumiaje nguvu na hekima yote hiyo? Andiko la 2 Mambo ya Nyakati 16:9 husema: “Maana macho ya BWANA hukimbia-kimbia duniani mwote, ili ajionyeshe mwenye nguvu kwa ajili ya hao, waliokamilika moyo kuelekea kwake.” Hakuna tatizo ambalo Mungu hawezi kutatua au kukusaidia kukabiliana nalo. Kijana mmoja anayeitwa Kayla akumbuka: “Hivi majuzi, wakati familia yetu pamoja nami tulipokuwa katika hali ngumu, nilisali kwa Yehova, na ninahisi kuwa alitusaidia kukabiliana na hali, matatizo, na hisia ambazo ingekuwa vigumu kuvumilia bila msaada wake.” Unapozungumza na Mungu, unaenda kwenye chanzo cha hekima. Hakuna jambo linaloweza kusaidia zaidi ya hilo!

Mungu Mwenye Haki na Upendo

Lakini unajuaje kwamba Mungu anataka kukusaidia? Kwa sababu Yehova hajachagua kujitambulisha kwa nguvu zake nyingi wala kwa hekima yake yenye kina kirefu au hata kwa haki yake imara. Badala yake, Yehova anajulikana hasa kwa sifa yake ya upendo. “Mungu ni upendo,” yasema 1 Yohana 4:8. Na upendo huo mkubwa ndio unaofanya sala kuwa ya maana sana. Wonyesho mkubwa wa upendo wake ulikuwa kumtoa Mwana wake kuwa dhabihu ya fidia ili tufurahie uhai udumuo milele.—Yohana 3:16; 1 Yohana 4:9, 10.

Kwa sababu Mungu ni upendo, hupaswi kamwe kuhofu kwamba hatakujali au hatakutendea kwa haki. “Njia zake zote ni haki,” yasema Kumbukumbu la Torati 32:4. Upendo wa Mungu kwako unakuhakikishia kuwa atakusikiliza kwa makini. Hilo latufanya tuwe na uhakika tunapomweleza mawazo na hisia zetu za siri.—Wafilipi 4:6, 7.

Urafiki Pamoja na Mungu

Kwa kweli, Yehova anatualika tuzungumze naye. Hataki awe kama mtu tusiyemjua. Kinyume chake, sikuzote Yehova amewaalika watu wawe rafiki zake. Kati ya wale waliofurahia urafiki pamoja na Mungu, watu waliokubaliwa naye, mlikuwemo wanaume na wanawake, vijana na wazee. Walitia ndani watu kama Abrahamu, Mfalme Daudi, na Maria, mama ya Yesu.—Isaya 41:8; Luka 1:26-38; Matendo 13:22.

Hata wewe waweza kuwa rafiki ya Yehova. Bila shaka, urafiki huo haumaanishi kuwa wapaswa kumwona Mungu kama jini unaloweza kuwasiliana nalo wakati tu unapotaka kitu au unapokuwa na tatizo fulani. Sala zetu haziwezi kuwa juu ya mahitaji yetu ya kibinafsi tu. Ikiwa tunataka urafiki pamoja na Mungu, twahitaji kupendezwa na mapenzi yake—si yetu tu—na twapaswa kufanya mapenzi ya Mungu. (Mathayo 7:21) Kwa hiyo, Yesu aliwafundisha wanafunzi wake wasali kuhusu mambo yaliyo ya maana kwa Mungu. Alisema: “Basi, nyinyi lazima msali kwa njia hii: ‘Baba yetu uliye katika mbingu, jina lako na litakaswe. Acha ufalme wako uje. Mapenzi yako na yatendeke, kama ilivyo katika mbingu, pia juu ya dunia.’” (Mathayo 6:9, 10) Sala zetu zapasa kujaa sifa na shukrani kwa Mungu!—Zaburi 56:12; 150:6.

Hata hivyo, hatupaswi kufikiri kuwa mahitaji au mahangaiko yetu ni madogo sana au si ya maana kwa sala. Steve asema: “Hata ingawa mimi hujaribu kusema wazi naye, nyakati nyingine mimi huhisi kuwa sipaswi kumsumbua Mungu kwa mambo yasiyo na maana.” Wakati wowote unapohisi hivyo, jaribu kukumbuka yale Yesu alifundisha wanafunzi wake: “Shore watano huuzwa kwa sarafu mbili za thamani ndogo, sivyo? Na bado hakuna hata mmoja wao hupata kusahaulika mbele ya Mungu. . . . Msiwe na hofu; nyinyi ni bora zaidi kuliko shore wengi.” (Luka 12:6, 7) Je, hiyo haitutii moyo?

Basi ni wazi kwamba, kadiri unavyomjua Yehova zaidi, ndivyo utakavyochochewa zaidi umfikie katika sala na kuwa na uhakika kwamba anaweza kukusaidia na atakusaidia. Kwa hiyo, unapaswa kuwa na mtazamo gani wa akili unaposali kwa Mungu? Unapaswa kuwa mwenye heshima, mnyenyekevu, na usiwe na ubinafsi. Je, unafikiri kuwa mtu mwenye mamlaka duniani atakusikiliza ukiomba kitu kwa kiburi au bila heshima? Basi usishangae kuwa Yehova anakutazamia umheshimu yeye na viwango vyake kabla hajajibu sala zako.—Mithali 15:29.

Maelfu ya vijana wanaomhofu Mungu wamejifunza kumfunulia Mungu yaliyo moyoni mwao. (Zaburi 62:8) Brett asema: “Yehova anapojibu sala zangu, hiyo hunitia moyo kwamba yeye bado ni rafiki yangu.” Vipi wewe? Unawezaje kufurahia urafiki kama huo pamoja na Mungu? Vijana wawili Wakristo walitoa maelezo yafuatayo:

Rachel: “Ili niwe karibu na Yehova, ninaona uhitaji wa kujifunza Neno lake kwa undani, na ninajaribu kusitawisha hamu ya funzo la aina hiyo.”—1 Petro 2:2.

Jenny: “Ninaona kuwa kadiri unavyojishughulisha zaidi katika utumishi wake, ndivyo unavyohisi u karibu zaidi na Yehova.”—Yakobo 4:8.

Je, umewahi kufikiria jinsi kusali kulivyo na faida kubwa? Kijana mmoja Mkristo asema: “Ningehisi nikiwa karibu zaidi na Mungu iwapo angezungumza nami au kunitumia ujumbe.” Kwa kuwa Yehova hatujibu kwa sauti tunaposali, sala hutusaidiaje? Toleo moja la wakati ujao litazungumzia jambo hilo.

[Sandkuku katika ukurasa wa 27]

Majibu ya maswali ya ukurasa 25

1. Yehova. Linamaanisha “Yeye Husababisha Iwe.”

2. Upendo, nguvu, haki, na hekima.

3. Alimtuma Mwana mzaliwa-pekee wake, Yesu, ili afe kwa ajili yetu.

4. Kwa kupendezwa na mapenzi ya Mungu badala ya kuhangaikia mahitaji yetu tu.

5. Twapaswa kuwa wanyenyekevu, wenye heshima, na tusiwe na ubinafsi.

[Picha katika ukurasa wa 26]

Kujifunza Biblia na kujifunza kutokana na uumbaji kutakusaidia kumjua Mungu vizuri zaidi