Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mbona Kuna Ukosefu wa Maji?

Mbona Kuna Ukosefu wa Maji?

Mbona Kuna Ukosefu wa Maji?

Cherrapunji, nchini India, ni mojawapo ya sehemu zenye mvua nyingi zaidi duniani. Wakati wa pepo za msimu, mvua nyingi ya kipimo cha milimeta 9,000 hunyesha kwenye vilima vilivyo karibu na Milima ya Himalaya. Hata hivyo, jambo la kushangaza ni kuwa Cherrapunji pia hukumbwa na ukosefu wa maji.

MAJI ya mvua hutiririka kasi sana kwani hakuna mimea inayoweza kuhifadhi maji hayo kwenye udongo. Kunakuwa na ukosefu mkubwa wa maji miezi miwili hivi baada ya mvua ya msimu kunyesha. Miaka mingi iliyopita Robin Clarke, katika kitabu chake Water: The International Crisis, alisema Cherrapunji ni “jangwa lenye mvua nyingi zaidi duniani.” *

Bangladesh iko upande wa chini wa Cherrapunji. Bangladesh ni nchi yenye watu wengi, iliyo kwenye uwanda wa chini, ambayo huathiriwa sana na mafuriko ya mvua ya msimu. Mafuriko hayo hutiririka kutoka sehemu zenye vilima nchini India na Nepal. Katika miaka mingine, theluthi mbili ya eneo la Bangladesh hufurika maji. Lakini mafuriko yanapopungua, maji ya Mto Ganges hupungua sana na nchi hukauka. Kila mwaka zaidi ya watu milioni 100 nchini Bangladesh hukumbwa na mafuriko na ukame unaosababisha hasara. Jambo la kusikitisha zaidi ni kwamba maji ya visima nchini humo yamechafuliwa na kemikali ya aseniki, na yaelekea sumu hiyo imeathiri mamilioni ya watu.

Maji katika jiji la Nukus, nchini Uzbekistan, karibu na Bahari ya Aral, yamejaa chumvi wala si aseniki. Mimea ya pamba imefunikwa na chumvi ambayo inaizuia kukua. Chumvi kutoka kwenye udongo wa chini uliojaa maji hurundikana juu ya ardhi. Tatizo hilo, la mrundikano wa chumvi si jipya. Miaka 4,000 iliyopita, kilimo kilididimia nchini Mesopotamia kwa sababu ya tatizo hilohilo. Umwagiliaji-maji mashamba kupita kiasi pamoja na kukwama kwa maji hufanya chumvi iliyo kwenye udongo irundikane juu. Ni lazima maji mengi yasiyo na chumvi yatumiwe ili kukuza mazao ya kutosha. Hata hivyo, mwishowe udongo hukosa rutuba kabisa kwa miaka mingi ijayo.

Mbona Kuna Ukosefu wa Maji?

Inasikitisha kwamba mara nyingi ni mvua kubwa inayonyesha kwenye eneo hilo. Hilo husababisha mafuriko na maji kutiririka kasi sana kuelekea baharini. Sehemu fulani hupata mvua nyingi ilhali nyingine hupata mvua kidogo. Cherrapunji imekuwa na sifa ya kurekodi mvua inayozidi milimeta 26,000 kwa muda wa miezi 12, ilhali Jangwa la Atacama kaskazini mwa Chile laweza kukosa mvua nyingi kwa miaka kadhaa.

Isitoshe, watu wengi duniani wanaishi sehemu zisizokuwa na maji ya kutosha. Kwa kielelezo, ni watu wachache sana wanaoishi kwenye maeneo ya kitropiki ya Afrika na Amerika Kusini yanayopata mvua nyingi sana. Asilimia 15 ya maji ya mvua inayonyesha duniani kila mwaka hutiririka kwenye Bahari ya Atlantiki kutoka kwenye Mto Amazon ulio mkubwa. Lakini eneo hilo lina wakazi wachache kwa hiyo ni kiasi kidogo sana cha maji hayo kinachotumiwa. Kwa upande mwingine, watu wapatao milioni 60 huishi nchini Misri, ambako mvua ni haba, na kiasi kikubwa cha maji wanayotumia hutoka kwenye Mto Nile uliopungua.

Miaka iliyopita upungufu huo wa maji haukusababisha matatizo makubwa. Uchunguzi mmoja ulionyesha kwamba katika mwaka wa 1950, hakuna sehemu hata moja duniani iliyokuwa na upungufu mkubwa sana wa maji. Lakini mambo yamebadilika. Kiasi cha maji yanayotumiwa na kila mtu katika maeneo yenye ukame ya Afrika Magharibi na Asia ya Kati, kimepungua hadi sehemu moja kwa kumi ya kiasi kilichotumiwa mwaka wa 1950.

Uhitaji mkubwa wa maji umesababishwa na hali nyinginezo mbali na kuongezeka kwa idadi ya watu na uhaba wa mvua katika maeneo yenye watu wengi. Katika ulimwengu wa leo, ufanisi na maendeleo huhusiana moja kwa moja na kuwapo kwa maji ya kutosha.

Uhitaji Unaoongezeka wa Maji

Iwapo unaishi katika nchi iliyositawi kiviwanda, bila shaka umeona kwamba viwanda vingi hujengwa karibu na mito mikubwa. Ni kwa sababu moja tu. Viwanda vinahitaji maji ili kutengeneza karibu kila bidhaa, kutia ndani kompyuta na vibanio vya karatasi. Viwanda vinavyotengeneza chakula pia hutumia maji mengi sana. Vituo vya nguvu za umeme hutumia maji mengi kupindukia na kwa hivyo hujengwa kandokando ya maziwa au mito.

Kilimo hutumia maji mengi hata zaidi. Maeneo mengi yanapata kiasi kidogo sana cha mvua au hainyeshi kwa ukawaida na hivyo si rahisi kupata mavuno mazuri. Kwa hiyo, umwagiliaji-maji mashamba ulionwa kuwa njia ifaayo ya kukuza chakula kwa ajili ya wanadamu wenye njaa. Kilimo cha umwagiliaji-maji mashamba kimesitawi sana hivi kwamba kiasi kikubwa cha maji safi duniani hutumiwa kwa kilimo.

Isitoshe, kiasi cha maji yanayotumiwa nyumbani kimeongezeka. Katika miaka ya 1990, idadi kubwa sana ya wakazi wapya wa mijini wapatao milioni 900 walihitaji maji safi na mazingira safi. Vyanzo vya asili vya maji, kama vile mito na visima, haviwezi kuandaa maji ya kutosha kwa majiji makubwa. Kwa mfano, Mexico City sasa inahitaji kusambaza maji kwa mabomba kwa umbali wa kilometa 125 na kuyasukuma kwa mashine kupitia milima yenye kimo cha meta 1,200 juu ya usawa wa bahari wa jiji hilo. Katika ripoti yake ya Water: The Life-Giving Source, Dieter Kraemer asema kwamba mabomba hayo ni “kama mikono ya pweza; yanaenea kutoka jijini ili kujaribu kuvuta maji.”

Kwa hiyo, viwanda, kilimo, na miji imekuwa iking’ang’ana ili kupata maji zaidi. Na kwa sasa sehemu hizo zimefaulu kupata maji kwa kuvuta maji yaliyo ardhini. Tabaka lenye maji ni mojawapo ya hifadhi kubwa zaidi za maji yasiyo na chumvi duniani. Lakini hifadhi hizo za maji zinaweza kwisha. Hifadhi hizo za maji zinaweza kulinganishwa na pesa katika benki. Pesa zilizo akibani zitakwisha iwapo utazitumia tu bila kuweka pesa zaidi katika akiba hiyo. Muda si muda, hutakuwa na pesa za kutoa.

Matumizi Yanayofaa na Yasiyofaa ya Maji ya Ardhini

Maji ya ardhini ni maji tunayoteka visimani. Ripoti ya Groundwater: The Invisible and Endangered Resource iliyoandikwa na Shirika la Hazina ya Watoto ya Umoja wa Mataifa yakadiria kwamba nusu ya maji yanayotumiwa nyumbani na katika kilimo hutoka visimani. Watu wa mijini na mashambani hupenda kunywa maji ya visima kwa sababu huwa si machafu kama maji yanayotiririka mitoni. Maji ya visima yangedumu kwa muda mrefu iwapo watu wangeyatumia kwa kiasi, kwa kuwa hifadhi hizo za ardhini hujaa wakati maji ya mvua yanapopenya taratibu ardhini. Lakini kwa miaka mingi wanadamu wamekuwa wakitumia maji mengi kupita ujazo wake wa kiasili.

Tokeo ni kwamba maji ya visima yanazidi kupungua, na basi kuyavuta maji hayo ni kazi bure kwa sababu inagharimu pesa nyingi sana na si kazi rahisi. Uchumi huzorota na watu huteseka wakati visima vinapokauka. Magumu hayo yameanza kuikumba India. Hali hiyo inatisha kwa sababu wakazi bilioni moja wa nyanda za kati za China na India hutegemea maji ya visima ili kupata chakula.

Mbali na kutumiwa kupita kiasi, maji ya visima yanachafuliwa sana. Maji hayo huchafuliwa na mbolea za kilimo, vinyesi vya wanadamu na wanyama na kemikali za viwandani. “Maji yaliyo katika tabaka la ardhini yanapochafuliwa, kazi ya kuyasafisha hugharimu pesa nyingi na huchukua muda mrefu, na huenda hata isiwezekane,” yaeleza ripoti moja iliyochapishwa na Shirika la Utabiri wa Hali ya Hewa Ulimwenguni. ‘Yasemekana kwamba kuchafuliwa polepole kwa maji ya visima kunawafanya wanadamu wahofu kuzuka kwa msiba mbaya kwa sababu ya maji yenye kemikali. Wanadamu wamo hatarini.’

Jambo la kushangaza ni kwamba huenda maji yanayovutwa kutoka visimani yakaharibu ardhi badala ya kuboresha kilimo kama ilivyokusudiwa. Sehemu kubwa sana ya mashamba yanayomwagiliwa maji katika nchi zenye ukame ulimwenguni imeharibiwa na chumvi. Huko India na Marekani—nchi zinazoandaa chakula kingi zaidi ulimwenguni—asilimia 25 ya mashamba yanayomwagiliwa maji tayari yameharibika kabisa.

Kuhifadhi Hufaidi

Licha ya matatizo hayo yote, hali haingekuwa mbaya kama maji muhimu sana yaliyo duniani yangetumiwa kwa uangalifu. Umwagiliaji-maji mashamba kwa njia isiyofaa hufanya asilimia 60 ya maji yapotee bure. Kutumia tekinolojia mpya na mbinu zifaazo kwaweza kupunguza maradufu matumizi ya maji viwandani. Na kiasi cha maji yanayotumiwa mijini kinaweza kupunguzwa kwa asilimia 30 ikiwa mabomba yaliyotoboka yatarekebishwa mara moja.

Jitihada za kuhifadhi maji zitafaulu watu wakiwa na nia na njia za kufanya hivyo. Je, kuna sababu nzuri za kutufanya tuamini kuwa maji muhimu ya dunia yetu yatahifadhiwa kwa ajili ya vizazi vijavyo? Makala yetu ya mwisho itajibu swali hilo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Ona makala “Cherrapunji—Mojawapo ya Sehemu Zenye Mvua Nyingi Zaidi Duniani,” katika gazeti la Amkeni! la Mei 8, 2001.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 7]

MAJI HUENDELEZA MAISHA DUNIANI

Karibu shughuli zote za viwandani hutumia maji mengi sana.

Utengenezaji wa tani moja ya feleji waweza kutumia tani 280 za maji.

Kutengeneza kilogramu moja ya karatasi kwaweza kutumia kilogramu 700 za maji (ikiwa kiwanda hakisafishi na kutumia maji yaleyale).

Watengenezaji wa magari hutumia kiasi cha maji ambacho ni mara 50 zaidi ya uzito wa gari lenyewe.

Maji mengi sana hutumika kwa kilimo hasa ikiwa mifugo imefugwa kwenye maeneo yenye ukame duniani.

Ili kutayarisha kilogramu moja ya nyama ya ng’ombe kutoka California, lita 20,500 za maji zinahitajika.

Kumsafisha na kumhifadhi kuku mmoja kwenye friji hutumia angalau lita 26 za maji.

[Grafu/Picha katika ukurasa wa 8]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

MAJI HUTUMIWA WAPI?

Kilimo asilimia 65

Viwandani asilimia 25

Nyumbani asilimia 10

[Picha katika ukurasa wa 9]

Mamilioni ya lita za maji humwagika kwa sababu ya mabomba yaliyotoboka na mifereji inayoachwa bila kufungwa

[Picha zimeandaliwa]

AP Photo/Richard Drew