Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kukabiliana na Msiba Mbaya Sana

Kukabiliana na Msiba Mbaya Sana

Kukabiliana na Msiba Mbaya Sana

KAMA ILIVYOSIMULIWA NA JAMES GIARRANO

Mojawapo ya mambo yaletayo shangwe kubwa maishani ni kuwa babu na nyanya. Mimi na mke wangu Vicki, tulitazamia kwa hamu nyingi kuzaliwa kwa mjukuu wetu wa kwanza. Binti yetu Theresa pamoja na mume wake Jonathan, walitazamia kupata mtoto mwanzoni-mwanzoni mwa Oktoba 2000. Hatukujua kwamba, punde si punde tungekumbwa na msiba mbaya sana.

MIMI na mke wangu, pamoja na mwana wetu na mke wake tuliondoka kwa ajili ya likizo siku ya Jumamosi, Septemba 23. Tulipanga kukutana na watu wengine wa ukoo ili tutembelee eneo la Outer Banks la North Carolina. Theresa na Jonathan waliamua kutoenda nasi kwa ajili ya likizo kwa sababu Theresa alikuwa katika mwezi wa tisa wa ujauzito na tungesafiri kwa muda mrefu kwa gari—kwa saa 11 hivi kutoka kwenye nyumba yetu kule Ohio.

Tulitaka kuahirisha safari yetu, lakini Theresa alisisitiza twende. Alituhakikishia kwamba angekuwa salama. Isitoshe, daktari wake alisema kwamba angekuwa mjamzito kwa kile kipindi cha kawaida cha miezi tisa, na angejifungua baada ya wiki mbili tu.

Siku ya Jumatano, Septemba 27, 2000, ilikuwa siku yenye kupendeza iliyonikumbusha ni kwa nini familia yetu huchagua kutembelea eneo hilo wakati wa likizo katika miaka kadhaa iliyopita. Hatukujua kwamba siku hiyohiyo, maisha yetu yangebadilika kabisa.

“Theresa Amepotea!”

Jioni hiyo nilipigiwa simu na ndugu yangu aliyekuwa Ohio. Alisitasita sana na alikuwa na wasiwasi. Hatimaye, alisema: “Theresa amepotea!” Polisi walihusika kwa sababu mambo fulani kuhusu kupotea kwake yalizusha shaka. Jonathan aliporudi nyumbani alasiri hiyo, alipata mlango wa mbele ukiwa wazi. Kiamsha-kinywa cha Theresa kilikuwa kingali mezani, na pochi lake lilikuweko. Kulikuwa na jambo jingine la ajabu: Viatu vyake—vilivyomtoshea tu katika mwezi wa tisa wa ujauzito—bado vilikuwa karibu na mlango.

Jonathan alikuwa amepiga simu nyumbani mwendo wa saa 3:30 asubuhi. Theresa alimwambia kuwa mwanamke mmoja alipiga simu na kusema kuwa atakuja kulitazama gari walilokuwa wakiuza. Baadaye, Theresa angeenda kufanya shughuli mbalimbali. Jonathan alipiga simu wakati wa chakula cha mchana, lakini hakumpata. Alipiga simu tena na tena wakati wa alasiri, lakini hakuna aliyejibu. Aliporudi nyumbani mwendo wa saa 10:15 alasiri, gari halikuweko. Alipiga simu hospitalini akifikiri kwamba huenda Theresa alikuwa amepata maumivu ya kujifungua. Hakuweko. Aliwapigia simu watu wa ukoo, lakini hakuna aliyemwona. Alikuwa na wasiwasi. Basi, akawaita polisi. Saa 12:00 hivi jioni, polisi walilipata gari hilo karibu na nyumba yao. Lakini bado Theresa hakuwa amepatikana.

Tulipopokea habari hizo tukiwa North Carolina, tulishtuka sana. Mimi na mke wangu pamoja na mwana wetu na mke wake tulifunga mizigo yetu tukarudi nyumbani. Ilikuwa safari ndefu yenye kuhuzunisha. Tulisafiri usiku wote na tukafika Ohio asubuhi, siku iliyofuata.

Kisa Chafumbuliwa

Wakati huohuo, Jonathan pamoja na watu fulani wa ukoo, marafiki wa karibu, na watu wengine walishirikiana pamoja na polisi ili kumtafuta Theresa usiku kucha. Walimtafuta kwa siku tano zenye kuhuzunisha. Hatimaye, siku ya Jumatatu, Oktoba 2, kisa hicho kilianza kufumbuliwa. Kufikia wakati huo, polisi walikuwa wamefuatilia simu aliyopigiwa Theresa Jumatano asubuhi. Mwanamke aliyeishi karibu nao ndiye aliyepiga simu hiyo kwa kutumia simu ya mkononi.

Baada ya kumhoji mwanamke huyo, polisi walimshuku. Baadaye usiku huohuo, polisi walirudi kwenye nyumba ya mwanamke huyo. Lakini walipokaribia mlangoni, walisikia mlio wa bunduki. Walipovunja mlango na kuingia ndani, walimpata mwanamke huyo akiwa amekufa. Alikuwa amejifyatua risasi. Walishangaa kuona kitoto kivulana ndani ya chumba kimoja kwenye orofa ya pili. Kwa kustaajabisha, kitoto hicho kilikuwa kimelala hata wakati wa mfyatuko huo!

Lakini bado Theresa hakuwa ameonekana. Kwa muda wa saa chache zilizofuata, polisi walikagua nyumba hiyo ili kupata dalili zozote za kuwapo kwa Theresa. Ukaguzi ulimalizika Jumanne asubuhi kwenye gereji. Walipata mwili wa Theresa mle ndani, katika shimo lenye kina kifupi. Baadaye, afisa anayechunguza vifo vya ghafula aligundua kwamba Theresa aligongwa na akapoteza fahamu, kisha akapigwa risasi mgongoni. Alikufa papo hapo, kisha mtoto wake alitolewa kwenye tumbo lake la uzazi. Tunapofikiria yaliyopita, twafarijika kwa kiasi fulani kujua kwamba hakuteseka.

Mtoto alipelekwa hospitalini, ambako alisemekana kuwa ana afya njema—salama salimini! Uchunguzi wa DNA uliohitajiwa, ulithibitisha kwamba yeye kweli ni mjukuu wetu. Jonathan alimpa jina alilochagua pamoja na Theresa—Oscar Gavin. Baada ya mjukuu wetu mwenye uzito wa kilogramu 3.9 kukaa hospitalini kwa muda mfupi, babake alimpokea siku ya Alhamisi, Oktoba 5. Tulisisimuka kuwa na mjukuu wetu, lakini hatuwezi kueleza jinsi tulivyoumia kwa kujua kwamba Theresa hakuweko ili kumpakata.

Itikio la Jumuiya

Mimi na familia yangu tulitokwa machozi kwa sababu ya utegemezo mkubwa tuliopokea—hasa kutoka kwa watu tusiowajua kamwe. Theresa alipopotea, mamia ya watu walijitolea kumtafuta. Wengi walitoa fedha. Maduka kadhaa yalichapisha maelfu ya karatasi za tangazo hilo bila malipo. Na wajitoleaji walisambaza karatasi hizo umbali wa kilometa nyingi kutoka kwenye nyumba ya Theresa.

Dada yetu mmoja Mkristo ameajiriwa na wakili na alipomweleza kuhusu hali yetu, wakili huyo alijitolea kusaidia. Tulikubali, na hiyo ilikuwa baraka kubwa sana. Alitusaidia kushughulika na waandishi wa vyombo vya habari na mambo ya kisheria yaliyozuka. Isitoshe, alitupendekezea wapelelezi wawili wa kibinafsi walioshughulikia sana kesi hiyo. Hangaiko lao la moyo mweupe kwa ajili yetu, liligusa sana mioyo yetu.

Mjukuu wetu alipopatikana, tulitegemezwa hata zaidi. Maduka kadhaa yalitupatia chakula na bidhaa za matumizi ya nyumbani. Watu wengi walitupatia nguo kwa ajili ya Oscar, vilevile nepi zinazotumiwa mara moja tu, maziwa ya kopo ya watoto, na vidude vya kuchezea vya watoto. Tulipata vitu vingi sana kuliko vile ambavyo Oscar angetumia, basi tulipeana vitu vya ziada kwa wodi ya wazazi ya hospitali moja ya karibu. Kwa sababu vyombo vya habari viliripoti kuhusu kisa hicho, tulipokea maelfu ya kadi na barua kutoka kwa watu wa jumuiya yetu na hata kutoka sehemu nyingine za ulimwengu.

Tulitegemezwa hata zaidi kwenye hotuba ya mazishi ya Theresa, siku ya Jumapili, Oktoba 8. Tulijua kwamba watu wengi walitaka kuhudhuria, lakini idadi ya wale waliokuja ilikuwa zaidi ya tulivyotarajia. Mipango ilifanywa ili tutumie ukumbi wa shule moja ya sekondari ya karibu. Ukumbi huo ulijaa zaidi ya watu 1,400. Kati ya waliohudhuria mlikuwemo watu wa ukoo, marafiki, maafisa wa polisi, meya, na watu wengine wa jumuiya yetu. Pia, waandishi wa vyombo vya habari walikuwepo, na vituo vya televisheni vilichukua filamu ya hotuba hiyo ambayo pia ilionyeshwa moja kwa moja kwenye Internet. Zaidi ya hayo, mamia ya watu walisimama kwenye sebule ya shule hiyo na wengine walikusanyika nje wakijikinga mvua kwa miavuli huku wakisikiliza hotuba kupitia vipaza-sauti vilivyoandaliwa. Hotuba hiyo ilitoa ushahidi mkubwa kuhusu imani zetu za Biblia.

Baadaye, mamia ya watu walisubiri kwenye foleni ili kutoa rambirambi. Tulikaa hapo kwa muda wa saa tatu, tukiwakumbatia watu wote waliofika na kuwashukuru kwa kuja. Baada ya hotuba ya mazishi, hoteli moja iliandaa chakula kwa ajili ya zaidi ya watu 300, wakiwemo watu wetu wa ukoo, marafiki wa karibu, na wengine waliosaidia kumpata mjukuu wetu.

Hatujui tuseme nini ili kuwashukuru watu waliokuja kutusaidia, hasa watu tusiowajua. Jambo hilo limetufanya tuazimie hata zaidi kushiriki kikamili katika huduma ya Kikristo kwa kuwa kuna watu wenye fadhili tunaotaka kuwapa habari njema ya Ufalme wa Mungu.—Mathayo 24:14.

Jinsi Kutaniko Lilivyoitikia

Tangu tulipopatwa na msiba huo, tulitegemezwa sana na ndugu na dada zetu Wakristo. Tulitegemezwa sana na kutaniko letu la Mashahidi wa Yehova na vilevile makutaniko jirani.

Hata kabla hatujafika nyumbani kutoka North Carolina, tayari wazee wa kutaniko letu walikuwa wamefanya mipango ya kumtafuta Theresa. Ndugu na dada zetu wengi waliomba ruhusa kazini ili wamtafute. Wengine waliwaambia waajiri wao kwamba walikuwa tayari kukatwa mshahara. Lakini, waajiri fulani waliwapa ruhusa bila kuwakata mshahara. Katika kipindi ambacho Theresa alikuwa amepotea, baadhi ya ndugu zetu wa kiroho walikaa pamoja na Jonathan ili asiwe peke yake. Akina ndugu na dada walikuja kusafisha na kupanga nyumba yetu. Wengine walisaidia kuwapikia wajitoleaji na kupokea simu.

Majuma sita hivi baada ya kifo cha Theresa, mke wangu na Jonathan walikabili kibarua kigumu—kuvikagua vitu vya Theresa na kuviondoa vitu visivyohitajiwa kutoka kwenye nyumba yake. Jonathan aliona hawezi kuishi ndani ya nyumba waliyokuwa wameishi pamoja na Theresa. Basi aliamua kuiuza. Kuvikagua vitu vya Theresa ilikuwa kazi yenye kuhuzunisha sana. Kila kitu kiliwakumbusha juu yake na jinsi walivyomkosa sana. Lakini, ndugu zetu walitusaidia pia na kazi hiyo. Walitusaidia kupakia vitu vya Theresa masandukuni na hata wakarekebisha sehemu fulani za nyumba ili iuzwe.

Jambo la maana zaidi ni kwamba ndugu na dada zetu walitegemeza familia yetu kiroho na kihisia-moyo. Walitupigia simu na kututembelea ili kututia moyo. Wengi walituma kadi na barua zilizotugusa moyo sana. Waliendelea kututegemeza kwa upendo kwa miezi mingi.

Baadhi ya ndugu na dada zetu walituambia kwamba iwapo tunahitaji tu mtu wa kutusikiliza basi tuwajulishe. Tumekubali msaada wao wa fadhili. Inafariji sana kuwaeleza marafiki unawaopenda na kutumaini jinsi unavyohisi! Kwa kweli, mfano wao unapatana na mithali hii ya Biblia: “Rafiki hupenda sikuzote; na ndugu amezaliwa kwa siku ya taabu.”—Mithali 17:17; 18:24.

Jinsi Familia Yetu Ilivyoathiriwa

Sina budi kusema kwamba kukabiliana na kifo cha Theresa hakujawa jambo rahisi kwangu na kwa familia yangu. Kifo chake kimebadilisha sana maisha yetu. Kuna nyakati ninapokasirika kwa sababu hayuko pamoja nami. Ninakosa makumbatio na mabusu yake.

Mke wangu na Theresa walikuwa marafiki wakubwa. Hakuna siku ambayo hawakuzungumza pamoja. Walitumia muda mwingi sana wakizungumza kuhusu mimba ya Theresa. Walitayarisha chumba cha mtoto pamoja.

Vicki aeleza anavyohisi: “Ninakosa mambo mengi sana. Ninakosa jinsi tulivyohubiri naye. Ninakosa jinsi tulivyonunua vitu pamoja. Jambo linaloniumiza zaidi ni kutomwona akimshika mtoto wake—linanihuzunisha sana. Ninajua jinsi alivyompenda sana Oscar hata kabla hajazaliwa. Alijua kuwa atapata mvulana. Baada ya kumpa Theresa blanketi niliyomtengenezea mtoto, aliniandikia kadi iliyosema hivi:

‘Mama Mpendwa,

Asante sana kwa blanketi maridadi ya mtoto. Ninathamini sana kazi ngumu uliyofanya ili kuitengeneza. Ningependa kukushukuru tena kwa ajili ya msaada wote na kitia-moyo ulichonipa ili nikabiliane na baadhi ya hali ngumu sana maishani mwangu. Nitakukumbuka na kukushukuru sikuzote kwa hilo. Nimesikia kwamba siku moja mtu hukua kisha anatambua kwamba rafikiye mkubwa ni mamaye. Naam, namshukuru Yehova kila siku kwamba nilitambua jambo hilo mapema. Nitakupenda daima.’”

Vilevile, tuliumia sana kuona hali ngumu iliyomkumba mwana-mkwe wetu. Oscar alipokuwa hospitalini, Jonathan alikabili mojawapo ya hali ngumu zaidi maishani mwake. Kwa kuwa aliamua kukaa kwa muda mfupi nasi, ilimbidi ahamishe vitu vya mtoto walivyokuwa wamepanga kwenye nyumba yao pamoja na Theresa. Alihamisha bembea-farasi, kitanda cha mtoto, na wanasesere kwenye nyumba yetu.

Mambo Yaliyotusaidia Kukabiliana na Hali Hiyo

Unapompoteza mpendwa kupitia msiba wa aina hiyo, maswali na hisia zenye kusumbua huzuka. Kuna wakati ambapo mimi nikiwa mzee Mkristo nimejitahidi kuwafariji wengine wanaopambana na maswali na hisia hizo. Lakini unapofiwa, hisia zaweza kukuvuruga usifikiri ifaavyo.

Kwa mfano, kwa kuwa nilijua hali ya Theresa na kwamba tungesafiri kwa juma moja, nilimwomba Yehova amlinde. Alipopatikana akiwa ameuawa, nakubali kwamba mwanzoni nilijiuliza ni kwa nini sala zangu hazikujibiwa. Bila shaka, ninajua kwamba Yehova hawahakikishii watu wake mmoja-mmoja ulinzi wa kimuujiza. Niliendelea kusali ili nielewe jambo hilo. Nimefarijiwa kujua kwamba Yehova huwalinda watu wake kiroho—yaani, yeye huandaa tunachohitaji ili kulinda uhusiano wetu pamoja naye. Ulinzi huo ndio wa maana zaidi, kwa kuwa unaweza kuathiri wakati wetu ujao wa milele. Katika maana hiyo, Yehova alimlinda Theresa. Alikuwa akimtumikia kwa uaminifu hadi wakati wa kifo chake. Nimepata amani kwa kujua kwamba mataraja yake ya kuishi wakati ujao yako mikononi mwa Yehova mwenye upendo.

Maandiko kadhaa yamenifariji sana. Yafuatayo ni baadhi ya yale yaliyonisaidia kukabiliana na hali hiyo:

“Kutakuwa na ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.” (Matendo 24:15) Kwa muda mrefu nimeamini ahadi ya Biblia ya kufufuliwa kuishi katika dunia paradiso, lakini sasa ninaliona tumaini hilo kuwa halisi hata zaidi. Kujua kwamba nitamkumbatia Theresa tena hunipa nguvu za kuvumilia kila siku.

“Yehova . . . ni Mungu, si wa wafu, bali wa walio hai, kwa maana kwake, wao wote wako hai.” (Luka 20:37, 38) Inafariji sana kujua kwamba wafu watakaofufuliwa siku moja “wako hai” kwa Yehova hata sasa. Basi, katika maana hiyo, Theresa wetu mpendwa bado yu hai.

Vicki angependa kutaja maandiko kadhaa ya Biblia ambayo yamemwimarisha:

“‘Haiwezekani Mungu kusema uwongo.’ (Waebrania 6:18; Tito 1:2) Kwa sababu Yehova hawezi kusema uwongo, ninajua kuwa atatimiza ahadi yake ya kuwafufua wafu.

“‘Msistaajabie hili, kwa sababu saa inakuja ambayo katika hiyo wote wale waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho watasikia sauti yake [Yesu] na kutoka.’ (Yohana 5:28, 29) Maneno ‘makaburi ya ukumbusho’ hudokeza kwamba Theresa yu katika kumbukumbu la Yehova hadi atakapomtumia Mwanawe, Yesu Kristo, kumfufua. Ninajua kwamba yu salama tu katika kumbukumbu kamilifu la Yehova.

“‘Katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na utoaji-shukrani acheni maombi yenu ya bidii yajulishwe kwa Mungu; na amani ya Mungu izidiyo fikira yote kwa ubora italinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili kwa njia ya Kristo Yesu.’ (Wafilipi 4:6, 7) Mimi husali hasa ili roho ya Yehova iniimarishe. Ninapohuzunika, mimi humfikia Yehova na kusema, ‘Ninahitaji roho yako zaidi,’ naye hunisaidia nivumilie siku nyingine moja. Nyakati nyingine hata siwezi kutamka maneno hayo, lakini yeye hunipa nguvu za kuendelea.”

Kwa hakika, Yehova ametusaidia kukabiliana na huo msiba mbaya sana. Naam, bado twahuzunika kuhusu mpendwa wetu Theresa. Twajua kwamba huzuni yetu haitaisha kabisa hadi tutakapomkumbatia tena katika ulimwengu mpya wa Yehova. Kwa sasa, tumeazimia hata zaidi kumtumikia Yehova kwa uaminifu. Jonathan ameazimia kufanya yote awezayo ili kumlea Oscar ampende na kumtumikia Yehova. Mimi na Vicki tutamsaidia kwa vyovyote. Ni tamaa yetu ya moyoni kumkaribisha tena Theresa katika ulimwengu mpya wa Mungu na kumwonyesha mwanawe ambaye hakumshika hata kidogo.

[Picha katika ukurasa wa 19]

Binti yetu Theresa, akisikiliza pigo la moyo la mtoto wake

[Picha katika ukurasa wa 21]

Tulitegemezwa sana kwenye hotuba ya mazishi

[Picha katika ukurasa wa 23]

Nikiwa na mke wangu Vicki, kwenye arusi ya Theresa

[Picha katika ukurasa wa 23]

Mjukuu wetu Oscar