Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sala Yaweza Kunisaidiaje?

Sala Yaweza Kunisaidiaje?

Vijana Huuliza . . .

Sala Yaweza Kunisaidiaje?

“Sala ndiyo iliyonisaidia kurekebisha maisha yangu.”—Brad. *

VIJANA wengi wanasali—wengi zaidi ya unavyoweza kuwazia. Uchunguzi wa Kura ya Maoni ya Gallup kuhusu vijana wenye umri wa miaka 13 hadi 17 katika Marekani ulifunua kwamba asilimia 56 ya vijana husali kabla ya kula chakula cha jioni. Uchunguzi kuhusu vijana waliokomaa ulionyesha kwamba asilimia 62 husali kila siku.

Hata hivyo, kwa vijana wengi, sala ni desturi tu isiyo na maana yoyote. Ni vijana wachache tu walio na kile ambacho Biblia huita “ujuzi sahihi wa Mungu.” (Wakolosai 1:9, 10) Basi, hawamwoni Mungu kuwa wa maana sana maishani mwao. Matineja fulani waliulizwa ikiwa wamewahi kumwomba Mungu msaada kabla ya kufanya uamuzi wa maana. Msichana mmoja alijibu hivi: “Mimi husali kwa Mungu sikuzote ili aniongoze kufanya maamuzi yanayofaa maishani.” Hata hivyo, alikiri hivi: “Sikumbuki mfano mmoja hususa kwa sasa.” Basi, haishangazi kwamba vijana wengi hawaamini kuwa sala ina nguvu au itawasaidia!

Hata hivyo, kama Brad, aliyetajwa mwanzoni, maelfu ya vijana wameona nguvu za sala maishani mwao. Hata wewe unaweza! Makala moja ya wakati uliopita ilionyesha ni kwa nini twaweza kuwa na uhakika kwamba Mungu atasikiliza sala zetu. * Sasa swali ni, Sala yaweza kukusaidiaje? Acheni kwanza tuchunguze jinsi Mungu hujibu sala zetu.

Jinsi Mungu Hujibu Sala

Katika nyakati za Biblia, wanaume fulani wenye imani walijibiwa sala zao moja kwa moja, au hata kupitia miujiza. Kwa mfano, Mfalme Hezekia alipojua kwamba ana ugonjwa usiotibika, alimwomba Mungu dua ili amwokoe. Mungu alijibu hivi: “Nimeyasikia maombi yako, na kuyaona machozi yako; tazama, nitakuponya.” (2 Wafalme 20:1-6) Wanaume na wanawake wengine wenye kumhofu Mungu waliona Mungu akiwaokoa kimuujiza.—1 Samweli 1:1-20; Danieli 10:2-12; Matendo 4:24-31; 10:1-7.

Hata hivyo, hata katika nyakati za Biblia kwa kawaida Mungu hakusuluhisha mambo kimuujiza. Mara nyingi, Mungu alijibu sala za watumishi wake kwa kuwasaidia ‘wapate kujazwa ujuzi sahihi wa mapenzi yake katika hekima yote na ufahamivu wa kiroho’ bali si kwa kutumia miujiza. (Wakolosai 1:9, 10) Naam, Mungu aliandaa msaada kwa kuwaimarisha watu wake kiroho na kiadili—akiwapa hekima na ujuzi wa kufanya maamuzi yenye hekima. Wakristo walipokabili hali ngumu, haikuwa lazima Mungu aondoe jaribu hilo. Badala yake, aliwapa “nguvu ipitayo iliyo ya kawaida” ili waweze kulivumilia!2 Wakorintho 4:7; 2 Timotheo 4:17.

Vivyo hivyo leo, huenda sala yako isijibiwe kwa njia yenye kustaajabisha. Lakini kama alivyofanya zamani, Mungu anaweza kukupa roho yake takatifu na kukuimarisha ili ushughulikie hali zozote unazokabili. (Wagalatia 5:22, 23) Ili tuonyeshe jambo hilo waziwazi, acheni tuchunguze jinsi sala inavyoweza kukusaidia katika njia nne hususa.

Msaada Unapofanya Maamuzi

Karen alikuwa akichumbiana na kijana mmoja aliyeonekana kuwa ana miradi mikubwa ya kiroho. “Kila mara alikuwa akiniambia kwamba angependa kuwa mzee wa kutaniko,” yeye asema. Hilo lilionekana kuwa jambo zuri. Lakini “alizungumza sana pia kuhusu biashara aliyokuwa akianzisha na vitu ambavyo ataweza kuninunulia. Nilianza kushuku unyofu wake.” Karen alisali juu ya jambo hilo. “Nilimsihi Yehova afumbue macho yangu na anionyeshe mambo niliyopaswa kujua kuhusu kijana huyo.”

Nyakati nyingine kusali hunufaisha kwa sababu kunakuwezesha kutua na kufikiria mambo kulingana na maoni ya Yehova. Lakini Karen alihitaji ushauri unaoweza kutumika. Je, angejibiwa kupitia muujiza? Hebu fikiria simulizi moja la Biblia kumhusu Mfalme Daudi. Alipojua kwamba Ahithofeli, rafikiye mwenye kutumainika, alikuwa akimshauri Absalomu, mwanawe aliyemsaliti, Daudi alisali hivi: “Ee BWANA, nakusihi, uligeuze shauri la Ahithofeli liwe ubatili.” (2 Samweli 15:31) Lakini Daudi alitenda pia kupatana na sala yake. Alimpa Hushai rafikiye utume huu: “Ndipo utayavunja mashauri ya Ahithofeli kwa ajili yangu.” (2 Samweli 15:34) Vivyo hivyo, Karen alitenda kupatana na sala yake kwa kuzungumza na mzee Mkristo mkomavu aliyemjua huyo kijana rafikiye. Mzee huyo alimthibitishia Karen mashaka yake: Kijana huyo hakuwa amefanya maendeleo mengi ya kiroho.

Karen asema: “Hali hiyo ilinionyesha waziwazi umuhimu wa sala.” Inasikitisha kusema kwamba, kijana huyo alifuatia utajiri na akaacha kumtumikia Mungu. “Iwapo ningeolewa naye, ningekuwa nikienda kwenye mikutano ya Kikristo peke yangu,” asema Karen. Sala ilimsaidia Karen kufanya uamuzi unaofaa.

Msaada wa Kudhibiti Hisia Zako

Biblia yasema hivi kwenye Mithali 29:11: “Mpumbavu hudhihirisha hasira yake yote; bali mwenye hekima huizuia na kuituliza.” Tatizo ni kwamba watu wengi leo hupata mikazo mingi ya kihisia na mara nyingi wanashindwa kudhibiti hasira. Nyakati nyingine, matokeo huwa balaa. Kijana mmoja anayeitwa Brian akumbuka hivi: “Kulikuwa na mizozo kati yangu na mfanya-kazi mwenzangu. Siku moja akachomoa kisu.” Ikiwa ni wewe ungefanya nini? Brian alisali. Anasema hivi: “Yehova alinisaidia kutulia, na nikamshawishi mfanya-kazi huyo asitumie kisu. Aliangusha kisu na kuondoka.” Brian alidhibiti hisia zake na hilo lilimfanya asitende kwa hasira. Huenda hilo liliokoa maisha yake pia.

Huenda usitishwe kwa kisu. Lakini kutakuwa na hali nyingi maishani ambapo utahitaji kudhibiti hisia zako. Sala yaweza kukusaidia kutulia.

Msaada Wakati Unapokuwa na Wasiwasi

Barbara anakumbuka alipokuwa “akikabili hali ngumu” miaka kadhaa iliyopita. Asema hivi: “Hakuna kitu kilichokuwa sawasawa iwe ni kazi yangu, familia, marafiki. Sikujua la kufanya.” Barbara alisali ili apate msaada. Lakini kulikuwa na tatizo. “Sikujua nitamwomba Yehova nini,” yeye asema. “Mwishowe, nilimwomba amani ya akili. Nilimwomba kila usiku anisaidie nisiwe na wasiwasi kuhusu kila kitu.”

Sala hiyo ilimsaidiaje? Asema hivi: “Siku chache baadaye, nilitambua kwamba ingawa matatizo yangu yote hayakuisha, sikuyafikiria sana wala kuyahangaikia tena.” Biblia huahidi hivi: “Acheni maombi yenu ya bidii yajulishwe kwa Mungu; na amani ya Mungu izidiyo fikira yote kwa ubora italinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili kwa njia ya Kristo Yesu.”—Wafilipi 4:6, 7.

Msaada wa Kumkaribia Mungu

Fikiria mfano wa kijana anayeitwa Paul. Yeye asema: “Nilikuwa tu nimeanza kuishi na watu fulani wa ukoo. Usiku mmoja nikashuka moyo sana. Nilikuwa nimemaliza tu shule ya sekondari na niliwakosa sana rafiki zangu wote. Usiku huo, nilitokwa machozi nilipokumbuka pindi tulizofurahia pamoja.” Paul angefanya nini? Kwa mara ya kwanza, alisali kwa bidii. Asema hivi: “Nilifunua mambo yaliyokuwa moyoni mwangu na kumwomba Yehova nguvu na amani ya akili.”

Matokeo yakawa nini? Paul akumbuka hivi: “Niliamka asubuhi nikiwa nimefarijiwa kuliko wakati mwingine wowote maishani mwangu. Badala ya kusumbuka kiakili nilipata ‘amani ya Mungu izidiyo fikira yote.’” Moyo wake ukiwa umetulia, Paul angeweza kuyaona mambo akiwa na mtazamo unaofaa. Punde si punde akang’amua kwamba ‘siku njema za kale’ hazikuwa njema hata kidogo. (Mhubiri 7:10) Kwa kweli, “marafiki” aliowakosa sana hawakuwa wenye uvutano mzuri.

Zaidi ya yote, Paul alikuja kuona kwamba Yehova anamjali. Aliona ukweli wa maneno haya ya Yakobo 4:8: “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia.” Hilo lilikuwa badiliko kubwa maishani mwa Paul. Alichochewa kumweka Yehova kwanza maishani mwake kabla ya mambo yote na kuweka maisha yake wakfu kwa Yehova.

Sema na Mungu!

Mambo hayo mazuri yaliyoonwa yanakuhakikishia kuwa sala yaweza kukusaidia. Bila shaka, hilo linawezekana iwapo tu unataka sana kumjua Mungu, naam, kusitawisha urafiki pamoja naye. Inasikitisha kwamba vijana wengi huahirisha kufanya hivyo. Carissa alilelewa katika familia ya Kikristo. Lakini yeye anakiri hivi: “Nafikiri ni katika miaka michache tu iliyopita ambapo nimetambua umuhimu mkubwa wa uhusiano wetu usio na kifani pamoja na Yehova.” Brad, aliyetajwa mwanzoni, alilelewa akiwa Mkristo lakini aliacha ibada ya kweli kwa miaka kadhaa. Yeye asema: “Nilimgeukia Yehova baada ya kutambua nilichokuwa nimepoteza. Sasa ninajua kwamba bila uhusiano huo, maisha hayapendezi na yanakosa maana.”

Hata hivyo, usisubiri hadi matatizo yatokee ndipo umkaribie Mungu. Anza kusema naye sasa—kwa ukawaida! (Luka 11:9-13) ‘Ufunue moyo wako mbele zake.’ (Zaburi 62:8) Punde si punde utagundua kwamba sala yaweza kukusaidia kwelikweli!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Majina mengine yamebadilishwa.

^ fu. 6 Ona makala “Vijana Huuliza . . . Je, Mungu Atasikiliza Sala Zangu?” katika toleo la Amkeni! la Juni 22, 2001.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 15]

Sala Yaweza Kukusaidia

Kufanya maamuzi mazuri zaidi

Kutulia unapopatwa na mikazo

Kupata faraja unapokuwa na wasiwasi

Kumkaribia Mungu zaidi