Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ni Nani Aliye Mpinga-Kristo?

Ni Nani Aliye Mpinga-Kristo?

Maoni ya Biblia

Ni Nani Aliye Mpinga-Kristo?

“MMESIKIA KWAMBA MPINGA-KRISTO ANAKUJA.”—1 YOHANA 2:18.

IKIWA ungeonywa kwamba mhalifu hatari ameonekana akielekea kwenye mtaa wenu, ungefanya nini? Yaelekea utatafuta habari kamili kuhusu sura na mbinu zake. Utakaa chonjo.

Hali kama hiyo ipo leo. Tumeonywa na maneno ya mtume Yohana: “Kila usemi uliopuliziwa ambao hauungami Yesu hautokani na Mungu. Zaidi ya hilo, huu ndio usemi uliopuliziwa wa mpinga-Kristo ambao mmesikia ulikuwa ukija, na sasa tayari umo katika ulimwengu.” (1 Yohana 4:3) Je, kuna mpinga-Kristo, adui wa Mungu na mdanganyifu, anayetisha ustawi wa wanadamu wote sasa?

Yohana alitumia neno “mpinga-Kristo” mara tano katika barua zake mbili. Linamaanisha kikundi kinachopinga yale ambayo Biblia hufundisha kuhusu Yesu Kristo na hutia ndani walaghai wanaojifanya kuwa Kristo au kwamba wametumwa naye. Biblia hutoa habari zinazotegemeka kuhusu mpinga-Kristo. Lakini kama inavyotokea nyakati nyingine kuhusiana na wahalifu, habari zisizotegemeka kuhusu kikundi hiki cha kifumbo zimepewa uangalifu zaidi ya zile za kweli.

Utambulisho Wenye Makosa

Tangu siku za mtume Yohana, watu wamedai kwamba maneno ya Yohana kuhusu mpinga-Kristo humaanisha mtu mmoja hususa. Watu mbalimbali wametajwa kuwa eti wao ndio mpinga-Kristo. Karne nyingi zilizopita wengi walifikiri kuwa Maliki Nero wa Roma ndiye aliyekuwa mpinga-Kristo. Chuki nyingi na hofu kubwa iliyosababishwa na Adolf Hitler iliwahakikishia watu wengi kwamba yeye ndiye mpinga-Kristo. Mwanafalsafa Mjerumani Friedrich Nietzsche hata alipewa jina “Mpinga-Kristo.” Na bado wengine wanaamini kuwa mpinga-Kristo bado hajatokea na atakuja kama mwanasiasa mjanja na mkatili anayetaka kuutawala ulimwengu. Wanaamini kwamba hayawani-mwitu anayetajwa kwenye Ufunuo sura ya 13 ndiye hasa yule mpinga-Kristo aliyetajwa na Yohana. Wanasema kwamba alama ya hayawani-mwitu ya 666 itamtambulisha kwa njia fulani huyo mtetezi wa uovu atakayekuja wakati ujao.

Watu wanaoendeleza maoni hayo hufikiri kwamba Yohana alikuwa akizungumzia mpinga-Kristo mmoja tu. Lakini maneno yake yanaonyesha nini? Ona andiko la 1 Yohana 2:18: “Kama vile ambavyo mmesikia kwamba mpinga-Kristo anakuja, hata sasa kumekuja kuwa wapinga-Kristo wengi.” Naam, “wapinga-Kristo wengi” ndio waliosababisha hali mbaya ya kiroho huko nyuma katika karne ya kwanza, wala si mmoja. Leo kuna wapinga-Kristo wengi, wala si mmoja, ambao wanafanyiza jamii ya wapinga-Kristo. Wakiwa kikundi, wamedhoofisha sana hali ya kiroho ya wanadamu. (2 Timotheo 3:1-5, 13) Ni nani walio sehemu ya jamii ya mpinga-Kristo?

Acheni tumchunguze hayawani-mwitu anayetajwa kwenye Ufunuo sura ya 13. Mtume Yohana aliandika: “Yule hayawani-mwitu niliyemwona alikuwa kama chui, lakini miguu yake ilikuwa kama ile ya dubu, na kinywa chake kilikuwa kama kinywa cha simba.” (Ufunuo 13:2) Sifa hizo zaonyesha nini?

Wasomi wa Biblia wametambua uhusiano uliopo kati ya Ufunuo sura ya 13 na Danieli sura ya 7. Mungu alimwonyesha Danieli njozi ya mahayawani-mwitu wa ufananisho, waliotia ndani chui, dubu, na simba. (Danieli 7:2-6) Nabii wa Mungu alisema wanafananisha nini? Aliandika kwamba wanyama-mwitu hao wanafananisha wafalme wa dunia, au serikali. (Danieli 7:17) Basi twaweza kukata kauli iliyo wazi kwamba hayawani-mwitu wa Ufunuo huwakilisha serikali za wanadamu. Kwa kuwa serikali hizo huupinga Ufalme wa Mungu, hizo hufanyiza sehemu fulani ya jamii ya mpinga-Kristo.

Ni Nani Wengine Wanaofanyiza Jamii ya Mpinga-Kristo?

Kristo, Mwana wa Mungu, alipokuwa duniani, alikuwa na maadui wengi. Ijapokuwa sasa hawezi kufikiwa na wanadamu, bado ana wapinzani leo. Ebu angalia baadhi ya wapinzani hao.

Mtume Yohana alisema: “Ni nani aliye mwongo ikiwa si yeye ambaye hukana kwamba Yesu ndiye Kristo? Huyu ndiye mpinga-Kristo, yeye ambaye hukana Baba na Mwana.” (1 Yohana 2:22) Waasi-imani na viongozi wa ibada bandia hupotosha mafundisho ya Yesu yaliyo wazi kuwa uwongo wa kidini unaotatanisha. Watu hao hukataa ukweli wa Biblia nao hueneza uwongo wakitumia jina la Mungu na la Kristo. Wao hukana uhusiano wa kweli uliopo kati ya Baba na Mwana kwa fundisho lao la Utatu. Kwa hiyo, wao pia ni sehemu ya mpinga-Kristo.

Katika Luka 21:12, Yesu aliwaonya hivi wanafunzi wake: “Watu watawawekea mikono ili wawashike na kuwanyanyasa nyinyi, wakiwakabidhi nyinyi kwenye masinagogi na magereza . . . kwa ajili ya jina langu.” Tangu karne ya kwanza, Wakristo wa kweli wamevumilia mnyanyaso mkali. (2 Timotheo 3:12) Wachochezi wa minyanyaso hiyo humpinga Kristo. Wao pia ni sehemu ya mpinga-Kristo.

“Yeye asiye upande wangu yuko dhidi yangu, naye asiyekusanya pamoja nami hutawanya.” (Luka 11:23) Hapo Yesu atangaza kwamba wote wanaompinga yeye na wanaopinga makusudi ya Mungu anayotegemeza ni sehemu ya mpinga-Kristo. Watu hao watapatwa na nini mwishowe?

Ni Nini Kitakachowapata Wapinga-Kristo?

‘[Mungu] atawaharibu wasemao uongo; Bwana humzira mwuaji na mwenye hila,’ yasema Zaburi 5:6. Je, hilo lawahusu wapinga-Kristo? Naam. Mtume Yohana aliandika hivi: “Wadanganyi wengi wameenda kuingia katika ulimwengu, watu ambao hawaungami Yesu Kristo kuwa alikuja katika mwili. Huyu ndiye mdanganyi na mpinga-Kristo.” (2 Yohana 7) Mungu Mweza Yote atawaharibu wapinga-Kristo kwa sababu ya uwongo na hila yao.

Huku wakati wa kutekeleza hukumu hiyo ukaribiapo, Wakristo wa kweli hawapaswi kuruhusu hila na mikazo ya wapinga-Kristo, hasa ya waasi-imani, idhoofishe imani yao. Onyo la Yohana ni la uharaka: “Jiangalieni nyinyi wenyewe, kwamba msipoteze mambo ambayo sisi tumefanya kazi kutokeza, bali kwamba mpate kuwa na thawabu yenye kujaa.”—2 Yohana 8.

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 20]

Nero kwenye ukurasa wa 2 na 20: Courtesy of the Visitors of the Ashmolean Museum, Oxford