Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Elimu Ninaandika kuwashukuru kwa ajili ya ule mfululizo “Elimu Inayoleta Maisha Bora.” (Desemba 22, 2000) Mfululizo huo ulionyesha waziwazi jinsi Yehova anavyojaribu kuwafikia wote wenye mioyo ifaayo, kupitia tengenezo lake. Nilisisimuka niliposoma jinsi kituo cha televisheni na magazeti yalivyoripoti juu ya kuanza kuchapishwa kwa gazeti la Amkeni! katika lugha ya Kisamoa. Hilo lilionyesha utimizo wa maneno ya Yesu kwenye Matendo 1:8: “Mtakuwa mashahidi wangu . . . hadi sehemu ya mbali zaidi sana ya dunia.”

J. D., Marekani

Akina Baba Waliotoroka Nyumbani Nina umri wa miaka 15 na ningependa kuwashukuru kwa dhati kwa ajili ya makala za “Vijana Huuliza . . .” zenye vichwa “Kwa Nini Baba Alituacha?” (Novemba 22, 2000) na “Naweza Kukabilianaje na Hali Baada ya Baba Kutuacha?” (Desemba 22, 2000) Nimekumbwa na hisia mbalimbali kama vile kukasirika, kuhuzunika, na kufadhaika. Makala hizo zilionyesha kwamba si mimi tu ninayekumbwa na hali hiyo na kwamba hisia zangu ni za kawaida kabisa. Tafadhali endeleeni kuandika makala hizo nzuri sana.

S. L., Ujerumani

Nina umri wa miaka 10, na ni kana kwamba nimekuwa nikisubiri makala hizo maisha yangu yote! Niliteseka sana babangu alipotuacha. Makala hizo zilikuja kwa wakati ufaao.

M. D., Ujerumani

Simulizi la Maisha Asanteni kwa makala “Nimeandaliwa Tumaini Linalonitegemeza.” (Desemba 22, 2000) Nimekuwa nikimchukia babangu kwa kuwa tangu nilipokuwa mtoto, nimemwona akimtenda vibaya mamangu. Nilijua kwamba chuki ni mbaya, lakini ilikuwa vigumu sana kudhibiti hisia zangu. Lakini nilisoma jinsi Tatjana Vileyska alivyojaribu kuacha kumchukia mwanamume aliyemwua mamake. Ningependa kumwiga.

A. K., Japani

Nilitokwa machozi niliposoma kuhusu hali ya kuhuzunisha iliyomkabili Tatjana alipowapoteza wazazi wake. Masimulizi hayo ya maisha hunikumbusha kila mara kwamba watu wengi ulimwenguni wanavumilia magumu makubwa kwa mafanikio na kupata shangwe licha ya matatizo yao ya kibinafsi.

J. R., Marekani

Nimemaliza tu kusoma simulizi linalovuta fikira la Tatjana Vileyska. Sitasahau simulizi lake kwa urahisi. Bila shaka, kuvumilia mambo aliyokabili kabla ya kujifunza ukweli wa Biblia na bado kuweza kutabasamu ni muujiza wa kiroho.

S. S., Marekani

Kuokoa Ndoa Nawashukuru kwa dhati kwa ajili ya ule mfululizo katika gazeti la Amkeni! la Januari 8, 2001, “Je, Twaweza Kuokoa Ndoa Yetu?” Mwaka mmoja uliopita mimi na mke wangu tulikuwa na matatizo ya ndoa. Sote wawili tulilelewa katika familia ambazo watu walifokeana kwa ukawaida. Basi tulikuwa tukirushiana maneno yanayoudhi, na mambo yalikuwa yakiharibika. Lakini tumeanza kutumia kanuni za Biblia, na tuna furaha nyingi sasa.

R. O., Marekani

Nikiwa mzee wa kutaniko, nimeona kwamba mojawapo ya hali ngumu zaidi ninazokabili ni kujaribu kuwasaidia wenzi wanaohisi kwamba ndoa zao hazina upendo. Kwa wazi, kwa miaka mingi tumepata mashauri mengi sana ya Kimaandiko kupitia vichapo. Hata hivyo, kwa kutazama jalada la gazeti hilo, niliona kuwa litatusaidia kuwaandalia watu hao msaada wa moja kwa moja. Makala hizo zilitimiza matarajio yangu!

L. R., Marekani