Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maisha Yangu Nikiwa Mchoraji

Maisha Yangu Nikiwa Mchoraji

Maisha Yangu Nikiwa Mchoraji

KAMA ILIVYOSIMULIWA NA SHIZUKO KAWABATA

“Mashahidi wa Yehova, Watu Wanaopendeza Sana Wanaotangaza Habari Njema Ulimwenguni Pote” ndicho kilichokuwa kichwa cha mojawapo ya picha zangu zilizoonyeshwa kwenye maonyesho ya sanaa huko Versailles, Ufaransa, mnamo mwaka wa 1999.

SIKU chache tu kabla ya maonyesho hayo, Mashahidi wa Yehova nchini Ufaransa walikuwa wamegawanya trakti milioni 12 kotekote nchini humo ambazo zilionyesha jinsi serikali ilivyowadhulumu. Nilituzwa zawadi ya pekee kwa sababu ya picha yangu ya kuwasifu Mashahidi. Baadaye, mtu aliyenikabidhi zawadi hiyo alisema hivi: “Wewe ni jasiri, lakini mimi pia ni jasiri. Ndiyo sababu ninakukabidhi tuzo hili la pekee.”

Wachoraji wengi hujaribu kuonyesha hisia zao katika picha zao. Hivyo ndivyo mimi hujaribu kufanya. Mimi huchora jinsi ninavyohisi, na picha zangu husisimua, zikionyesha shangwe na furaha yangu. Nilipokuwa mchanga nilipata shangwe kwa kutumia uwezo wa kubuni nilipokuwa nikichora.

Kwa Nini Nilianza Kuchora

Nilizaliwa mnamo mwaka wa 1920 na wazazi matajiri huko Morioka, Japani. Mimi na dadangu mkubwa tulifundishwa na walimu wetu dansi za Kijapani, kupanga maua, sherehe za chai, kucheza ala ya muziki ya koto (zitha ya Kijapani), piano, kuimba, na kadhalika. Nilichukia mambo hayo yote. Walimu walipokuja, nilikimbia kujificha. Iliwabidi watumishi wanitafute na kunileta kwa nguvu.

Nilichukia jinsi masomo hayo yalivyofanya nihisi nimebanwa. Watu nisiowajua waliamua jinsi nilivyopaswa kucheza dansi, kupanga maua, na kuandaa chai. Nilihisi kuwa nimebanwa, ni kana kwamba singeweza kujibunia mambo na kujiwekea miradi. Hata hivyo, nilipokuwa nikichora picha hakuna aliyenichunga. Hakuna aliyeniambia la kufanya. Huo ndio uhuru niliotamani.

Kwa kuwa sikuwa na mwalimu wa somo la sanaa, nilijibunia michoro na hakuna mtu aliyenichambua. Pole kwa pole nikawa mchoraji shupavu. Nilipokuwa na miaka 12 hivi, nilianza kuchukua tai za babangu za hariri na kuchora juu ya tai hizo. Punde si punde, tukatengeneza nguo shuleni. Mwalimu alishangaa alipoona nimekata nusu ya upande wa mbele wa nguo hiyo na kuishonelea kitambaa cheupe. Hata hivyo, sawa na babangu, mwalimu huyo hakusema lolote.

Mambo Niliyotarajia na Niliyotimiza

Tangu nilipokuwa katika shule ya msingi, nilisema kwamba nitakapokuwa mkubwa nitakuwa mchoraji. Mradi wangu haukubadilika, na nilitaka kwenda chuo kikuu ili kusomea uchoraji; lakini wazazi wangu hawakukubali. Walisema kwamba nchini Japani, mhitimu wa somo la uchoraji hangeolewa. Basi nikasomea kozi ya kutunza nyumba.

Nilipenda mashairi na vitabu vya lugha za kigeni na nilivisoma sana. Hata hivyo, wakati huo vilionwa kuwa vichapo vya adui. Hata ilikuwa hatari kupatikana na vichapo hivyo. Nilikuwa nimefunzwa Kifaransa shuleni kwa miaka mitano na mwalimu Mfaransa, lakini hali zilibadilika nchini Japani hivi kwamba endapo ungependezwa na lugha ya kigeni watu wangekushuku. Tulinyimwa uhuru wa usemi.

Mnamo mwaka wa 1943, wakati Vita ya Pili ya Ulimwengu ilipochacha, nilifurahi niliposikia kwamba mwanamume mmoja alinichagua niwe mchumba wake baada ya kutazama picha 40 za wasichana waliofikia umri wa kuolewa. Baadaye nilijua kwamba mamake na rafikiye walikuwa wametembelea mtaa wetu ili kunichunguza kwa siri. Baadaye, familia yao iliitumia familia yetu posa, na nikashawishiwa nikubali. Nilikutana na mwanamume huyo mara moja tu kabla ya arusi yetu.

Baada ya kuolewa, mashambulio makubwa ya ndege za kijeshi yalitisha maisha yetu kila siku. Hatimaye nyumba yetu pamoja na jiji liliteketezwa kwa moto. Walioponyoka walikimbilia milimani, na hata tukiwa huko tulisikia ving’ora na tuliona ndege za vita. Hali hiyo iliogopesha. Kila mtu aliteseka. Ile miaka kumi baada ya vita ilikuwa migumu sana pia.

Mbali na watoto wetu watatu, tuliishi pamoja na mama mkwe, ndugu wakwe na dada wakwe zangu sita. Ijapokuwa tuliwaajiri watumishi, sote tulihitaji kufanya kazi mashambani ili tupate chakula. Katika kipindi hicho nilihuzunika sana wala sikuwa na raha. Lakini nilihofu kwamba kusema nilivyohisi kungetokeza kutoelewana. Hata hivyo, pole kwa pole, nilitambua kwamba ningeeleza hisia zangu kupitia michoro yangu.

Kutambuliwa Kama Mchoraji

Hata mtu mwenye kipaji cha kuchora apaswa kujitahidi sana kabla ya kupata matokeo bora. Nilinunua vitabu vya sanaa, na nilifunzwa na wachoraji fulani bora nchini Japani. Hakuna mmoja wao aliyenitia moyo kubadili mbinu niliyokuwa nimesitawisha nikiwa kijana.

Wachambuzi wa michoro walianza kutambua kazi yangu, hata hivyo nilichora ili kujiridhisha wala si kuwaonyesha watu wengine michoro yangu. Hata hivyo, baada ya muda nilitaka kujua watu hufikiri nini kuhusu picha zangu. Kwa hiyo, mnamo mwaka wa 1955, nilifanya maonyesho yangu ya kwanza katika eneo la Ginza huko Tokyo. Maonyesho hayo yalikuwa na kichwa hiki “Kupambana Kimya-kimya, Usemi wa Kimya-kimya, Rekodi Yangu,” na yalionyesha jinsi maisha ya kila siku yalivyo kupitia michoro. Maonyesho hayo yalifanikiwa.

Kukutana na Mashahidi

Familia yetu ilihamia Tokyo mnamo mwaka wa 1958, kwa kuwa mimi na mume wangu tulitaka watoto wetu waingie katika shule nzuri ili wapate elimu bora. Maisha yangu yalikazia uchoraji. Ilikuwa desturi yangu kuchora kwa saa tano hivi kila siku. Usiku, nilikuwa nikienda kutembea pamoja na rafiki zangu wachoraji, ilhali mume wangu alitembea pamoja na watu wengine. Hatukujua jinsi ya kuwalea watoto wetu.

Kazi ya mume wangu ilimlazimu kutokuwepo nyumbani mara nyingi, hivyo nikaachiwa daraka la kuwalea watoto, na sikuwazia kuwa nitaweza kulitimiza. Nilipokuwa mtoto, nilikwenda kwenye shule ya misheni ya Kikatoliki, basi nikajiuliza iwapo mafunzo fulani ya Biblia yatawasaidia. Kulikuwa na kanisa la Kilutheri ng’ambo ya barabara kutoka kwenye nyumba yetu huko Omori, Tokyo. Basi nikawaambia watoto twende huko. Lakini hatukwenda kanisani.

Badala yake, siku iliyofuata—mapema katika mwaka wa 1959—mmoja wa Mashahidi wa Yehova alitutembelea nyumbani. Niliwakusanya watoto haraka, na tukaketi chini kusikiliza. Shahidi huyo alieleza kupitia Biblia kwamba twaishi katika kipindi muhimu wakati ambapo Mungu ataondoa uovu duniani hivi karibuni. Niliagiza Biblia nne pamoja na vichapo vingine vya Biblia na nikakubali mwaliko wake wa kututembelea kila juma ili kutufundisha. Niliuliza analipishaje karo kila mwezi na nikashangaa kujua kwamba Mashahidi wa Yehova hawatozi malipo kwa ajili ya mafundisho yao. Walikuwa tofauti sana na walimu wengine niliowajua!

Binti zangu walikubali kweli za Biblia kwa utayari, na hata tulianza kuwa na kikundi cha funzo nyumbani mwetu kila juma kwa ukawaida. Lakini baada ya vipindi kadhaa vya funzo, nilianza kuwa na wasiwasi. Kilikuwa kipindi kigumu kwangu, kwa hiyo nyakati nyingine nilijificha au kutoka nje wakati ulipowadia kwa ajili ya funzo langu la Biblia.

Tatizo langu lilikuwa kwamba nilitambua kuwa kila kitu ambacho Biblia ilisema kilikuwa kweli na kwamba nilipaswa kufuata mwongozo wake. Hata hivyo, wakati huohuo nilikuwa nimeazimia kuwa mchoraji stadi, na niliamini kwamba nilihitaji kufikiria kwa uhuru ili niweze kubuni mambo. Kwa sababu nilihisi uchungu, sikuchora vyema. Picha zangu ziliwekwa pembeni kwenye maonyesho.

Safari Yangu Kwenda Paris

Nilihisi kwamba kutembelea Paris kungenisaidia kuboresha uchoraji wangu. Kwa hiyo, mnamo mwaka wa 1960, nilienda huko kwa kuwa maonyesho makubwa yalikuwa yakifanywa ili kuingiza michoro ya Kijapani nchini Ufaransa kwa mara ya kwanza. Kwenye maonyesho hayo, mimi tu ndiye niliyekuwa mchoraji wa kike kutoka Japani. Huko Paris, nilipendezwa na tofauti iliyokuwepo katika hali ya maisha, mavazi, mawazo, na rangi. Kila kitu kilinipendeza. Maonyesho hayo yalichukua siku nne, na nilishangaa kuwaona viongozi wa nchi hiyo wakihudhuria maonyesho hayo. Pia, jambo jingine lililonishangaza ni kwamba wanawake walivutiwa na nguo za kimono nilizovaa. Niliamua kukaa huko zaidi.

Kwa kuwa sikujua namna ya kutumiwa pesa kutoka Japani, nilianza kuuza nguo zangu za kimono. Hivyo, kwa kipindi cha miezi mitatu, niliweza kuchunguza michoro iliyokuwepo kwenye nyumba za sanaa. Nilikumbuka mara nyingi maneno ya mchoraji mmoja aliyekuwa ameweka picha yake karibu na yangu kwenye maonyesho. Alisema hivi: “Mimi huchora mwanga wa jua. Ni wazi kwamba michoro yako imefifia na ni myeusi kwa sababu umeathiriwa na wanafalsafa wa Mashariki.”

Wenzi wawili wa ndoa kutoka kwenye ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova huko Paris walinitembelea nyumbani. Baada ya kunitembelea mara kadhaa, nilikubali mwishowe kuandamana nao kwenye mkutano wa Kikristo. Nilipofika, nilishangazwa na mambo niliyoona. Mwanamke mmoja alikuwa amevaa kofia kubwa nyekundu maridadi, yenye ukingo mpana. Mwingine alivalia nguo ya kijani inayong’aa. Mavazi yaliyovaliwa yalikuwa yenye mtindo mzuri na maridadi, hivi kwamba nilibadili maoni yangu kabisa kuhusu Mashahidi.

Pia, programu ilinipendeza. Nilipoona utaratibu huohuo na mafundisho yaleyale yakifuatwa ulimwenguni pote, nilitambua kwamba kikundi hicho na shughuli zake ni za kipekee. Moyo wangu uliguswa sana nilipotambua kwamba nilikuwa nikishirikiana na watu wanaoongozwa na Mungu.

Kufanya Maamuzi

Niliporudi Japani, nilianza kujifunza Biblia kwa bidii. Nilitambua kwamba kanuni za Muumba wetu hutoa uhuru mwingi zaidi ya vile nilivyokuwa nimedhania. Kwa upendo, ametupa nyutu na vipawa mbalimbali na vilevile uhuru wa kuvisitawisha. Basi nikatambua kwamba kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova hakumaanishi kuacha kupenda sanaa.

Mimi na binti zangu tuliendelea na funzo letu la Biblia. Binti mmoja alionyesha wakfu wake kwa Yehova kupitia ubatizo wa maji mnamo mwaka wa 1961, na yule mwingine mnamo mwaka wa 1962. Hadi leo hii, wote wamedumu wakiwa watumishi waaminifu wa Mungu. Hata hivyo, mimi nilisitasita. Mnamo mwaka wa 1965, Lloyd Barry, ambaye kwa wakati huo alikuwa akisimamia kazi ya kuhubiri ya Mashahidi wa Yehova nchini Japani, alinitia moyo kwa kusema hivi: “Hebu wazia namna watu wakamilifu watakavyochora picha nzuri ajabu katika Paradiso!” Nilibatizwa mwaka uliofuata.

Jinsi Hilo Lilivyoathiri Uchoraji Wangu

Ninapofikiria yaliyopita, ninatambua jinsi mabadiliko katika maisha na utu wangu yameathiri uchoraji wangu. Picha zangu za awali zilikuwa nyeusi na hazikupendeza, zikionyesha hisia zangu za huzuni, kuteseka, na kukosa tumaini. Lakini nilijifunza katika Biblia juu ya Muumba wetu, sifa zake za ajabu, furaha inayotokana na kumsifu, na kanuni zinazopaswa kutumiwa maishani. Kadiri hisia zangu zilivyobadilika ndivyo picha zangu zilivyobadilika.

Mimi hutumia muda mwingi sasa nikiwaeleza wengine ujumbe wa Biblia. Mimi hufanya hivyo kwa ukawaida. Kuzungumza na watu kuhusu sifa za Mungu, na pia kusudi lake la kuifanya dunia hii kuwa paradiso chini ya utawala wa Mwanawe, Yesu Kristo, hunipa shangwe nyingi na uradhi. Kazi hiyo inayotegemea Biblia hunichochea, nami husukumwa kuchukua brashi yangu ya rangi na kuchora jinsi ninavyohisi. Na kadiri furaha yangu imeongezeka miaka baada ya miaka, ndivyo na picha zangu zimependeza zaidi.

Kukazia Biblia

Mimi hupata mialiko kutoka sehemu zote ulimwenguni ili nionyeshe michoro yangu—kutoka Sydney, Vienna, London, New York. Lakini picha zangu hupendwa zaidi na Wazungu. Wataalamu wa Chuo cha Kifahari cha Sanaa cha Louvre huko Paris wameuliza hivi: “Ikawaje kwamba Mjapani akasukumwa sana na Biblia na Ukristo hivi kwamba picha zake zinaonyesha shangwe ambayo haijapata kamwe kuonekana kwa karne nyingi katika sanaa ya dini?”

Mtunga-zaburi wa Biblia, Daudi, alionyesha hisia zake kupitia muziki, na alitumia vipawa vyake vya muziki kuwafundisha wengine maajabu ya Mungu. Nina lengo hilohilo. Nataka kumsifu Yehova. Natamani sana watu waone katika picha zangu shangwe inayopatikana kwa kumjua Yehova na sifa zake za ajabu. Mchambuzi mmoja wa sanaa alisema hivi kuhusu vichwa vyangu: “Mchoraji anaepuka kwa ustadi kutumia maneno yake mwenyewe, naye huiacha Biblia iseme yenyewe.” Yanisisimua kuona kwamba watu hutambua uvutano wa Biblia katika picha zangu.

Mnamo mwaka wa 1995, Baraza la Sanaa Ulimwenguni, ambalo ni shirika la kimataifa la sanaa lenye makao makuu huko Tokyo, liliniweka katika nafasi ya kwanza kati ya wachoraji wengine bora ulimwenguni. Baraza hilo liliripoti hivi kuhusu michoro yangu: “Mchoraji hunukuu maneno ya Biblia katika vichwa . . . Picha zake zote huonyesha Biblia, lakini hayo hasa ndiyo maisha ya mchoraji anayetembea pamoja na Mungu.”

Maneno hayo yalionyesha jinsi mimi mara nyingi hutia ndani picha ya Biblia iliyofunguliwa katika michoro yangu. Hivi karibuni, nimebandika kurasa zilizochapishwa za Biblia kwenye michoro yangu. Kwa hiyo, fikira za mtazamaji huvutwa kwenye kichwa changu, kwenye maneno ya Biblia, na kisha jinsi ninavyoeleza mambo hayo katika michoro yangu.

Mnamo mwaka wa 1999, baadhi ya picha zangu zilionyeshwa huko Bangkok, Thailand. Moja ilikuwa na kichwa “Jinsi Mungu Alivyoiumba Dunia Kwa Njia ya Ajabu, Akampa Mwanadamu Iwe Makao Yake,” kisha nyingine ilikuwa na kichwa, “Sala ya Mfalme Daudi: ‘Yehova, Acha Moyo wa Watu Hawa Upatane na Wako.’” Nilialikwa kwenye jumba la kifalme la mfalme wa Thailand pamoja na wachoraji wengine kadhaa. Mfalme alitaka kuzungumza nami kuhusu picha zangu, naye aliniuliza maswali mengi. Niliweza kuzungumza naye kirefu, hata kuhusu imani zangu za Biblia. Baadaye nikampa picha kama zawadi.

Katika muda wa miaka 35 iliyopita, nimetumikia pia katika halmashauri inayotoa maoni kuhusu picha za wachoraji wengine. Picha ninazopenda ni zile zinazowasilisha hisia. Kwa maoni yangu, picha nzuri ni ile inayoniacha nikihisi vizuri, ikinifanya niwe na amani moyoni. Mimi hupenda sana picha zilizo katika vichapo vya Mashahidi wa Yehova, ambazo hutimiza kusudi lake la kuwasilisha ujumbe wa Biblia kwa uaminifu.

Baraka za Kuwa Mtumishi wa Mungu

Kwa sababu ya uchoraji wangu, nimefurahia fursa za kipekee za kutoa ushahidi kumhusu Yehova Mungu na makusudi yake matukufu kuhusu dunia. Nimekuwa nikifanya hivyo ninapohojiwa kwa ajili ya makala za magazeti na katika vipindi vya televisheni. Kwa hakika, ninapoenda mahala popote au ninapozungumza na mtu yeyote, mimi hujaribu kuwajulisha watu kwamba imani, shangwe, na furaha inayotokana na kumtumikia Yehova Mungu ndiyo huniwezesha kuchora picha zangu.

Nina hakika kwamba nikitupilia mbali imani yangu, sitaweza kuchora vyema. Lakini mimi huchora vyema kwa sababu mimi ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova na kwa sababu ukweli wa Neno la Mungu umenipa shangwe na furaha nyingi sana.

[Picha katika ukurasa wa 21]

Nilipokuwa Paris

[Picha katika ukurasa wa 22]

Pamoja na binti zangu wawili sasa