Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maoni Kuhusu Uzee Yanabadilika

Maoni Kuhusu Uzee Yanabadilika

Maoni Kuhusu Uzee Yanabadilika

MZEE ni mtu mwenye umri gani? Yaonekana jibu la swali hili lategemea yule anayeulizwa. Bila kusitasita vijana watasema kwamba mzee ni mtu aliye na umri wa zaidi ya miaka 25.

Kwa upande mwingine, waimbaji wa opera wanafikia upeo wao wa kuimba wanapokuwa na umri mkubwa zaidi. Na gazeti la Australia la The Sun-Herald linasema hivi kuhusu wale wanaotaka kupanda cheo kazini: “Ukweli ni kwamba, kama hujafanikiwa unapofikia umri wa miaka 40, hutafanikiwa kamwe.”

Dhana za Kawaida

Baadhi ya watu huenda wakadhani kwamba wazee hupatwa na aksidenti mara nyingi na hujifunza mambo mapya polepole na kudhoofika haraka kimwili. Je, dhana hizo ni za kweli? Kulingana na Shirika la Afya Ulimwenguni, huko Ulaya, “thuluthi moja ya watu wote wanaokufa kwa sababu ya aksidenti barabarani hawajafikia umri wa miaka 25.” Isitoshe, mtu hudhoofika haraka kimwili akiwa na umri wa kuanzia miaka 30 hadi 40, na hakuna uthibitisho kwamba uwezo wa akili wa mtu mwenye afya nzuri unapunguka kwa sababu ya uzee.

Namna gani dhana kwamba wazee wote ni wagonjwa? Jarida la The Medical Journal of Australia linasema hivi: “Watu wengi hudhani kimakosa kwamba uzee ni ugonjwa.” Ukweli ni kwamba, wazee wengi wana afya nzuri kwa kadiri fulani na hawajioni kuwa wazee. baadhi ya wazee wana maoni ya mwanasiasa Mmarekani, Bernard Baruch, aliyesema hivi: “Kwangu, wazee ni wale wanaozidi umri wangu kwa miaka 15.”

Kwa nini basi, kuna ubaguzi mwingi dhidi ya wazee? Mara nyingi ni kwa sababu ya maoni yasiyofaa kuhusu uzee.

Maoni Mbalimbali Kuhusu Uzee

Max Frankel anasema hivi katika gazeti la The New York Times Magazine: ‘Wamarekani wanavutiwa sana na ujana hivi kwamba wamefanya vyombo vya habari vitoe maoni yasiyofaa juu ya uzee.’ Analalamika kwamba “wazee wamezuiwa kabisa wasiajiriwe na vyombo vya habari.” Huenda hiyo ikawa sababu ya hali iliyozungumziwa katika jarida la The UNESCO Courier: ‘Jamii inafanya mengi zaidi leo ili kusaidia wazee kuliko katika pindi yoyote nyingine. Wanapewa msaada wa kifedha na ulinzi wa kijamii, lakini kwa ujumla wanaonwa kuwa wasiofaa.’

Hata madaktari wana ubaguzi huo. Jarida la tiba The Medical Journal of Australia lasema hivi: “Madaktari wengi, na vilevile watu kwa ujumla, wanadhani kwamba watu walio na umri unaozidi miaka 65 hawafaidiki na mipango ya kukinga ugonjwa. . . . Maoni hayo yasiyofaa . . . yamefanya wazee wasihusishwe katika uchunguzi mbalimbali muhimu.”

Jarida hilohilo linasema hivi: “Maoni yasiyofaa kuhusu wazee na kuwaita ‘wakongwe’ yanaweza kutumiwa kuwa udhuru wasipewe matibabu yanayofaa. Matatizo madogo ya afya yaliyo ya kawaida kama vile matatizo ya kuona na kusikia hayatibiwi na madaktari kwa sababu yanaonwa kuwa jambo la kawaida mtu anapozeeka. . . . Maoni mapya juu ya wazee ni muhimu ili kuwe na mipango bora ya kukinga magonjwa ya wazee.”

Jarida la tiba la Uingereza la The Lancet linapendekeza kwamba “huenda sasa tungeanza kuhesabu uzee kuanzia umri mkubwa zaidi kuliko vile tulivyokuwa tumezoea, angalau katika nchi zilizoendelea.” Kwa nini hilo ni muhimu? Jarida hilo laeleza hivi: “Huenda kufanya hivyo kungeondoa maoni yasiyofaa kuhusu matatizo yanayodhaniwa yatakuja, na matabiri yenye kutia wasiwasi kwamba ‘wazee wengi mno’ watamaliza ‘sehemu kubwa’ ya fedha chache zilizotengwa kwa ajili ya tiba ya umma.”

Idadi ya Wazee Inaongezeka

Kusema kweli, idadi ya wazee imekwisha ongezeka, nayo inaendelea kuongezeka. Jarida la The UNESCO Courier lasema hivi: “Ulimwenguni pote, idadi ya watu wenye umri wa miaka 65 na zaidi itakuwa imeongezeka mara nne kuanzia mwaka wa 1955 hadi 2025, hiyo inamaanisha kwamba idadi yao itakuwa imeongezeka maradufu ikilinganishwa na ongezeko la watu wote ulimwenguni.”

Nchini India tayari wazee ni wengi kuliko wakazi wote nchini Ufaransa. Na inasemekana kwamba huko Marekani watu milioni 76 waliozaliwa katika kipindi cha miaka 18 iliyofuata Vita ya Pili ya Ulimwengu watastaafu katika kipindi cha miaka 50 ijayo. Ingawa ongezeko hilo la wazee duniani hufanya wataalamu na madaktari wawe na wasiwasi, hata hivyo linatulazimisha pia kubadili maoni yetu yasiyofaa juu ya uzee.

Je, Hati Iandikwe Upya?

Huenda wengine wakalinganisha maisha na mchezo wa kuigiza wenye sehemu tatu. Shauku ya ujana na elimu zinatarajiwa katika sehemu ya kwanza. Madaraka ya kulea watoto na uchovu wa kazi isiyoisha zinaonekana katika sehemu ya pili. Katika sehemu ya tatu, waigizaji wanatiwa moyo kurudi nyuma ili wasionekane sana na kukalia kiti huku wakingoja mwisho wa mchezo wakiwa wamevunjika moyo.

Lakini, kwa sababu ya maendeleo ya huduma ya afya na usafi na mambo mengine katika karne ya 20, muda ambao “waigizaji” wanakaa nyuma katika “sehemu ya tatu” umeongezeka kwa miaka 25. Wengi hawataki tena kustaafu tu na kukaa bure. Wazee hao wenye nguvu wanaoongezeka wameanza kusisitiza kwamba hati ya mchezo huo wa kuigiza iandikwe upya.

Wanaleta Faida Nyingi

Wengi hudhani kwamba wazee wengi hutegemea watu wengine. Hiyo si kweli. Gazeti la The New York Times Magazine lilisema kwamba nchini Marekani, ‘wazee wengi wanaojitegemea ni watu wa tabaka ya kati katika jamii ambao wana fedha nyingi kuliko wenzi wachanga walioana, na watu wanaochunguza jamii wametambua kwamba idadi ya wazee wenye nguvu walio matajiri inaogezeka.’ Philip Kotler aliye profesa wa mauzo kwenye Chuo Kikuu cha Northwestern huko Marekani alisema hivi: “Wataalamu wa mauzo wataona hivi karibuni kwamba wateja wenye fedha nyingi ni watu wenye umri wa miaka 55 na zaidi.”

Wazee si wateja wazuri tu, wanafaidi wengine kwa njia nyingine nyingi pia. Gazeti la The Sunday Telegraph la Sydney lilisema kwamba huko Australia “nusu ya watoto walio na wazazi wawili wanaofanya kazi ya kuajiriwa wanatunzwa na nyanya zao, na thuluthi moja ya wanawake wanaofanya kazi ya kuajiriwa wanaacha watoto wao watunzwe na nyanya zao.”

Hekima ya wazee inaonwa kuwa yenye thamani kubwa katika jiji la Troyes huko Ufaransa na mahali penginepo. Hekima hiyo inafaidi watoto wanaofundishwa na wazee ufundi mbalimbali kama vile useremala, kutengeneza kioo, kukata mawe, ujenzi, na ufundi wa mabomba, baada ya shule. Mbali na kufundisha, wazee wengi huenda shule pia ili kujifunza stadi mbalimbali.

Kulingana na Toleo la Januari 1999 la jarida la The UNESCO Courier, “Shirika la Kimataifa la Vyuo Vikuu vya Wazee huko Paris” lasema kwamba “kuna vyuo vikuu vya wazee 1,700 ulimwenguni.” Kuhusu vyuo vikuu hivi jarida hilo lasema hivi: “Ijapokuwa usimamizi na mfumo wake hutofautiana sana katika nchi mbalimbali, kusudi la vyuo vikuu vya wazee kwa kawaida ni kusaidia wazee wawe sehemu muhimu katika jamii.” Iliripotiwa kwamba chuo kikuu kimoja cha aina hiyo huko Japani kina wanafunzi 2,500!

Alexandre Kalache, kiongozi wa kikundi cha Programu ya Uzee na Afya ya Shirika la Afya Ulimwenguni anasema hivi: “Msaada ambao familia za wazee zinapokea kutoka kwa wazee wao ni mkubwa, ingawa ni vigumu kuukadiria kwa sababu mara nyingi wazee hao hawalipwi.” Anasisitiza hivi: “Nchi . . . zapaswa kuona wazee kuwa suluhisho la matatizo mbalimbali wala si tatizo . . . , tunapaswa kwanza kuwaona kuwa wenye faida.”

Bila shaka, furaha yetu ya uzeeni inaweza kuathiriwa kwa sababu ya ubaguzi na maoni ya wengine, lakini kwa kawaida inaathiriwa pia na mtazamo wetu. Wewe mwenyewe unaweza kufanya nini ili uwe mtendaji, kimwili na kiakili, hata ingawa mwili wako unazidi kuzeeka? Soma sanduku kwenye ukurasa wa 12 na 13, na uzingatie jinsi baadhi ya wazee wanavyofanikiwa kuwa watendaji na kufurahia maisha.

Jitahidi Kuwa Mtendaji

Utaona kwamba wazee hao wote wanaendelea kufanya kazi—ama kazi ya kuajiriwa ama ya kujitolea. Wanafanya mazoezi kwa ukawaida pia, wanapendezwa na watu wa umri wote, na kuridhisha mahitaji yao ya kiroho. Huenda ukaona kwamba madokezo haya ya jinsi ya kupata furaha na kuwa watendaji hunufaisha vijana kwa wazee.

Ukweli usiofurahisha ni kwamba, sasa hivi unaposoma habari hii wewe pia unaendelea kuzeeka. (Mhubiri 12:1) Hata hivyo, kwa hekima utatii maneno haya ya gazeti la Bulletin of the World Health Organization: “Kama vile afya nzuri inavyomwezesha mtu kuwa mtendaji, ndivyo utendaji unavyofanya mtu awe mwenye afya.”

[Sanuku/Picha katika ukurasa wa 12, 13]

Wao Ni Watendaji Wanaofurahia Maisha

AFRICA KUSINI: Piet Wentzel, mwenye umri wa miaka 77, ni mfanyakazi wa kujitolea wa wakati wote.

“Ninatambua kwamba ili niwe na afya nzuri ni lazima nifanye mazoezi kwa ukawaida. Nimekuwa nikitunza bustani ndogo kwa muda wa miaka michache iliyopita. Ninajisikia vizuri sana baada ya mazoezi hayo. Ili nitimize mengi iwezekanavyo nimejitahidi kufuata kanuni hii: ‘Kusitasita ni mwizi wa wakati; na kuahirisha mambo ni msaidizi wake.’”

[Picha]

“Ninatambua kwamba ili niwe na afya nzuri ni lazima nifanye mazoezi kwa ukawaida.” —Piet

JAPANI: Yoshiharu Shiozaki, mwenye umri wa miaka 73, anafanya kazi ya kushauri wale wanaotaka kununua au kuuza ardhi au nyumba.

“Nina maumivu ya viuno, msukumo mkubwa wa damu, na ugonjwa wa masikio. Ninasafiri kwa baiskeli kutoka nyumbani hadi ofisini siku nne kila juma; kwenda na kurudi ni umbali wa kilometa 12. Mazoezi hayo ni mazuri, kwa kuwa hayaumizi mgongo wangu lakini huimarisha misuli yangu ya miguu. Ninajitahidi kuishi kwa amani pamoja na wengine, kutia ndani majirani. Ninajitahidi kutozingatia udhaifu na makosa ya wengine. Nimetambua kwamba watu huitikia upesi wanapotiwa moyo kuliko wanapochambuliwa.”

[Picha]

‘Ninajitahidi kutozingatia udhaifu wa wengine.’ —Yoshiharu

UFARANSA: Léone Chalony, mwenye umri wa miaka 84, ni mweneza-Injili wa wakati wote.

“Haikuwa rahisi kuacha kazi nilipostaafu mwaka wa 1982 kwa kuwa nilipenda kazi yangu ya kutengeneza nywele. Sikuwa na wajibu wowote, kwa hiyo nilianza kutumikia kama painia, kama wanavyoitwa waeneza-Injili wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova. Nimesaidiwa kudumisha uwezo wa akili kwa kuongoza mafunzo mengi ya Biblia. Sina gari, kwa hiyo ninatembea mara nyingi. Hiyo hudumisha afya yangu.”

[Picha]

“Nimesaidiwa kudumisha uwezo wa akili kwa kuongoza mafunzo mengi ya Biblia.”—Léone

BRAZILI: Francisco Lapastina, mwenye umri wa miaka 78, anafanya kazi ya kujitolea wakati wote.

“Kwa kawaida siudhiki wakati mtu anaponiumiza kihisia au kunipuuza. Ninaelewa kwamba yule mtu ana matatizo na anakabili hali ngumu. Sisi sote tunashindwa kuwa wenye urafiki nyakati nyingine. Ninajitahidi kutokuwa na kinyongo na kukumbuka kwamba watu wanahitaji kunivumilia pia. Hilo limenisaidia kupata marafiki wengi wa kweli.”

[Picha]

“Ninajitahidi kutokuwa na kinyongo.”—Francisco

AUSTRALIA: Don MacLean, mwenye umri wa miaka 77, bado anafanya kazi kwa muda wa saa 40 kila juma.

“Licha ya upasuaji wa moyo miaka minne iliyopita nina afya nzuri kufikia leo. Sikuuona upasuaji huo kuwa jambo lenye kulemaza. Bado ninakwenda matembezi kila siku, kama vile ambavyo nimekuwa nikifanya kwa miaka mingi. Nilipokuwa mchanga na kuona watu wakizeeka kabla ya wakati kwa sababu ya mtazamo usiofaa, niliamua kwamba sitakuwa na mtazamo huo. Ninapendezwa sana na kufahamu watu na kuanzisha mazungumzo. Tukifanya mambo ya kiroho yawe sehemu ya maisha yetu tutaona ukweli wa maneno ya mtunga-zaburi katika Zaburi 103:5: ‘[Yehova] aushibisha mema uzee wako, ujana wako ukarejezwa kama tai.’”

[Picha]

“Usizeeke kabla ya wakati.”—Don

JAPANI: Chiyoko Chonan, mwenye umri wa miaka 68, ni mweneza-Injili wa wakati wote.

“Ili kudumisha afya nzuri mtu anahitaji kuepuka mfadhaiko na kuchoka kupita kiasi. Sihangaishwi sana na hali mbalimbali na nimeona kwamba kufanya mambo mapya hunisaidia. Hivi majuzi nilianza kujifunza jinsi ya kufanya hesabu kwa kutumia abakusi (kibao chenye shanga kinachotumika kuhesabia) ili nifanye mazoezi ya vidole na akili. Kujifunza mambo mapya hunufaisha.”

[Picha]

“Kujifunza mambo mapya hunufaisha.”—Chiyoko

UFARANSA: Joseph Kerdudo, mwenye umri wa miaka 73, anafanya kazi ya kujitolea wakati wote.

“Ili pindi ya uzee ifurahishe ni muhimu kuwa mtendaji kwa muda mrefu iwezekanavyo. Kufanya kazi huridhisha na ni lazima kuwa mwangalifu kwa habari ya chakula na kufanya mabadiliko yanayofaa. Nadhani kwamba mtu aliye na kusudi maishani huwa tofauti. Nadhani pia kwamba hali nzuri ya kiroho ni muhimu sana ili kudumisha afya nzuri. Kabla ya kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova nilikuwa mtu mwenye kusitasita na kutazamia mabaya. Kujua kweli za Biblia ni nguvu ya ajabu inayotia mtu uwezo wa akili wa kukabili hali mbalimbali.”

[Picha]

“Hali nzuri ya kiroho ni muhimu sana.”—Joseph