Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mfadhaiko Utakoma

Mfadhaiko Utakoma

Mfadhaiko Utakoma

HUENDA wewe ni mwanajeshi aliyestaafu na husumbuliwa na ndoto zinazotisha na kumbukumbu za ghafula, ambazo hufanya uhisi kana kwamba vita inaendelea hata leo. Huenda umetendwa kwa ukatili kama vile kubakwa na unahisi kana kwamba sehemu fulani ndani yako imekufa kwa sababu ya tisho hilo. Au huenda mpendwa wako alikufa katika msiba wa asili au aksidenti na maisha bila huyo mpendwa ni magumu sana.

Je, unajiuliza ikiwa hisia hizo zinaweza kwisha? Tunaweza kujibu kwa uhakika kwamba: Ndiyo, zinaweza kwisha! Kwa sasa, wote wanaoathiriwa na tukio lenye kutisha wanaweza kupata faraja kutokana na Neno la Mungu, Biblia.

Tunaweza Kusaidiwa Kuvumilia Mfadhaiko Huo

Karibu miaka elfu mbili iliyopita, mtume Paulo alipitia matukio yenye kutisha yaliyohatarisha maisha yake. Maelezo yake ya baadhi ya matukio hayo yamo katika Biblia. Aliandika hivi: “Hatutaki nyinyi mwe wasio na ujuzi, akina ndugu, juu ya dhiki iliyotupata katika wilaya ya Asia, kwamba tulikuwa chini ya mkazo mkali mno upitao nguvu yetu, hivi kwamba tulikuwa bila hakika kabisa hata juu ya uhai wetu. Kwa kweli, tulihisi ndani yetu wenyewe kwamba tulikuwa tumeipokea hukumu ya kifo.”—2 Wakorintho 1:8, 9.

Ijapokuwa hatujui yote yaliyotukia, bila shaka pindi hiyo ilikuwa yenye kutisha. (2 Wakorintho 11:23-27) Paulo alivumiliaje hali hiyo?

Anapotafakari tukio hilo lenye kutisha alilopitia huko Asia, Paulo aliandika hivi: “Mbarikiwa na awe Mungu na Baba ya Bwana wetu Yesu Kristo, Baba ya rehema nyororo na Mungu wa faraja yote, ambaye hutufariji katika dhiki yetu yote, ili tupate kuweza kufariji wale walio katika namna yoyote ya dhiki kupitia faraja ambayo kwayo sisi wenyewe tunafarijiwa na Mungu.”—2 Wakorintho 1:3, 4.

Naam, “Baba ya rehema nyororo na Mungu wa faraja yote,” atawasaidia wote wanaonusurika kwenye tukio lenye kutisha. Unawezaje kupata msaada huo?

Jinsi ya Kupata Msaada

Kwanza—omba msaada. Ikiwa hisia zako zote zimekufa ganzi kumbuka kwamba wengine wamepatwa na hali hiyo pia. Wale ambao wameshinda hali hiyo kwa kawaida hufurahia kuwasaidia wengine. Mara nyingi hao huhisi jinsi mtume Paulo alivyohisi kwamba inawabidi kushiriki faraja waliyokuwa wamepokea kutoka kwa Mungu wakati wa majaribu yao pamoja na “wale walio katika namna yoyote ya dhiki.” Usikawie kuzungumza na mmoja wa Mashahidi wa Yehova—yeyote ambaye unaweza kuongea naye kwa uhuru—na kuomba akusaidie kupata msaada kutoka kwa Yehova, “Mungu wa faraja yote.”

Dumu katika sala. Ikiwa unaona ugumu kutoa sala kwa sababu ya hasira, omba mtu aliyekomaa kiroho atoe sala pamoja nawe. (Yakobo 5:14-16) Unaposema na Yehova Mungu katika sala, usisahau ‘kutupa hangaiko lako lote juu yake, kwa sababu anakujali.’ (1 Petro 5:7) Mara nyingi Maandiko huonyesha kwamba Mungu anajali kila mmoja wa watumishi wake.

Yamkini mwandishi wa Zaburi ya 94 alikuwa amepitia tukio lenye kutisha kwa kuwa aliandika hivi: “Kama BWANA asingalikuwa msaada wangu, nafsi yangu kwa upesi ingalikaa penye kimya. Niliposema, Mguu wangu unateleza; Ee BWANA, fadhili zako zilinitegemeza. Katika wingi wa mawazo ya moyoni mwangu, faraja zako zaifurahisha roho yangu.”—Zaburi 94:17-19.

Baadhi ya watu walio na mfadhaiko uliosababishwa na tukio lenye kutisha wanasumbuliwa hasa na “wingi wa mawazo,” ambayo nyakati nyingine yanaweza kusababisha hofu au hasira kubwa zenye kulemea. Hata hivyo, sala kutoka moyoni inaweza ‘kukutegemeza’ hadi hisia hizo zipite. Mwone Yehova kuwa mzazi mwenye upendo na ujione mwenyewe kuwa mtoto mchanga ambaye Yehova anamlinda kwa upendo. Kumbuka ahadi hii ya Biblia: “Amani ya Mungu izidiyo fikira yote kwa ubora italinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili kwa njia ya Kristo Yesu.”—Wafilipi 4:7.

Mtu hupona hatua kwa hatua iwe ni kimwili, kiakili, au kiroho. Kwa hiyo, wale wenye mfadhaiko mbaya kwa sababu ya matukio yenye kutisha hawapaswi kutarajia kupata amani ya akili mara moja tu wanaposali. Hata hivyo, kudumu katika sala ni muhimu. Kutamsaidia anayeteseka asilemewe kabisa na kukata tamaa.

Soma na utafakari Neno la Mungu. Ikiwa huwezi kuelekeza fikira, omba mtu mwingine asome pamoja nawe masimulizi ya Biblia yanayofariji. Unaweza kuchagua masimulizi yanayoonyesha jinsi Yehova anavyowahurumia waaminifu wake, haidhuru wameshuka moyo au kukata tamaa kadiri gani.

Jane, aliyetajwa mapema, alifarijika aliposoma sehemu nyingi za Biblia za kitabu cha Zaburi. Hizo zinatia ndani Zaburi 3:1-8; 6:6-8; 9:9, 10; 11:1-7; 18:5, 6; 23:1-6; 27:7-9; 30:11, 12; 31:12, 19-22; 32:7, 8; 34:18, 19; 36:7-10; 55:5-9, 22; 56:8-11; 63:6-8; 84:8-10; 130:1-6. Usisome sehemu nyingi za Biblia kwa wakati mmoja. Badala yake, chukua muda kuzitafakari na kusali.

Mfadhaiko Usio na Kifani wa Siku Hizi

Kwa kusikitisha, haipasi kutushangaza kwamba ubakaji, mauaji, vita, na ujeuri usio wa lazima, zinazidi leo. Kwa nini? Kwa sababu Yesu Kristo alisema kwamba katika wakati wetu kungekuwa na ‘ongezeko la uasi-sheria.’ Aliongeza kusema hivi: “Upendo wa idadi iliyo kubwa zaidi utapoa.”—Mathayo 24:7, 12.

Mfadhaiko unaosababishwa na tukio lenye kutisha umekuwa jambo la kawaida sana katika miaka ya majuzi, na mara nyingi unasababishwa na matukio yale ambayo Yesu alitabiri. Kama vile Biblia inavyoonyesha katika Mathayo sura ya 24, Marko sura ya 13, na Luka sura ya 21, Yesu alisema kwamba katika siku za mwisho za ulimwengu huu, kungekuwapo vita vya kimataifa, misiba ya asili, ongezeko la uhalifu, na ukosefu wa upendo. Hata hivyo, Yesu alionyesha pia kwamba faraja iko karibu.

Baada ya kuonyesha ongezeko la duniani pote la matukio yenye kutisha na mwanzo wa “dhiki kubwa” ambayo ingefuata, sikiliza kile ambacho Yesu aliwaambia watu wafanye: “Jisimamisheni wenyewe wima na kuinua vichwa vyenu juu, kwa sababu ukombozi wenu unakaribia.” (Mathayo 24:21-31; Luka 21:28) Ndiyo, hali ya ulimwengu inapozidi kuwa ngumu, tunaweza kuwa na uhakika kwamba dhiki kubwa itakayokuja juu ya mfumo huu wenye kusababisha mfadhaiko itamaliza uovu wote ili mfumo mpya wenye uadilifu uanze.—1 Yohana 2:17; Ufunuo 21:3, 4.

Hatupaswi kushangaa kwamba wokovu wetu utakuja tu baada ya uovu na ujeuri kufikia upeo wake. Hivyo ndivyo ilivyokuwa wakati Mungu alipohukumu ulimwengu wa siku za Noa na wakazi waovu wa Sodoma na Gomora. Hukumu hizo za kale za Mungu zaonyesha jinsi atakavyotekeleza hukumu wakati ujao.—2 Petro 2:5, 6.

Mwisho wa Mfadhaiko

Ikiwa unaugua mfadhaiko unaosababishwa na tukio lenye kutisha, huenda ukajiuliza ikiwa kumbukumbu zako zenye kuumiza zitakwisha kamwe. Jibu la hakika ni: Ndiyo, zitakwisha! Katika andiko la Isaya 65:17, Yehova Mungu anasema hivi: “Maana, tazama, mimi naumba mbingu mpya na nchi mpya, na mambo ya kwanza hayatakumbukwa, wala hayataingia moyoni.” (Italiki ni zetu.) Ijapokuwa mfadhaiko unaosababishwa na tukio lenye kutisha unaonekana kuwa wa kudumu, andiko hili latuonyesha kwamba siku moja hautakuwapo tena.

Leo, mwaka mmoja baada ya kushambuliwa na mbakaji, Jane anatumikia kama mhudumu painia (mweneza-Injili wa wakati wote) wa Mashahidi wa Yehova. ‘Nilirudia hali yangu ya kawaida baada ya kesi tu na baada ya yule aliyenishambulia kupatikana na hatia—zaidi ya miezi minane baada ya shambulio hilo. Mwaka mmoja uliopita sikuweza kuwazia amani na furaha niliyo nayo sasa. Ninamshukuru Yehova kwa tumaini la ajabu la kuishi milele na fursa ya kushiriki tumaini hilo na wengine,’ alisema hivi majuzi.—Zaburi 27:14.

Ikiwa wewe unapambana na majonzi na mfadhaiko unaotokana na tukio lenye kutisha, tumaini hilo linaweza kukuimarisha vilevile.

[Picha katika ukurasa wa 8]

Kuhudhuria mikutano ya Kikristo kunaweza kukusaidia kuvumilia hali

[Picha katika ukurasa wa 8, 9]

Kusoma Neno la Mungu na kutoa sala kunaweza kukuimarisha

[Picha katika ukurasa wa 10]

Mfadhaiko wote utaondolewa hivi karibuni