Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mfadhaiko wa Tukio Lenye Kutisha Ni Nini?

Mfadhaiko wa Tukio Lenye Kutisha Ni Nini?

Mfadhaiko wa Tukio Lenye Kutisha Ni Nini?

MIAKA MINGI ILIYOPITA, mfadhaiko huo ulichunguzwa hasa ulipowaathiri maaskari waliostaafu vitani waliopatwa na ugonjwa wa akili kwa sababu ya mshtuko wakati wa vita. * Leo hali imebadilika. Si lazima uwe askari ili utambuliwe kuwa na hali hiyo. Ikiwa tu umenusurika kwenye tukio lenye kutisha waweza kupatwa na hali hiyo.

Matukio kama vita, shambulio la mbakaji, au aksidenti ya gari, na kadhalika yanaweza kusababisha hali hiyo. Hati inayotaarifu juu ya hali hiyo kutoka kwa Kitovu cha Taifa cha Mfadhaiko wa Tukio Lenye Kutisha, huko Marekani, yasema hivi: “Mtu aliye na tatizo hilo lazima awe amepatwa na tukio lenye kutisha.” Na lazima awe “amejeruhiwa au kutishwa kujeruhiwa KIMWILI.”

Jane, aliyetajwa katika sehemu iliyotangulia asema hivi: “Nimejifunza kwamba tisho la ghafula hufanya homoni fulani ziongezeke ghafula, na homoni hizo hufanya mtu awe macho kutambua hatari. Kwa kawaida homoni hizo hurudia kiwango cha kawaida baada ya hatari kupita, lakini kiwango cha homoni hizo huendelea kuwa juu katika wale walio na mfadhaiko huo.” Tukio hilo lilikuwa limepita, lakini hofu kubwa ya kipindi hicho ilidumu katika akili ya Jane kama vile mpangaji asiyetakikana anavyokataa kuondoka katika nyumba, japo ameambiwa aondoke.

Ikiwa umenusurika kwenye tukio lenye kutisha na unahisi mifadhaiko hiyo, ni muhimu kukumbuka kwamba wengine pia wana hisia kama hizo. Katika kitabu ambacho aliandika kuhusu ubakaji mwandishi Linda E. Ledray alisema kwamba mfadhaiko huo, “ni hali ya kawaida katika watu wa kawaida ambao wamepatwa na tukio lenye kutisha ambalo walishindwa kulizuia.”

Hata hivyo, ijapokuwa hisia hizo ni za kawaida haimaanishi kwamba kila mtu anayenusurika kwenye tukio lenye kutisha atakuwa nazo. Ledray anasema hivi: “Uchunguzi mmoja wa mwaka wa 1992 unaonyesha kwamba, asilimia 94 ya wale waliobakwa walikuwa na mfadhaiko huo juma moja baada ya tukio hilo, na asilimia 12 waliendelea kuwa nao baada ya majuma 47. Asilimia 50 ya wanawake waliotibiwa kwenye kituo cha Kuhudumia Walioshambuliwa Kingono cha Minneapolis mwaka wa 1993 walikuwa na mfadhaiko huo mwaka mmoja baada ya kubakwa.”

Si watu wengi wanaotambua kwamba hali hiyo ni ya kawaida sana kama vile taarifa hiyo inavyoonyesha. Na watu wa aina zote wanaweza kukumbwa na mfadhaiko huo, na unaweza kusababishwa na matukio ya aina mbalimbali. Waandishi Alexander C. McFarlane na Lars Weisaeth wanasema hivi: “Uchunguzi wa hivi karibuni unaonyesha kwamba matukio yenye kutisha yanaathiri watu wakati wa amani, na vilevile maaskari wa vita, na huonyesha vilevile kwamba wale wanaoathiriwa na vita, na wengi wanaonusurika kwenye matukio hayo ya kawaida hupatwa na mfadhaiko huo.” Mara nyingine hali hiyo imesababishwa na tiba mbalimbali na mshtuko wa moyo.

Waandishi walionukuliwa hapo juu wanaeleza kwamba “mfadhaiko huo ni wa kawaida sana siku hizi.” Na wanaongeza kusema hivi: “Uchunguzi wa vijana Wamarekani 1,245 ulionyesha kwamba asilimia 23 ya vijana hao walikuwa wametendwa vibaya kimwili au kingono, na pia walikuwa wameshuhudia wengine wakitendwa kwa ukatili. Mmoja kati ya vijana watano alishikwa na mfadhaiko. Hiyo inadokeza kwamba vijana Wamarekani milioni 1.07 hivi wanapatwa na hali hiyo.”

Kwa hiyo, ikiwa taarifa hiyo ni sahihi, inamaanisha kwamba kuna vijana wengi wanaoteseka katika nchi hiyo moja tu! Vijana hao na vilevile mamilioni wengine wanaoteseka kotekote duniani wanaweza kusaidiwaje?

Suluhisho Ni Nini?

Ikiwa unafikiri kwamba wewe au mtu fulani unayemjua ana mfadhaiko huo, madokezo yanayofuata huenda yakasaidia.

Jitahidi kuwa na mpango wa kiroho wa kila siku. Jane anasema hivi: “Sikuzote nilihudhuria mikutano kwenye Jumba letu la Ufalme. Nilijua kwamba Yehova Mungu alitaka niwe mkutanoni hata niliposhindwa kuelekeza fikira kwenye habari iliyozungumziwa. Ndugu na dada kutanikoni walionyesha upendo na kunitia moyo sana. Na nilithamini sana upendo wao na jinsi walivyonijali muda wote nilipoteseka. Jane anaongeza kusema: “Kusoma zaburi mbalimbali kulinisaidia pia. Ni kana kwamba sala katika zaburi hizo za wale walioteseka zilisema kwa niaba yangu. Niliposhindwa kusema kile nilichotaka kusema katika sala niliweza kusema tu ‘Ameni.’”

Mtie moyo yule anayeteseka. Ikiwa mpendwa wako anafadhaika kupita kiasi kwa sababu ya kumbukumbu mbaya ya tukio lenye kutisha, fahamu kwamba yeye hana hisia hizo kwa sababu anataka kusumbua. Huenda hataweza kuonyesha uthamini unapojitahidi kumsaidia kwa sababu hisia zake zimekufa ganzi, au kwa sababu ya wasiwasi au hasira. Lakini usife moyo! Biblia yasema hivi: “Rafiki hupenda sikuzote; na ndugu amezaliwa kwa siku ya taabu.”—Mithali 17:17.

Mwenye kuteseka apaswa kuwa macho na kuepuka mazoea yote yasiyo ya hekima yanayoweza kumdhuru anapojitahidi kuvumilia hali yake. Mazoea hayo yatia ndani utumizi wa dawa za kulevya au kutumia vileo kupita kiasi. Ijapokuwa matumizi ya dawa za kulevya na vileo yanaweza kutuliza kwa muda, punde si punde hufanya tatizo lizidi. Kwa kawaida hufanya mtu ajitenge na wengine, akataliwe na watu wanaotaka kusaidia; huchangia pia mtu kufanya kazi kupita kiasi; hasira isiyothibitiwa; kula kupita kiasi au kutokula, au tabia nyingine za kujiumiza au hata kujiua.

Omba ushauri kutoka kwa mtaalamu stadi wa tiba. Huenda ikawa mwenye kuteseka hana mfadhaiko wa aina hiyo, lakini ikiwa anao, kuna matibabu yanayofanya kazi. * Ikiwa unatibiwa na daktari mwombe msaada ili kushinda tabia zozote zilizotajwa juu.

Kumbuka: Mara nyingi majeraha ya mwili hupona kwanza, lakini watu wanaougua mfadhaiko huo, huenda wamejeruhiwa kwa njia nyingi kimwili, kiakili na kihisia. Sehemu inayofuata itazungumzia yale ambayo mwenye mfadhaiko anaweza kufanya, na jinsi wengine wanavyoweza kumsaidia kupona, na itazungumzia vilevile tumaini kwa wote walio na mfadhaiko unaosababishwa na tukio lenye kutisha.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 2 Soma “Do They Come Back the Same?” (Je, Wanaporudi Watakuwa Wamebadilika?), na “He Came Back a Stranger,” (Alirudi Akiwa Amebadilika Sana), katika toleo la Kiingereza la Amkeni! la Agosti 8, 1982.

^ fu. 15 Mashahidi wa Yehova hawapendekezi matibabu yoyote ya kimwili wala ya akili.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 6]

Dalili za Mfadhaiko Unaosababishwa na Tukio Lenye Kutisha

Wengi walionusurika tukio lenye kutisha wanarudia-rudia tukio hilo akilini. Kwa kawaida hawawezi kujizuia wasifanye hivyo. Huenda matokeo yakawa:

• Kumbukumbu za ghafula za tukio hilo—kuhisi kana kwamba linatukia tena

• Ndoto zenye kuhofisha

• Tabia ya kushtuka sana kwa sababu ya kelele au mtu anapowakaribia ghafula kutoka nyuma

• Kutetemeka na kutoa jasho

• Moyo kupiga-piga na tatizo la kupumua

• Kuvurugika akili wakati wanapokumbushwa tukio hilo kwa kuona, kusikia, kuhisi, kunusa, au kuonja kitu fulani

• Wasiwasi au hofu—kuhisi kwamba wamo hatarini tena

• Kushindwa kujizuia kwa kuwa kumbukumbu zinasababisha wasiwasi, mvurugo, au hasira za ghafula

• Kushindwa kuwa makini au kufikiri vizuri

• Kushindwa kupata usingizi au kulala vizuri

• Wasiwasi na hali ya kuwa macho daima

• Hisia za moyoni zilizo kufa ganzi

• Ugumu wa kupenda wengine au kuwa na hisia za moyoni zenye nguvu

• Kuhisi kwamba mahali wanapoishi pamebadilika au si halisi

• Kutopendezwa na mambo waliyopenda mbeleni

• Kushindwa kukumbuka mambo muhimu ya tukio hilo

• Kuhisi kwamba hawahusiki na maisha wala na mambo yanayowapata

[Picha katika ukurasa wa 5]

Matukio mbalimbali yenye kutisha yanaweza kusababisha mfadhaiko