Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ninaweza Kufanyaje Usomaji wa Biblia Ufurahishe Zaidi?

Ninaweza Kufanyaje Usomaji wa Biblia Ufurahishe Zaidi?

Vijana Huuliza . . .

Ninaweza Kufanyaje Usomaji wa Biblia Ufurahishe Zaidi?

“Nyakati nyingine ni vigumu kuielewa Biblia, na hilo laweza kuvunja moyo.”—Annalieza, mwenye umri wa miaka 17.

“Biblia ilinichosha.”—Kimberly, mwenye umri wa miaka 22.

WATU wengi hawafurahii kusoma. Basi kitabu kikubwa kama Biblia chaweza kuonekana kuwa kina mambo mengi sana—hata kwa wasomaji wenye bidii. Tammy, mwenye umri wa miaka 17, asema: “Kwangu mimi, Biblia kilikuwa kitabu kikubwa chenye maneno magumu yasiyoeleweka kwa urahisi. Kusoma Biblia huhitaji kumakinika na uvumilivu.”

Kwa kuongezea, kazi za shule, kazi za nyumba, na tafrija zaweza kuchukua muda na nishati zetu nyingi. Hilo pia laweza kufanya iwe vigumu kumakinika na kufurahia usomaji wa Biblia. Alicia, aliye pia mmoja wa Mashahidi wa Yehova, hutenga wakati pia wa kutayarisha na kuhudhuria mikutano ya Kikristo na kuwaeleza wengine mambo anayoamini. Akubali hivi: “Usomaji wa Biblia waweza kuwa mgumu kwa kuwa ni kana kwamba kazi haziishi.”

Hata hivyo, Alicia, Tammy, na vijana wengine wengi wamefaulu. Sasa, wao husoma Biblia kwa ukawaida na kuifurahia. Wewe pia waweza! Fikiria mambo matatu unayoweza kufanya ili usomaji wa Biblia ufurahishe zaidi.

Tenga Wakati wa Usomaji wa Biblia

“Nafikiri vijana husema kwamba usomaji wa Biblia unachosha kwa kuwa hawajaisoma vya kutosha,” asema Kelly, mwenye umri wa miaka 18. Kama vile unavyofurahia mchezo kwa kuwa umeucheza mara nyingi, ndivyo utakavyofurahia usomaji wa Biblia unapoufanya kwa ukawaida.

Lakini vipi ikiwa huna nafasi ya kutosha? Mtume Paulo ashauri hivi: “Fulizeni kuangalia sana kwamba jinsi mnavyotembea si kama wasio na hekima bali kama watu wenye hekima, mkijinunulia kabisa wakati unaofaa, kwa sababu siku ni za uovu.” (Waefeso 5:15, 16) Waweza ‘kununua wakati kabisa’ kwa kutotumia wakati mwingi kwa mambo yasiyo muhimu kama kutazama televisheni. Usemi ambao Paulo alitumia kwa “wakati” unaweza kumaanisha wakati uliotengwa kwa ajili ya kusudi hususa. Waweza kutenga wakati gani kwa ajili ya kusoma Biblia?

Wengi husoma Biblia asubuhi, baada ya kuchunguza Andiko na maelezo yanayopatikana katika kijitabu Kuyachunguza Maandiko Kila Siku. * Wengine hupenda kusoma kabla hawajalala usiku. Chagua wakati unaokufaa, na ubadilikane kulingana na ratiba yako. Alicia asema: “Kubadilikana ndiko hasa hunisaidia kusoma kwa ukawaida.”

Vijana fulani Wakristo huratibu dakika 10 au 15 kila siku ili wasome Biblia. Kwa kufanya hivyo, wamemaliza kusoma Biblia yote nzima kwa mwaka mmoja au miwili! Hata ikiwa huwezi kufanya hivyo, weka mradi wa kusoma sehemu fulani ya Biblia kila siku. Kwa kuazimia kushikamana na wakati uliotenga kwa ajili ya usomaji wa Biblia, upendo wako kwa Neno la Mungu utakua.—Zaburi 119:97; 1 Petro 2:2.

Sali Upate Hekima

Ni kweli kwamba, hata wale wanaosoma Biblia kwa ukawaida huona sehemu fulani za Neno la Mungu zikiwa ngumu kuelewa. Mtungaji wa Biblia, Yehova Mungu, ataka ulielewe Neno lake. Kitabu cha Matendo chaeleza kuhusu msafiri mmoja Mwethiopia ambaye hakuelewa kikamili unabii fulani katika Isaya sura ya 53. Mwanamume huyo alikuwa tayari kuomba msaada, na malaika wa Yehova alimtuma yule mishonari Filipo ili amweleze unabii huo.—Matendo 8:26-39.

Basi, usomaji wa Biblia unaonufaisha huanza kwa sala wala si kwa kusoma. Kabla ya kufungua Biblia, wengine husali kwa Yehova ili wapate hekima ya kuelewa na kutumia masomo wanayojifunza kupitia usomaji wao. (2 Timotheo 2:7; Yakobo 1:5) Roho ya Mungu yaweza kukukumbusha mistari ya Biblia itakayokusaidia kujibu maswali au kukabiliana na majaribu.

Kijana mmoja Mkristo akumbuka hivi: “Nilipokuwa na umri wa miaka 12, babangu aliacha familia yetu. Usiku mmoja nilikuwa nikisali kitandani, nikimsihi Yehova amfanye babangu arudi. Kisha nikachukua Biblia yangu na kusoma Zaburi 10:14: ‘Mtu duni hukuachia [Yehova] nafsi yake, maana umekuwa msaidizi wa yatima [mvulana asiye na baba, NW].’ Nilitua kidogo. Nilihisi kwamba Yehova alikuwa akizungumza nami, akinijulisha kwamba alikuwa msaidizi wangu; alikuwa Babangu. Je, ninaweza kuwa na Baba mwingine mwenye upendo kuliko yeye?”

Je, waweza kufanya liwe zoea lako kusali kila mara unapoketi ili kusoma Biblia? Adrian adokeza hivi: “Ili kuwe na mawasiliano baina yako na Yehova, sali kabla na baada ya kusoma.” Sala ya kutoka moyoni itaimarisha azimio lako la kushikamana na ratiba ya usomaji wa Biblia na kuimarisha uhusiano wako pamoja na Mungu.—Yakobo 4:8.

Fanya Usomaji Usisimue

Kimberly, aliyenukuliwa mwanzoni, aliona Biblia kuwa yenye kuchosha. Ni kweli kwamba Biblia ni kitabu cha kale sana. Iliandikwa kabla ya kompyuta, televisheni, au ndege kubuniwa. Watu wanaotajwa katika Biblia walikufa maelfu ya miaka iliyopita. Hata hivyo, mtume Paulo aliandika hivi: “Neno la Mungu liko hai na hukazia nguvu.” (Waebrania 4:12) Kitabu cha kale chawezaje kukazia nguvu?

Katika siku za mwandishi Ezra, maelfu ya wanaume, wanawake na “wote walioweza kusikia na kufahamu” walikusanyika pamoja huko Yerusalemu ili kusikiliza Sheria ya Musa iliposomwa. Kufikia wakati huo, Sheria ilikuwa imekuwepo kwa zaidi ya miaka 1,000! Hata hivyo, Ezra na wasaidizi wake “wakasoma katika kitabu, katika torati ya Mungu, kwa sauti ya kusikilika; wakaeleza maana yake, [wakatia maana, “NW”] hata wakayafahamu yaliyosomwa.” Wanaume hao walipoeleza Maandiko na kuyasoma kwa njia ya kusisimua, matokeo yalikuwa nini? “Watu wote wakaenda zao kula na kunywa, na kuwapelekea watu sehemu, na kufanya furaha nyingi, kwa sababu walikuwa wameyafahamu maneno yale waliyohubiriwa.”—Nehemia 8:1-12.

Waweza ‘kutiaje maana’ katika usomaji wako wa Biblia? Cathy, anayeona kusoma kuwa jambo gumu, husoma kwa sauti ili akaze fikira. Nicki hujaribu kujihusisha katika simulizi hilo. Yeye asema: “Mimi huwazia jinsi ningalihisi nikiwa katika hali hiyo. Sikuzote nimependelea zaidi hadithi ya Ruthu na Naomi. Ninaweza kuisoma mara nyingi. Nilipohamia jiji jingine, hadithi hiyo ilinifariji kwa sababu nilifikiria jinsi Ruthu alivyohisi alipokwenda mahala pageni pasipo kumjua mtu yeyote. Niliona jinsi alivyomtumaini Yehova, na hilo likanisaidia kufanya vivyo hivyo.”—Ruthu, sura ya 1-4.

Ili Biblia ‘ikazie nguvu,’ kutafakari kwahitajiwa. Kila usomapo, chukua wakati kutafakari maandiko uliyosoma na ufikirie jinsi utakavyotumia mambo uliyojifunza. Huenda ungependa kuchunguza vichapo vinavyotegemea Biblia vilivyochapishwa na Mashahidi wa Yehova ili kuboresha usomaji wako. *

Dumu!

Si rahisi kushikamana na ratiba ya usomaji wa Biblia. Hata ratiba bora ya usomaji wa Biblia huhitaji kurekebishwa mara kwa mara. Waweza kudumishaje mradi wako wa kusoma Biblia kila siku?

Rafiki zako na washiriki wa familia yako waweza kusaidia. Amber, mwenye umri wa miaka 15, asema hivi: “Mimi na dadangu hutumia chumba kimoja. Jioni fulani mimi huwa nimechoka sana hivi kwamba ninahisi nikitaka tu kulala, lakini dadangu hunikumbusha kusoma. Hivyo sisahau kamwe kusoma!” Ikiwa wapendezwa na andiko au simulizi fulani, zungumza na wengine kulihusu. Hilo litaongeza uthamini wako kwa Neno la Mungu na huenda hata likawachochea wapendezwe kusoma Biblia. (Waroma 1:11, 12) Usiposoma Biblia kwa siku moja au zaidi, usikate tamaa! Endelea kusoma ulipoachia, na uazimie sana kushikamana na ratiba yako.

Usisahau kamwe faida za kusoma Biblia kila siku. Kwa kumsikiliza Yehova kupitia Neno lake, waweza kufurahia uhusiano wa karibu pamoja naye. Utajua fikira na hisia zake. (Mithali 2:1-5) Kweli hizo zenye thamani kutoka kwa Baba yetu wa kimbingu zitakulinda. “Jinsi gani kijana aisafishe njia yake?” aliuliza mtunga-zaburi. “Kwa kutii, akilifuata neno lako.” (Zaburi 119:9) Basi anza na ushikamane na kusoma Biblia kwa ukawaida. Utaona kufanya hivyo kutakufurahisha sana zaidi ya ulivyodhania!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 11 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 22 Toleo la Oktoba 1, 2000, la Mnara wa Mlinzi, ukurasa wa 16-17, latoa madokezo kadhaa yenye kutumika yatakayokusaidia kuchunguza Biblia kwa undani.

[Picha katika ukurasa wa 24]

Sala na kufanya utafiti kutaboresha usomaji wako wa Biblia na kukusaidia kuelewa maana ya Maandiko

[Picha katika ukurasa wa 25]

Kujihusisha katika simulizi kutafanya Maandiko yasisimue