Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kizazi Kilicho Hatarini

Kizazi Kilicho Hatarini

Kizazi Kilicho Hatarini

“Kufikia miezi miwili iliyopita, nilikuwa mwenye furaha na nilikuwa chapuchapu. Sasa, kila mara nipatapo nafasi ya kufanya kitu, mimi huhisi nimechoka sana. Sina raha na mimi hukasirika haraka, sifikiri mtu aweza kuvumilia kuwa pamoja nami. Sielewi ni kwa nini mimi huhisi vibaya ghafula.”—Paul.

“Mimi hulia na kuumia sana moyoni. Wakati ambapo sina maumivu hayo, mimi huhisi ni kana kwamba nimekufa ganzi. Sifurahii chochote. Sifurahii kuwa na marafiki wangu tena. Mimi hulala sana. Kwa siku nyingi siwezi kuamka ili kwenda shule na maksi zangu zimeshuka sana.”—Melanie.

HALI hiyo haiwakumbi tu Paul na Melanie. Uchunguzi waonyesha kwamba karibu asilimia 8 ya vijana waliobalehe nchini Marekani wamekumbwa na mshuko wa moyo wa aina fulani na kwamba kila mwaka karibu asilimia 4 ya vijana hao hushuka moyo sana. Lakini takwimu hizo hazionyeshi waziwazi jinsi hali ilivyo, kwani mara nyingi mshuko wa moyo hautambuliwi vyema au hupuuzwa kabisa. David G. Fassler, mwanasaikolojia wa masuala ya vijana waliobalehe, aandika hivi: “Kwa hakika, baada ya kupitia uchunguzi uliofanywa kuhusiana na watoto na matineja, nafikiri kwamba zaidi ya robo moja ya vijana watashuka moyo sana kwa kipindi fulani kabla ya kufikia umri wa miaka kumi na minane.”

Matokeo Yanayofadhaisha

Mshuko wa moyo huwafadhaisha matineja. Kwa kweli, wataalamu wanaamini kwamba kushuka moyo huchangia sana matatizo ya kula miongoni mwa vijana wanaobalehe, magonjwa yanayosababishwa na matatizo ya akili, matatizo shuleni, na kutumia dawa za kulevya.

La kusikitisha hata zaidi ni kwamba matineja hujiua kwa sababu ya kushuka moyo. Kwa mujibu wa Taasisi ya Kitaifa ya Marekani ya Masuala ya Akili, asilimia 7 ya vijana walioshuka moyo sana hujiua. * Hata takwimu hiyo haifunui waziwazi tatizo lenyewe, kwani yaaminika kwamba kati ya kila kijana anayejiua, wengine wengi huwa wamejaribu kufanya hivyo. Basi ndiyo sababu ripoti moja ya Baraza la Carnegie la Ustawi wa Vijana Wanaobalehe yasema hivi kwa kufaa: “Siku hizi kupuuza matatizo ya vijana wanaobalehe ni kusababisha msiba. Kupuuza mambo hivyo huhatarisha kizazi.”

Eti Hawajali?

Wengine hawaamini kwamba matineja wanaweza kushuka moyo. Huenda watu wazima fulani wakasema: ‘Wao ni watoto tu. Wao hawajali, na bila shaka hawana mahangaiko ambayo watu wazima wanayo.’ Au, wanayo? Ukweli ni kwamba vijana wanaobalehe hukabili mikazo mingi ambayo watu wazima wengi hawatambui. Dakt. Daniel Goleman asema hivi: “Tangu karne [ya 20] ilipoanza, kila kizazi ulimwenguni pote kimekabili hatari kubwa ya kushuka moyo sana maishani kuliko hatari ambayo wazazi wao walikabili. Si kuhuzunika tu, bali ni kulegea legelege, kuwa na majonzi, kujihurumia, na kukosa tumaini kabisa. Na vipindi hivyo vya kushuka moyo huanza wakiwa wachanga zaidi na zaidi.”

Hata hivyo, wazazi wengi waweza kupinga jambo hilo hivi: ‘Sisi tulipita kipindi cha kubalehe bila kushuka moyo. Mbona mtoto wetu ana majonzi mengi?’ Lakini watu wazima hawapaswi kulinganisha maisha ya vijana ya sasa na maisha yao wakati walipobalehe. Kwani, watu huona na kuitikia mambo yanayowazunguka kwa njia tofauti.

Isitoshe, matineja wa leo wanakabili kibarua kingine. “Wanakua katika ulimwengu ulio tofauti kabisa na ule ambao wazazi wao walikulia walipokuwa vijana,” aandika Dakt. Kathleen McCoy katika kitabu chake Understanding Your Teenager’s Depression. Baada ya kutaja baadhi ya mabadiliko makubwa yaliyotukia katika miongo ya karibuni, Dakt. McCoy amalizia hivi: “Matineja leo hawajihisi salama sana, hawajiamini sana na hawana tumaini sana kama tulivyohisi katika kizazi kilichopita.”

Kwa kuwa matineja wengi wameshuka moyo sana, makala zifuatazo zitazungumzia maswali matatu:

• Ni nini baadhi ya dalili zinazoonyesha kwamba tineja ameshuka moyo?

Ni nini husababisha hali hiyo?

• Matineja walioshuka moyo waweza kusaidiwaje?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 7 Wataalamu fulani wanaamini kwamba takwimu sahihi ya vijana wanaojiua ni kubwa zaidi, kwani vifo fulani vinavyosemwa kuwa vya aksidenti vyaweza kuwa ni visa vya kujiua.