Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Ndoa Zisizo na Upendo Ilionekana kana kwamba ndoa yangu haikuwa na kusudi lolote tena. Mimi na mume wangu hatukupendana bali tulivumiliana tu. Mara kwa mara nilifikiria kupata talaka. Lakini upendo wetu umefufuka kwa sababu ya mfululizo wa Januari 8, 2001 yenye kichwa “Je, Twaweza Kuokoa Ndoa Yetu?”

E. R., Hispania

Mimi ni mke Mkristo, lakini kwa muda wa mwaka mzima nimekosa furaha kabisa katika maisha yangu ya ndoa. Mimi na mume wangu tulikuwa tumeumizana sana hivi kwamba ilionekana kama haingewezekana kurekebisha uhusiano wetu. Lakini niliposoma mfululizo huo, ilikuwa kana kwamba Yehova ananiambia, ‘Usife moyo!’ Nilisukumwa kuchukua hatua ili kuhuisha upendo mchangamfu tuliokuwa nao awali. Tayari nimeanza kuhisi kwamba mume wangu anaitikia. Nitasoma mfululizo huo tena na tena.

N. H., Japani

Nilibatizwa hivi majuzi na mke wangu asiyeamini amekuwa akinipinga. Mfululizo huo umenisaidia kuona jinsi ninavyoweza kufanya ndoa yangu ifanikiwe. Ulikuja kwa wakati unaofaa kabisa.

W. S., Australia

Kwa kuwa ndoa yangu ni yenye furaha, nilianza kusoma mfululizo huo kwa madhumuni ya kuwasaidia wengine. Lakini kuanzia maneno ya kwanza, mfululizo huo ulikuwa na ushauri unaoweza kuimarisha ndoa yangu mwenyewe.

M. D., Italia

Dada mmoja Mkristo katika kutaniko letu aliniambia kwamba alikuwa amegombana na mume wake asiyeamini na kwamba walikuwa wametengana. Baada ya muda aliniambia kwamba hali imekuwa afadhali. Alikuwa amesoma mfululizo huo kwa hamu, nao ulimsaidia sana kutatua tatizo lao. Alisema kwamba ushauri kuhusu mawasiliano hasa ulikuwa wenye manufaa. Yeye na mume wake wameungana tena.

N. S., Kanada

Utoaji-Sauti Nilivurugika akili niliposoma makala “Ni Nani Anayeongea?” (Januari 8, 2001) Je, Shetani hakutumia njia hii ili kumdanganya Hawa? Udanganyifu na ulaghai haupasi kuwa sehemu ya maisha ya Mkristo.

B. H., Marekani

Hatujui Shetani alitumia njia gani kumdanganya Hawa, lakini haingaliweza kuwa utoaji-sauti kwa kuwa hiyo inafanywa kwa kutumia mbinu mahususi za kupumua na kusema, na Shetani ni kiumbe wa kiroho. Maandiko hayakatai kufurahia utoaji-sauti wakati wa burudani. Ni wazi kwamba si vizuri kutumia stadi hiyo ili kudanganya mtu ukiwa na nia mbaya au kuendeleza mazoea ya uwasiliani-roho, kama ambavyo huenda wengine walifanya katika siku za Biblia. (Isaya 8:19)—Mhariri.

Mimi pia ninafurahia ustadi wangu wa utoaji-sauti na nimewatumbuiza wengine mara nyingi kwenye karamu za Kikristo. Kama vile makala hiyo ilivyoonyesha, sikio la mwanadamu haliwezi kutambua kwa urahisi upande ambao sauti hutoka. Jambo la kushangaza ni kwamba huwezi kumdanganya mnyama kwa njia hiyo. Ikiwa mimi ninaongea na mbwa wangu kupitia mwanasesere, ataniangalia mimi wala si mwanasesere. Yehova aliwapa wanyama masikio makali sana.

L. R., Marekani

Mbwa Asiye na Manyoya Sikuzote mimi huanza kusoma makala zisizonipendeza. Kwa kuwa sipendi mbwa, makala ya kwanza ambayo nilisoma katika toleo la Januari 8 ilikuwa, “Je, Umewahi Kukutana na Xoloitzcuintli?” Baada ya kumaliza kusoma makala hiyo, nilitaka mbwa wa aina hiyo! Hata hivyo nilibadili maoni haraka. Kwa vyovyote vile, nimesoma magazeti yenu kwa miaka 40, na sijakatishwa tamaa kamwe. Mara nyingi mimi hufurahia zaidi makala ambayo sikudhani ningeipenda.

D. W., Marekani