Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ninawezaje Kuacha Kuwa na Wasiwasi Mwingi Mno?

Ninawezaje Kuacha Kuwa na Wasiwasi Mwingi Mno?

Vijana Huuliza . . .

Ninawezaje Kuacha Kuwa na Wasiwasi Mwingi Mno?

“Huenda mojawapo ya mambo yanayomfadhaisha sana kijana ni maisha yake ya baadaye. Una wasiwasi mwingi kuhusu maisha yako. Je, nihame nyumbani? Je, niende chuoni? Je, niingie katika huduma ya wakati wote? Je, nioe? Una mambo mengi sana ya kuchagua hivi kwamba unaogopa.”—Shane, mwenye umri wa miaka 20.

JE, WEWE huwa na wasiwasi sana? Vijana wengi huwa na wasiwasi mwingi kwa sababu mbalimbali. Jarida moja la habari lililochapishwa ili kuwapa wazazi mwongozo liliripoti hivi: “Uchunguzi uliofanywa hivi majuzi ulimwenguni pote kuhusu matineja walio na umri wa miaka 15 hadi 18 katika nchi 41, ulifunua kwamba matineja wa sasa wanahangaikia hasa kupata kazi nzuri.” Jambo la pili linalowatia wasiwasi ni afya ya wazazi wao. Pia, sababu nyingine kuu ya wasiwasi ni kifo cha mpendwa.

Uchunguzi uliofanywa na Wizara ya Elimu huko Marekani ulionyesha kwamba vijana wengi nchini humo walikuwa na wasiwasi sana kwa sababu ya “mikazo ya kupata maksi za juu.” Uchunguzi huohuo ulifunua kwamba vijana wengi huhisi kama Shane (aliyenukuliwa mwanzoni). Kijana mwingine, anayeitwa Ashley, asema hivi: “Nina wasiwasi kuhusu maisha yangu ya baadaye.”

Na bado vijana wengine huwa na wasiwasi kuhusu usalama wao. Kwa mujibu wa uchunguzi uliofanywa mwaka wa 1996, asilimia 50 hivi ya vijana nchini Marekani walihisi kwamba jeuri ilikuwa inaongezeka shuleni mwao. Zaidi ya matineja milioni nane (asilimia 37) waliripoti kwamba walijua mtu fulani aliyekuwa amepigwa risasi!

Hata hivyo, si mahangaiko yote yanayoogofya sana. Vijana wengi wana wasiwasi mkubwa kuhusu uhusiano wao na vijana wengine. Gazeti moja kwenye Internet lililoandikwa kwa ajili ya wazazi, lilisema hivi: “Matineja huwa na wasiwasi juu ya kuwa na mpenzi wa kiume au wa kike, lakini mara nyingi wao huwa na wasiwasi juu ya kukosa marafiki kabisa.” Msichana mmoja tineja anayeitwa Meagan aeleza wasiwasi wake: “Nifanye nini ili nionekane kuwa kijana wa kisasa? Ninahitaji marafiki.” Vivyo hivyo, kijana mmoja Mkristo mwenye umri wa miaka 15 anayeitwa Natanael asema hivi: “Vijana shuleni huhangaikia mtindo. Wao huhangaikia jinsi wanavyotembea, wanavyoongea, na jinsi wengine wanavyowaona. Wanaogopa kuonekana washamba.”

Matatizo Ni Kawaida

Ingekuwa vizuri sana iwapo tungeweza kuishi bila wasiwasi. Hata hivyo, Biblia husema hivi: “Mwanadamu aliyezaliwa na mwanamke siku zake za kuishi si nyingi, naye hujaa taabu.” (Ayubu 14:1) Kwa hiyo, matatizo—na wasiwasi unaosababishwa nayo—ni kawaida. Lakini ukifikiria sana mahangaiko yako, waweza kujiumiza sana. Biblia huonya: “Uzito [hangaiko, NW] katika moyo wa mtu huuinamisha.”—Mithali 12:25.

Njia moja ya kuepuka kuwa na wasiwasi usiofaa ni kuangalia tabia yako. Ana, mwenye umri wa miaka 16 asema hivi: “Wengi wa wanadarasa wenzangu wana wasiwasi juu ya kupata mimba au ugonjwa unaoambukizwa kingono.” Lakini unaweza kuepuka wasiwasi huo kwa kufuata kanuni za Biblia za maadili. (Wagalatia 6:7) Hata hivyo, matatizo yako yote hayatatatuliwa kwa urahisi hivyo. Basi, utaachaje kuwa na wasiwasi mwingi mno?

‘Tumia Hekima Unapokuwa na Wasiwasi’

Watu wengi huruhusu wasiwasi uwagandamize. Lakini makala moja katika gazeti la matineja ilidokeza kwamba mtu aweza kuwa na ‘hekima anapokuwa na wasiwasi’ kwa kutumia wasiwasi kwa faida yake! Biblia ina kanuni nyingi zinazoweza kukusaidia kufanya hivyo. Fikiria Mithali 21:5: “Mawazo ya wenye bidii huuelekea utajiri tu.” Kwa mfano, tuseme unataka kualika rafiki zako wa kutaniko kwenye tafrija. Unaweza kuepuka wasiwasi mwingi kwa kupanga mambo vizuri. Jiulize, ‘Ni nani hasa nitakaoalika? Ninataka wafike saa ngapi? Ninataka waondoke saa ngapi? Ninahitaji viburudisho vingi kiasi gani? Ni michezo gani ambayo kila mtu atafurahia?’ Kadiri unavyofikiria zaidi kuhusu mambo hayo, ndivyo mipango yako ya kuwa na tafrija itakavyofanikiwa zaidi.

Hata hivyo, unaweza kujiletea wasiwasi kwa kufanya mambo kupita kiasi. Yesu Kristo alitoa shauri hili kwa mwanamke aliyejishughulisha kupita kiasi ili kumhudumia mgeni wake: “Ingawa hivyo, mambo machache yahitajiwa, au moja tu.” (Luka 10:42) Basi jiulize hivi, ‘Ni nini hasa jambo la muhimu ili tafrija hiyo ifanikiwe?’ Huenda kufanya mambo yawe sahili kukakusaidia kupunguza wasiwasi.

Huenda jambo jingine linalokupa wasiwasi ni usalama wako shuleni. Labda huwezi kubadili hali shuleni. Lakini unaweza kuchukua hatua zinazofaa ili ujilinde. “Mwenye busara huyaona mabaya na kujificha,” yasema Mithali 22:3. Kuepuka tu sehemu hatari—sehemu zisizokuwa na watu na pia sehemu ambazo vijana wakora hupenda kukusanyika—kwaweza kupunguza uwezekano wa kuingia hatarini.

Jambo jingine linaloweza kusababisha wasiwasi ni kazi za shule. Huenda ukawa na kazi muhimu za shule na una wasiwasi kwamba hutazimaliza zote kwa wakati. Kanuni iliyo kwenye Wafilipi 1:10 husaidia: ‘Hakikisha mambo yaliyo ya maana zaidi.’ Naam, jifunze kupanga mambo yanayofaa kutangulizwa! Tambua ni kazi gani inayohitajika haraka, na uifanye kwanza. Kisha, fanya kazi ya pili. Pole kwa pole utaona kwamba unashughulikia mambo hayo kwa utulivu.

Omba Mashauri

Aaron alipokuwa kijana, alikuwa na wasiwasi sana kuhusu kufaulu mtihani wake wa mwisho hivi kwamba alipata maumivu ya kifua. Yeye akumbuka hivi: “Nilizungumza na wazazi wangu, kisha wakanipeleka kwa daktari. Daktari alitambua mara moja kwamba moyo wangu haukuwa na kasoro yoyote na akaeleza jinsi kuhangaika kunavyoweza kuathiri mwili. Baadaye, wazazi wangu walinisaidia kung’amua kwamba nilikuwa nimejitayarisha vilivyo kwa ajili ya mtihani na kwamba sasa nilipaswa kujitunza. Wasiwasi wangu ulipoisha, maumivu ya kifua yaliisha, na nilifaulu sana katika mtihani.”

Ukihisi kwamba umelemewa na wasiwasi mwingi, mweleze mtu mwingine. Andiko la Mithali 12:25, lililonukuliwa kwa sehemu hapo awali, lasema hivi: “Uzito [hangaiko, NW] katika moyo wa mtu huuinamisha; bali neno jema huufurahisha.” Ni lazima ueleze “hangaiko” lako ndiposa upate “neno jema” la kukutia moyo!

Kwanza kabisa, huenda ukapenda kuzungumza na wazazi wako; wanaweza kukupa madokezo kadhaa. Watu waliokomaa kiroho katika kutaniko lako la Kikristo watakutegemeza pia. Janelle, mwenye umri wa miaka 15, asema hivi: “Nilikuwa na wasiwasi juu ya kwenda shule ya sekondari kwa kuwa niliogopa kila kitu—dawa za kulevya, ngono, jeuri—hadi nilipozungumza na mzee wa kutaniko. Alinipa madokezo mengi yafaayo. Mara moja nikahisi vizuri kwa kuwa sasa nilitambua kwamba ningeweza kushughulikia hali hiyo ifaavyo.”

Usiahirishe Mambo

Mara kwa mara kuna mambo tunayopaswa kufanya, lakini tunayaahirisha kwa kuwa hatupendezwi nayo. Kwa mfano, Shevone, mwenye umri wa miaka 19, alikosana na Mkristo mwenzake. Alijua kwamba alipaswa kuzungumza naye kuhusu jambo hilo, lakini aliahirisha kufanya hivyo. Yeye akiri hivi: “Kadiri nilivyoahirisha jambo hilo, ndivyo lilivyonisumbua zaidi.” Kisha Shevone alikumbuka maneno ya Yesu kwenye Mathayo 5:23, 24, yanayowahimiza Wakristo watatue matatizo kama hayo mara moja. Shevone akumbuka hivi: “Nilipofanya hivyo mwishowe, nilihisi vizuri sana.”

Je, kuna jambo unaloahirisha—mgawo usiopenda au mkwaruzano pamoja na mtu fulani? Naam, usikawie kulitatua, na utakuwa umepunguza mahangaiko yako.

Mambo Mazito

Si mambo yote yanayotatuliwa kwa urahisi. Fikiria kisa cha mwanamume anayeitwa Abdur. Mamake ana ugonjwa wa kansa, na Abdur huhitajika kutafuta riziki ili kumtunza mamake na nduguye mdogo. Bila shaka, Abdur huhangaikia hali ya mamake. Lakini yeye asema hivi: “Mimi hufuata maneno haya ya Yesu, ‘Ni nani kati yenu kwa kuhangaika aweza kuongeza dhiraa moja kwenye muda wake wa uhai?’ Badala ya kuvunjika moyo, mimi hujaribu kufikiria hali hiyo na kutafuta utatuzi bora.”—Mathayo 6:27.

Si rahisi kutulia unapokabili hali ngumu. Wengine hufadhaika sana hivi kwamba wanaacha kujitunza na kukataa kula. Hata hivyo, kitabu Helping Your Teenager Deal With Stress, chaonya kwamba ukijinyima chakula, ‘hata hutaweza kukinza madhara ya mfadhaiko na utakabili hatari kubwa hata zaidi ya kupata magonjwa mabaya sana.’ Basi, tunza afya yako. Pumzika na ule vya kutosha.

Unaweza kupata kitulizo kikubwa zaidi kwa kufuata shauri hili la Biblia: “Umtwike BWANA mzigo wako naye atakutegemeza, hatamwacha mwenye haki aondoshwe milele.” (Zaburi 55:22) Shane, aliyenukuliwa hapo mwanzoni, alihangaikia maisha yake ya baadaye. Yeye akumbuka hivi: “Nilianza kukazia fikira zaidi Neno la Mungu na kusudi lake.” Punde si punde akatambua kwamba maisha yake ya baadaye yatakuwa yenye furaha iwapo atamtumikia Mungu. (Ufunuo 4:11) Shane asema hivi: “Niliacha kujifikiria sana. Nilikuwa na jambo la maana zaidi la kufikiria.”

Basi, ukiwa na wasiwasi mwingi mno, tafuta njia zinazofaa za kukabiliana na tatizo lako. Tafuta mashauri ya mtu aliyekomaa. Zaidi ya yote, mweleze Yehova mahangaiko yako ‘kwa sababu yeye hukujali wewe.’ (1 Petro 5:7) Kwa msaada wake, huenda utaacha kuwa na wasiwasi mwingi mno.

[Picha katika ukurasa wa 13]

Zungumza na wazazi wako kuhusu wasiwasi wako

[Picha katika ukurasa wa 14]

Ukishughulikia matatizo yako upesi, wasiwasi wako utaisha upesi