Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ukweli Kuhusu Sherehe Zinazopendwa

Ukweli Kuhusu Sherehe Zinazopendwa

Ukweli Kuhusu Sherehe Zinazopendwa

WACHAWI na mazimwi, maboga na mioto mikubwa ya sherehe, vitisho vya kupata peremende. Mambo mengi kuhusu sherehe ya Halloween yanajulikana kwa urahisi. Lakini ni mambo yapi yasiyojulikana kuhusu sherehe hiyo na sherehe nyinginezo za aina hiyo? Neno la Kiingereza “Halloween” ni ufupisho wa usemi, “All Hallows’ Eve” unaomaanisha, mkesha wa Siku ya Watakatifu Wote. Lakini, jina hilo linalodhaniwa kuwa la Kikristo huficha vyanzo vya sherehe hiyo ambavyo si vitakatifu. Kwa kweli, wasomi wanasema kwamba sherehe ya Halloween ilianza mapema kabla ya Ukristo—wakati Waselti wa kale walipoishi Uingereza na Ireland. Kwa kutumia kalenda inayotegemea mzunguko wa mwezi, Waselti waligawanya mwaka katika majira mawili—miezi yenye giza ya baridi kali na miezi yenye nuru ya kiangazi. Wakati wa mwezi mpevu, karibu Novemba 1, Waselti walisherehekea sikukuu ya Samhain, iliyoashiria “Mwisho wa Kiangazi.” *

Sherehe hiyo, iliyoashiria mwanzo wa mwaka mpya wa Waselti, ilifanywa mwishoni mwa kiangazi, baada ya mavuno kukusanywa na mifugo kuingizwa vizimbani kutoka malishoni. Waselti waliamini kwamba kadiri siku zilivyozidi kuwa fupi, ndivyo ilivyokuwa muhimu kulitia jua nishati mpya kupitia desturi za kichawi na dhabihu mbalimbali. Mioto yote ilizimwa wakati mwaka ulipokuwa ukimalizika, na mwaka mpya ulifunguliwa kwa kuwasha mioto mikubwa mitakatifu ambayo ilitumiwa kuwasha mioto midogo katika kila nyumba. Mioto hiyo mikubwa ni kama ile inayowashwa leo wakati wa sherehe ya Usiku wa Guy Fawkes nchini Uingereza na Brazili mnamo mwezi wa Juni. Ilidhaniwa kwamba mioto hiyo ingefukuza roho waovu.

Iliaminika kwamba mipaka inayotenga wanadamu na viumbe wa roho iliondolewa wakati wa sherehe ya Samhain, na hivyo roho wazuri na waovu, walitangatanga ulimwenguni. Ilidhaniwa kwamba nafsi za wafu zilirejea nyumbani, na familia ziliandaa chakula na kinywaji kwa ajili ya wageni hao wa roho zikitumaini kwamba vitu hivyo vingeweza kuwatuliza na hivyo kuwaepusha na misiba. Kwa hiyo, watoto wanapovalia kama mazimwi au wachawi na kwenda nyumba kwa nyumba wakiomba zawadi ya Halloween au wakiwatisha watu, wanaiga desturi za kale za Samhain pasipo kujua. Jean Markale anasema hivi katika kitabu chake Halloween, histoire et traditions (Historia na Desturi za Halloween): “Watoto wanapopokea zawadi, wanaonyesha kwa njia ya mfano na pasipo kujua, ushirikiano wa kidugu uliopo kati ya wanadamu na viumbe wa roho. Ndiyo sababu Halloween . . . huonwa kuwa sherehe takatifu.”

Kwa kuwa watu waliamini kwamba mipaka kati ya ulimwengu halisi na makao ya viumbe wa roho iliondolewa, walifikiri kwamba wanadamu wangeweza kuvuka kwa urahisi kwenye makao ya viumbe wa roho. Kwa hiyo sherehe ya Samhain ilikuwa pindi nzuri ya kujua siri za wakati ujao. Mitofaa au miti ya kokwa za hazel ilionwa kuwa mitakatifu, na matunda yake yalitumiwa kubashiri habari za ndoa, ugonjwa, na kifo. Kwa mfano, matofaa yenye alama za pekee yalitiwa katika beseni la maji. Mwanamume au mwanamke angeweza kuchagua mwenzi wake wa ndoa wa wakati ujao kwa kutwaa tofaa kwa kinywa chake tu. Zoea hilo la kubashiri lingali linaendelea leo katika mchezo wa kutwaa matofaa kwa kinywa wakati wa Halloween.

Sherehe ya Samhain ilikuwa pia na karamu za ulevi zenye vifijo na nderemo na watu walifanya walivyopenda. “Maadili ya kawaida yalivunjwa au kupotoshwa,” asema Markale. “Mambo yaliyokatazwa yalikubaliwa, na mambo yaliyokubaliwa yalikatazwa.” Mtazamo huo ungali unadhihirishwa leo katika sherehe ya Halloween. Ndiyo sababu inapendwa sana na wengi. Kikizungumzia jambo hilo, kichapo The Encyclopedia of Religion chasema kwamba leo Halloween ni ‘wakati ambapo watu wazima wanaweza pia kuvuka mipaka ya kitamaduni na kupuuza hadhi yao kwa kufanya mambo mapotovu kupindukia. Hivyo basi, maoni ya msingi ya Waselti ya kwamba sherehe hiyo ya kila mwaka ni jioni ya kukiuka mambo ya kawaida ya maisha na kupuuza kanuni zilizopo yamedumu hadi karne ya 20.’

Uadui wa Kidini

Baada ya njaa ya viazi katika karne ya 19, wahamaji wa Ireland waliendeleza Halloween na desturi zake nchini Marekani. Sasa sherehe hiyo imerejea Ulaya katika miaka michache iliyopita. Hata hivyo, si kila mtu anayependa sherehe ya Halloween. Gazeti la Le Monde linasema kwamba ‘Halloween, ambayo inaambatana na Siku ya Watakatifu Wote na Siku ya Nafsi Zote (Novemba 1 na 2), huenda ikachukua mahali pa sikukuu hizo. Makasisi wanahofu mwelekeo huo lakini wafanyabiashara wanafurahia jambo hilo.’

Wawakilishi wa kanisa nchini Ufaransa wanahangaika kwa sababu sikukuu hizo za Kikatoliki zilizoanza kale zinapuuzwa na badala yake watu wanapendelea Halloween. Wanaona hiyo ni ishara ya kwamba “upagani unaenea katika jamii.” Stanislas Lalanne, msemaji wa Mkutano wa Maaskofu Wakatoliki nchini Ufaransa alisema kwamba, Halloween ‘inapotosha maana ya uhai na kifo.’ Askofu wa Nice, Jean Bonfils, alisema kwamba “sherehe hiyo na desturi zake hazihusiani kwa vyovyote na utamaduni wa Mediterania na wa Kikristo,” naye akawaonya Wakatoliki dhidi ya “sherehe muhimu zaidi ya waabudu wa Shetani ulimwenguni pote.”

Hippolyte Simon, askofu wa Clermont-Ferrand, asema hivi kuhusu hali ya Wafaransa kuacha desturi za Kikatoliki na kufuata sherehe za kipagani: ‘Ni kana kwamba Wafaransa wanatafuta dini fulani ya kitamaduni itakayoweza kuchukua mahali pa Ukristo.’ Yeye aandika hivi: “Wakati wa sherehe ya Halloween wafu wanaigwa, na ‘mazimwi’ yao yanaibuka ili kutuogopesha na kutisha kutuua. Kwa upande mwingine, wakati wa Siku ya Watakatifu Wote tunathibitisha kwamba wafu wako hai na tunapata ahadi ya kwamba tutajiunga nao katika Mji wa Mungu.”—Vers une France païenne? (Je, Ufaransa Inaelekea Kuwa ya Kipagani?)

Vivyo hivyo, Carlo Maria Martini, kadinali wa Milan, Italia, aliwasihi Waitalia wasiache kuadhimisha sikukuu za Kikatoliki, kisha akasema kwamba Halloween ni “sherehe ngeni katika desturi zetu, ambazo ni muhimu na ni lazima ziendelezwe. Siku ya Nafsi Zote ni sherehe ya kihistoria. Ni wakati ambapo tumaini la kuishi milele linapofunuka, wakati ambapo Bwana anatujulisha kwamba kuna maisha mengine bora kuliko maisha ya duniani.” Bila shaka Wakatoliki wengi wenye mioyo minyofu wanahisi vivyo hivyo. Lakini, je, tofauti kati ya sherehe ya Halloween na Siku ya Nafsi Zote ni wazi kama maelezo hayo yanavyojaribu kutusadikisha? Twagundua nini tuchunguzapo kwa uangalifu chanzo cha sikukuu hizo za Kikatoliki?

Sherehe ya Kipagani Inayoonwa Kuwa Takatifu

Kichapo The Catholic Encyclopedia chafafanua Siku ya Watakatifu Wote kuwa sherehe ya “kuheshimu watakatifu wote, wanaojulikana na wasiojulikana.” Mwishoni mwa karne ya pili, wale waliodai kuwa Wakristo walianza kuwaheshimu wafia-imani. Waliamini kwamba tayari watu hao walikuwa mbinguni pamoja na Kristo na hivyo waliomba watu hao wasali kwa niaba yao. Mwadhimisho wa kawaida ulianza Mei 13, * 609 au 610 W.K., wakati Papa Boniface wa 4 alipoweka wakfu Pantheon—hekalu la Roma la miungu yote—kwa Mariamu na wafia-imani wote. Markale asema hivi: “Mahali pa miungu ya Roma palichukuliwa na watakatifu wa dini bandia ya Kikristo.”

Papa Gregory wa 3 (731-741 W.K.), ndiye aliyebadili tarehe hiyo hadi mwezi wa Novemba. Aliweka wakfu kanisa moja huko Roma kwa watakatifu wote kisha akaamuru waheshimiwe Novemba 1. Sababu iliyomfanya abadili tarehe hiyo haijulikani. Lakini huenda ni kwa sababu sikukuu hiyo ilikuwa ikiadhimishwa tarehe hiyohiyo huko Uingereza. Kichapo The Encyclopedia of Religion kinasema kwamba, ‘sherehe ya Samhain iliendelea kupendwa na Waselti kotekote Uingereza wakati Ukristo ulipokuwa ukienea nchini humo. Kanisa la Uingereza lilijaribu kukengeusha fikira za watu kutoka kwa desturi hizo za kipagani kwa kuanzisha sherehe ya Kikristo siku ileile ya sikukuu ya Samhain. . . . Huenda sherehe ya Siku ya Watakatifu Wote iliyoanza katika enzi za kati nchini Uingereza ilienea upesi katika makanisa ya Kikristo ulimwenguni pote.’

Markale anataja kwamba uvutano wa watawa wa Ireland ulikuwa ukiongezeka wakati huo kotekote katika Ulaya. Pia, kichapo New Catholic Encyclopedia chasema hivi: ‘Wakazi wa Ireland walisherehekea sikukuu muhimu tarehe moja ya mwezi. Kwa kuwa majira ya baridi kali ya Waselti yalianza Novemba 1, basi yamkini siku hiyo ingefaa kuwa sikukuu ya watakatifu wote.’ Hatimaye, Papa Gregory wa 4 aliifanya siku hiyo kuwa sikukuu ya kimataifa mnamo mwaka wa 835 W.K.

Katika karne ya 11, watawa wa mji wa Cluny nchini Ufaransa waliteua Novemba 2 kuwa Siku ya Nafsi Zote. Siku hiyo sala hutolewa ili kusaidia nafsi zitoke toharani na kuishi raha mustarehe mbinguni. Ijapokuwa inadhaniwa kwamba Siku ya Nafsi Zote ni sikukuu ya Kikatoliki, yaonekana wazi kwamba watu wa kawaida walitatanishwa na siku hiyo. Kichapo cha New Catholic Encyclopedia chasema kwamba “katika Enzi za Kati watu wengi waliamini kwamba nafsi zilizo toharani zingeweza kutokea siku hiyo kama mwanga kwenye vinamasi, wachawi, vyura, na kadhalika.”

Kanisa lilikubali imani za kipagani kana kwamba ni za Kikristo kwa sababu lilishindwa kuwazuia waumini kufuata imani hizo. Kichapo The Encyclopedia of Religion chakazia jambo hilo kwa kusema hivi: ‘Sherehe ya Kikristo ya Siku ya Watakatifu Wote, ni ya kukumbuka watakatifu wanaojulikana na wasiojulikana wa dini ya Kikristo kama vile sherehe ya Samhain ilivyoheshimu na kusifu miungu ya Waselti.’

Msimamo Wako Kuhusu Sherehe Zinazopendwa

Unapaswa kufikiria kwa kadiri gani mwanzo mwovu wa Halloween na sherehe nyinginezo kama hiyo? Watu wengi hudhani kwamba Halloween ni wakati tu wa kujipamba na kuburudika. Lakini je, hukubali kwamba ni muhimu kwa wazazi kuhakikisha kwamba watoto wao wanafurahia vitumbuizo vinavyofaa na visivyodhuru?

Mkaguzi mmoja wa shule nchini Ufaransa ambaye amekuwa mwalimu kwa zaidi ya miaka 20 aliulizwa jinsi Halloween inavyoathiri watoto wadogo. Alisema hivi: “Nina wasiwasi kwamba kwenda nyumba kwa nyumba na kuwatisha watu wazima ili kupata peremende kwaweza kuwa na matokeo mabaya ya kudumu kwa watoto. Kufanya hivyo kunaweza kuwafanya wawe na ubinafsi na wajifikirie tu. Wanajifunza kwamba wanaweza kupata chochote wanachotaka kwa kutumia nguvu, kuwatisha, na kuwaogopesha wengine.” Basi lazima wazazi wajiulize hivi, ‘Watoto wangu watajifunza nini kwa kusherehekea sikukuu hii?’

Haishangazi kuwa familia nyingi zinajua kwamba kuwapa watoto zawadi na mavazi wanapodai kinguvu hugharimu pesa nyingi sana. Robert Rochefort, mkurugenzi mkuu wa Kituo cha Ufaransa cha Utafiti na Uchunguzi wa Hali ya Maisha, alisema “Halloween . . . si sikukuu, ni siku ya biashara.” Halloween ni kipindi maalumu cha kununua bidhaa kabla ya Krismasi. Yaani, ni tukio linalowalazimu watu kutumia pesa—pesa ambazo mara nyingi wanahitaji sana. Je, ni lazima ufanye hivyo kwa sababu watu wengi wanafanya hivyo?

Hata hivyo, jambo linalowashtua zaidi Wakristo ni uhakika wa kwamba Halloween na sherehe nyinginezo kama hiyo zimejaa mambo ya kipagani. Mtume Paulo aliandika hivi: “Sitaki nyinyi mwe washiriki pamoja na roho waovu. Hamwezi kuwa mkinywa kikombe cha Yehova na kikombe cha roho waovu.” (1 Wakorintho 10:20-22) Aliuliza hivi pia: “Je, wema na uovu vyapatana kweli? Mwanga na giza vyawezaje kukaa pamoja? Kristo anawezaje kupatana na Shetani? Muumini ana uhusiano gani na asiyeamini?” (2 Wakorintho 6:14-16, Biblia Habari Njema) Kwa hiyo Biblia inashutumu hali ya kufuata mazoea ya kipagani kana kwamba ni ya Kikristo!

Pia, Biblia inaonya kuhusu zoea la uwasiliani-roho. (Kumbukumbu la Torati 18:10-12) Ingawa ni kweli kwamba idadi kubwa ya watu wanaosherehekea Halloween watadai kwamba wanachukia mazoea ya Kishetani, hata hivyo, twapaswa kujua kwamba historia inaonyesha kuwa sikukuu hiyo inahusiana sana na mizungu. Hivyo basi, inaweza kumtumbukiza mtu kwa uwasiliani-roho, hasa vijana wanaovutiwa na kila jambo. Ni wazi kwamba desturi na mila za kipagani zinazohusiana na uwasiliani-roho hazikubaliwi kabisa katika ibada ya Kikristo; ni hatari sana.

Mwishowe, sherehe ya Halloween, Siku ya Watakatifu Wote, na Siku ya Nafsi Zote zinategemea imani ya kwamba wafu huteseka au wanaweza kuwadhuru walio hai. Hata hivyo, Biblia inaonyesha wazi kwamba imani kama hizo si za kweli, inasema: “Walio hai wanajua ya kwamba watakufa; lakini wafu hawajui neno lo lote.” (Mhubiri 9:5) Ndiyo sababu Biblia inashauri: “Lo lote mkono wako utakalolipata kulifanya, ulifanye kwa nguvu zako; kwa kuwa hakuna kazi, wala shauri, wala maarifa, wala hekima, huko kuzimu [kaburini] uendako wewe.” (Mhubiri 9:10) Hatupaswi kuwahofu wafu kwa sababu hawana fahamu na hivyo hawawezi kuteseka wala kuwadhuru wengine. Isitoshe, kusali kwa niaba yao ni kazi ya bure. Je, hilo lamaanisha kwamba wapendwa wetu waliokufa hawana tumaini? La. Biblia inatuhakikishia kwamba “kutakuwa na ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.”—Matendo 24:15. *

Mtu mwenye ujuzi ana uhuru wa kuchagua. Hatutarajiwi kufanya uamuzi wa hekima iwapo hatujui ukweli wa mambo. Baada ya kuchunguza mambo hakika yaliyozungumziwa katika mfululizo huu wa makala, utaamuaje?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 2 Yaelekea Samhain si jina la mungu wa kifo wa Waselti kama inavyosemekana mara nyingi, bali ni jina la sherehe hiyo. Kulingana na Jean Markale, mtaalamu Mfaransa wa historia ya Waselti, huenda mungu wa nuru, aitwaye Lug, ndiye aliyeheshimiwa wakati wa sherehe ya Samhain.

^ fu. 13 Inastaajabisha kwamba tarehe hiyo ililingana na sherehe ya Kiroma ya Lemuria, iliyofanywa Mei 9, 11, na 13 ili kutuliza nafsi za wafu zisisumbue na kudhuru jamaa zao.

^ fu. 24 Kwa habari zaidi kuhusu fundisho la Biblia la ufufuo, ona “Inakuwaje kwa Wapendwa Wetu Waliokufa?,” katika sura ya 9 ya kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Blabu katika ukurasa wa 6]

Sherehe ya Halloween huendeleza uwongo wa kwamba wafu wako hai

[Blabu katika ukurasa wa 7]

Desturi za Waselti za uaguzi ziliendelezwa na michezo ya Halloween

[Picha katika ukurasa wa 6]

Sherehe ya “Halloween” ilitokana na sherehe ya Waselti, labda ibada ya Lug, mungu wa nuru

[Picha katika ukurasa wa 6]

Makaburi yenye misalaba ya kale ya Waselti

[Picha katika ukurasa wa 7]

Kutwaa matofaa kwa kinywa ni mojawapo ya michezo iliyoanzishwa na Waselti

[Hisani]

Kutoka kwa gazeti: The Delineator October 1911

[Picha katika ukurasa wa 8]

Papa Boniface wa 4 aliweka wakfu hekalu la kipagani la Pantheon huko Roma kwa Maria na wafia-imani wote wa kanisa

[Picha katika ukurasa wa 9]

Sherehe ya Halloween inawaathirije watoto wako?

[Picha katika ukurasa wa 10]

Wakristo wa kweli hufurahia tafrija nzuri ya familia