Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuna Ubaya Gani Kulipiza Kisasi?

Kuna Ubaya Gani Kulipiza Kisasi?

Vijana Huuliza . . .

Kuna Ubaya Gani Kulipiza Kisasi?

“Alinitusi.”—Conneel, mwenye umri wa miaka 15, amefungwa gerezani kwa sababu ya kuua.

Andrew, mwenye umri wa miaka 14, aliyemuua mwalimu kwenye dansi ya shule, alidai kwamba aliwachukia walimu na wazazi wake, hata aliwakasirikia wasichana kwa kumkataa.

GAZETI la Time linautaja kuwa “mwelekeo hatari.” Kijana mwenye hasira aingia na silaha hatari shuleni na kuwafyatua risasi wanashule wenzake na walimu. Visa hivyo vya kusikitisha vimeanza kuonekana kuwa vya kawaida sana nchini Marekani hivi kwamba kituo kimoja cha habari cha televisheni kilifafanua mwelekeo huo kuwa “jeuri iliyopamba moto.”

Angalau visa vya kutumia bunduki shuleni bado ni vichache sana. Hata hivyo, visa vya karibuni vya uhalifu vinavyochochewa na hasira kali vinaonyesha waziwazi jinsi vijana fulani walivyo na ghadhabu. Ni nini huchochea milipuko hiyo ya hasira? Hapana shaka kwamba baadhi ya vijana hao walikasirika sana kwa kudhulumiwa au kuonewa na watu wenye mamlaka. Wengine walikasirika wakati wenzao walipoendelea kuwafanyia mzaha. Mvulana mmoja mwenye umri wa miaka 12 aliyemfyatua risasi mwanadarasa mwenzake—kisha akajifyatua—alikuwa amefanyiwa mzaha kuwa yeye ni mnene kupita kiasi.

Ni kweli kwamba huenda vijana wengi hawanuii kufanya matendo hayo mabaya sana ya jeuri. Hata hivyo, si rahisi kuzuia hisia za uchungu unapobaguliwa, unapoonewa, au unapotukanwa. Ben asema hivi anapokumbuka wakati alipokuwa shuleni: “Mimi ndiye niliyekuwa mfupi zaidi kati ya watoto wa umri wangu. Na kwa kuwa nilinyoa upara, watoto wengine walikuwa wakinifanyia mzaha kila wakati na kunipiga ngoto kichwani. Hilo lilinikasirisha sana. Jambo lililochochea hali hiyo hata zaidi ni kwamba nilipowaomba wenye mamlaka msaada, walinipuuza. Hilo lilinikasirisha hata zaidi!” Ben aongezea kusema hivi: ‘Ningewafyatua risasi watu hao lakini jambo moja tu lililonizuia ni kwamba singeweza kupata bunduki.’

Wapaswa kuwaonaje vijana wanaotaka kuwaumiza watu waliowaumiza? Na wapaswa kufanya nini ukitendewa vibaya? Ili kujibu maswali hayo, fikiria yale ambayo Neno la Mungu husema.

Kujidhibiti—Ni Ishara ya Nguvu!

Kutendewa vibaya na kudhulumiwa ni mambo yaliyoanza zamani. Mwandikaji mmoja wa Biblia alishauri hivi: “Ukomeshe hasira, uache ghadhabu, usikasirike, mwisho wake ni kutenda mabaya.” (Zaburi 37:8) Mara nyingi, watu hughadhibika kwa sababu ya kutojidhibiti na huonyesha ghadhabu yao bila kujali matokeo. Kujiruhusu ‘kukasirika’ kwaweza kutokeza mlipuko wa ghadhabu! Na matokeo yaweza kuwa nini?

Fikiria mfano wa Biblia wa Kaini na Abeli. ‘Kaini akamkasirikia sana’ Abeli nduguye. Tokeo ni kwamba “walipokuwa shambani, Kaini akamvamia Abeli nduguye, akamwua.” (Mwanzo 4:5, 8, BHN) Mtu mwingine ambaye hakudhibiti ghadhabu yake ni Mfalme Sauli. Kwa kumwonea kijana Daudi wivu kwa sababu ya mafanikio yake makubwa vitani, alimrushia Daudi mikuki na pia Yonathani mwanawe!—1 Samweli 18:11; 19:10; 20:30-34.

Ni kweli kwamba kuna wakati ambapo yafaa kukasirika. Lakini hata wakati huo, hasira adilifu isipodhibitiwa yaweza kutokeza uovu. Kwa mfano, pasipo shaka Simeoni na Lawi walikuwa na haki ya kumkasirikia Shekemu walipojua kwamba alimbaka dada yao Dina. Lakini badala ya kutulia, walichochea ghadhabu kama inavyoonyeshwa na maneno haya waliyosema baadaye: “Je! Ni vema amtendee umbu letu kama kahaba?” (Mwanzo 34:31) Na walipopandwa na hasira kabisa “walizitwaa panga zao, wakauvamia mji ghafla na kuwaua wanaume wote” walioishi katika kijiji cha Shekemu. Hasira yao iliwaathiri wengine kwani “wana wengine wa Yakobo” walijiunga katika mashambulizi hayo ya mauaji. (Mwanzo 34:25-27, BHN) Hata miaka mingi baadaye, Yakobo, baba ya Simeoni na Lawi, alishutumu hasira yao isiyodhibitiwa.—Mwanzo 49:5-7.

Twajifunza hoja muhimu kutokana na hayo: Hasira isiyodhibitiwa si ishara ya nguvu bali ni ya udhaifu. Mithali 16:32 husema hivi: “Asiye mwepesi wa hasira ni mwema kuliko shujaa; na mtu aitawalaye roho yake kuliko mtu atekaye mji.”—Italiki ni zetu.

Upumbavu wa Kulipiza Kisasi

Hivyo, Maandiko hushauri hivi: “Msirudishe ovu kwa ovu kwa yeyote. . . . Msijilipizie kisasi wenyewe.” (Waroma 12:17, 19) Kulipiza kisasi—kuwe kwahusisha ujeuri wa kutumia nguvu au maneno tu yanayoudhi—ni kumwasi Mungu. Vilevile, kulipiza kisasi si jambo la akili wala la hekima. Kwani, kwa kawaida jeuri hutokeza jeuri zaidi. (Mathayo 26:52) Na maneno yanayoudhi hutokeza maneno zaidi yanayoudhi. Pia, kumbuka kwamba mara nyingi hakuna sababu maalumu ya kukasirika. Kwa mfano, je, waweza kweli kujua kwamba mtu aliyekukosea alikuwa na nia mbaya? Si yawezekana kwamba mtu huyo hakufikiri au hakujua anachofanya? Na hata ikiwa alikuwa na nia mbaya, je, kweli yafaa kulipiza kisasi?

Fikiria maneno ya Biblia yanayopatikana kwenye Mhubiri 7:21, 22: “Usitie moyoni mwako maneno yote yaliyosemwa; usije ukamsikia mtumwa wako mwenyewe ali anakutukana. Kwa kuwa mara nyingi moyo wako pia unajua ya kwamba wewe mwenyewe umewatukana watu wengine.” Naam, watu wanaposema mambo mabaya kukuhusu huwezi kufurahi. Lakini Biblia yakubali kwamba hilo ni jambo la kawaida. Je, si ni kweli kwamba huenda umesema mambo kuhusu wengine ambayo hukupaswa kusema? Basi kwa nini ukasirike sana mtu asemapo jambo baya kukuhusu? Mara nyingi, njia bora ya kushughulikia mzaha ni kuupuuza tu.

Vivyo hivyo, si jambo la hekima kukasirika sana unapohisi kwamba umetendewa vibaya. Tineja mmoja anayeitwa David akumbuka yaliyotukia alipocheza mpira wa vikapu pamoja na Wakristo wenzake. David asema hivi: “Mtu fulani wa timu ile nyingine alinigonga kwa mpira.” David alipokata shauri mara moja kwamba mtu huyo alikuwa na nia mbaya, alilipiza kisasi, akamtupia mpira mchezaji huyo. David akubali hivi: “Nilikasirika sana.” Lakini David alisali kwa Yehova kabla ya mambo kuharibika sana. Alijiuliza hivi, ‘Ninafanya nini, eti ninataka kupigana na ndugu yangu Mkristo?’ Baadaye, waliombana msamaha.

Katika hali kama hizo, ni vizuri kukumbuka mfano wa Yesu Kristo. “Alipokuwa akitukanwa, hakuwa akitukana kwa kurudisha. Alipokuwa akiteseka, hakutisha.” (1 Petro 2:23) Naam, unapokazwa na maisha, badala ya kukasirika, sali kwa Mungu na umwombe akusaidie kuendelea kujidhibiti. Kwa ukarimu, “atawapa roho takatifu wale wanaomwomba.” (Luka 11:13) Badala ya kulipiza kisasi mtu anapokukosea, huenda jambo bora la kufanya ni kumfikia na mzungumzie jambo hilo. (Mathayo 5:23, 24) Au iwapo unaendelea kusumbuliwa, labda na kijana anayekuchokoza shuleni, usitafute vita. Badala yake, unahitaji kuchukua hatua zinazofaa ili ujilinde. *

Kijana Aliyeacha Ghadhabu

Vijana wengi wametumia kanuni hizo za Biblia na wakapata matokeo bora. Kwa mfano, Catrina alitunzwa na wazazi wa kambo alipokuwa mchanga. Asema hivi: “Nilighadhibika kwa kuwa sikuelewa ni kwa nini mamangu mzazi aliniacha. Kwa hiyo nilimwelekezea hasira mamangu wa kambo. Kwa upumbavu, nilifikiri kwamba kwa kumuumiza ningekuwa nikimuumiza kwa njia fulani mamangu mzazi. Basi nilifanya kila kitu—kumtukana, kupiga-piga miguu chini, na kulia kwa ghadhabu. Nilipenda hasa kufunga milango kwa vishindo. Nilikuwa nikisema, ‘Nakuchukia!’—eti kwa sababu nilikuwa nimekasirika sana. Ninapokumbuka yaliyopita, siwezi kuamini kwamba nilifanya mambo hayo.”

Ni nini kilichomsaidia Catrina kudhibiti hasira yake? Yeye ajibu hivi: “Kusoma Biblia! Hiyo ni muhimu sana kwa sababu Yehova ajua jinsi tunavyohisi.” Catrina pia alifarijiwa wakati yeye na familia yao waliposoma makala za Amkeni! zilizoshughulikia hali ya familia yao. * Yeye akumbuka hivi: “Sote tuliweza kuketi chini pamoja na kuelewa hisia za kila mmoja wetu.”

Wewe pia waweza kujifunza jinsi ya kudhibiti ghadhabu. Unapofanyiwa mzaha, kuchokozwa, au kutendewa vibaya, kumbuka maneno ya Biblia kwenye Zaburi 4:4, [The Old Testament in Swahili (Mombasa)]: “Kasirikani, lakini msitende dhambi.(Italiki ni zetu.) Maneno hayo yaweza kukusaidia kuepuka hasira inayosababisha hasara.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 18 Ili upate ushauri unaofaa wa kushughulika na walimu waonevu, vijana wachokozi shuleni, na wanaokusumbua, ona makala za “Vijana Huuliza . . . ” katika matoleo ya Amkeni! ya Machi 8, 1985; Januari 8, 1987; na toleo la Kiingereza la Agosti 8, 1989.

^ fu. 21 Ona mfululizo wenye kichwa “Uasilishaji—Shangwe na Magumu,” kwenye toleo la Amkeni! la Mei 8, 1996.

[Picha katika ukurasa wa 15]

Mara nyingi, njia bora ya kushughulikia mzaha ni kuupuuza tu