Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Watu Hukata Tamaa ya Kuishi?

Kwa Nini Watu Hukata Tamaa ya Kuishi?

Kwa Nini Watu Hukata Tamaa ya Kuishi?

“Kila mtu anayejiua huwa na sababu zake mwenyewe: za kibinafsi, zisizojulikana, na zinazohangaisha.”—Kay Redfield Jamison, mtaalamu wa magonjwa ya akili.

“KUISHI ni kuteseka.” Hivyo ndivyo Ryunosuke Akutagawa, mwandishi maarufu wa Japani aliyeishi katika miaka ya mapema ya karne ya 20, alivyoandika muda mfupi kabla ya kujiua. Hata hivyo, alianza sentensi hiyo kwa maneno haya: “Kwa wazi, sitaki kufa, lakini . . . ”

Kama Akutagawa, watu wengi wanaojiua hawataki kufa lakini wanataka “kukomesha mambo yanayotukia,” ndivyo alivyosema profesa mmoja wa saikolojia. Barua ambayo watu wanaojiua huandika huonyesha hivyo. Sentensi kama vile ‘Singevumilia zaidi ya hapo’ au ‘Kwa nini niendelee kuishi?’ huonyesha tamaa kubwa ya kuepuka magumu ya maisha. Lakini kama vile mtaalamu mmoja alivyoeleza, kujiua ni “kama kutibu mafua kwa kutumia bomu la nyukilia.”

Ijapokuwa visababishi vya kujiua hutofautiana, kwa ujumla mambo fulani hususa maishani huwachochea watu kujiua.

Mambo Yanayowachochea

Si ajabu kwamba vijana hufadhaika na kujiua hata kwa sababu ya mambo yanayoonekana kuwa madogo kwa watu wengine. Wanapofadhaika na kutoweza kubadili hali hiyo, huenda vijana wakaona kuwa wakijiua watakuwa wakilipiza kisasi dhidi ya watu waliowaumiza. Hiroshi Inamura, mtaalamu anayeshughulika na watu wanaotaka kujiua nchini Japani, aliandika hivi: ‘Watoto hukuza tamaa ya kumwadhibu mtu aliyewanyanyasa kwa kujiua.’

Uchunguzi uliofanywa hivi majuzi huko Uingereza ulionyesha kwamba watoto wanapodhulumiwa sana, uwezekano wa kujiua huwa karibu mara saba zaidi ya ilivyo kawaida. Watoto hao huumia sana kihisia. Mvulana mmoja mwenye umri wa miaka 13 aliyejitia kitanzi, aliacha barua iliyowataja vijana watano waliomnyanyasa na kumlazimisha awape pesa. Aliandika hivi: “Tafadhali waokoeni watoto wengine.”

Huenda wengine wakajaribu kujiua wanapokuwa na matatizo shuleni au wanapovunja sheria, uhusiano wao wa kimapenzi unapovunjika, wanapoanguka mtihani, wanapofadhaishwa na mitihani, au wanapolemewa sana na mahangaiko kuhusu maisha ya baadaye. Vijana wanaobalehe ambao hufanya vyema shuleni na kupenda kufanya mambo barabara kabisa wanaweza kujaribu kujiua wasipofanikiwa au wanapokabili kipingamizi iwe ni jambo halisi au la kuwazia tu.

Mara nyingi, matatizo ya kiuchumi au ya kikazi huwachochea watu wazima kujiua. Baada ya uchumi kuzorota kwa miaka mingi nchini Japani, hivi karibuni watu zaidi ya 30,000 walijiua katika mwaka mmoja. Kwa mujibu wa gazeti la Mainichi Daily News, robo tatu hivi ya watu wa umri wa makamo waliojiua walifanya hivyo “kwa sababu ya matatizo yanayosababishwa na madeni, kufilisika kwa biashara, umaskini na kukosa kazi.” Matatizo ya familia yanaweza pia kuwafanya watu wajiue. Gazeti moja la Finland liliripoti kwamba kuna uwezekano mkubwa kwa “wanaume wa umri wa makamo waliopata talaka hivi majuzi” kujiua. Uchunguzi uliofanywa huko Hungaria ulifunua kwamba wasichana wengi wanaofikiria kujiua ni wale waliolelewa katika familia zilizovunjika.

Kustaafu na ugonjwa ni mambo mengine pia yanayochochea watu kujiua, hasa wazee-wazee. Mara nyingi mgonjwa huamua kujiua ili kuepuka mateso, si tu anapougua ugonjwa usio na tiba, bali wakati anapoona kuwa hawezi kuvumilia kuteseka.

Hata hivyo, si watu wote wanaojiua wanapokabili matatizo hayo. La, watu wengi wanapokabili hali hizo zenye mikazo hawajiui. Basi, ni kwa nini watu fulani hufikiri kujiua ni suluhisho, na wengine hawafikiri hivyo?

Visababishi Visivyoonekana Wazi

Kay Redfield Jamison, profesa wa magonjwa ya akili kwenye Shule ya Tiba ya Chuo Kikuu cha Johns Hopkins, asema hivi: “Uamuzi wa kujiua hutegemea hasa jinsi mtu anavyoelewa mambo.” Aongezea hivi: “Akili za watu wengi, zinapokuwa timamu, hazioni kuwa jambo lolote lile linaweza kumfadhaisha mtu hata ajiue.” Eve K. Mościcki, wa Taasisi ya Kitaifa ya Marekani ya Masuala ya Akili, asema kwamba visababishi vingi—vingine visivyoonekana wazi—hujumlika kuwaongoza watu kujiua. Visababishi hivyo visivyoonekana wazi vyatia ndani magonjwa ya akili na magonjwa yanayosababishwa na uraibu, maumbile ya chembe za urithi, na utendaji wa kemikali ubongoni. Tutachunguza baadhi ya visababishi hivyo.

Visababishi vikuu zaidi ni magonjwa yanayosababishwa na uraibu na magonjwa ya akili, kama vile kushuka moyo, magonjwa ya hisia zinazobadilika-badilika, sizofrenia (kuchanganyikiwa kiakili), na kutumia vibaya vileo au dawa za kulevya. Uchunguzi uliofanywa huko Ulaya na Marekani unaonyesha kwamba zaidi ya asilimia 90 ya watu wanaojiua huugua magonjwa hayo. Kwa kweli, watafiti wa Sweden waligundua kwamba visa vya kujiua miongoni mwa wanaume wasiougua magonjwa hayo vilikuwa 8.3 kati ya wanaume 100,000, lakini miongoni mwa wale walioshuka moyo viliongezeka hadi visa 650 kati ya wanaume 100,000! Na wataalamu wanasema kwamba hivyo ndivyo visababishi vya kujiua pia katika nchi za Mashariki. Lakini, hata mambo yanayochochea watu kujiua yakijumlishwa pamoja na kushuka moyo, bado yawezekana kuepuka kujiua.

Profesa Jamison, ambaye wakati mmoja alijaribu kujiua, asema hivi: “Watu huonekana kuwa wanaweza kustahimili au kuvumilia kushuka moyo maadamu wanatumai kwamba mambo yatakuwa afadhali.” Hata hivyo, amegundua kwamba mtu asipoweza kustahimili mfadhaiko unaoongezeka hatua kwa hatua, uwezo wa mfumo wa akili wa kuzuia tamaa ya kujiua hupungua pole kwa pole. Analinganisha hali hiyo na jinsi breki za gari zinavyokwisha kwa sababu ya mkazo mwingi.

Ni muhimu kutambua mwelekeo huo kwani yawezekana kutibu mshuko wa moyo. Mtu anayehisi kuwa hajiwezi anaweza kurudia hali yake ya kawaida. Visababishi visivyoonekana wazi vikishughulikiwa, watu wanaweza kutenda kwa njia tofauti wanapokumbwa na maumivu ya kihisia na mikazo ambayo mara nyingi huchochea watu kujiua.

Watu fulani hufikiri kwamba maumbile ya chembe za urithi ni kisababishi kisichoonekana wazi cha visa vingi vya kujiua. Ni kweli kwamba chembe za urithi huchangia hisia za mtu kwa njia fulani, na uchunguzi umefunua kwamba familia nyingine huwa na visa vingi vya kujiua zaidi ya nyingine. Lakini, “mwelekeo wa kujiua uliorithiwa haumaanishi kamwe kwamba mtu hawezi kuepuka kujiua,” asema Jamison.

Utendaji wa kemikali ubongoni ni kisababishi kingine kisichoonekana wazi. Mabilioni ya chembe za neva huwasiliana ubongoni kupitia utendaji wa kemikali. Kwenye ncha zilizotengana za nyuzi za neva kuna mapengo madogo yanayoitwa sinapsi. Vitu fulani hupitisha habari kwenye sinapsi kupitia utendaji wa kemikali. Huenda kiasi cha serotonin, kimojawapo cha vitu vinavyopitisha habari, huchangia uwezekano wa kibiolojia wa mtu kujiua. Kitabu Inside the Brain chaeleza hivi: “Kiasi kidogo cha serotonin . . . chaweza kumnyang’anya mtu furaha maishani, kwa kupunguza tamaa yake ya kuishi na kuongeza uwezekano wa kushuka moyo na kujiua.”

Hata hivyo, jambo la hakika ni kwamba hakuna mtu aliyepangiwa kujiua. Mamilioni ya watu hukabiliana na maumivu ya kihisia na mikazo. Wengine hujiua kutokana na jinsi ubongo na moyo unavyotenda wanapokabili mikazo. Mbali na kushughulikia mambo yanayochochea watu kujiua, ni lazima visababishi visivyoonekana wazi vishughulikiwe pia.

Hivyo basi, ni jambo gani linalopasa kufanywa ili mtu awe na maoni yanayofaa yatakayomfanya afurahie tena kuishi?

[Sanduku katika ukurasa wa 6]

Jinsia na Kujiua

Kwa mujibu wa uchunguzi uliofanywa huko Marekani, ingawa uwezekano wa wanawake kujaribu kujiua ni mara mbili au tatu ya ule wa wanaume, uwezekano wa wanaume kufaulu kujiua ni mara nne ya ule wa wanawake. Uwezekano wa wanawake kushuka moyo ni mara mbili ya ule wa wanaume. Huenda hilo likaonyesha ni kwa nini wanawake wengi hujaribu kujiua. Hata hivyo, huenda magonjwa yao ya kushuka moyo hayawafanyi kuwa hatari sana. Hivyo hawatumii njia hatari sana za kujiua. Kwa upande mwingine, huenda wanaume wakatumia njia hatari za kujiua ili kuhakikisha kwamba watafaulu.

Hata hivyo, nchini China, wanawake ndio hufaulu kujiua zaidi ya wanaume. Kwa hakika, uchunguzi unafunua kwamba asilimia 56 hivi ya visa vya wanawake wanaojiua ulimwenguni hutukia China, hasa katika maeneo ya mashambani. Yasemekana kuwa mojawapo ya sababu za wanawake kujaribu na kufaulu kujiua nchini humo ni kwamba ni rahisi kupata dawa hatari za kuua wadudu.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 7]

Kujiua na Upweke

Upweke ni mojawapo ya mambo yanayofanya watu washuke moyo na kujiua. Jouko Lönnqvist, ambaye aliongoza uchunguzi mmoja kuhusu visa vya kujiua nchini Finland, alisema hivi: “Watu wengi [waliojiua], walihisi upweke kila siku. Walikuwa na wakati mwingi lakini hawakushirikiana sana na watu.” Kenshiro Ohara, mtaalamu wa magonjwa ya akili kwenye Shule ya Tiba ya Chuo Kikuu cha Hamamatsu nchini Japani, alitaarifu kwamba “kujitenga” kulisababisha ongezeko la hivi majuzi la idadi ya wanaume wa makamo waliojiua nchini humo.

[Picha katika ukurasa wa 5]

Mara nyingi, matatizo ya kiuchumi au ya kikazi huwachochea watu wazima kujiua