Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tatizo la Ulimwenguni Pote

Tatizo la Ulimwenguni Pote

Tatizo la Ulimwenguni Pote

“Kujiua ni tatizo kubwa kwa afya ya jamii.”—David Satcher, ofisa mkuu wa afya wa Marekani, mwaka wa 1999.

HIYO ndiyo mara ya kwanza kabisa kwa ofisa mkuu wa afya wa Marekani kutaarifu kwamba tatizo la kujiua ni jambo la kuhangaikiwa na jamii. Idadi ya watu wanaojiua nchini humo yazidi idadi ya watu wanaouawa. Haishangazi kuwa Bunge la Marekani lilitangaza kwamba kuzuia visa vya kujiua ni jambo linalopasa kushughulikiwa kwanza kotekote nchini humo.

Hata hivyo, visa vya kujiua nchini Marekani, ambavyo vilikuwa 11.4 kati ya kila watu 100,000 mwaka wa 1997, havijafikia vile vya ulimwenguni pote vilivyochapishwa na Shirika la Afya Ulimwenguni mnamo mwaka wa 2000, yaani, visa 16 kati ya kila watu 100,000. Visa vya kujiua ulimwenguni pote vimeongezeka kwa asilimia 60 katika miaka 45 iliyopita. Sasa, katika mwaka mmoja tu, watu wapatao milioni moja ulimwenguni pote hujiua. Yaani, yakadiriwa kuwa baada ya kila sekunde 40, mtu mmoja hujiua!

Hata hivyo, takwimu hazionyeshi tatizo hilo waziwazi. Katika visa vingi, familia nyingi hukana kwamba mshiriki wao alijiua. Isitoshe, yakadiriwa kwamba kila mara mtu mmoja anapojiua, watu 10 hadi 25 huwa wamejaribu kujiua. Uchunguzi mmoja ulifunua kwamba asilimia 27 ya wanafunzi wa shule za sekondari nchini Marekani walikubali kwamba walikuwa wamefikiria sana kujiua katika mwaka uliotangulia; asilimia 8 ya wale waliohojiwa walisema kwamba walijaribu kujiua. Uchunguzi mwingine umefunua kwamba asilimia 5 hadi 15 ya watu wazima wamefikiria kujiua wakati fulani.

Tofauti za Kitamaduni

Watu huwa na maoni yanayotofautiana kuhusu kujiua. Wengine huona kujiua kuwa uhalifu, wengine huona ni tendo la woga, na bado wengine huona ni njia ya heshima ya kuomba radhi kwa kosa. Hata wengine huona kujiua kuwa njia bora ya kuendeleza harakati fulani. Kwa nini kuna maoni tofauti-tofauti? Utamaduni huchangia sana. Kwa hakika, jarida la habari la The Harvard Mental Health Letter ladokeza kwamba huenda hata utamaduni “ukachangia uwezekano wa kujiua.”

Fikiria nchi moja katika Ulaya ya kati—Hungaria. Dakt. Zoltán Rihmer afafanua kiwango cha juu cha kujiua nchini humo kuwa “‘utamaduni’ unaohuzunisha” wa Hungaria. Béla Buda, mkurugenzi wa Taasisi ya Kitaifa ya Afya nchini Hungaria, alisema kwamba Wahungaria huwa tayari kujiua kwa sababu yoyote. Kulingana na Buda, hili ni itikio moja la kawaida: “Anaugua kansa—anajua jinsi ya kukomesha hali hiyo.”

Hapo zamani kulikuwa na desturi ya kidini nchini India iliyoitwa suttee. Ijapokuwa desturi hiyo ya mjane kujitupa juu ya rundo la kuni za kuchomea mwili wa mumewe ilikatazwa kwa muda mrefu, bado haijakwisha kabisa. Mwanamke mmoja alipojiua kwa njia hiyo, watu wengi wa eneo hilo walisifu sana msiba huo. Kwa mujibu wa gazeti la India Today, katika eneo hilo la India ‘wanawake wapatao 25 wamejichoma kwenye marundo ya kuni za kuchomea miili ya waume zao katika kipindi cha miaka 25.’

Kwa kushangaza, idadi ya watu wanaojiua nchini Japani ni mara tatu ya idadi ya wanaokufa kupitia aksidenti za barabarani! Kichapo Japan—An Illustrated Encyclopedia chasema hivi: ‘Utamaduni wa Japani ambao haujashutumu kamwe kujiua, unatambuliwa kwa desturi fulani maarufu ya kujipasua matumbo (seppuku au hara-kiri).’

Katika kitabu chake BushidoThe Soul of Japan, Inazo Nitobe, ambaye baadaye alikuwa msaidizi wa katibu mkuu wa Ushirika wa Mataifa, alieleza desturi hiyo ya kufurahia kifo. Aliandika hivi: ‘Desturi hiyo [seppuku] iliyoanzishwa katika enzi za kati, ilitumiwa na maaskari wa vita kulipia matendo yao ya uhalifu, kuomba radhi kwa makosa yao, kuhepa aibu, kulipia maovu waliyowatendea rafiki zao, au kuonyesha unyofu wao.’ Ijapokuwa desturi hiyo ya kujiua haionekani sana siku hizi, bado watu wachache huitumia ili kuathiri jamii.

Kwa upande mwingine, katika Jumuiya ya Wakristo, kujiua kulionwa kwa muda mrefu kuwa uhalifu. Kufikia karne ya sita na ya saba, Kanisa Katoliki liliwatenga watu waliokuwa wamejiua na likakataa kuwafanyia ibada ya mazishi. Katika sehemu fulani, ushupavu wa kidini umetokeza desturi za kiajabu kuhusu watu waliojiua kama vile kuning’iniza mwili wa mtu aliyejiua, na hata kudunga moyo wake kwa mti uliochongoka.

Kwa kushangaza, wale waliojaribu kujiua wangeweza kuhukumiwa kifo. Mwingereza mmoja wa karne ya 19 alinyongwa kwa sababu alijaribu kujiua kwa kujikata koo. Hivyo, wenye mamlaka walitimiza jambo ambalo mtu huyo alishindwa kufanya. Ijapo adhabu ya jaribio la kujiua ilibadilika baadaye, ni katika mwaka wa 1961 tu ndipo Bunge la Uingereza lilitangaza kwamba kujiua na majaribio ya kujiua hayakuwa tena matendo ya uhalifu. Katika Ireland, kujiua kulionwa kuwa uhalifu hadi mwaka wa 1993.

Siku hizi waandishi fulani husema kwamba kujiua ni njia nyingine ya kusuluhisha matatizo. Kitabu kimoja cha mwaka wa 1991 kilichozungumzia jinsi watu wanaougua ugonjwa usio na tiba wanavyoweza kusaidiwa kujiua, kilidokeza njia mbalimbali za kufanya hivyo. Baadaye, watu wengi ambao hawakuugua ugonjwa usio na tiba walitumia mojawapo ya madokezo hayo.

Je, kweli kujiua husuluhisha matatizo? Au, je, kuna sababu nzuri za kuendelea kuishi? Kabla hatujajibu maswali hayo, acheni kwanza tuchunguze mambo yanayofanya watu wajiue.

[Blabu katika ukurasa wa 4]

Katika mwaka mmoja tu, watu wapatao milioni moja ulimwenguni pote hujiua. Yaani, baada ya karibu kila sekunde 40, mtu mmoja hujiua!